chuo cha biblia - spiritual life ministries ho... · web viewhii ni kweli duniani kote, kitaifa,...
TRANSCRIPT
[Front Cover]
MBWEHA TALLY HO!
Msingi Kwa Ajili Ya Kujenga Wanafunzi Wa Yesu
Wanaojiongeza Na Wenye Maono Ya Kuigusa Dunia Nzima
Kimeandikwa NaHerb Hodges
Kimefasiriwa NaMch. Simon Joel Vomo
[Back Cover]
Herb Hodges aliyezaliwa na kukulia jimbo la Arkansas Marekani, aliokoka siku alipotimiza miaka kumi na nane, na akaitwa kuwa mhubiri muda mfupi baada ya hapo.
Ndugu Hodges alisoma katika Chuo Kikuu cha Biblia kiitwacho Southwestern Seminary huko Fort Worth Texas, na kuhitimu shahada ya Masters of Divinity mwaka wa 1962. Alichunga makanisa kwa miaka 27 katika majimbo ya Arkansas, Texas na Tennessee. Mwaka wa 1980, Ndugu huyu akawa mwinjilisti, mwenye kufanya mikutano ya uamsho, makongamano ya Biblia, makongamano ya Maisha ya Kiroho na Ufuasi. Huduma hii imemfanya atembelee karibu majimbo yote hamsini ya Marekani.
Amesafiri sana katika nchi za nje kwa ajili ya kufundisha wachungaji na viongozi kuhusu mkakati wa kujenga wanafunzi wa Yesu wanaojiongeza na wenye maono ya kuigusa dunia nzima katika kutimiza Agizo Kuu la Kristo. Amefanya safari kwa ajili ya kusudi hilo katika nchi za nje ni zaidi ya 70.
Ndugu Hodges na Judy mkewe wanakaa mjini Memphis, jimbo la Tennessee.
ii
ORODHA YA YALIYOMO
UTANGULIZI.......................................................................................................................IV
SHUKRANI.........................................................................................................................VII
SURA YA 1.............................................................................................................................1
MAONO NI MUHIMU KIASI GANI?......................................................................................1
SURA YA 2...........................................................................................................................34
AGIZO LENYE KUAMUA WAJIBU WETU...........................................................................34
SURA YA 3...........................................................................................................................85
WAZO LENYE KUAMUA NJIA TUTAKAYOTUMIA..............................................................85
SURA YA 4.........................................................................................................................104
UFUNGUO ULIOKO MLANGONI MWA HISTORIA YA KANISA.........................................104
SURA YA 5.........................................................................................................................133
VINAVYOTAKIWA ILI KUFANYA WANAFUNZI.................................................................133DAWA YA DAKTARI KUTIBU TATIZO LA KUACHA AGIZO KUU....................................133
SURA YA 6.........................................................................................................................158
MPANGO WA MUNGU WA KUONGEZA...........................................................................158
SURA YA 7.........................................................................................................................177
HEKIMA YA MKAKATI WA YESU...................................................................................177
SURA YA 8.........................................................................................................................197
JINSI KIWANGO HIKI KIFANYAVYO KAZI KANISANI......................................................197
SURA YA 9.........................................................................................................................219
MANENO YAKE YA MWISHO, WOSIA WAKE..................................................................219
SURA YA 10.......................................................................................................................241
MBWEHA TALLY HO!......................................................................................................241Maana Ya Jina La Kitabu..........................................................................................241
KUMALIZIA......................................................................................................................253
MAISHA YA MBWA WA MWITUNI..................................................................................253
MUHTASARI WA KILA SURA......................................................................................264
Maswali Na Mapendekezo Kwa Ajili Ya Kujifunza Hiki Kitabu........................................270
iii
Utangulizi
Kanisa la kawaida mahali popote lina kundi kubwa la
“watendaji” wasiotumiwa ndani ya washirika wake. Mkristo wa
kawaida hana kazi kulingana na viwango vya Kristo vya ajira, na
yule Mkristo wa kawaida ambaye ana ajira, mara nyingi “hana kazi
ya kutosha”. Basi anatumia muda mwingi na juhudi nyingi katika
shughuli zenye kutoa matokeo madogo sana kwa habari ya kuwafikia
na kuwajenga watu. Kanisa la kawaida la Kikristo hukutana Jumapili
kwa Jumapili katika “jengo” na washirika wake ni “wasikilizaji”
binafsi, ambao ni sehemu ya “wasikilizaji” wengine. Kwa kifupi ni
kwamba, kanisa la kawaida limejaa “walioketi” ambao kusudi lao
pekee ni kuja kanisani, kusikiliza mahubiri na kuondoka,
wakitazamia kwamba mpango huo utasaidia katika kufikisha roho
zao mbinguni kwa namna fulani na kuwawezesha kuwa na maisha
mazuri kabla ya kufika huko. Kufanana kwa maisha hayo na maisha
ya Kikristo yanayo-onekana katika Agano Jipya ni kwa bahati tu.
Ni dhahiri kwamba sisi Wakristo lazima tujifunze tena Agano
Jipya, ambalo ndicho kitabu chetu cha kuongoza utendaji, na
tujilazimishe kuona mambo kama yalivyo wakati tunapofanya hivyo.
Lazima tujitangaze kuwa huru kutokana na mapokeo na desturi, na
tugundue Agano Jipya linatuambia nini juu yetu sisi wenyewe, na
kazi ambayo tumepewa na Mungu.
iv
Mwandishi maarufu aitwaye Charles Swindoll aliandika hivi:
“Hakuna kundi katika historia lililojithibitisha kuwa na uwezo katika
utendaji kama ile timu ya uinjilisti ya karne ya kwanza – wale watu
waliokuwa karibu sana na Kristo.” Huo ni ukweli usiokanika. Kwa
nini? Bila shaka kilichochangia sana ni utaratibu ule ambao Yesu
aliutumia katika kuwafundisha. Utaratibu huo umejengwa juu ya
neno kubwa sana – “mwanafunzi”. Neno hilo linaonekana kwa
nguvu sana katika vitabu vitano vya kwanza vya Agano Jipya,
likitokea mara 269 (katika Injili ya Mathayo hadi Kitabu cha
Matendo). Linatumika kama jina na tendo. Tena, linapotumika kama
tendo, neno lenyewe ndilo amri pekee katika Agizo Kuu ambalo
Yesu aliwapa wanafunzi Wake. Alisema hivi, “Wafanyeni watu
kuwa wanafunzi”. Sasa, kwa uhalisi wa makundi makubwa ya
waamini wasioendelezwa katika kanisa la leo (tena wengi wao wako
kanisani kila tunapokutana), ni halali kwetu kuendelea kusema
kwamba tumelifafanua vizuri neno ‘mwanafunzi’? Au kwamba sisi
tumeelewa ipasavyo maana (au utaratibu) ya “kuwafanya watu kuwa
wanafunzi”? Kwa uhalisi wa kanisa kutokuwa na mguso mkubwa
kwa ujumla, pamoja na mabilioni ya watu ambao hawafikiwi na Injili
duniani siku hizi, tunaweza kweli kuendelea kuamini kwamba
tunatimiza Agizo Kuu? Sidhani.
Kurasa hizi ni mtazamo mpya na juhudi mpya za kutafsiri
kwa kifupi sana kwamba sisi ni nani kama waamini wa Kristo, na
kazi yetu kama wafuasi Wake. Ni maombi yangu kwamba Mungu v
atatusumbua na kutuamsha kupitia kurasa hizi kuwa na mtazamo
mpya, kutaka kujihusisha kwa upya, na kuwa na matokeo mapya
katika kutimiza Agizo Kuu la Bwana wetu.
Ninawiwa na marafiki wengi sana na waandishi wasio na
idadi – wa kawaida na wa kanisa – kwa ajili ya mawazo tele na
mbinu ambazo zimefupishwa na kuandikwa hapa. Pia, ninawiwa na
wengi ambao wamenitia moyo kuandika vitu hivi, na wachache
ambao wamenisaidia kufanya hivyo. Ushawishi wao ninauacha
mpaka tutakapofika kwenye Kiti cha Hukumu cha Kristo, ambapo
utatathminiwa kwa ubora sana na kupewa thawabu nzuri na bora
kuliko niwezayo kuitoa mimi.
Herb Hodges - Mwandishi
vi
Shukrani
Haiwezekani hata kuzaliwa kama mwanadamu bila kudaiwa
sana. Kila mwanadamu anapozaliwa anakuwa na deni la pango la
miezi tisa huko alikokuwa anakaa!
Kati ya wote wenye madeni, mimi ni mmoja mwenye
kudaiwa sana, japo si kifedha. Watu wengi sana – walio hai na
walikwisha pumzika – wamechangia faida nyingi sana maishani
mwangu – hata siwezi kutaja yote. Ukweli ni kwamba siwezi hata
kulipia riba ya kile walichowekeza kwangu.
Kwa habari ya kijitabu hiki, ninawiwa sana na makundi ya
waandishi walioandika mawazo yao na kuhakikisha kwamba
nimeyapata. Ninawiwa na wahubiri, waalimu na wenzangu ambao
wametia kweli nyingi katika akili zangu, katika kipindi chote cha
Ukristo wangu. Ninawiwa na watu kama Dom Fosco, ambaye kwa
uvumilivu na uangalifu sana alihariri na kupanga upya kurasa hizi
mara kadhaa; na Clint Davis, aliyeandika sura inayohusu Utangulizi
wa Injili ya Luka (akitumia maandishi niliyotoa pamoja na kanda).
Zaidi, ninawiwa sana kwa mke wangu mpenzi Judy, anayehudumia
vile vile kama msaidizi wangu na mwandishi wangu, kwa sababu ya
kunipenda na kuniunga mkono kwa hali yake tulivu, na kwa
kuongezea hekima yake kubwa katika yangu ndogo niliyo nayo.vii
Ninawathamini na kuwaheshimu na kuwashukuru hao na
wengine wengi. Wamenibariki sana! Narudia kusema tena –
wamenipa deni kubwa sana. Rafiki zangu, asanteni mno.
Herb Hodges
viii
Sura Ya 1Maono Ni Muhimu Kiasi Gani?
“Mahali ambapo hakuna maono, watu huangamia.” Mithali 29:18
Katika lugha ya kiroho, “mtazamo wa KiMungu”, “hekima”,
“uwezo wa kuona”, “kuangaziwa” na “maono” ni maneno
yanayofanana kwa kiasi fulani. Maandiko mengi katika Neno la
Mungu hudhihirisha umuhimu wa maono kama hayo. Tunasoma hivi
katika Zaburi 119:18, “Unifumbue macho yangu niyatazame
maajabu yatokayo katika Sheria Yako”. Na katika Zaburi 119:130
tunasoma hivi, “Kufafanusha maneno yako kuwatia nuru, na
kumfahamisha mjinga.” Katika Yakobo 1:5 tunaambiwa hivi,
“Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa
Mungu”. Katika Waefeso 1:15-19 – pamoja na mantiki yake – Paulo
ameandika mojawapo ya sala zake kuu. Ninaamini kwamba hii ndiyo
sala muhimu zaidi ambayo mwanadamu anaweza kumwombea
mwenzake. Ni maombi ya “kuangaziwa”, kitu kimoja muhimu sana
kwa ajili ya kuelewa mambo ya Mungu baada ya Kuzaliwa Mara Ya
Pili. “Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuona”. Mambo mawili
ya lazima kwa ajili ya ufahamu wa kiroho ni kuzaliwa upya na
kuangaziwa.
