11. k - hakielimu : home ya elimu tanzania.pdf · watu wazima na chenye manufaa. elimu ya watu...
TRANSCRIPT
Nyaraka ya Kufanyia Kazi
11.3.k
Hali ya Elimu Tanzania Tafiti na uhalisia vinatuambia nini?
Elizabeth Missokia & Mtemi Zombwe
Hali ya Elimu Tanzania Tafiti na Uhalisia vinatuambia nini?
Elizabeth Missokia & Mtemi Zombwe1
1.0 Utangulizi Katika dunia ya leo, ili kila mtu aweze kuboresha maisha yake ni lazima awe na elimu. Elimu ndiyo inayomwezesha mtu kujitambua na kujimiliki yeye mwenyewe kwanza, pia kuzikabili changamoto zinazomsonga, kuyatawala na kuyatumia mazingira yanayomzunguka ili kuboresha maisha yake. Ndani ya utandawazi, elimu isiyotosheleza, tafsiri yake ni umaskini zaidi; wakati elimu zaidi tafsiri yake ni maisha bora zaidi.
Nelson Mandela, Rais mstaafu wa Afrika Kusini amewahi kusisitiza umuhimu wa elimu kwa maendeleo ya jamii, kwa kusema kuwa;
“........elimu ni injini kubwa ya maendeleo ya mtu. Ni kupitia elimu ndipo binti wa mkulima mdogo anaweza kuwa daktari bingwa, kwamba mtoto wa kibarua wa mgodini anakuwa Mkuu wa Mgodi, na mtoto wa kibarua wa mashambani anakuwa Rais wa taifa kubwa”. (Mandela, 1991).
Ili elimu iweze kuleta mabadiliko ya kweli kimaendeleo ni lazima iwe elimu bora-ambayo
inalenga kumbadilisha mtu na kumwezesha kufikiri, kubuni, kujitambua, kuhoji, kudadisi,
kupenda kazi, kuwa na mwenendo mwema na kuboresha afya na maisha yake binafsi na ya
jamii. Elimu ni ukombozi iwapo italenga kumpatia mtu uwezo wa kupambana na
changamato zinazoikabili jamii na taifa kwa ujumla. Elimu inamjenga mtu kuwa raia makini
na mzalishaji ndani ya nchi yake (Zombwe, 2007)
2.0 Historia (kwa ufupi) ya Elimu Tanzania
1 Elizabeth Missokia ni Mkurugenzi Mtendaji wa HakiElimu na Mtemi Zombwe ni Mwalimu, Mchambuzi wa Sera na Mtafiti, HakiElimu. Waandikie kwa [email protected] au
[email protected]/[email protected]
“Elimu inakuwa na maana sana kama malengo yake yalikuwa ni kuhakikisha kuwa kipindi wanafunzi wanamaliza shule, kila mvulana na msichana anapaswa kufahamu kwa kiwango gani hajui, na hivyo kuhamasika kujenga matamanio ya kutaka kufahamu muda wote maishani mwake” (William Haley, 1901-1987).
Historia ya Elimu nchini inatukumbusha malengo ya msingi ya elimu Tanzania. Ukiacha
elimu ya kibaguzi iliyokuwa inatolewa kabla ya uhuru, elimu ya Tanzania baada ya uhuru
ililenga kumjenga mtu katika nyanja zote ili awe mzalishaji mzuri katika nchi yake. Ndio
maana elimu na kazi vilisisitizwa sana, na vyuo vya ufundi pamoja na kazi za mikono
vilipewa msisitizo mkubwa, huku suala la usawa, haki na misingi ya umoja wa kitaifa
vikichanua na kushamiri kwenye nyaraka za serikali na kwenye vichwa vya watu.
Dhamira hii ikaleta maboresho makubwa yakiwemo ongezeko kubwa la uandikishaji, kutaifishwa kwa shule za binafsi na kufanywa za umma na kuzaliwa kwa Azimio la Arusha lililokuja kua dira ya kusimamia misingi ya haki, usawa, udugu na utu. Solomon Eliufoo ndiye aliyeongoza michakato hii kama Waziri wa Elimu kutoka mwaka 1962 hadi 1965. Katika kipindi chake, Eliufoo alipiga marufuku ada kwa wanafunzi wa sekondari, kuendeleza ujenzi wa shule za msingi na sekondari na upanuzi wa mafunzo kwa walimu wa daraja A na C na elimu ya watu wazima. Pia ndani ya miaka hii mabadiliko mengine tuliyoshuhudia ni kuruhusiwa kwa Kiswahili kutumika kama lugha ya kufundishia katika elimu ya msingi na Kiingereza sekondari, kupinga ubaguzi wa rangi katika elimu na elimu ya msingi kutangazwa kutolewa kwa miaka nane. Kipindi cha 1965 hadi 1970 chini ya Chediel Mgonja, kilishuhudia maamuzi ya aliyekuwa Rais wa awamu ya kwanza, Julius Nyerere akitangaza rasmi falsafa mpya ya elimu iliyojulikana kwa jina la Elimu ya Kujitegemea, kuanzishwa kwa Taasisi ya Elimu na uundwaji wa Baraza la Mitihani la Afrika Mashariki. Mabadiliko mengine katika kipindi hiki yalihusu kutungwa kwa Sheria ya Elimu ya mwaka
1969, shule za msingi kufundishwa na Watanzania pekee na kuimarishwa kwa kisomo cha
watu wazima na chenye manufaa. Elimu ya watu wazima ndiyo iliyojenga nchi na kuiweka
kwenye hadhi ya juu katika medani za kimataifa, hasa kwenye suala la upunguzaji wa
ujinga. Hadi kufikia mwaka 1986 kiwango cha watanzania kujua kusoma na kuandika
kilikuwa ni asilimia 91, tofauti na sasa kimeshuka hadi asilimi 692.
