hotuba ya mhe wka uzinduzi wa bodi.pdf
TRANSCRIPT
1
HOTUBA YA MHE. GAUDENTIA KABAKA (MB), WAZIRI WA KAZI NA
AJIRA KWENYE UZINDUZI WA BODI YA WADHAMINI YA MFUKO WA
FIDIA KWA WAFANYAKAZI KATIKA UKUMBI WA WIZARA YA KAZI
NA AJIRA TAREHE 4 SEPTEMBA, 2015
Bw. Eric Shitindi, Katibu Mkuu, Wizara ya Kazi na Ajira;
Bw. Emmanuel Humba, Mwenyekiti, Bodi ya Wadhamini, Mfuko wa
Fidia kwa Wafanyakazi;
Wajumbe wa Bodi ya Wadhamini, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi;
Wakuu wa Idara na Vitengo hapa Wizarani Wizarani;
Mkurugenzi Mkuu, Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Hifadhi ya
Jamii (SSRA);
Bw. Masha Mshomba, Mkurugenzi Mkuu, Mfuko wa Fidia kwa
Wafanyakazi (WCF);
Mwakilishi, Shirika la Kazi Duniani (ILO);
Mwakilishi, Chama cha Waajiri Tanzania (ATE);
Mwakilishi, Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA);
Wageni waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Habari za asubuhi!
2
1. Awali ya yote ninapenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa
Rehema kwa kutujaalia uzima, nguvu na afya njema kwa kutuwezesha
kukutana hapa leo katika siku hii muhimu.
Aidha,napenda nitumie fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa
heshima kubwa mliyonipa ya kunialika kuwa Mgeni Rasmi katika hafla
hii ya Uzinduzi wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa
Wafanyakazi.
Pia, nitumie nafasi hii, kutoa pole kwako Mwenyekiti na kwa
Wajumbe wote kwa kufiwa na mmoja wenu aliyekuwa Mjumbe wa
Bodi ya Wadhamini ya ya Mfuko wa fidia kwa Wafanyakazi
Marehemu Bw. Henry Nyamubi. Mungu amlaze mahala pema
peponi Amina.
2. Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi,
Napenda pia nitumie fursa hii kutoa pongezi zangu za dhati kwako
wewe Mwenyekiti pamoja na wajumbe wote wa Bodi ya Wadhanini ya
Mfuko wa Fidia kwa kuteuliwa kwenu kuwa wasimamizi wa shughuli za
Mfuko huu. Ninazo taarifa kwamba, pamoja na Uzinduzi kutokufanyika
kwa wakati, lakini kwa kutambua umuhimu, wa majukumu ya Bodi hii,
tayari mlikwishaanza utekelezaji wa majukumu yenu. Ninawapongeza
sana!
3. Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi,
Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi Na. 20 ya Mwaka 2008, imetungwa
kutokana na sababu mbalimbali, lakini kubwa ni kupitwa na wakati kwa
Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi Sura 263 iliyotungwa toka Mwaka
3
1949 na kufanyiwa marekebisho mengi hivyo kuleta ugumu katika
utekelezaji. Aidha, mafao yanayotolewa chini ya Sheria hii ya zamani ni
machache na viwango vya malipo ya Fidia ni vidogo sana na hivyo
kutokukidhi mahitaji ya sasa ya wafanyakazi pindi wanapoumia, kuugua
ama kufariki kutokana na kazi wanazozifanya.
4. Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi,
Kuundwa kwa Mfuko wa Fidia ni hatua muhimu sana kwa nchi yetu
katika kupanua wigo wa Hifadhi ya Jamii nchini. Ujio wa Sheria Mpya ya
Fidia kwa Wafanyakazi Na. 20 ya Mwaka 2008 ni mkombozi si kwa
wafanyakazi pekee, bali hata kwa waajiri na Wananchi kwa ujumla. Hii
ni kutokana na sababu kwamba, kupitia Sheria Mpya ya Fidia kwa
Wafanyakazi, idadi ya mafao imeongezeka, viwango vya malipo Fidia
kwa wafanyakazi na wategemezi wao vitaboreshwa, na hata utaratibu
wa kushughulikia madai ya Fidia utaboreshwa. Tunatarajia kwamba
hata mchakato wa kufuatilia na kulipa fidia utakuwa rahisi na wa muda
mfupi zaidi kuliko ilivyo sasa.
5. Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi,
Kazi kubwa niliyopewa kwa siku ya leo ni kuzindua Bodi ya Wadhamini
ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, lakini naomba nitumie fursa hii
kueleza yafuatayo;
4
Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi imeundwa kwa
mujibu wa matakwa ya kifungu cha 12 cha Sheria ya Fidia kwa
Wafanyakazi, Na. 20 ya Mwaka 2008, na inajumuisha wajumbe kutoka
Serikalini, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Vyama vya
Wafanyakazi, Vyama vya Waajiri, OSHA, Benki Kuu, Taasisi za Elimu
ya Juu, pamoja na wawakilishi kutoka kwa watu wenye ulemavu
unaotokana na ajali ama magonjwa yanayotokana na kazi.
6. Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi,
Katibu Mkuu ameelezea kwa kifupi madhumuni ya kuanzisha Mfuko wa
Fidia pamoja na majukumu ya Mfuko. Mimi najielekeza kwenye
majukumu ya Bodi ya Wadhamini. Majukumu ya Bodi ya Wadhamini ya
Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi yameainishwa bayana katika kifungu
cha 13 cha Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi, Na. 20 ya Mwaka 2008.
Majukumu hayo ni pamoja na:
(i) Kusimamia uendeshaji wa shughuli za Mfuko;
(ii) Kutengeneza, kutekeleza na kupitia Sera zinazohusiana na
Fidia kwa wafanyakazi kulingana na matakwa ya Sheria;
(iii) Kumshauri Mhe. Waziri wa Kazi kuhusu maswala yote
yanayohusu Fidia kwa wafanyakazi, marekebisho ya sheria ya
fidia kwa wafanyakazi , kanuni ama sheria nyingine
zinazohusiana na Sheria hii;
(iv) Kukuza mbinu za kuzuia ajali na magonjwa katika sehemu za
kazi kwa kushirikiana na Mamlaka ya Afya na Usalama mahala
pa kazi (OSHA);
5
(v) Kutoa elimu juu ya haki na wajibu wa mwajiri, mfanyakazi na
wategemezi wao.
7. Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi,
Majukumu haya ni makubwa na muhimu sana kwa ustawi wa Mfuko.
Hivyo nina matumaini makubwa kwamba, mtatekeleza majukumu hayo
na mengine ambayo sikuyataja lakini yameelezwa katika Sheria husika
ili kuhakikisha kwamba, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi unakidhi
matarajio ya wadau na kuleta tija na mahusiano mazuri sehemu za kazi.
Hamkuchaguliwa kuwa Wajumbe kwa bahati mbaya isipokuwa
tulizingatia sana sifa mlizonazo pamoja na uzoefu wenu. Hivyo,
tunaimani na nyinyi kwamba mtatumia weredi wenu kwa uadilifu katika
kutekeleza majukumu yenu.
8. Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi,
Taasisi mnayosimamia ni Sehemu ya Wizara ya Kazi na Ajira. Hivyo
nitumie nafasi hii kuwakaribisha sana kwenye familia ya Taasisi zilizo
chini ya Wizara ya Kazi na Ajira. Taasisi nyingine ambazo ziko chini ya
Wizara ni pamoja na Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Hifadhi ya
Jamii (SSRA), Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Shirika la Tija la Taifa
(NIP), Wakala wa Afya na Usalama Mahali pa Kazi (OSHA), Wakala
wa Huduma za Ajira Tanzania (TaESA) na Tume ya Usuluhishi na
Uamuzi (CMA), Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF).
6
Ni matarajio yangu mtatekeleza majukumu yetu kwa Ushirikiano wa
karibu na Wizara pamoja na Taasisi nyingine kwa kuzingatia Sera,
Sheria, Kanuni na mikakati ya Wizara.
9. Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi,
Nafahamu kwamba zipo changamoto nyingi ambazo mfuko utakabiliana
nazo hasa katika siku hizi za mwanzoni. Changamoto hizo ni pamoja na
uelewa mdogo wa jamii kuhusu Mfuko huu, zoezi la kuwasajili waajiri
wote wa sekta ya Umma na binafsi Tanzania Bara na uendelevu wa
mfuko. Serikali kwa kushirikiana na wadau tutaendelea kuzikabili
changamoto hizo hatua kwa hatua ili kuhakikisha kwamba malengo
yaliyokusudiwa yanafikiwa.
Kazi kubwa iliyo mbele yenu ni kuhakikisha elimu na uhamasishaji
unafanyika ili kuwezesha wafanyakazi na Waajiri wengi wanashiriki na
kujiunga na mfuko huu.
10. Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi,
Kwa kumalizia napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa
maandalizi makubwa yaliyowezesha kufanikisha hafla hii, na
7
ninawashukuru wote mlioshiriki kwa namna moja ama nyingine
katika uzinduzi huu.
Baada ya kusema hayo machache, ninayo heshima kubwa kutamka
kwamba, BODI YA WADHAMINI YA MFUKO WA FIDIA KWA
WAFANYAKAZI imezinduliwa rasmi.
Asanteni kwa kunisikiliza