1
Andiko kiongozi katika somo hili linatuonyesha kwa hali ya
kinyume jinsi ambavyo “maono” ni muhimu. Kuona kwa mtu
hutegemea “vioo” anavyotumia kuonea, kama ambavyo kusikia
kwake kunavyotegemea “chujio” analotumia kusikiliza. Tunapoanza
mafunzo haya kuhusu Agizo Kuu la Bwana Yesu kwa watu Wake, ni
muhimu sana tuelewe thamani ya maono. Tunaambiwa na Mithali
29:18 kwamba, “Mahali ambapo hakuna maono, watu huangamia.”
Huu ni mstari kamili: unafanya kazi kila mahali kwa ukamilifu
kabisa.
WAZO LA KIROHO
Kwanza kabisa, fikiri kuhusu wazo la kiroho litolewalo hapa
– wazo la “maono”. Likitazamwa katika mantiki yake, ni dhahiri
kwamba maono yanayotajwa hapa ni ya aina pekee, maalum. Hapa
kinachosemwa ni maono ya kiroho, ambayo ni maono ya maana sana
mtu anayoweza kuwa nayo.
Kila kitu huanza kwa maono. Utakuwa kama unavyoona.
Usichokiona huwezi kuwa. Utakuwa unachotazama, lakini
usichokitazama, huwezi kuwa. Yaani, kile unachotazama kwa
upendo sana, kwa kutamani, na kwa muda mrefu, ndivyo
utakavyokuwa. Utakuwa kama kitu unachokitazama.
Hili jambo ni dhahiri katika dunia ya teknolojia ya vitu vya
umeme siku hizi. Ukiacha picha fulani kwenye kioo cha kompyuta
kwa muda mrefu sana, kitajiingiza mpaka katika mfumo mzima wa 2
kompyuta na kuingia katika kila eneo na programu yoyote
itakayotumika baada ya hapo. Kanuni hiyo ni halisi hata kwako: Kile
unachotazama kwa muda mrefu sana kitaamua maisha yako.
Mkayun mmoja kutoka jimbo la Louisiana alikuwa anamwuza
punda wake. Mtu mmoja aliyetaka kumnunua akamwuliza hivi: “Je,
punda mwenyewe ana matatizo yoyote?” Yule Mkayun akajibu,
“Haonekani vizuri” (japo kwa lugha yake alimaanisha haoni vizuri).
Mnunuzi akasema, “Sijali sana kwa hilo. Je, anafanya kazi sana?”
Akajibiwa, “Naam, ana bidii sana katika kazi, ila, haonekani vizuri
tu” (kumbuka maana yake). Basi yule mtu akamnunua, na mwenye
kumwuza akampandisha kwenye gari la huyo bwana mpya. Alipofika
shambani kwake, alifungua nyuma ya gari lake na kumshusha yule
punda. Mara, punda akagonga mti, halafu akajigonga kwenye zizi.
Mkulima akapiga kelele kwa hasira, “Nimedanganywa! Huyu punda
ni kipofu!” Akampakia punda kwenye gari, akamrudisha kwa
mwenyewe na alipomfikisha, alipiga kelele na kusema, “Wewe
ulinidanganya kuhusu huyu punda. Punda mwenyewe kipofu.
Uliniambia uongo!” Yule mwuza punda akasema, “Hapana,
sikukudanganya. Nilikwambia vizuri kabisa kwamba, ‘punda
haonekani vizuri’!” (Bila shaka unakumbuka maana yake kwa
kikwao.)
Ndugu Oswald Chambers ambaye ni mwandishi maarufu wa
kitabu kiitwacho My Utmost For His Highest na vitabu vingine vizuri
sana vya kujisomea kwa ajili ya kukua kiroho, aliandika kwa 3
utambuzi mkubwa sana, kama ifuatavyo: “Ni rahisi zaidi kumtumikia
Mungu bila maono. Ni rahisi kumfanyia Mungu kazi bila ya mwito.
Kwa sababu, hapo husumbuliwi na yale Mungu anayotaka.
Unaongozwa na akili za kawaida, ila juu yake unatia hisia za
Kikristo. Lakini kama ukisikia agizo kamilifu la Yesu Kristo hata
mara moja tu, ufahamu wa kile Mungu anachotaka kitakuwa lengo
lako tangu wakati huo na kuendelea, nawe hutaweza kumtumikia kwa
msingi wa akili zako za kawaida.” Hebu soma maneno hayo mara
kadhaa kabla ya kuendelea mbele katika mafunzo haya. Nimetumia
wino mwepesi kutilia mkazo.
Kuona kimwili ni muunganiko wa vidokezo vyenye
kuonekana (yaani, kitu halisi katika dunia inayomzunguka mtu) na
ujuzi pekee (jinsi mtu anavyotambua hivyo vidokezo vinavyo-
onekana). Kidokezo chenye kuonekana kinaweza kisibadilike
kamwe, lakini kikiisha onekana na kunasa kwenye macho ya mtu,
kinaweza kupotoshwa, kukataliwa, au kupokelewa – yaani,
kinategemea tafsiri ya mtu aliyekiona
Katika zile hisia tano za asili, kuona ni hisia mojawapo
ambayo mtu hafai kupoteza. Ralph Sockman alikuwa sahihi
aliposema hivi, “Jicho ndiyo askofu wa hisia”. Claud Monet, mchora
picha maarufu wa Kifaransa alisema hivi, “Mimi ni mfungwa kamili
wa macho yangu”. Kwa sehemu kubwa, hiyo ni kweli kwa kila mtu.
Kuona (au kutambua) ndicho kiini cha kila kitu. Kanuni ifuatayo
itakuwa kweli: Kuona hupelekea kwenye Hatua (au Utaratibu), na 4
Hatua zitaongoza kwenye Matokeo. Ni dhahiri kwamba katika
kanisa la Yesu Kristo tuna matatizo sana kwa habari ya matokeo. Ni
kwamba hatutoi aina ya Wakristo waliosababisha Kitabu cha
Matendo! Basi, kama tunachotoa kina upungufu, ni kwamba kuona
kwetu kuna upungufu pia.
Maono ya kiroho ni kitu gani? Tafsiri moja ya Biblia kwa
lugha rahisi inafafanua Wakolosai 1:9 kwa njia itakayotusaidia.
Paulo aliandika hivi, “Ninaomba kwamba mwone mambo kwa
mtazamo wa Mungu.” Maono ya kiroho ni kuona mambo kwa
mtazamo wa Mungu. Lakini Biblia inatuambia wazi kwamba
mtazamo Wake hautakubaliana na wa kwetu (ktk Isaya 55:10). Basi,
ni muhimu kuwepo na urekebishwaji wa dhati kiroho ili tuweze
kufikisha mtazamo wetu kwenye hali ya kukubaliana na mtazamo wa
Mungu.
Ndugu Dawson Trotman, mtu mwenye maono makubwa
kiroho, alisema hivi, “Maono ni kupata moyoni mwako kile kilicho
moyoni mwa Mungu.” Lakini, Mungu ana nini moyoni Mwake?
Mstari wetu kiongozi unajibu swali hilo kwa neno moja tu: “watu”.
Moyoni mwa Mungu kuna watu. Watu wangapi? Watu wote.
Moyoni mwa Mungu yuko kila mtu aliyeko duniani. Naye
anatazamia watoto Wake kukubaliana Naye katika jambo hili
linalomgusa sana.
Anatazamia sana kwamba watoto Wake wataigusa dunia
nzima. Basi, utume wa dunia nzima unahitaji maono ya dunia nzima. 5
Hii inamaanisha kwamba Wakristo wengi wanahitaji kufikishwa
mahali ambapo wataanza kuona wajibu wao wa kuibeba dunia nzima
ili waweze kuanza kuigusa kwa ajili ya Kristo.
Hebu fikiri tena swali hili: Je, moyoni mwa Mungu kuna
nini? Je, kinachotakiwa kuwa kiini cha moyo wa kila aaminiye, na
katika ndoto zake na maono yake ni nini? Mstari wetu unatoa jibu:
watu. “Mahali ambapo hakuna maono, watu huangamia.” Basi, ni
kwa nini kiasi cha 4 kwa 5 ya watu wa duniani ndiyo wamepelekewa
Injili kwa udhaifu sana, na kufundishwa kwa udhaifu sana kuhusu
yaliyomo katika Injili na mkakati wake, huku nusu ya binadamu
hawajawahi kusikia jina la Yesu kwa kiwango cha kufikia
ukombozi? Je, Ukristo uliofunuliwa katika Kitabu cha Matendo
ungevumilia hali hii? Hapana kamwe! Basi, nini tofauti kati ya
Ukristo wa Kitabu cha Matendo na Ukristo wa siku za leo, ulioko
katika kanisa? Je, Yesu wa kanisa la leo ni tofauti na yule wa kanisa
la kwanza? Hapana. Je, Roho Mtakatifu ni tofauti. Hapana. Je, Biblia
ni tofauti? Ndiyo, lakini uzuri wa hili uko kwetu, si kwa Wakristo wa
kwanza. Wao hata hawakuwa na Agano Jipya lililokamilika. Sisi
tunalo, lakini pamoja na hilo, hatujafikia karibu na jinsi wao
walivyoweza kuigusa dunia yao.
Basi, nini tofauti kati ya Ukristo uliosababisha Kitabu cha
Matendo, na Ukristo wetu sisi? Pamoja na kwamba itaonekana kama
nimerahisisha sana, mawazo yangu ni kwamba tofauti ya msingi kati
ya “Ukristo wao” na “wetu” ni mkakati. Mkakati wao ulionyesha 6
kutokujali kwao kujenga taasisi na kukazia zaidi kuwajenga watu.
Mkakati wao ulikuwa wa kulipuka (kuelekea nje) badala ya
kubomokea ndani. Yesu alifundisha watu kumi na mbili, “ambao
aliwaita mitume” (ktk Luka 6:13). Kwa nini akawapa jina tofauti? Ni
kitu gani kikubwa, ni kitu gani anachokazia, na anataka tuone nini
wakati mtindo Wake mkuu (hata unaweza kusema, wa pekee) wa
kufundisha uliwalenga watu kumi na mbili, na kuacha neno la
kawaida la “mwanafunzi” na kuwapa jina tofauti na la kipekee sana
la “Mtume”? Nadhani siri iko katika maana ya neno lenyewe. Ni
neno la Kiyunani linalotokana na kuunganika kwa maneno mawili
madogo. “Stolos” maana yake ni “kutuma”. “Apo” maana yake ni
“mbali na.” Hapo ndipo penye siri. Aliwajenga hao watu maalum
waliochaguliwa ili “kuwa pamoja Naye” (ktk Marko 3:14) kwa muda
aliohitaji tu kuwafundisha na kuwaingizia uzima Wake, maono Yake,
na mkakati Wake. Baada ya hapo, mpango Wake ulikuwa kuwatuma
waende mbali na eneo lao la mafunzo kiasi ambacho wangeweza, au
ingewezekana, au wangetaka kwenda. Mwongozo Wake ulikuwa:
Kuingia ndani kwa muda, lakini Kutoka kikazi! Na ukweli kwamba
orodha ya Zawadi (Watu Wenye Karama) alizotoa kwa Kanisa Lake
inaanza kwa neno “mitume” (ktk Waefeso 4:11) unaonyesha
kwamba mtume alitolewa kwa kanisa ili kuwafanya washirika na
huduma ya kanisa kuelekea nje.