Miaka ya 1975 hadi 1980 ilishuhudia mabadiliko mengi tu kwenye mfumo wa elimu yetu. Ni kati ya miaka hiyo Ujenzi wa Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi ulifanyika, kutolewa kwa Tamko la Elimu ya Msingi kwa wote, ujenzi wa vituo vya ufundi kwa wahitimu wa elimu ya msingi na kuzuiwa kwa mtihani wa darasa la nne. Pia Taasisi ya Ukuzaji Mitaala na Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima zilianzishwa. Na mwaka 1978 ndicho kipindi ilipotungwa Sheria ya Elimu namba 25 chini ya Waziri Nicholas Kuhanga. Kuanzia mwaka 1995 hadi 2005, mengi yamefanyika ikiwemo kuanza kwa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Elimu (ESDP), kuanza kwa Mpango wa Maendeleo wa Elimu ya Msingi (MMEM) na Mpango wa Maendeleo wa Elimu ya Sekondari (MMES). Mipango hii ndiyo inayoshika hatamu za kuiendesha elimu yetu kuelekea kwenye ubora na fursa sawa kwa wote. Je, tija ya mabadiliko haya toka uhuru ina mwelekeo gani kwa taifa? Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025, Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini,
(MKUKUTA), Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi(MMEM), Mpango wa Maendeleo
2 Taarifa ya idadi ya watu wasiojua kusoma na kuandika aliyoitoa Naibu Waziri wa Elimu, Philip Mulugo; bungeni tarehe 15 februari 2011
ya Elimu ya Sekondari(MMMES) na Sera ya Elimu na Mafunzo vyote vinabainisha ukweli
huu kuwa ili Tanzania ipige hatua kali za kimaendeleo ni lazima wananchi wake wapate
elimu bora iliyokamilika. Lakini je, elimu inayotolewa hapa Tanzania, inakidhi haya yote?
Ama ni kwa kiasi gani inawawezesha watoto na vijana kufikia malengo hayo? Hili ndilo
swali la msingi linalopaswa kutuongoza kuelekea kwenye mipango na vitendo
vinavyoipeleka mbele elimu yetu na siyo kuirudisha nyuma.
2.0 Mafanikio ni mengi. Tumepiga hatua kubwa! Tanzania imeweza kupiga hatua kubwa kwenye utaoji elimu kwa wananchi wake. Kwa
kupitia MMEM, MMES na MEMKWA; watoto wengi wa Kitanzania wamepata fursa ya
kujiunga na elimu ya msingi na sekondari. Hadi mwaka 2010 zaidi ya watoto milioni 8
(ambao ni zaidi ya 90% ya uandikishaji halisi) wameandikishwa shule za msingi na zaidi ya
wanafunzi 1, 638, 699 wako sekondari. (Tazama chati namba 1)
Chanzo: BEST 2001 & 2010
Idadi ya shule na walimu imeongezeka maradufu. Hadi mwaka 2010 shule za sekondari
zimeongezeka kutoka shule 937 na kufikia idadi ya 4,2663 mwaka 2010. Walimu nao
wameajiriwa kwa idadi kubwa ili kusaidia mchakato wa kuwapatia watoto elimu. Kwa
mfano, hadi mwaka 2010 idadi ya walimu wa shule za msingi na sekondari imefikia walimu
206, 3734 kutoka idadi ya walimu 54,869 mwaka 2001. Ongezeko hili limechangiwa na
ongezeko kubwa la wanafunzi kwa kuanzia miaka ya 2001 hadi 2010.(tazama jedwali na
1). Hii ni dhahiri kuwa fursa za elimu kwa wote zimeongezeka nchini, na hatuna budi
kuipongeza serikali na wadau wa elimu kwa jitihada hizo.
3 BEST 2010 4 BEST 2010
4,875,185
8,419,305
0
1,000,000
2,000,000
3,000,000
4,000,000
5,000,000
6,000,000
7,000,000
8,000,000
9,000,000
Mwaka 2001 Mwaka 2010
Chati 1: Ongezeko la Idadi ya wanafunzi elimu ya msingi 2001-2010
Jedwali 1: Hali ya ongezeko la uandikishaji na walimu shule za msingi na sekondari nchini Tanzania mwaka 2001 na 2010
Mwaka Shule za msingi Shule za sekondari
Idadi ya
wanafunzi
Idadi ya
Shule
Idadi ya
walimu
Idadi ya
wanafunzi
Idadi ya
Shule
Idadi ya
walimu
Mwaka 2001 4,875,185 11,873 105,921 289,699 937 14,352
Mwaka 2010 8,419,305 15,816 165,856 1,638,699 4266 40,517
Chanzo: Kitabu cha takwimu za elimu: BEST 2002 &2010
11,873
15,816
0
2,000
4,000
6,000
8,000
10,000
12,000
14,000
16,000
18,000
Mwaka 2001 Mwaka 2010
Ida
di
ya
wa
na
fun
zi
Chati 2: Ongezeko la idadi ya shule za msingi mwaka 2001-2010
105,921
165,856
0
50,000
100,000
150,000
200,000
Mwaka 2001 Mwaka 2010
Idad
i ya
shu
le
Chat 3: Ongezeko la idadi ya walimu shule za msingi 2001-2010
3.0 Tafiti zinatuambia nini? Licha ya mafanikio haya ni dhahiri kuwa elimu yetu bado inakabiliwa na changamoto
nyingi. Tafiti na tathmini za serikali5, vyuo vikuu, wanaharakati na mashirika binafsi
zinabainisha ukweli huo, ambao ni muhimu kuuzingatia ili kutafuta majibu kwa pamoja.