Imani yangu thabiti kabisa ni kwamba, Yesu Kristo
anamtazamia kila mtu aliyeokoka atawaliwe na maono ambayo 7
daima yanafanya macho yake na miguu yake kutoka nje – kwenda
hadi miisho ya dunia. Ni kweli alitupa sisi utume wa dunia nzima,
lakini lazima nirudie tena kwamba utume wa dunia nzima unahitaji
maono ya dunia nzima. Pia ninaamini kwamba maono na shughuli
yenyewe vinapaswa kuwa kitu binafsi, wala siyo kitu kinachofanywa
kitaasisi. Mkristo wa kanisa la siku hizi “asiyefanya kitu”,
asiyejihusisha katika kazi ya kugusa dunia nzima, hafikiriki na
hawezi kuvumiliwa katika mpango wa Mungu. Ninaamini kwamba
Yesu anamtazamia kila mtu aliyeokoka awe na maono na mkakati
(ambao ulionyeshwa na Yeye Mwenyewe) wa kuigusa dunia nzima
hadi miisho ya dunia na mpaka ukamilifu wa dahari!
Kumbuka kwamba Mungu anao watu wote katika moyo
Wake, Naye anatazamia sisi pia tuwe hivyo. Henrietta Mears,
mwalimu maarufu sana Mkristo, alisema hivi: “Ninapoitazama
huduma yangu, nafikiria dunia nzima. Kingine chochote
hakitamsahili Kristo wala mapenzi Yake kwa ajili ya maisha yangu.”
Mkristo asiyekuwa na maono kama hayo ni kama chombo cha
kusafiria katika anga za juu kilichopoteza ratiba yake ya safari.
Mwendo kasi wake utakifanya kufika mahali, lakini lengo lake
linaweza kufutwa kama kitakataa kufanya kazi kulingana na ratiba
yake. Sisi kama Wakristo ratiba yetu siku zote ni ile yenye kulenga
Kugusa Dunia Nzima, na mkakati wake maalum umetamka katika
Agizo Kuu la Bwana wetu. Kitu chochote kinyume cha hicho
kimetokana na mwanadamu, na hakimtoshelezi Mungu. 8
Ni kitu muhimu sana kutambua kwamba, Roho Mtakatifu
aliposhuka siku ile ya Pentekoste katika uwezo mkamilifu wa
ukombozi, tokeo la kwanza linalotajwa la kuja Kwake ni kwamba
“vijana wenu wataona maono na wazee wenu wataota ndoto” (ktk
Matendo 2:17). Mara nyingi hili limegeuzwa na kuonekana ni kitu
cha kipekee na cha siri sana kiasi kwamba kimetengwa kwa ajili ya
watu waonaji wasiokaa na watu. Sivyo. Ukweli ni kwamba hii
inapaswa kuwa kawaida ya maisha kwa Wakristo wa kiroho.
Kulingana na mantiki, hayo maono na ndoto si yale yanayotokea
wakati watu wamelala, bali ni yale yanayopatikana na kujulikana na
moyo uliojaa Roho Mtakatifu. Kwa mantiki hiyo, ndoto hizi na
maono ni ndoto za mkakati pamoja na maono yatakayopelekea
kwenye kufanya kikamilifu kabisa Agizo Kuu la Bwana wetu. Ndoto
na maono ya mikakati aina hiyo vinatakiwa kuwa vitu vya kawaida
na vya kila siku katika maisha ya Wakristo wa Agano Jipya wa
kawaida, wala si mambo ya kiajabu na kushangaza yanatokea kwa
watu fulani wachache wenye aina fulani ya maisha.
[USHUHUDA WA MWANDISHI – Nilikuwa nafundisha
kwenye mkutano wa viongozi wa kanisa miaka kadhaa iliyopita.
Nikapewa kisa hiki kifuatacho na ndugu asiyekuwa mchungaji.
Alianza kwa kunionyesha jengo lenye ghorofa kumi na nne, kisha
akasema kitu alichokuwa ameambiwa kuhusu wakuu wa shirika la
hapo.
9
“Lile jengo ni makao ya shirika tajiri sana. Wakati fulani
huko nyuma, viongozi kadhaa wa ngazi ya juu katika shirika hilo
walimwendea kiongozi mkuu wakamwuliza, ‘Hivi huyo makamu
wako wa kwanza ana nini juu yako kiasi kwamba inabidi aendelee
kuwepo? Mbona unamlipa mshahara mkubwa kiasi hicho wakati
hazalishi chochote?’ Yule mkuu alipowauliza maana yao,
walimpeleka hadi ofisini kwa msaidizi wake huyo na kumwambia
achungulie dirishani. Makamu wake alikuwa ameegama kwenye kiti
chake kinachozunguka, na hakikuwa kinatazama mezani. Alikuwa
ameweka mikono nyuma ya kichwa chake, na miguu ameiweka
kwenye dirisha. Hakuwa anajigusa – pengine alikuwa kalala au
alikuwa anachungulia nje. Wakamwambia, ‘Unaona tunachosema?
Hiyo tu ndiyo kazi yake, lakini analipwa mshahara mzuri sana. Kwa
nini?’ Yule mkuu wa shirika akajibu kwa upole sana, hivi:
‘Nisikilizeni kwa makini sana. Mwaka jana, huyo jamaa aliyeketi
kwenye hicho kiti katika hiyo ofisi alipata wazo lililoletea shirika hili
zaidi ya Dola milioni 85 za Marekani… Mwaka huu, ana kazi moja
tu ….’!” MWISHO WA USHUHUDA]
Wapendwa waamini wenzangu, yuko wapi mtu katika kanisa
la leo anayefikiri kuhusu wazo la Mungu la Dola milioni 85? Yuko
wapi mtu anayeona maono ya Mungu ya Dola milioni 85, au
mwenye kuota ndoto ya mkakati wa Mungu wa Dola milioni 85?
Mungu Muumbaji wa Biblia hakosi mawazo makubwa ya kiumbaji,
lakini, wako wapi watakatifu Wake wa kawaida kabisa ambao 10
wanaona mkakati kwa mtazamo Wake, na kupata moyoni mwao yale
ambayo Mungu anayo moyoni Mwake kimkakati?
Hebu nitaje kanuni nyingine inayohusu maono.
Hakuna maono = kushindwa kabisa;
Maono yenye mpaka = mafanikio kidogo;
Maono – mpango – matendo = ni ndoto tu;
Maono + mpango – matendo = ndoto yenye kutisha (kusikia hatia);
ila
Maono + mpango + matendo = huduma ya kiroho yenye matokeo.
Ona kwamba kipimo cha maono ya mtu ni matendo
yanayosababishwa na maono hayo. Pasipo matendo, wewe na vipawa
ulivyo navyo mnabakia kwenye kiwango cha “kuwa na uwezo wa
kufanya kitu”. Hali hiyo ni uwezo uliolala ambao haufanyiwi kazi
kamwe kupitia maono.
Myles Munroe ambaye ni kiongozi Mkristo alisema hivi
kuhusu uwezo wa mwamini kufanya kitu katika kitabu chake
kiitwacho Understanding Your Potential: “Mahali penye utajiri sana
hapa duniani si katika maeneo ya mafuta huko Kuwaiti, Iraki au
Saudi Arabia. Wala si katika machimbo ya dhahabu na almasi huko
Afrika Kusini, au machimbo ya uranium huko Urusi au katika
machimbo ya shaba yaliyoko Bara Afrika. Utashangaa tu lakini,
utajiri mkubwa sana katika dunia yetu uko mita chache tu kutoka
nyumbani kwako. Uko katika makaburi yenu. Huko chini,
kumezikwa ndoto ambazo hazikuwahi kutimizwa, nyimbo ambazo 11
hazikuwahi kuimbwa, vitabu ambavyo havikuandikwa, picha ambazo
hazikuchorwa, mawazo ambayo hayakutolewa, maono ambayo
hayakufanyika uhalisi, vitu vilivyobuniwa ambavyo
havikutengenezwa, mipango ambayo haikutoka kwenye mawazo ya
mtu na makusudi ambayo hayakutimizwa. Makaburi yetu yamejaa
uwezo wa kufanya vitu ambao haukufanikiwa.
“Uwezo wa kufanya vitu unadai kwamba usikubali kutosheka
na kitu ulichofanikisha. Adui mmoja ambaye ni mkubwa sana wa
uwezo wako kufanya vitu ni mafanikio. Mafanikio kidogo huharibu
uwezekano mkubwa! Ili uweze kufikia uwezo wako kamili wa
kufanya vitu, hutakiwi kutosheka na ulichofanikisha. Pia ni muhimu
kwamba usiruhusu kile usichoweza kufanya kiingiliane na kile
unachoweza kufanya. Janga kuu maishani si kifo, bali ni maisha
ambayo hayakufikia kilele chake katika uwezo wa kufanya vitu.
“Katika kurahisisha dhana hii, hebu tutazame kitu kimoja
katika uumbaji ambacho kina nguvu sana … mbegu. Nikishika
mbegu mkononi na kuukuliza, ‘Nina nini mkononi?’ utasemaje?
Pengine utajibu kilicho wazi kabisa … ni mbegu. Lakini, ukielewa
asili ya mbegu, jibu lako linaweza kuwa uhalisi japo halitakuwa
ukweli. Ukweli ni kwamba nimeshika msitu mkononi mwangu. Ni
hivi: Katika kila mbegu kuna mti, na katika kila mti kuna matunda au
maua yenye mbegu ndani yake. Na hizo mbegu nazo zina miti
ambayo ina matunda yenye mbegu ndani yake … ambazo zina miti
yenye matunda yenye mbegu, na kadhalika na kuendelea. 12
Unachokiona hapa si yote. Kwa hiyo, tofauti kati ya mbegu moja na
utoaji wa chakula kama vile ngano inayoweza kulisha dunia nzima ni
kitu kinachoitwa ‘uwezo wa kufanya vitu.’ Hicho ndicho kiwango
cha tofauti kati ya unachoona na kinachowezekana.
“Kama Musa angekufa kabla hajaona kile kichaka
kilichokuwa kinawaka moto … au Paulo kabla ya kukutana na Yesu
akiwa njiani kwenda Dameski … au Ibrahimu kabla ya Isaka
kuzaliwa. Maandiko na historia vingekuwa tofauti sana. Kama
Martin Luther angekufa bila ya kuandika yale matangazo yake … au
Charles Wesley bila ya kutunga nyimbo zake … au John Wycliff bila
kufasiri Biblia katika lugha ya Kiingereza. Historia ya Kanisa
ingekuwa tofauti sana.
“Sijui ingekuwaje kama baba yako angekufa kabla
hujatungwa mimba, au mama yako kabla hujazaliwa. Dunia
ingepoteza nini kama usingezaliwa? Je, dunia itakosa nini kwa
sababu unashindwa kuishi kufikia kiwango cha uwezo wako wote?
Je, utakwenda kaburini na nyimbo, vitabu, magunduzi au dawa?”
Mimi nimetumia wino mwepesi hapa kuweka msisitizo maneno ya
mwandishi.
Je, inawezekana kwamba dhambi kuu ya Wakristo imo katika
uwezo wao wa kufanya mambo ambao haujafikiwa? Tena, uwezo
mkuu wa kufanya mambo ambao haujatumiwa katika siku za leo ni
katika eneo la kutimizwa Agizo Kuu la Bwana wetu. Yeye amekupa
wewe nafasi maalum katika Kuufikia Ulimwengu Kikamilifu, na ni 13
nafasi kubwa kuliko yoyote uliyowahi kuwa nayo. Hii nafasi
haiwezekani bila ya maono kwamba inawezekana. Basi, kitu
muhimu kuliko vyote katika maisha yako ni kuwa na maono
yanayokubaliana na Mungu, na kuyafuatilia. Kwa kuwa kazi
uliyopewa inahusu dunia nzima, maono yako lazima yawe hivyo
hivyo. Je, una maono ya aina hiyo?
Sasa – watu kama wewe na mimi – wenye ubinafsi, kujijali,
wenye kujali kwao na wenye kujiona wanapataje maono ya Mungu?
Angalia kanuni hii, inayoweza kufanya kazi: habari sahihi
ukijumlisha na kuangaziwa kiroho vitaleta maono, ambayo
yatasababisha motisha, na hiyo motisha itapelekea utendaji wa
kiroho wenye matokeo. Hapo, ona kwamba maono huanza kwa
kupata habari sahihi. Sawa na ambavyo kuona kimwili kunavyoanza
kwa kuwepo kwa kivutio cha nje, ndivyo na maono kiroho
yanavyoanza kwa ukweli wa Mungu katika Maandiko na kila kitu
ambacho kinahusiana na Maandiko. “Matofali” ya kujengea maono
hayo ni: kufahamu Maandiko kiasi cha kutosha na moyo sikivu wa
kusikia Maandiko na kuyatii, halafu ufahamu wa jiografia ya dunia
na tamaduni za nchi mbalimbali, utambuzi kiroho wa matukio,
maombi, kujisomea ili kupata habari, ujuzi binafsi (“njoo uone”
katika Maandiko) wa baadhi ya maeneo ya kimisheni duniani,
ushirikiano na waamini wenye maono, kujitoa kwa ajili ya kutoa
kuhusu mambo ya umisheni, kukutana na wamishenari na Wakristo
wenye kugusa dunia, na maamuzi mbalimbali katika maisha. 14
Unaweza kuanza kushirikiana na Mungu katika kujenga maono ya
kiroho katika maisha yako leo. Lakini, ni dhahiri – na inasikitisha
sana – kwamba Wakristo wengi unaoshirikiana nao mara kwa mara
hawana maono kama hayo.
HALI YA KUSIKITISHA
Pili – fikiri kuhusu hali ya kusikitisha ambayo inatajwa hapa,
kwamba, “Mahali pasipo na maono.” Neno “mahali” linaweza pia
kutamkwa hivi: “popote”. Basi, haya ni maneno yanayohusu kila
mahali. Kwa lugha ya KiBiblia, nini maana ya “pasipo maono”?
Maana yake ni kwamba Mungu hatambuliwi, wala mpango Wake
mkamilifu. Maana yake ni kwamba Shetani, “mungu wa dunia hii”
ame”pofusha mawazo ya watu” wasione mambo ambayo ni ya
muhimu na yenye maana! Hawawezi kuona wala kuyaelewa mambo
haya bila ya kuzaliwa upya pamoja na kuangaziwa (ona 1Wakor.
2:9-14). Basi, hakuna mawasiliano ya kudumu baina ya mbingu na
mioyo ya watu. Hakuna biashara na kile kisichoonekana, cha milele,
cha kiroho, na ambacho ni halisi. Hakuna kumsikiliza Mungu na
kumtazama Yeye. Kwa kifupi ni kwamba, “pasipo maono” maana
yake ni kwamba watu hawamwoni “Aliye Juu na Mtakatifu, mwenye
kutamalaki Milele.” Basi, tunakuwa na mipaka na kuona maeneo
yetu madogo pamoja na upeo wetu, na mipango yetu midogo, ya
kibinafsi, ya kidhambi tu. Mtu mwenye mipaka kiasi hicho, na
mwenye mipango yenye mipaka kiasi hicho hatimaye anabomokea 15
ndani yake mwenyewe. Ni hivi: Kila kitu huanza kwa maono ya
kweli. Ona lile neno “kweli”. Ninalitumia kama kinyume cha
kutokuwa na maono, maono bandia na maono yenye mipaka.
Lazima tukubali – kwa huzuni sana – kwamba, watu wengi
walio-okoka wana ubinafsi, wanajipenda wenyewe na wametawaliwa
na hali ya kujilinda kwa kiwango sawa na watu waliopotea tu. Yaani,
wengi katika watu walio-okoka ni wenye dhambi (tafsiri “dhambi”
kuwa ni ubinafsi) kama waliopotea tu. Kwa nini? Hapo tena, andiko
letu la msingi linatoa jibu: Hakuna maono. Si mara nyingi tunaona
mambo “kwa mtazamo wa Mungu”. Si mara nyingi mioyo yetu
inakuwa na kile ambacho Mungu anacho moyoni Mwake – dunia
nzima ya watu mmoja mmoja waliopotea.
Mtazamo ni muhimu sana. Kuona kwa mtu hutegemeana na
aina ya vioo anavyotazamia, sawa na jinsi kusikia kwa mtu
kunavyotegemeana na chujio analotumia kusikilizia. Hebu tutoe
mfano wa kusaidia kueleweka kweli hiyo.
Mwaka wa 1877, mtaalamu wa nyota Mmarekani aliyeitwa
Percival Lowell aliushangaza ulimwengu wa sayansi kwa kutoa wazo
kwamba, kutokana na ushahidi aliokuwa amekusanya, kulikuwepo na
dalili za uhai na viumbe wenye akili katika sayari ya Mars. Nadharia
yake – kwa sehemu – ilitokana na yeye kuona vitu alivyoita
“mifereji” kwenye sayari hiyo. Wanasayansi wakabebwa na tamko
hilo kwa kishindo. Lakini, walikuwepo watu wachache ambao tangu
mwanzo walikuwa wamefahamu kwamba hiyo sayari haina mifereji. 16
Baadaye, Bwana Lowell alipata tatizo kubwa kiafya, lililoanza
kujitokeza. Jopo la matabibu walimpima na kugundua tatizo lenyewe.
Ugonjwa wake haukuwa umejulikana sana siku zile, basi wakauita
jina lake – “Lowell’s Syndrome”. Ishara mojawapo ilikuwa kwamba,
alipoketi muda mrefu akichunguza kitu fulani, sura na ukubwa wa
mishipa ya kupitisha damu katika macho yake ilikuwa inaonekana
kwenye hicho kitu alichokuwa anakichunguza. Basi, badala ya kuona
“mifereji” kwenye sayari ya Mars kwa njia ya darubini, alichokuwa
anakiona ni mishipa yake mwenyewe ya damu. “Alibeba” kile
alichodhani anakiona, katika kichwa chake mwenyewe. Mtazamo!
Ufuatao ni mfano mwingine tena.
Dakta Harold Lindsell, mhariri mstaafu wa jarida liitwalo
Christianity Today, alihudhuria kliniki ya macho ya Kijapani zamani
kidogo. Akiwa darasani siku moja, mkufunzi aliinua chati kwa
ghafula mbele ya darasa. Akauliza hivi: “Ni wangapi mnao-ona
namba nane?” Lindsell peke yake ndiye aliinua mkono wakati huo.
Alisema baadaye kwamba alidhani ni njama – kwamba darasa lote
lilikuwa limekusudia kumcheza shere. Lakini, mkufunzi akauliza, “Ni
wangapi mnaoweza kuona namba kumi na nne?” Kila mtu darasani
aliinua mkono! Ndipo mwalimu akazungumza na Ndugu Lindsell na
kumwambia, “Mheshimiwa! Kuna mtu ambaye amewahi kukwambia
kwamba wewe una matatizo ya kuona rangi?” Ni kwamba hapakuwa
na hila yoyote. Kila mtu siku hiyo katika lile darasa alikuwa
anasema ukweli – kulingana na alivyouona. Mtu mmoja kweli aliona 17
mamba nane huku wengine wote wakiona namba kumi na nne.
Mtazamo huo!
Ni hivi: Mtazamo hufunika kila kitu ambacho hakihusiki, na
kusababisha maono yatawaliwe na kile ambacho kinahusika. Kwa
hiyo ni muhimu sana.
Mwanamke mmoja alisogea karibu na Dakta G. Campbell
Morgan, mwalimu maarufu wa Biblia wa zamani. Akamwuliza huvi:
“Hivi Dakta Morgan, unaamini kweli kwamba Mungu anajali
mambo madogo madogo ya maishani mwetu?” Dakta Morgan
akamjibu kwa upole sana, hivi: “Mama. Hivi kweli unaamini
kwamba katika maisha yako kuna kitu kikubwa sana kwa Mungu?”
Mtazamo huo.
Hayo ndiyo yanayofanywa na mtazamo. Yanaondolea mbali
habari fulani au mambo fulani kuwa si ya maana, na kukuza mengine
kuwa muhimu mpaka kufikia kiwango cha “kweli”. Lakini, mtazamo
unaweza kutokana na mtazamaji mwenyewe kiasi cha kutokuwa
halisi katika hali ya kawaida kabisa. Yaani, hata unaweza usitoe
nafasi ya kitu halisi kabisa kilichopo kuonekana. Acha nikupe mfano
wa KiBiblia kuhusu mtazamo.
Sura ya kumi na tatu ya kitabu cha Hesabu ni taarifa ya
hadithi ya taifa la Israeli wakiwa Kadeshi Barnea, kusini kidogo tu
ya nchi ambayo Mungu alikuwa amewaahidi. Bila shaka walikuwa
tayari kuingia katika Nchi yenyewe. Lakini, walipatwa na hali ya
kutokuamini, wakatuma kikundi cha wapelelezi kumi na mbili 18
kwenda kutazama udhaifu wa nchi ile. Wapelelezi wake wakarudi na
taarifa iliyogawanyika. Wote walikubaliana kwamba nchi ilikuwa
inakaliwa na watu ambao hawakuwa na wazo la kuiachia. Halafu,
wapelelezi kumi – idadi kubwa kabisa – wakapendekeza kwamba
wasiiteke nchi kwa msingi kwamba wakazi waliokuwemo nchini
“wana nguvu kuliko sisi,” na kwamba wana wa Israeli walionekana
kama mapanzi, wakilinganishwa na majitu. Wapelelezi wawili
walitosha ushauri “wa wachache”. Wakikiri ukweli ule ule, wao
waliendelea na kusema hivi: “Hebu na tupande mara moja na
kuitwaa nchi, kwa sababu tuna uwezo kabisa wa kuiteka” (ktk
Hesabu 13:30). Ni hivi: Wale wachache walimwingiza Mungu katika
uamuzi wao, kitu ambacho wale wengi hawakukifanya. Basi,
mitazamo miwili ikaamua mashauri yale mawili yaliyotolewa:
mtazamo mmoja ulimhusisha Mungu, ule wa pili haukufanya hivyo.
Wote waliona “majitu”; wengi wao walijiona kuwa “mapanzi”.