Uchambuzi huu mfupi haudai kuchambua na kutoa ufumbuzi wa matatizo yote, bali kwa
kiasi kuchambua na kuchangia mapendekezo ambayo yatakuwa mchango katika kuleta
mabadiliko. Baadhi ya changamoto kubwa kwenye elimu yetu ni hizi:
3.1 Dira ya elimu: Kuna mkanganyiko wa uelewa wa nini maana ya elimu, ambapo watanzania tumekosa dira ya pamoja inayoelekeza ni elimu ya aina gani tunayotaka watoto wetu wapate. Tafiti nyingi ikiwemo ule wa HakiElimu, uliofanyika mwaka 2007, zimebainisha kuwa kuna uelewa tofauti wa nini maana na malengo ya elimu nchini. Wananchi wengi waliohojiwa walisema kuwa elimu ni kuwa na vitendea kazi vya kutosheleza kama vile vitabu, majengo, madawati na vifaa vya kufundishia. Wengine walielezea elimu ni kujua kiingereza, na wengine walidai elimu ni uwezo wa kufaulu mtihani tu. Huku ni wachache sana (chini ya 20%) waliweza kuelezea kwa mapana zaidi na kutoka nje kidogo ya vitendea kazi kwa kueleza kuwa, elimu ni uwezo, maarifa, ujuzi na mabadiliko anayopata mtu baada ya kujifunza. Kulingana na mtazamo huu wananchi wengi wameendelea kuhimizwa kufanya bidii zaidi kwenye kujenga majengo na kuzipendezesha shule, kulipia watoto tuisheni kuliko kuweka mkazo na kufuatilia nini mtoto anajifunza pale darasani. Na kwa sababu hizi, tulio wengi tumeendelea kuhesabu viwango vya ufaulu mitihani kuwa ndio elimu, badala ya uwezo na ujuzi waliopata, na kufanya hivyo watoto wanaendelea kuambulia matupu kwenye baadhi ya shule nyingi. Yaani, wanamaliza shule bila hata kujua kusoma na kuandika (Uwezo, 2011). 3.2 Lugha ya kufundishia: Lugha ya Kiingereza kama lugha ya kufundishia sekondari imeendelea kuwa kikwazo kikubwa, ambacho kimechangia katika kushindwa kuelewa masomo kwa umakini darasani. Utafiti wa HakiElimu wa mwaka 2007 ulibaini zaidi ya 60% ya wanafunzi wa sekondari hawajui lugha hii ya Kiingereza kwa ufanisi na walishindwa kusoma ama kutafsiri aya rahisi ya kiingereza iliyoandaliwa kwa ngazi ya darasa la pili. Na wanafunzi wa shule ya msingi hali ni mbaya zaidi, karibu 75% walishindwa kusoma aya rahisi ya darasa la pili. Na matokeo ya hivi karibuni ya Utafiti wa Uwezo6, yanaonesha watoto 7 kati 10 wenye umri kati ya miaka 5-16 wanashindwa kusoma aya rahisi ya Kiingereza ya darasa la pili. Na kwa sababu shule za sekondari lugha ya kujifunzia na ya mitihani ni Kiingereza, huwezi kutarajia mwanafunzi asiyejua Kiingereza kuelewa masomo darasani na hatimaye kufaulu
5 Kama ufuatiliaji wa Matumizi ya fedha za umma (PETS) 2009, Mapitio ya utekelezaji wa MMEM, MMES na Ripoti za Mkaguzi na Mdhibti Mkuu wa Hesabu za Serikali, zinabainisha madhaifu mengi kwenye mfumo wetu wa elimu. 6 Uwezo ni mradi wa kupima stadi za msingi za kujua kusoma, kuandika na kuhesabu. Uko chini ya Asasi ya TEN/MET. Utafiti wao wa kwanza umefanyika wilaya 40 za Tanzania bara mwezi Aprili 2010.
mtihani. Pia siyo siri, kuwa hata baadhi ya walimu wetu pia wanapata shida sana kufundisha kwa lugha ya Kiingereza, kwani walimu pia ni matunda ya mfumo huu huu wa elimu. Na bila shaka kushuka kwa ufaulu kwenye mitihani ya kidato cha nne mwaka 2010 (nusu ya wanafunzi wote waliofanya mtihani walipata daraja sifuri7) kumechangiwa na wanafunzi kutojua lugha hasa kwenye shule za kata. Lugha ya kujifunzia na kufundishia ni muhimu sana kwa wanafunzi na walimu kuweza kuilewa kikamilifu, ili kuwawezesha kuwasiliana na kujifunza. Lugha inaweza kuwa kikwazo kikubwa katika kuchangia kushuka kiwango cha elimu iwapo wanafunzi hawataimudu, maana watashindwa kupokea maarifa kikamilifu na wao kushindwa kujieleza ipasavyo. Hali na mwenendo wa matokeo ya kidato cha nne inaleta picha ya kufikirika. Tazama mchoro hapo chini unaolinganisha matokeo ya kidato cha nne kwa miaka 10.
Chanzo: Takwimu za NECTA 2001-2010
7 Taarifa ya Matokeo ya Baraza la mitihani, Januari 2011
90.3 %
50.4%
0
20
40
60
80
100
20
00
20
01
20
02
20
03
20
04
20
05
20
06
20
07
20
08
20
09
20
10
Asi
lim
ia y
a u
fau
lu (
Da
raja
la
I-I
V)
Mwaka
Chati 4: Matokeo ya Kidato cha 4 (Daraja la I-IV)
3.3 Kama matokeo ya kidato cha nne mwaka 2010 yanaonesha watoto wetu 88%
wamepata daraja la nne na sifuri. Na pia Naibu Waziri wa Elimu hivi bungeni alisema
Watanzania 31%8 hawajui kusoma na kuandika. Huu ni USHAHIDI TOSHA kuwa bado
jitihada za ziada zinahitajika kuikomboa nchi yetu kutoka kwenye dimbwi la UJINGA.
(tazama chati namba 6).
Ongezeko la wanafunzi wanaopata daraja sifuri, linakwenda sambamba na ongezeko la
watu wasiojua kusoma na kuandika. Ukilinganisha takwimu vitu hivi viwili vina uhusiano
wa karibu sana.
8 Majira Februari 15, 2011.
0
0.2
0.4
0.6
0.8
1
1.2
Asi
lim
ia
Chati 5: Uchanganuzi wa kina wa idadi ya wanafunzi Waliopata daraja sifuri mwaka 2010
49.6%
0.0
10.0
20.0
30.0
40.0
50.0
60.0
20
00
20
01
20
02
20
03
20
04
20
05
20
06
20
07
20
08
20
09
20
10
Pe
rce
nt
Chati 6: Matokeo ya Kidato 4
Daraja I Daraja II Daraja III
Daraja IV Waliofeli
Chanzo: Naibu Waziri wa Elimu, Philipo Mulugo bungeni Februari 15, 2011
Ikumbukwe kuwa Tanzania iling’ara katika bara lote la Afrika, hasa Kusini mwa Jangwa la
Sahara, miaka ya 1970 na 1980, kutokana na kupunguza kwa kasi idadi ya wananchi wake
wasio jua kusoma na kuandika. Chini ya Sera ya Elimu ya watu wazima, nchi iliongeza idadi
ya watu wanaojua kusoma na kuandika kila kukicha. Na manufaa yake yalionekana bayana
maana watu waliweza kupambana na changamoto zinazowakabili. Lakini pia waliongeza
uzalishaji mashambani na kuongeza uelewa wa kujikinga na maradhi na magonjwa
mbalimbali. Hadi kipindi Mwalimu Nyerere anaondoka madarakani, idadi ya watanzania
waliokuwa hawajui kusoma na kuandika ilikuwa takribani asilimia 9 tu.