Wawili tu ndiyo walimwona Mungu. Au basi: wengi walimwona
Mungu kupitia hao majitu, na hao wakaonekana kuwa wakubwa
kuliko Mungu. Wale wachache waliwaona majitu kupitia Mungu,
na Mungu akawa mkubwa kuliko majibu. Basi, mtazamo wao
uliamua mapendekezo yao na utendaji wao. Hapo ndipo penye
tofauti kati ya “maono” na “pasipo maono”!
Akili ya kibinadamu siku zote itakupa mtazamo wako
kulingana na maoni yako. Muujiza tu wa kuangaziwa ndiyo
utakaokupa mtazamo wa Mungu. Hapo ndipo kuna tofauti kati ya 19
“pasipo maono” ambayo hatima yake ni “watu huangamia”, na
“maono” ambayo kwa hiyo watu hustawi na kufanikiwa.
Jaribu kufikiri kutokuwepo na maono ya kiroho katika
madhabahu ya kanisani unapoabudu. Huna haja ya kufikiri sana
kama utatembelea makanisa mengi! 1Samweli 3:1 inasema, “Neno la
Mungu lilikuwa adimu katika siku hizo. Hayakuwepo maono ya wazi
(au, ya mara kwa mara).” Ukisoma historia ya taifa iliyotokana na
wakati huo utagundua kwamba mambo ya kusikitisha sana yalitokea
kwa sababu ya kutokuwepo na maono.
Ingekuwaje kama isingekuwepo Injili inayohubiriwa kutoka
madhabahu ya kanisa unalohudhuria? Kutokuwepo kwa kutambua
kwamba mtu amepotea pasipo Kristo? Kutokuwepo na kuamini
nguvu zenye kubadili maisha za Roho Mtakatifu? Kutokuwepo kwa
mafafanuzi ya ndani sana na wa milele wa mausia ya Mungu?
Kutokuwepo kwa mafunuo ya hazina nyingi sana zisizomalizika
zilizomo katika Neno la Mungu? Kutokuwawezesha wasikilizaji
“waishi mbinguni na duniani kwa wakati mmoja”? Kutofundishwa
kwa upana wa maisha ya Kikristo yaliyojaa Roho, yanayofuata
Neno, yaliyo na mwelekeo wa maombi, na yenye kujenga
wanafunzi? Jaribu kufikiri madhabahu “pasipo maono”.
Mchungaji: Una mashaka kiasi gani kuhusu uwezo wa kile
unachofanya sasa? Mashaka mazuri ndiyo nyundo yenye kuvunja
madirisha yaliyofunikwa na kiwingu cha mambo yanayowavutia
wanadamu. Mashaka aina hiyo ni ishara yenye kuleta matumaini. 20
Bila ya ukiri wa kweli kuhusu mashaka kama hayo, na uchunguzi
kwa njia ya maombi kuhusu njia mbadala itolewayo na Mungu,
madhabahu unayosimama ndani yake itadumu kutokuwa na maono.
Miaka kadhaa iliyopita, mchungaji maarufu wa Kibaptisti
alikuwa kwenye maombi ofisini mwake asubuhi moja. Alikuwa
amelala kifudifudi akimwomba Mungu upako wa nguvu za Roho
Mtakatifu juu ya huduma yake. Alimsihi Mungu tena na tena, “Ee
Bwana! Nipe nguvu Zako. Usiache nihubiri na kufanya huduma
pasipo nguvu Zako.” Kila mhubiri wa maana amewahi kuomba sala
hii kwa uzito sana na mzigo. Anasema, mara ikaonekana kama paa
juu yake limefunguka na mkono ukamshukia na kumgusa kwenye
bega. Ikawa ni kama sauti ya Mungu imezungumza ndani yake, hivi:
“Mwanangu, acha kuomba!” Alipotulia, Sauti ni kama ilimwambia
hivi, “Mwanangu! Kwa mipango yako isivyokuwa mikubwa, huhitaji
nguvu Zangu!”
Ewe Mkristo – maono yako ni makubwa kama ya Mungu,
kwa ajili ya utukufu Wake? Iko wapi mipango, ndoto, maono,
mikakati kwa ajili ya kuifikia dunia nzima – vitu ambavyo kwa kweli
vinasukuma rasilmali ya miujiza ya Mungu? Uko wapi mkakati
unaotaka miujiza endelevu ili kuudumisha? Yako wapi maono
ambayo ni makubwa kiasi kwamba rasilmali za kibinadamu (za aina
yoyote na kiwango chochote) hazina uwezo wa kuyategemeza?
Maono pekee yenye ukubwa wa umilele ambayo yeyote kati yetu
anaweza kuyahitaji yanapatikana katika lile Agizo Kuu ambalo 21
tumepewa na Bwana Yesu Kristo. Kama madhabahu yako
haisumbuliwi na maneno “kuwafanya kuwa wanafunzi” na “mataifa
yote”, Mungu anawezaje kutazamiwa kuunga mkono kutoka
mbinguni? Bila kutatizwa na hilo, madhabahu ya kanisa lako ina
ubao unaosema hivi: “hakuna maono”.
Halafu, ni hatua ndogo tu kufikia kwenye viti, watu ambao
hawana maono ya kiroho ya hayo. Sheria ya maisha ya ndani ya
kanisa ni hii: “watu wako kama mchungaji alivyo”. Watu watapokea
jinsi mchungaji wao alivyo kiroho. Hebu tuseme katika mfuatano
huu, watu waketio kanisani hawana, au wamepoteza maono yao
kuhusu utukufu wa kushangaza sana wa Injili. Inakuwaje? Na
wamepoteza uzuri wa pekee wa Yesu Kristo. Inakuwaje? Na
wamepoteza maono ya ukuu na utukufu wa kazi yetu ya dunia nzima.
Inakuwaje? Na wamepoteza maono ya uwezekano wa kuigusa dunia
nzima kwa ujumbe wa Injili na uwezo wa Yesu Kristo kama
Wakristo wa kwanza walivyofanya. Inakuwaje? Mtu mmoja
amesema, na ni kweli kabisa, “Hatua kutoka aliye tayari kujitoa hadi
mtunzaji na hatimaye mzikaji ni fupi sana.”
Kwa nini washirika wa makanisa wanasisimka zaidi kuhusu
vitu vingine elfu na zaidi, kuliko kuhusu Mungu, mambo ya kiroho,
mbinguni, jehanamu, na umilele? Jibu lake: Hakuna maono, kwa
hiyo hakuna motisha. Maana, motisha hutokana na maono.
Kujifunza Injili na Kitabu cha Matendo kwa makini sana
kutadhihirisha kwamba Kanisa la kawaida la Kikristo linaendeshwa 22
kwa misingi ya desturi na taratibu kuliko kwa misingi ya kuangaziwa
[na Roho Mtakatifu]. Mtu mmoja – kwa mzaha tu – alisema hivi: “Ni
vizuri makanisa yafanye na kusema kila kitu kwa usahihi mara ya
kwanza, kwa sababu yatafanya na kusema kwa njia hiyo hiyo tangu
sasa na kuendelea.”
Maono yanapotoweka katika madhabahu na kwa washirika,
tuwe na uhakika kabisa kwamba hayatakuwepo maono ya kiroho
katika maisha ya kila siku. Itakuwaje ikiwa Wakristo watapoteza
kabisa maono ya nafasi yao kama chumvi na nuru (ktk Mathayo
5:14-16) katika dunia inayoharibika na yenye giza? Itakuwaje kama
sisi tutapoteza maono juu yetu kwamba ni wawakilishi wa Yesu
Kristo (ktk 2Wakor. 5:20), “katikati ya kizazi kiovu kilichopotoka,
ambacho kati yake tunang’aa kama taa duniani, tukilishika na
kulitangaza Neno la Uzima” (ktk Wafilipi 2:14-16)? Itakuwaje ikiwa
tutapoteza maono yetu juu ya daraja yetu kuu kama “mabalozi kwa
ajili ya Kristo”, tulioagizwa kusemea jambo la Mfalme wetu katika
dunia hii yenye giza na uhasama? Mbona si kitu cha kufikiri na
kukisia kabisa. Kutokuwepo na maono ni kitu kinacho-onekana
waziwazi katika madhabahu, kwa washirika, na katika maisha ya kila
siku – ukitazama tu mambo yanayotokea, kama yanavyotajwa katika
maandiko haya.
23
MATOKEO YAKE, MAZITO
Hebu fikiri juu ya matokeo mazito yanayofuata hali ile ya
kusikitisha sana ya “pasipo maono”. Mahali ambapo hakuna maono,
watu huangamia.” Neno linalotafsiriwa “kuangamia” ni la Kiebrania,
lenye kushangaza sana. Yaani – limejaa maneno, na linatisha. Lina
maana kadhaa tofauti. Maana yake ni “kutokuwa na kujizuia,
kujiachilia, kuyeyuka, kuvunjika, kusambaratika vipande-vipande,
kutembea uchi, kuangamia.” Sasa, tazama matokeo ya kusikitisha
sana ya kupotea kwa maono miongoni mwa Wakristo.
Kwanza – maono yanapokuwa hayapo, watu wa jamii, wa
jumuiya, wa kanisa, wa nyumbani “huacha kujizuia”. Hayo ni
matokeo ya kiadili ya maono kupotea. Kupoteza maono husababisha
vurugu kiadili, ambapo “kila mtu hufanya kilicho sawa machoni pake
mwenyewe”. Ona kwamba, kunapokuwa hakuna utambuzi wa uhalisi
kamili, watu hufanya “yaliyo sawa machoni pao wenyewe”, wala si
kile ambacho kinaonekana kuwa makosa kwao. Kumbuka pia
kwamba “sawa” na “kosa” siku zote ni maneno tu kwa wale wenye
akili za kawaida au za kimwili. “Sawa” na “kosa” ni vitu halisi kwa
wale tu ambao wana akili timamu kiroho. “Iko njia ionekanayo kuwa
sawa kwa mtu, lakini mwisho wake ni mauti” (ktk Mithali 14:12).
Ona kwamba huyo mtu ana uhakika kwamba njia yake ni sawa –
kamwe haoti kwamba njia yake ni ya KiShetani na yenye uharibifu.
Hapo tena, tofauti ni katika ufunuo, katika maono na mtazamo wa
mtu binafsi. Inashangaza sana kuona jinsi ambavyo watu walio 24
vipofu kwa mambo ya kiroho wanavyohalalisha ukweli wa kuelewa
kwao!
Kwamba watu kila mahali siku hizi wameacha kujizuia ni
kitu kinachokubaliwa na kila mmoja. Kujitawala, fujo na vurugu na
kujiamulia mambo mwenyewe ni mambo yanayozidi kuenea. Tofauti
kati ya Mwana wa Mungu na wenye dhambi inadhihirishwa hapo.
Yesu alisema hivi: “Siku zote mimi hufanya mambo ambayo
yanampendeza Baba Yangu” (ktk Yohana 8:29). Lakini, kauli mbiu
ya wenye dhambi (au kiini cha dhambi) ni: “Siku zote mimi hufanya
mambo yanayonipendeza”. Pengine atatokea msanii wa siku zijazo
atakayetengeneza sanamu au kuchora picha itakayomwonyesha mtu
wa karne ya ishirini akiwa amejikumbatia mwenyewe kwa upendo
sana, akijipiga busu mwenyewe katika kioo. Lakini, bila ya kupoteza
uzito wa hali halisi katika maneno ya utani, hebu maneno ya Shetani
aliyopewa na John Milton katika kitabu kinachoitwa Paradise Lost
yaturekebishe. Shetani alionyesha ukiri usioepukika wa wenye
dhambi wenye kufuata ubinafsi wao bila ya mipaka aliposema hivi:
“Mimi mwenyewe ndiye jehanamu”.
Miaka kadhaa iliyopita, magazeti yaliandika kisa cha
msaidizi wa fundi uchundo wa Uwanja wa Ndege wa Idlewild huko
New York, Marekani. Huyu alikuwa na miaka ishirini, naye
alimwandikia rafiki yake mmoja barua, aliyekuwa katika Jeshi la
Anga la Marekani katika jimbo la Texas. Barua ilieleza jinsi
ambavyo kijana huyo alikuwa ameachana na mchumba wake, na 25
jinsi alivyopanga kuchukua ndege mojawapo ya shirika la Pan
American. Akaiba ndege aina ya DC-3 yenye injini mbili, akaanza
kuiendesha. Ikashindwa kupaa, ikaanguka, naye akafa. Habari
gazetini zilimalizika kwa maneno yake kutoka kwenye ile barua,
kwamba, “Nitakuwa nikiendesha mimi mwenyewe, kama ambavyo
nimekuwa siku zote – peke yangu.” Kisa hiki hurudiwa tena na tena,
katika mavazi tofauti, kila siku – na matokeo ni yale yale.
Kujisimamia mwenyewe ni kujiharibu mwenyewe. Mtu
anayejisimamia mwenyewe siku zote ataanguka na kuungua! Kwa
kuwa mawazo ya wanadamu hupingana sana wakati kila mmoja
anapochukuwa sheria yake mwenyewe, machafuko duniani
yanaendelea kukua na kuongezeka, na hali ya wasiwasi itokanayo
nayo. Mahali ambapo hakuna maono ya mara kwa mara miongoni
mwa watu, ambapo hakuna neno lililo wazi kutoka kwa Mungu aliye
hai, ambapo hakuna Ukristo halisi wenye maana, basi watu hutupilia
mbali vizuizi.
Pili – neno hili lenye nguvu sana la Kiebrania pia
linamaanisha “kusambaratika”. “Mahali ambapo hakuna maono,
watu husambaratika”. Hayo ni matokeo ya kijamii ya kupoteza
maono. Dhambi, inayozidi kuongezeka katika jamii yenye utovu wa
maono ya kiroho, ina nguvu ya mvutano fulani. Inawafukuza watu
watoke kwenye Kiini cha Kweli cha Uzima ambacho ni Mungu
Mwenyewe, na kwa njia hiyo kuwatenganisha wao kwa wao. Basi,
tunakuwa na dunia iliyotengana, iliyogawanyikana. Jamii huanza 26
“kulegea, kuyeyuka, kuvunjika, kuwa vipande-vipande”. Neno
“kugawanyika” linaelezea hali nyingi tofauti zilizomo katika dunia
yetu. Tunazo familia zilizogawanyika, mataifa yaliyogawanyika,
dunia iliyogawanyika, na watu wenye haiba zilizogawanyika. Siku
moja, daktari wa magonjwa ya akili aliingia kwenye kituo cha
mafuta akiwa na gari aina ya pikap. Nyuma alikuwa amebeba viti
vitatu. Alipoulizwa anakwenda wapi, alijibu, “Ninakwenda
kumtembelea mwenda wazimu (ambaye tatizo lake ni kuona kwamba
yeye si mmoja, bali wengi)!” Mara nyingi sana watu binafsi
wana”sambaratika”. Binti mmoja msomi wa chuo kikuu fulani
alimwambia mwenzake wanayekaa chumba kimoja, “Ninajisikia
kama Vita ya Wenyewe kwa Wenyewe, inayotembea”. Mwenzake
akamjibu, “Wala hiyo si kitu. Mimi ni Vita Kuu ya Dunia,
inayotembea!” Mtu binafsi anaweza kuvumilia tatizo la aina yoyote
ile kama ameunganika ndani, lakini atashindwa na shambulio la aina
yoyote ile kama ndani yake mwenyewe kuna ubishi na hali ya
kutoelewana.
Habari za Yuda katika Agano Jipya zinamalizika kwa maneno
haya: “Basi, mtu huyu alinunua konde kwa ijara ya udhalimu;
akaanguka kwa kasi akapasuka, matumbo yake yote yakatoka”
(Matendo 1:18). Kama mjuavyo, Yuda alijinyonga, na huku
kuharibikiwa kimwili pengine kulitokana na kutokufanikiwa katika
kujaribu kujinyonga, au kama matokeo ya kuvimba na kuharibika
kulikotokana na maiti yake kuning’inia kwenye kamba yake kwa 27
muda mrefu. Tafsiri ya Biblia Fafanuzi inasema hivi, “Alipasuka
katikati ya mwili wake”. Pamoja na kwamba maelezo hayo
hayavutii, tunapata picha nzuri. Tafsiri nyingine inasema kwamba
Yuda “alisambaratika”. Yaani, “aliachana”. Lakini hii ilikuwa ni
tokeo la mwisho la kimwili la yale ambayo yalikuwa yametokea kwa
miaka mitatu huko nyuma. Alikuwa ameharibu kile kiini pekee –
“saruji” ya KiMungu ambayo ingeunganisha na kushikamanisha
haiba yake na kuifanya kamilifu na yenye umoja.
Kweli,“alisambaratika katikati”. Na Yuda angefaa kabisa kuwa
“mtakatifu mwangalizi” wa majira ya siku hizi. Biblia inatuambia
(ktk Wakolosai 1:17) kwamba “vitu vyote hushikamana pamoja”
katika Yesu Kristo tu. Lakini, watu wanapopoteza “Maono ya
Kuvutia Sana ya Yesu Kristo,” basi jamii inakosa nguvu za
kuunganisha, za kufanya vitu kuwa umoja, za kushikamanisha vitu
vyote.
Katika mchezo uitwao Green Pastures uliotungwa na Marc
Conally, malaika Gabrieli anaonekana akipita hapa na pale katika
kumbi na maeneo mbalimbali ya mbinguni, huku akizidi kusumbuka
kutokana na vurugu na fujo anazo-ona hapa duniani. Mwishowe
anamgeukia Mungu na kusema, “Bwana! Bwana! Inaonekana
kwamba kila kitu kilichopigiliwa ili kushikamana kinaanza
kuachana!”Watu binafsi na taasisi husambaratika wakati Kristo
anapokosa kutawala. Hayo ni matokeo ya kijamii ya upotevu wa
maono ya kiroho.28
Tatu – hili neno katika Kiebrania lina maana nyingine ya
“kutokuvaa” au “kutembea uchi”. Sasa – kwa kuwa kila matumizi
ya neno hili yamekuwa ya kiroho, bila shaka maana hii ni ya kiroho
pia. Tunapata uwanja mpana kiasi gani kwa ajili ya kujifunza Biblia
kama tutaona maana hii kuwa inahusu hali ya kiroho ya wanadamu.
Tafsiri kwamba “watu hawajavaa nguo” hudhihirisha matokeo
binafsi ya kutokuwa na maono. Katika Biblia – tena kwa mtiririko
dhahiri kabisa – kuokolewa kwa wenye dhambi, “kuhesabiwa haki”
kwao, ni kitu kinachoonekana kwa lugha ya wao “kuvikwa” na ile
haki yenye kulinda na kuhifadhi ya Kristo, na kuhukumiwa kwao
kunaonekana katika wao kutokuwa na mavazi na walio wazi kwa
ajili ya hukumu. Ukweli ni kwamba, katika Biblia nzima, mavazi ni
mfano wa dhambi na haki pia. Mavazi machafu mara nyingi
hutumika kama picha ya dhambi na kujihesabia haki, na mavazi safi
na meupe hutumika kama picha ya ile haki ya Kristo ifunikayo,
inayohifadhi. Ukitaka kufuatilia wazo hilo kwa upana zaidi katika
Maandiko, mafungu yafuatayo yatakuwa na maana sana kwako:
Mwanzo 3:7, 21; Zekaria 3:1-5; Mathayo 22:11-13; Luka 15:22;
Warumi 13:11-14; Waefeso 4:22-24; Wakolosai 3:5-14 na Ufunuo
19:7, 8.
Kitu kimojawapo cha kufurahisha sana katika kuwa Mkristo
ni kujua kwamba Mungu amenivika Vazi Bora Zaidi la Mbinguni –
tena, kwa gharama Yake Mwenyewe! Hili linaonekana katika
simulizi maarufu sana la John Bunyan liitwalo, Safari ya Msafiri. 29
Wakati yule msafiri aliyetambua hatia yake anapofika Msalabani pa
Yesu na kumwamini, mzigo wa dhambi zake unamwacha na
kuanguka, naye anainuka akiwa anasherehekea msamaha na uzima
wa milele. Ndipo anapokutana njiani na “Watatu Wenye Kung’aa”
ambao ni mfano wa Mungu baba, Mungu Mwana, na Mungu Roho
Mtakatifu. Mungu Baba anamwambia msafiri huyo aliyeokoka,
“Amani iwe kwako. Dhambi zako zimesamehewa.” Mungu Mwana
anamvua zile nguo chafu alizokuwa amevaa, na badala yake,
anampa joho jipya, safi, jeupe. Na Mungu Roho Mtakatifu anaweka
alama kwenye uso wake (ambayo ni mfano wa muhuri wa Roho
Mtakatifu), na kumpa mkononi mwake gombo lililokunjwa vizuri
(ambalo ni mfano wa Biblia).
Hiyo kazi ya pili – kazi ya kumvua mwenye dhambi mavazi
yake ya kale na kumvika upya – ndiyo inayolengwa wakati andiko
letu la msingi linaposema, “Mahali ambapo hakuna maono, watu
hawana mavazi.” Tunasoma hivi katika Yohana 3:36, “Yeye
amwaminiye Mwana anao uzima wa milele, lakini yeye
asiyemwamini Mwana hataona uzima, bali hasira ya Mungu inakaa
juu yake.” Mwamini anayemtumaini Kristo amefunikwa kwa haki ya
Kristo naye huepuka hasira ya Mungu kuhusu dhambi. Lakini,
mwenye dhambi asiyeamini hana nguo, na kwa hali hiyo, yuko wazi
kupatikana na kila kitu kinachotaka kumharibu.
30
“Mahali ambapo hakuna maono,” watu zaidi na zaidi hubaki
“bila nguo” au, pasipo ulinzi kwa kitambo na milele. Hayo ndiyo
matokeo binafsi ya kutokuwa na maono.
Mwisho, neno la Kiebrania linatafsiriwa kwa usahihi kabisa
hapa. Maana yake ni “kuangamia”. “Mahali ambapo hakuna maono,
watu huangamia.” Kweli, huruma inahitajika hapa kwa sababu,
kilicho hatarini ni “watu”. Wangekuwa wanyama au mimea, mambo
yasingekuwa mabaya sana. Lakini ni watu – kama wewe na kama
mimi. “Wanaangamia”. Katika Yohana 3:16, neno “kuangamia”
linawekwa kinyume na kuwa na “uzima wa milele”. Kuangamia
maana yake ni kuhusika milele katika kifo hai na maisha ya kufa
katika mahali paitwapo jehanamu. Hapo hapo tena, 1Wakor. 1:18
inaonyesha kwamba watu wasiokuwa na Kristo wako katika hali ya
sasa ya kuangamia. Huku kuangamia kwa watu ni matokeo ya kiroho
na ya milele ya kutokuwa na maono katika Wakristo. Watu watatu
huangamia pasipo Kristo kila sekunde, na Kanisa kwa sehemu kubwa
limepoteza maono yake! Jehanamu inajaa, na Mbingu bado ina nafasi
tele za kujazwa! Yote kwa sababu maono ya Kanisa yamechuja!