Hivyo, tungeweza kwenda na mwenendo huo hadi mwaka 2010 tungekuwa na angalau
95% ya watanzania wanaojua kusoma na kuandika. Na tungebaki tunafikiria mambo
makubwa ya ugunduzi, uvumbuzi viwanda na teknolojia ya hali ya juu. Kuongezeka kwa
idadi ya wananchi wasiojua kusoma na kuandika ni ushahidi kuwa tunarudi nyuma badala
ya kusonga mbele.
3.4 Uhaba wa walimu hasa katika masomo ya hisabati na sayansi: Asili ya masomo ya
sayansi na hisabati ni mantiki, kutafiti, kufikiri na kuchambua. Hivyo, ni ngumu sana
kukariri masomo haya na kufaulu mtihani. Uhaba wa walimu kwenye masomo haya
umetajwa karibu sehemu zote kuwa ni chanzo kikubwa cha ufaulu duni wa wanafunzi. Na
kwa sababu masomo haya hayakaririki wanafunzi ni ama wapate walimu wa kuwafundisha
wenye uwezo au wafeli mitihani yao. Na kwa sababu sayansi ni msingi mzuri wa teknolojia
na uvumbuzi hasa kwa dunia ya leo ya utandawazi, wanafunzi kukosa walimu kwenye
11%
31%
89%
69%
0%
20%
40%
60%
80%
100%
Mwaka 1986 Mwaka 2010
Chati 7: Asilimia ya idadi ya watanzania wanaojua na wasiojua kusoma na kuandika
Wasiojua kusoma Wanaojua kusoma
masomo hayo inakuwa changamoto kubwa kwa nchi kwani uzalishaji utakuwa duni na
hatuwezi kuendeleza teknolojia ndani ya nchi yetu. Tutasubiri tu teknolojia za kuletewa!
3.5 Uwezo mdogo wa baadhi ya walimu na motisha ndogo kwao inachangia kuwafanya
washindwe kuwasaidia watoto kwa viwango tarajiwa. Walimu wenye uwezo duni
wamekuwa wakisema wazi kuwa hawawezi kufundisha masomo fulani. Na wale
wanaolazimishwa kufundisha masomo hayo wengi huyafundisha bila kuleta tija. Wanaingia
darasani wanajaza ubao lakini watoto hawaelewi, na hawajifunzi. Hivyo, ujifunzaji
unakuwa mdogo sana na wakati fulani haupo kabisa kwa watoto japo walimu wanaingia
darasani na kufundisha.
Na kutokana na baadhi ya walimu kukosa hisia za kazi na motisha kwenye ufundishaji,
hawajitumi, kujiendeleza na wala kuwa wabunifu wa namna ya kuwasaidia watoto
kujifunza. Wanafanya kazi kwa mazoea tu. Kwa mwalimu, hamasa ya ndani na hisia za
kufundisha ndio msingi wa ualimu ambao unajengwa na saikolojia ya walimu. Walimu
wanaaminiwa kuwasaidia watoto kuutambua ukweli ndani ya dunia ili kuibua vipaji na
vipawa vyao. Hili kwa sasa ni changamoto kubwa!
3.6 Ucheleweshaji wa ruzuku kwa wanafunzi nalo linatajwa karibu katika kila utafiti kuwa
ni tatizo kubwa ndani ya mfumo wetu wa elimu. Ruzuku kwa kila mwanafunzi ni fedha
inayomtunza mtoto shuleni, kwa kununulia mahitaji yake ya msingi katika usomaji kama
vitabu na chaki. Lakini katika shule nyingi fedha ya ruzuku kwa wanafunzi hazifiki kama
inavyotakiwa, zinachelewa kufika shule. Na kwenye baadhi ya shule fedha hazifiki kwa
kiasi kilichopangwa au kinachohitajika.
Hivyo, walimu wakuu wamekuwa katika wakati ngumu wa kupanga namna ya kuzitumia
fedha kidogo zinazofika ilihali wanafunzi wakiongezeka kila kukicha. Mathalani, Fedha za
rukuzu kwa mwanafunzi kwa mujibu wa MMEM ni Sh 10,000 kwa kila mwanafunzi elimu
ya msingi, lakini kutokana na tafiti za hivi karibuni fedha inayofika shuleni ni wastani wa
Sh 5000. Kwa sekondari kati ya Sh 25,000 zinazopaswa kupelekwa ni wastani wa sh 7500
ndizo hufika shuleni9. Kwa mwendo huu ni vigumu sana kupiga hatua (Tazama chati
namba 8)
9 Takwimu za MOVET-PETS, 2009 na HakiElimu PETS-2010 zinabainisha ukweli huo
3.7 Mitaala ya sasa haikidhi mahitaji ya jamii pana. Wananchi wanatarajia mwanafunzi
akifundishwa mabadiliko yaonekane bayana. Pia aweze kujimudu maisha yake pindi
anapomaliza shule. Hili ndio tegemeo la wengi.
“...Mimi nafikiri lengo kubwa la elimu ni kurithisha vizazi vyetu na vizazi vijavyo, maarifa,
ujuzi, na stadi za maisha ili mtu anapotoka shuleni aweze kujitegemea kuendesha maisha
yake wakati wowote na popote kuendana na mabadiliko” (Mzazi, Monduli, 2010)
3.8 Mabadiliko ya mitaala ya mara kwa mara ni kikwazo kikubwa cha utoaji elimu bora:
Walimu na wanafunzi walibainisha hili kwa kina. Mabadiliko yanapotokea ya mtaala, vifaa
au vitabu havifiki na wakati fulani unakosa hata kitabu kimoja kinachoendana na mtaala
mpya. Na vinapopatikana huchelewa sana kuwafikia walengwa. Walimu wanakosa la
kufanya. Wanabaki wanasubiri huku watoto wanaelekea kwenye mitihani wakiwa hawajui
kitu. Ilitolewa mfano kuwa kwa mwaka 2010, mpaka kufikia mwezi wa nane, darasa la sita
walikuwa hawana hata kitabu kimoja kwa baadhi ya masomo ambayo yalihusisha
mabadiliko yaliyohitaji vitabu vipya.