Zamani kidogo, mfanya biashara tajiri alisafiri kwenda India
kuwinda simba marara wa Bengali. Akakaa huko majuma sita.
Aliporudi nyumbani, alihudhuria ibada ya katikati ya juma katika
kanisa lake kubwa sana. Alikuta wanajadili kuhusu bajeti ya mwaka
ya kanisa. Mfanya biashara huyo alishtua kanisa zima kwa kutoa
pendekezo kwamba sadaka zote kwa ajili ya utume wa nchi za nje 31
ziondolewe kwenye bajeti. Mzee mmoja akauliza sababu ya
pendekezo hilo la ajabu sana. Jibu likatoka, hivi: “Ndiyo nimerudi
kutoka safari ya majuma sita huko India, na katika kipindi chote
hicho, sikuona mishenari hata mmoja.” Yule mzee akauliza tena,
“Na kusudi la safari yako hasa lilikuwa nini?” Jibu: “Nilikwenda
kuwinda simba marara wa Bengali.” Akaulizwa, “Na ulifanikiwa
kuona wangapi?” Akajibu, “Niliwaona sita.” Yule mzee akasema,
“Hiyo ni ajabu kabisa. Mimi nimekaa India miaka kumi na tatu kama
mishenari, na niliwaona wamishenari mamia kwa mamia. Lakini
mpaka sasa sijaweza kumwona simba marara mmoja wa Bengali
huko India!” Kwa hiyo, mengi sana yanategemeana na mtazamo
wetu, na maono yetu.
Maneno ya Mithali 29:18 yaliandikwa na Mfalme Sulemani,
mtu ambaye katika utawala wake, maono yalipotea. Na hapakuwa na
kushindwa kubaya zaidi katika historia ya Israeli kuliko kule kwa
Sulemani. Watu walisambaratika! Taifa liliporomoka! Ufalme
uligawanyika!
Basi, uchaguzi mbele yetu ni dhahiri kabisa: Aidha ni
“maono au mgawanyiko”! Hii ni kweli duniani kote, kitaifa, katika
mahali pamoja, lakini sana ni kweli katika Kanisa la Yesu Kristo na
katika maisha ya Mkristo binafsi!
Ni lazima – na ni lazima – tumngoje Mungu katika utulivu na
maombi, tukiwa na hali ya ndani sana ya uhitaji na moyo wenye
kufundishika, na kumwomba Yeye arejeshe maono ya Utukufu Wake 32
mkuu sana, naya Mpango Wake mkuu mno kwa ajili yetu, na dunia!
Maono yanaporejezwa, tutagundua tena kwamba Mpango Wake
wote umefunuliwa katika Agizo Kuu la Bwana wetu, na kwamba
jukumu hapo ni “kuwageuza watu wawe wanafunzi”.
Dawson Trotman alikuwa sawa aliposema hivi: “Maono ya
kiroho ni kupata moyoni mwako kile kilicho kwenye moyo wa
Mungu – yaani, dunia!” Paulo aliomba kwamba Wakristo wa Kolosai
wapate “kuona mambo kwa mtazamo wa Mungu” (ktk Wakolosai
1:9, TLR). Kama tungefanikiwa hapo, yangekuwepo mapinduzi
makubwa sana!
“Mtu mmoja aliyeamkaAnaweza kumwamsha mwingine;
Na huyo wa pili anaweza kumwamshaNdugu yake aliyeko jirani.
Hao watatu walioamkaWanaweza kuamsha mji mzima
Kwa kugeuza hapo poteJuu chini.
Wengi walioamkaWanaweza kufanya vurugu
Kiasi kwamba hatimayeSisi wote tunaamshwa.Mtu mmoja aliyeamka,
Alfajiri ikiwa machoni mwake,HUONGEZEKA!”
33
Sura Ya 2Agizo Lenye Kuamua Wajibu Wetu
“Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi. Na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.”
Mathayo 28:18-20
Tunapoondoka nyumbani, mara nyingi tunatoa maagizo yetu
muhimu sana na maelezo – mambo ambayo hatutaki watu wengine
wasahau. Mke wangu mimi huyaweka mezani au kwenye mlango wa
friji. Nini maana yake? Kwamba, hayo ni muhimu!
George Peters katika kitabu chake kiitwacho A Biblical
Theology of Missions aliandika hivi: “Agizo Kuu ndiyo taa yenye
kutuongoza katikati ya ukungu wa kibinadamu na mawazo.
Tunahitaji sana kujifunza upya na kwa undani sana Agizo Kuu. Ni
waalimu wachache sana na wafafanuzi wanaoshughulika kwa upana
sana na mafungu yanayohusu Agizo Kuu. Kanisa linahitaji kufikiri
upya na kwa uzito sana lile Agizo la kufanya watu kuwa wanafunzi.”
Mishenari mstaafu John McGee aliyefanya kazi huko Nigeria,
alisema hivi: “Kuna mengi sana katika Agizo Kuu kuliko mtu
34
anavyoweza kuota, au kufikiri, au kutenda, hata kama angekuwa na
uwezo wa kuishi mara kumi.”
Katika fungu la Maandiko ambayo ni pamoja na Agizo Kuu
(ktk Mathayo 28:16-20), tunasoma kwamba “wale wanafunzi kumi
na moja wakaenda Galilaya hadi kwenye mlima ambao Yesu alikuwa
amewaagizia.” Huku ndiko kuonekana kwa Yesu kwa kipekee baada
ya ufufuo ambako kulikuwa kumepangwa kabla. Alipoonekana mara
zile nyingine zote, alikuwa anatokea tu. Bila shaka kulikuwa na kitu
fulani cha muhimu sana alichotaka kukisema au kukifanya wakati
huu. Na kweli, ndivyo ilivyokuwa! Hapa “alibandika” maagizo Yake
ya Mwisho. Kuna msemo mmoja wa kawaida sana miongoni mwa
watu wenye kutumia vyombo aina mbalimbali – “Kila Kitu
Kikishindikana, Soma Maelekezo”. Katika sura hii, tunakwenda
kujifunza na kusoma Maelekezo Yake ya Mwisho. Tutagawanya
maelekezo hayo katika mafungu mawili: Uhakikisho Ulioko Katika
Hilo Agizo, na Kazi Iliyoko Katika Hilo Agizo. Ikiwa tunataka
kuelewa na kutimiza Agizo Kuu, ni lazima tuchunguze kwa makini
sana mambo hayo mawili.
UHAKIKISHO ULIOKO KATIKA HILO AGIZO (MS. 18, 20A)
Agizo lenyewe linaanza kwa tamko la kushangaza sana
lililowahi kutolewa. Yesu alisema, “Mamlaka yote nimepewa
Mimi,mbinguni na duniani.” Hapo, sifa Yake na agizo letu
35
vinategemea sentensi hiyo. Nini maana yake, na ni muhimu kiasi
gani maneno hayo?
“Mamlaka” yanayotajwa hapa ni mamlaka ya KiMungu.
Kanuni kuu katika Maandiko yote ni kwamba, “hakuna mamlaka
isipokuwa itokayo kwa Mungu” (ktk Warumi 13:1), na kanuni hiyo
inaonekana hapa pia. Katika Kiyunani, neno linalotumiwa kueleza
mamlaka ni exousia, ambalo maana yake halisi ni “kutokana na
kuwa”. Fikiri kidogo jambo hili. Maana yake ni kwamba mamlaka
yote ya lazima kutoka kwa Mungu mwenyewe yametolewa kwetu
kwa njia ya mahusiano yetu na Kristo ili kutimiza Agizo hilo.
Halafu, mamlaka hii ni mamlaka iliyotolewa. Yesu Kristo
anayo mamlaka katika Nafsi Yake, ambayo anaimiliki kwa sababu ya
kuwa Yeye. Mamlaka aliyokuwa nayo wakati wa maisha Yake hapa
duniani ilionyeshwa kwa njia nyingi zilizo wazi.
Alionyesha mamlaka Yake juu ya nguvu za asili wakati
alipotuliza dhoruba kali iliyokuwa imewatisha hata wavuvi
waliozoea, kwa neno tu la kinywa Chake na kunyoosha mkono
Wake. Alikuwa amesema na mtini nao ukakauka mbele ya macho ya
wanafunzi, waliokuwa wameshangaa sana.
Vile vile alikuwa na mamlaka juu ya dhamiri ya mwanadamu.
Kwa kutumia mazungumzo rahisi tu naye, Mwokozi wetu aliamsha
dhamiri ya mwanamke Msamaria aliyekuwa amejaa dhambi, na
kuanzisha hali ya matumaini katika nafsi yake. Wakati mwingine,
akiwa amezungukwa kabisa na kundi lililotaka kujua mambo mengi, 36
kwa kutaja tu jina la mtu na kumwambia ashuke kutoka kwenye mti,
aliweza kuiamsha dhamiri ya Zakayo, Myahudi aliyechukiwa na
asiyemcha Mungu, wa mjini Yeriko.
Vile vile alionyesha mamlaka makuu juu ya ile dunia ya
kiroho isiyoonekana wakati wa maisha Yake hapa duniani. Kwa neno
tu au mguso, aliweza kufukuza falme na mamlaka za uovu
zilizokuwa zimetawala maisha ya mtu.
Tena alikuwa na mamlaka ya kupendeza sana katika eneo la
udhaifu na magonjwa ya mwanadamu. Akitumia nguvu Zake bila
kutaka kujionyesha, lakini kwa ajili ya kusaidia maisha ya watu
waliokuwa wanateseka, aliwafanya viziwi wasikie, vipofu waone,
bubu waseme, viwete watembee, vilema wanyooke katika viungo
vyao, na wafu warudie uhai wao.
Hata mafundisho Yake pia yalikuwa na mamlaka. Baada ya
mafundisho Yake ya kwanza katika sinagogi fulani, watu
“walishangazwa na mafundisho Yake, kwa sababu aliwafundisha
kama mtu aliyekuwa na mamlaka, si kama waandishi” (ktk Marko
1:22, TLR). Yesu hakusita kuchukua mamlaka kamili kabisa. Alidai
kuwa na mamlaka ya kusamehe dhambi (ktk Marko 2:10). Alitoa
matamko yaliyorekebisha kanuni za Torati ya Musa, ambayo kila
mtu aliikubali kuwa ilitokana na Mungu (ktk Mathayo 5:21, 27, 33).
Hata alidai kwamba Yeye Mwenyewe ndiye angemhukumu kila mtu
(ktk Yohana 5:27).
37
Lakini, mamlaka inayoonekana katika madai haya si ile
mamlaka inayotajwa katika Mathayo 28:18. Yesu alisema kwamba
haya mamlaka “yametolewa” bila shaka kwa msingi wa mafanikio
Yake katika Kifo na Kufufuka Kwake. Mamlaka ambayo alikuwa
nayo wakati huo katika utukufu Wake wa ufufuo yalizidi sana yale
aliyokuwa nayo wakati wa maisha Yake. Kila aina ya mamlaka
ilikuwa Yake kwa sasa. Mamlaka hiyo alikuwa amepewa kwa amri
ya Baba Yake mbinguni. Wanafunzi walijua kwamba wao walikuwa
watumishi wa Bwana ambaye mamlaka Yake mbinguni na duniani
haikuwa na utata hata kidogo wala swali la aina yoyote ile.