3.9 Uelewa mdogo wa masuala ya elimu: Baadhi ya wananchi vijijini, hasa jamii za wafugaji,
na wakulima walio pembezoni mwa nchi yetu bado hawana ulewa wa kina juu ya masuala
mbalimbali ya elimu na hata umuhimu wa elimu kwa watoto wao. Hivyo, kutojua tu
masuala ya elimu kwa ujumla ni changamoto. Maana wazazi hawawezi kufuatilia watoto
wanajifunza nini. Na baadhi ya wazazi walidai hawawezi kufuatilia ujifunzaji wa watoto
wao maana hawajui Kiingereza, ambacho ndiyo lugha wanayoandika watoto wao kwenye
0 0
0.2
0.4
0.6
0.8
1
Basic Salary Deduct PPF
Ru
zuk
u
(Sh
.bil
ion
i)
Chati 8: Tofauti kati ya ruzuku halisi iliyofika wilayani na Iliyopaswa kufika wilayani kwa mujibu
wa MMEM II.
vitabu. Lakini pia wazazi walidai hawashirikishwi na walimu, ili kuweza kufuatilia
maendeleo ya elimu ya watoto wao, hivyo hawajui waanzie wapi. (HakiElimu, 2009)
3.10 Vifaa vya maabara na vifaa vya sayansi bado ni changamoto kubwa maeneo mengi.
Walimu wanaandaa masomo ya sayansi na kuyafundisha bila kuwa na vifaa vya kufanyia
hivyo. Na baadhi ya vifaa hata vikipelekwa shuleni walimu hawajui kuvitumia wala
kufundishia wanafunzi. Kwa sehemu kubwa walimu na wanafunzi walisema hakuna
maabara, na hiki ni kikwazo kikubwa katika kufundishia masomo ya sayansi. Ni vigumu
sana kufundisha masomo kama Biolojia, Kemia na Fizikia bila maabara na vifaa vyake.
Wanafunzi10 walisema kwa kejeli kwamba hata “Bunsen burner” wanaijua kwa picha tu,
lakini ngumu kabisa ni kujua matokeo ya uchanganyaji wa kemikali mbalimbali kwa njia ya
kufikirika!
3.11 Walimu wengi kukosa mafunzo ya ualimu kazini. Wengi wanashindwa kumudu kazi
zao vizuri kwa sababu ya kukosa mafunzo hayo. Hasa walimu wa leseni ambao waliletwa
kwa lengo la kusaidia kutoa elimu huku wakijiendeleza. Udhaifu wa walimu umezaa tatizo
jingine pia la walimu kukataa baadhi ya masomo wanayopewa kufundisha. Na kutokana na
hilo masomo kama Hisabati na Sayansi yana upungufu mkubwa wa walimu. Swala hili
lilikuwa la utata kiasi kwani wakati, wilayani maafisa elimu waliripoti kuwa mafunzo kazini
yamekuwa yakifanyika mara kwa mara, lakini kwa walimu wengi waliohojiwa walikanusha
na kushangaa kuhusu suala hili.
3.12 Uhaba wa vitabu na uwepo wa vitabu vya kiada vya waandishi tofautitofauti hasa
shule za msingi unaathiri elimu nchini Tanzania. Maana wanafunzi wanachanganywa na
uwingi wa vitabu hivyo. Na kibaya zaidi, vitabu hivyo vingi vina makosa. Kwa hiyo, kwa
watoto wadogo wakifundishwa dhana moja kitofauti ni lazima watachanganyikiwa na
kupoteza dira.
Lakini kwa wilaya za vijijini suala kubwa ni uhaba wa vitabu vyenyewe kwenye maeneo
mengi. Wauza vitabu na wasambazaji hawapeleki vitabu vyote, ni baadhi tu vitafika wilaya
za pembezoni. Hali hii inasababisha baadhi ya shule kutoweza kupata baadhi ya vitabu
hasa ambavyo wanaamini ni vizuri zaidi kwenye maudhui na uchambuzi wa mada. Na kwa
sababu mtihani unatungwa mmoja nchi nzima, kutokuwa na usawa katika mgawanyo wa
vitabu kunawapa faida ya upendeleo wanafunzi wa mijini wanaopata vitabu, na hivyo
wanakuwa kwenye nafasi nzuri kufaulu zaidi mitihani kuliko walioko shule za vijijini.
3.13 Wingi wa masomo shule za msingi ni tatizo kubwa kwenye baadhi ya maeneo yenye
upungufu wa walimu na vifaa. Yaani mwanafunzi anakuwa na mzigo mkubwa na akimaliza
10 Sehemu ya mahojiano na wanafunzi katika shule mbalimbali za wilaya ya Monduli katika utafiti wa mahusiano kati ya ubora wa mitaala na elimu bora, Agosti 2010
hapo anakuwa hana stadi nyingi anazozimudu ili zimsaidie kujitegemea katika maisha.
Walimu wanaona ni vyema huko mbeleni wanafunzi waelekezwe kwenye masomo
machache tu na kwenye taaluma ambayo watakwenda nayo hadi ngazi za juu kisha
itawasaidia kufanikiwa maishani. Ndivyo wanavyofanya wenzetu walioendelea. (Mtemi,
2011).
4.0 Tufanye nini ili tuboreshe elimu yetu? Upatikanaji wa elimu bora unategemea mambo mengi sana, lakini, hapa tumejaribu tu
kutaja mambo muhimu machache, kama mapendekezo ambayo yanaweza kuchangia kutoa
dira. Uwepo wa mitaala bora na nyenzo bora za kufundishia na kujifunzia pamoja na
ushiriki wa wadau muhimu katika michakato ya maendeleo na utekelezaji wa mtaala ni
mambo muhimu sana ya kuzingatiwa. Utafiti wa HakiElimu na mashirika mengine, ikiwepo
serikali pia umebaini kwamba shule nyingi hapa nchini hazina nyenzo bora za kufundishia
na kujifunzia. Na mtaala wa taifa haukidhi tena mahitaji ya jamii pana. Ili kuboresha
michakato ya maendeleo na utekelezaji wa mtaala, mapendekezo yafuatayo yametolewa:-
4.1 Mitaala yetu inapaswa kuboreshwa ili ishabihiane na mahitaji ya jamii kubwa na
mabadiliko makubwa yanayoendelea kutokea. Wananchi wengi wanaonekana kutaka
kurudi kwenye mtaala unaoendana na elimu ya kujitegemea11, ili wahitimu waandaliwe
kujitegemea na kumudu changamoto ndani ya jamii yao, hata kama watakosa fursa za
kuendelea mbele waweze kuishi maisha ya ustawi. Wananchi na hata wanafunzi shuleni,
wangependa kuona vijana wanapatiwa mafunzo ambayo yatawapatia ujuzi na maarifa ili
waweze kujiajiri na kushiriki katika shughuli za kilimo, ufundi, biashara kwa kutumia
mbinu za kisasa na za kuleta tija.
4.2 Wananchi wengi wanadai kuwa mfumo wa matumizi ya vitabu vya aina nyingi hauna
tija kwa kuwa unawafanya wanafunzi wajifunze dhana zinazotofautiana wakati
wakitarajiwa wafanye mtihani wa aina moja12. Kwa mfano, iwapo kitabu kimoja kitasema,
ini ni sehemu ya ubongo na kitabu kingine kikasema ini linapatikana tumboni maana yake
ni kwamba watoto watakuwa wanachanganywa. Hii ni kuwadanganya watoto ukizingatia
ukweli kwamba upatikanaji wa vitabu hivi hauko sawa (baadhi watapata A, wengine
watapata B), lakini wote wanatarajiwa kufanya mtihani wa aina moja na wanatarajiwa
kutoa majibu sahihi. Kwa kuwa Tanzania tumeamua kuwa na mtihani mmoja nchi zima,
basi ni vema tukawa na vitabu ambavyo vinapatikana kwa usawa kwa shule zote, ili
ushindani nao uwe wa usawa.
11 Elimu ya kujitegemea chini ya utawala wa Nyerere ndiyo iliyopandikiza fikra za watanzania kupenda kufanyakazi na kufanyakazi kwa ujumla. 12 Utafiti wa HakiElimu: Mahusiano kati ya ubora wa mitaala na Ubora wa Elimu, 2011
4.3 Wananchi wengi, wazazi, walimu na wanafunzi walipendekeza matumizi ya vitabu vya
aina moja, hasa shule za msingi. Na kwa hiyo serikali inapaswa kuliangalia hili kwa faida ya
wote na ili kuhakikisha kuwa kunakuwa na elimu bora na inayotolewa kwa usawa. Kwa
hiyo, kuna haja ya kuifanyia marekebisho sera ya matumizi ya vitabu vya kiada iliyopo kwa
sasa ili iwe kama ilivyokuwa zamani ambapo kitabu cha aina moja chenye ubora kilikuwa
kinatumika nchi nzima.
4.4 Ubora katika vitabu ni jambo nyeti na la muhimu sana. Vitabu ndiyo kiongozi kikubwa
kwa walimu na wanafunzi hivyo waandishi wa vitabu hivi lazima wazingatie ubora na
ukweli wa mambo. Wakati soko huria la utengenezaji na usambazaji wa vitabu lililenga
kupunguza uhaba mkubwa wa vitabu, kuna haja ya kudhibiti ubora wa vitabu ili
kuhakikisha kuwa vitabu vinavyopendekezwa kutumika mashuleni vinakuwa na ubora
unaohitajika. Kwa sasa utafiti unaonesha, vitabu vinavyochapishwa na wachapishaji
mbalimbali vinatofautiana sana kwa ubora na kwamba baadhi ya vitabu havina ubora
unaohitajika.
4.5 Ushiriki wa wazazi na wanajamii katika maendeleo na utekelezaji wa mtaala ni suala
muhimu katika kufanikisha kitendo cha ujifunzaji kwa wanafunzi. Kwa sasa ushiriki wa
wazazi na wanajamii katika maendeleo na utekelezaji wa mtaala ni mdogo hapa nchini.
Kuna haja ya kuchukua hatua madhubuti, kwanza kuwahamasisha wazazi na viongozi
katika jamii juu ya umuhimu wa ushiriki wao katika maendeleo ya watoto wao shuleni. Pili,
suala la mabadiliko ya mtaala ni sharti lizingatie maoni ya wadau wote muhimu
ukijumuisha wazazi, walimu, wanafunzi na wanajamii wengine. Walimu na wazazi wana
mchango mkubwa katika elimu na ni lazima wawe na uwezo wa kuchangia masuala
mbalimbali ya elimu likiwemo la utunzi wa mitaala kwa nafasi na kiwango chao cha ujuzi.
Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kuwa
“wale wenye wajibu wa kufanya na vijana wa umri mdogo, wana nguvu kubwa zisizozidiwa
na nguvu za yeyote yule kwa kutilia maanani hali ya baadaye ya jamii yetu. Nguvu hizi ziko
katika makundi mawili, wazazi na walimu” (Agosti 27, 1966).
4.6 Matumizi ya Kiingereza kama lugha ya kufundishia katika shule za sekondari
inaonekana kama kikwazo kikubwa katika ushiriki wa wazazi katika kuwasaidia watoto
wao kwa kuwa wazazi wengi hawaimudu lugha hiyo. Suala la lugha ya kufundishia
limekuwa likiibua mijadala mizito na kwamba mwafaka umekuwa haufikiwi katika suala
hili. Kuna haja kwa Serikali kuchukua hatua madhubuti katika kuongoza majadiliano
kuhusu lugha ya kufundishia katika mfumo wetu wa elimu ili kufikia muafaka. Watoto
hujifunza vizuri zaidi iwapo wataimudu lugha ya kufundishia, vivyo hivyo kwa walimu
wakati wa kufundisha. Suala hili linapaswa kutazamwa kwa makini zaidi ili kuhakikisha
kuwa lugha ya kufundishia inafahamika vyema kwa walimu na wanafunzi.
4.7 Ukosefu wa nyenzo na vifaa vya kufundishia na kujifunzia ulionekana kama kikwazo
katika utekelezaji wa mtaala. Tatizo hili ni kubwa zaidi kwa vitabu vya sayansi na
maabara. Ukosefu wa nyenzo hizi za kufundishia na kujifunzia hauwezi kupuuzwa kwa
kuwa umebainishwa pia kwenye tafiti zilizopita. Kuna haja kwa wasimamizi katika sekta
ya elimu kutilia mkazo suala la upatikanaji wa nyenzo za kutosha za kufundishia na
kujifunzia katika shule zetu kwa kuwa bila upatikanaji wa nyenzo hizo muhimu ufanisi
katika utekelezaji wa mtaala hautakuwepo. Wengi walikiri kuwa serikali imeamua jambo
jema kupanua fursa za watoto wengi kupata elimu ya msingi na sekondari. Lakini
waliongeza kusema kuwa, ni muhimu pia shule hizi ziwe bora na ni bora sasa kuboresha
shule zilizopo na kuziwekea walimu wa kutosha, kuboresha mazingira ya kujifunzia, vifaa
na vitabu, badala ya kuendelea kujenga shule nyingi ambazo hazina mafanikio.
Tunarudia tena kunukuu maneno ya busara ya Mwalimu Nyerere, aliyewahi kusema
kwamba,
“.....tunaposema kupanua elimu ya sekondari, tunaharakisha sana kusema kwamba, watu
watachangia ujenzi kwa juhudi zao, lakini majengo hayana umuhimu wa kwanza, ...vitu
muhimu katika elimu ni walimu, vitabu kwa sayansi ni maabara” (The situation and
Challenges of Education inTanzania, Nyerere 1984)
4.8 Utekelezaji wenye ufanisi katika mtaala hutegemea mazingira bora ya kufundishia na
kujifunzia. Wanafunzi wengi walioshiriki katika utafiti walikosoa mazingira ya ujifunzaji.
Japokuwa walimu walipongezwa na wanafunzi wengi, bado mazingira yao ya kazi ni
magumu kwa kuwa wanafundisha madarasa makubwa, kuna ukosefu wa nyenzo za
kufundishia, nyumba zao za kuishi siyo bora, mishahara yao ni midogo na hawapati
mafunzo ya mara kwa mara. Kuna haja kwa wadau wa elimu kuchukua hatua madhubuti ili
kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto na hatimaye kuwafanya watoto wawe na
furaha, wawe salama. Shule inapaswa kuwa sehemu ambayo itawafanya watoto
wafanikiwe kitaaluma na kimaisha. Hakuna ubishi kwamba, walimu wengi wamekata
tamaa na ualimu imekuwa ni sehemu tu ya waliokosa, hivyo ni vema nchi ifanye jitihada za
makusudi kurejesha upya hadhi na taaluma ya ualimu.
4.9 Mafunzo kwa walimu: Kama kweli tunahitaji elimu bora hatuwezi kukwepa kuandaa
walimu bora. Na walimu bora wanatokana na msingi bora wa mafunzo bora ya kutosheleza
na yanayoendana na mtaala na dira za maendeleo za nchi. Walimu wakiandaliwa
hovyohovyo watatoa elimu ya hovyohovyo-na hatimaye tutakuwa na wasomi wa
hovyohovyo-wanaofanya kazi hovyohovyo na kuwa na maendeleo duni. Muda wa mafunzo
kwa walimu tarajali lazima uwe kamilifu. Wakufunzi wao lazima wawe bora, na mafunzo
kwa walimu kazini lazima yafanyike kwa ukamilifu wake bila kuleta visingizio vingi. Kama
sekta nyingine wanapata semina, kozi fupifupi kwanini walimu wasipate hivyo. Hakuna njia
ya mkato. Ili fedha inayotengwa na serikali kwenye elimu ilete tija basi mafunzo ya walimu
ni muhimu ili kuandaa watekelezaji wazuri wa sera ya elimu. Na kwa sababu tayari Serikali
ina Mkakati wa Usimamizi na Maendeleo ya Walimu (TDMS), ni muhimu mkakati huu
utekelezwe kwa vitendo kama ulivyopangwa ili kusaidia kupunguza na hata kuondoa
kabisa tatizo la walimu.
4.10 Siasa – Ni lazima wanasiasa watambue kuwa sekta ya elimu siyo sehemu wala jukwaa
lao la kuoneshana umahiri wa kuongea na kutoa maamuzi hata yanayotupeleka kuzimu.
Wakati ni muhimu sana kwa viongozi wetu kuwa wabunifu na kuleta mawazo bunifu
kuboresha sekta ya elimu, lakini pia wakumbuke wizara ya elimu inakuwa na mipango na
bajeti yake kama wizara nyingine. Kabla ya kutoa maagizo kwa mashindano, ni lazima kuwe
na uratibu na utekelezaji wa sera kikamilifu. Na mawazo ya kisiasa yazingatie na kufikiria
athari za maagizo yasiyo na tija katika elimu. Mambo ya kitaalamu kuhusu elimu yashauriwe
na wataalamu hasa walimu.
4.11 Kuna mgawanyo usio sawa wa rasilimali za taifa hasa kwenye elimu. Shule za mijini
zinaonekana kupendelewa kwa kila hali. Tafiti nyingi zinaonesha walimu wenye sifa wengi
hupangwa mijini. Bado, hata mgawo wa ruzuku kwa wanafunzi shule za vijijini zinaonekana
kupata kiasi na mara nyingi fedha zinachelewa kuliko shule za mjini13. Hii sio sawa.
Watanzania wengi wako vijijini. Hivyo, ni lazima kuwe na mgawanyo sawa unaozingatia
haki za watoto wote wa Tanzania.
4.12 Kushangilia matokeo ya mitihani zaidi badala ya ujuzi na maarifa sio sahihi. Kila mtu
anapenda kufanikiwa na kusifiwa, ndiyo hulka yetu binaadamu na hili si kosa. Watanzania
tumeacha kushangilia tija sasa tunashangilia kufaulu mtihani, bila kujali tunapataje
mafanikio hayo, kwa kuiba mitihani, ama kuweka mkazo mwaka wa mwisho tu (darasa la
saba na Kidato cha nne) katika kufundisha. Tunapoteza nguvu nyingi sana kufundisha
watahiniwa ili wafaulu mitihani na kutaka wilaya ama shule zetu ziongoze kwenye ufaulu ,
badala ya kutumia muda mwingi kuwasaidia watoto kupata maarifa, ujuzi na ubunifu ili
uwasaidie maishani.
4.13 Kwa nini tusijiulize swali, kwanini baadhi ya watoto wetu wanafaulu na kuchaguliwa
kuendelea na sekondari lakini hawajui kusoma na kuandika vizuri? Je hii ni elimu na
mafanikio ya kushangilia? Elimu siyo cheti, bali ni uwezo, kama mwalimu Nyerere alivyowahi
kusema,
13 MOVET –PETS 2009 na HakiElimu PETS 2010
..“kinyume kabisa na elimu, ni aina ya mafunzo inayomfundisha mtu kujifananisha na bidhaa,
ambazo thamani yake inapimwa kwa vyeti, shahada, au sifa nyingine za kitaaluma”(Nyerere
20 Mei 1974)
4.14 Kiuhalisia, elimu ya kweli hupatikana kwenye mchakato unaoendelea kati ya mwalimu
na mwanafunzi darasani. Hivyo, mbinu za kufundishia na vitendo vya ujifunzaji vinapaswa
viboreshwe kikamilifu. Kazi za kujifunza darasani na mbinu za kuibua vipaji na kuchagiza
maarifa ni muhimu viboreshwe. Na walimu wanapaswa kuwa na hamasa ya kufanya hivyo ili
tupate manufaa ya haraka.
4.15 Mazingira mazuri ya kazi ndicho kigezo muhimu zaidi kinachoamua kiwango cha
moyo wa kujitolea walio nao walimu katika kufundisha, na matokeo yake kigezo hiki huwa
na nguvu sana katika kuleta matokeo mazuri ya wanafunzi kitaaluma. Bila kurekebisha hili
uwekezaji mkubwa katika elimu hautaleta tija katika taaluma ya ualimu na elimu kwa ujumla
4.16 Mwalimu kuwa na sifa nzuri za kitaaluma pekee yake bila moyo wa kujitolea haitosho
kuimarisha ufaulu wa mwanafunzi. Shule zenye walimu wenye moyo wa kujitolea wa hali ya
juu bila kujali iwapo walikuwa na sifa za juu kitaaluma (shahada au zaidi) au la zilifanya
vizuri katika mitihani ya taifa. Jitihada mahsusi zifanyike kurejesha hamasa, kujituma na
moyo wa kufundisha.
4.17 Serikali na wadau wengine washirikiane kuboresha mazingira ya kazi na makazi ya
walimu. Usimamizi thabiti kuhakikisha kuwa walimu wanatimiza wajibu wao, hii itasaidia
kujituma zaidi na kuleta ufanisi katika kazi. Maslahi ya walimu yaboreshwe, na pia walimu
wapandishwe madaraja na kulipwa stahili zao bila kucheleweshwa; hii itachangia kurejesha
hamasa. Na Mafunzo kwa walimu kazini ya uongozi kwa wakuu na wasimamizi wa shule
yatolewe kwa ukamilifu na mara kwa mara, kwani yatasaidia sana kuongeza ufanisi na
ufundishaji wa walimu
4.18 Vigezo vitumike bila upendeleo au woga kuhakikisha kwamba kila shule inafikia
viwango vinavyokubalika ndiyo ifunguliwe na iendeshwe kama shule; shule ziwezeshwe
kufikia viwango hivi; na zile ambazo zitashindwa kwa kipindi kilichokubaliwa zisiruhusiwe
kuendelea ‘kupotosha’ ama ‘kupotezea’ muda wanafunzi. Zifungwe kama zinavyofungwa
zahanati zisizofikia viwango kubalifu.
4.19 Jitihada mahsusi za baadhi ya walimu zitambuliwe na walimu hao watuzwe ili
kuwatia moyo, na kuwahamasisha wengine kufanya kazi yao kwa bidii. Kujituma na
kuwajibika ni sehemu muhimu ya maadili ya walimu, hivyo inawapasa walimu wote nchini
wazingatie hili; hata kama wakiwa na hoja ama madai mengine ya msingi.
5.0 Hitimisho
Nchi haiwezi kuendelezwa na watu wachache wanaopata fursa za kipekee kwenye shule chache huku elimu ya jamii pana ikiwa mashakani. Hakuna haja kulumbana wala kuingiza siasa katika elimu, bali serikali itekeleze mipango na sera zilizopo na kuboresha mapungufu kwa kushirikisha wadau. Na ukweli wa hali ya elimu nchini usisulubiwe wala kubezwa bali tuupokee na kuuwekea mikakati kwa pamoja tuweze kuboresha elimu yetu. Pa kuanzia ni kila mmoja katika eneo lake, na kikubwa kufanya zaidi ya mazoea.
6.0 Marejeo MEOC, (1995). Education and Training Policy, Adult Education Press, Dar es Salaam
Nyerere, J. K. (1967). “Elimu ya Kujitegemea”, Hotuba kuhusu Waraka wa Sera, ya Marchi
1967, Dar es Salaam.
Nyerere, J. K. (1968). “Education for Self-Reliance”, in Freedom and Socialism, Uhuru na
Ujamaa, Oxford University Press, Oxford.
Nyerere, J. K. (1974). “Education for Liberation”, a speech at Dag Hammarskjold Seminar on
20th May, 1974, Dar es Salaam
Simba, I. (2002). “Sababu za kushindwa na Namna ya kujikwamua”, makala katika
chapisho Kwanini Tanzania ni Maskini Miaka 40 Baada Ya Uhuru? Jumuiya ya
Wahitimu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
URT, (2010) Basic Education Statistics in Tanzania. Ministry of Education and Vocational
Training, Dar es Salaam
Zombwe G. (2007) Elimu Ina Umuhimu Gani kwa Maendeleo ya Jamii. Dar es salaam