Tunasoma hivi katika Warumi 1:4, “Alitangazwa kuwa Mwana wa
Mungu kwa nguvu (mamlaka) … kwa ufufuo kutoka kwa wafu”
(TLR). Hayo mamlaka ndiyo msingi wa Agizo analotoa kwa
wanafunzi Wake.
Ni dai la ajabu sana! A.T. Robertson alisema hivi: “Ni
onyesho la hali ya juu sana katika historia ya dunia, kumwona Kristo
aliyefufuka, pasipo fedha wala jeshi wala taifa, akiwaagiza kundi hili
la watu mia tano – waume kwa wake – waende kuiteka dunia na
kuwafikisha mahali pa kuamini kwamba inawezekana kufanyika,
kwa mguso na udhati na nguvu.”
Vile vile, mamlaka hii ni mamlaka anayostahili Yeye. Yesu
alisema hivi: “Mimi nimepewa mamlaka yote.” Ona kwamba hii
mamlaka hatujapewa sisi, bali kapewa Yeye. Lakini, hilo lisitupe 38
hofu, kwa sababu chochote kilicho Chake ni mali ya kila mtu
aliyeokoka. Kila mtu aliyezaliwa mara ya pili ni mrithi wa Mungu
kwa sababu yeye ni “mrithi pamoja na Kristo” (ktk Warumi 8:17).
Kila kitu katika milki ya Baba ambacho kihalali ni mali ya Kristo
kwa sasa ni mali yangu pia kwa sababu ya mahusiano yangu kiimani,
au kujitambulisha kwangu kiimani, na Yeye. Chochote kilicho Chake
ni changu, si kwa sababu mimi ninastahili kuwa nacho, bali kwa
sababu mimi niko ndani Yake. Ona pia kwamba, hakupewa mamlaka
haya kwa sababu Yeye ni Mwana wa Mungu. Kama Mungu, hakuna
kitu anachoweza kuongezewa, na hakuna kitu kinachoweza
kupunguzwa Kwake. Mamlaka ambayo Yesu anadai hapa ni
mamlaka ambayo ameipata (ameistahili) kama Mwana wa Mtu.
Neno “aliyopewa” linaonyesha tendo la wakati uliopita, na bila shaka
humaanisha kukabidhiwa mamlaka hiyo siku ile alipofufuka toka
kwa wafu. Hii inakubaliana na yale maandiko katika Wafilipi 2:5-11,
yanayohusu Kunyenyekezwa na Kutukuzwa Kwake. Baada ya Paulo
kuonyesha jinsi Yesu alivyoshushwa na kunyenyekezwa, ndipo
anapodhihirisha kutukuzwa Kwake kulikofuata. “Kwa hiyo tena
Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina;
ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya
duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa Yesu
Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba” (ktk Wafilipi 2:9-
11). Kwa hiyo, kutukuzwa Kwake na mamlaka Yake vilimstahili
kutokana na kifo na kufufuka Kwake.39
Mwisho – mamlaka aliyodai kabla ya kutoa Agizo Lake Kuu
yalikuwa mamlaka yaliyoelezwa na kuwekwa wazi. “Nimepewa
mamlaka yote, mbinguni na duniani.” Maeneo hayo mawili
yanayotajwa ndiyo pekee ambayo sisi tunahusika nayo, na bila shaka
Yesu Kristo anatenda kazi katika maeneo hayo pia. “Mbinguni na
duniani.” Mamlaka yote ya mbinguni ni Yake, na mamlaka yote ya
duniani ni Yake. Anawatangazia wanafunzi Wake kwamba
“nimepewa Mimi mamlaka yote mbinguni”, mahali alipopokea “Jina
lipitalo majina yote”, mahali ambapo “ametukuzwa na kuketishwa
mkono wa kuume wa mamlaka”, mahali ambapo “ametiwa taji ya
heshima na utukufu”. Anatangaza pia kwamba “Mimi nimepewa
mamlaka yote duniani”. Hivyo, Yeye ndiye Bwana mkuu wa kote
kuwili.
Katika mchezo maarufu sana wa Shakespeare, mwandishi
Mwingereza maarufu, anaonekana Liwali wa Kent akimjia mfalme
kwa siri, akiwa amejibadilisha. Mfalme huyo Lear anamwambia,
“Unataka nini wewe?” Yule Liwali anamjibu, “Nataka nikutumikie.”
Mfalme anamwuliza, “Kwa nini?” Ndipo linatoka jibu maarufu la
Liwali wa Kent, kwamba, “Kwa sababu katika uso wako naona kitu
ambacho kwa hiari yangu mwenyewe naweza kukiita bwana”.
Mfalme akamwuliza, “Kitu gani hicho?” Liwali anajibu, “Mamlaka”.
Yesu anatoa madai halali kabisa kwamba mamlaka yote ni
Yake. Na katika mamlaka hiyo ndipo tunapaswa kutekeleza ule
mradi wa utume (na ile amri ya kufanya watu kuwa wanafunzi). 40
Mamlaka Yake hayajapungua wala kumalizika kutokana na miaka
kupita. Basi, kwa msingi wa mamlaka hiyo, tunapaswa kutekeleza
agizo au kazi tuliyopewa katika Agizo Kuu.
KAZI ILIYOKO KATIKA HILO AGIZO (MS. 19, 20)
AMRI PEKEE KWA KANISA (KWA MKRISTO) KUSONGA
MBELE
Agizo Kuu ndiyo “amri pekee ya kusonga mbele” iliyowahi
kutolewa na Yesu Kristo kwa Kanisa Lake. Agizo Kuu ni kazi ya
kuvuna roho na utume, lakini ni zaidi ya hayo. Kuna maelezo kuhusu
Agizo Kuu la Bwana wetu katika Agano Jipya mara tano. Linatajwa
kwa njia tofauti katika Mathayo 28:18-20 (kwa maelezo yaliyo
dhahiri zaidi), katika Marko 16:15 (kwa kifupi lakini wazi), katika
Luka 24:47, Yohana 20:21 na Matendo 1:8 (kwa ufafanuzi mpana
zaidi).
Katika maelezo ya Mathayo, Kanisa la Yesu Kristo linapata
msingi kwa ajili ya kazi yake. Hakuna swali kabisa katika maneno
anayotoa Mathayo kuhusu kile ambacho Yesu alikusudia wafuasi
Wake kufanya. Si swala la hisia au kujisikia. Si kazi ya kufanywa
tutakapoona inafaa. Yesu aliacha maagizo dhahiri. Maagizo hayo ni
kamilifu (yaani, hayapitwi na wakati wala kubadilika) na ni ya mara
moja. Agizo Kuu ni la sasa hivi, na linamfunga kila Mkristo
kulitimiza wakati huu. Maneno ya Agizo hili ni maneno tendaji:
Enendeni, fanyeni watu kuwa wanafunzi, batizeni, na fundisheni. 41
Kwa kifupi tu, Kanisa liko chini ya amri, lakini uhalisi wa hiyo amri
unaweza kuwashangaza waamini wengi.
KULIGAWA AGIZO SEHEMU SEHEMU
Ningependa kuligawa Agizo Kuu katika sehemu saba.
Muhtasari ni kama ifuatavyo: Kwanza, sisi tunawajibika kutumia kila
mtenda kazi anayepatikana (neno “ninyi” la ms. 19 liko katika
wingi). Halafu, tunatakiwa kuingia shambani (“enendeni”). Tatu,
tunatakiwa kila wakati kupanua maono yetu (“mataifa yote”). Nne,
tunapaswa kuwashuhudia wahusika (“kufanya wanafunzi”). Tano,
tunapaswa kuwahusisha walioshuhudiwa (“mkiwabatiza katika jina
la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu”). Sita, tunatakiwa
kuwaelimisha na kuwajenga waliojiunga nasi (“na kuwafundisha
kuyashika yote niliyowaamuru ninyi”). Na mwisho, tunapaswa
kutarajia Yeye kutenda kazi (“na tazama, Mimi niko pamoja nanyi
siku zote, hata mwisho wa dunia”). Bila shaka unaona sasa kwamba,
yapo mengine mengi sana kuhusu Agizo Kuu la Bwana wetu kuliko
ambavyo sisi tumekuwa tukiheshimu!
Tunapochunguza kwa makini na dhati kabisa hili Agizo,
tunagundua kitu cha kushangaza sana. Tunapata kwamba, kwa karibu
karne mbili, Agizo lilifanya kazi vizuri kabisa na kuigusa dunia
iliyokuwa inajulikana siku zile kwa haraka sana. Lakini, kitu cha
ajabu kikatokea. Kitu fulani kiliharibika kabisa. Ili kuona hilo,
ningependa tutazame kila hoja katika zile saba ambazo nimetaja. 42
Chini ya kila hoja, ninataka utazame vichwa vidogo viwili. Kimoja ni
“Mkakati wa Mwokozi”, na kingine kinaitwa “Mbadala wa Shetani”.
Tutafanya hivyo na kila hoja.
1. KUTUMIA KILA MTENDA KAZI
Hoja ya kwanza katika Agizo Kuu ni kutumia kila mtenda
kazi. Katika mstari wa 19, neno “ninyi” liko katika wingi, na maana
yake hasa ni “ninyi wote”.
Mkakati Wa Mwokozi
Mtu mmoja ameeleza nia ya Yesu kuhusu kutimizwa kwa
Agizo hili Kuu kwa maneno haya: “Waamini wote wanatakiwa
kuhusika, na wanapaswa kutenda wakati wote”. Kitu kimoja – licha
ya nguvu za Mungu – kilichofanya Agizo Kuu kufanikiwa sana hapo
mwanzoni ni kwamba, watenda kazi wake wote walihusishwa
kufanya huduma mahali palipotakiwa. Lengo lilikuwa kwamba kila
mwanafunzi awe mzalishaji wa wavuna roho na wafanya watu kuwa
wanafunzi kama yeye. Wote walikuwa wasemaji, waenezaji na
wainjilisti! Ukweli ni kwamba, kushiriki kulikuwa kwa kila mtu
miongoni mwao mpaka ikabidi sheria ziwekwe ili kuondoa vurugu
au kuchanganyikiwa (ona 1Wakor. 14:31). Hapakuwepo na
watazamaji miongoni mwao. Adolph Harnack, mwanahistoria
maarufu wa kanisa, alisema hivi: “Wakati kanisa liliposhinda sana
katika siku za mwanzo za Dola ya Rumi, halikufanya hivyo kwa 43
waalimu au wahubiri au mitume, bali kwa wamishenari wa kawaida
kabisa.” Hili Agizo linataka huduma binafsi kutoka kwa kila
aaminiye. Wote walio viungo vya Mwili wa Kristo hawawezi
kufanya hivyo bila ya kila mshirika kufanya hivyo. Kanisa moja
katika eneo la Manhattan huko Marekani lina ujumbe ufuatao
kwenye kibao chake: “Mchungaji, --------“. “Wahudumu: Kila
mshirika.” Huo ndiyo mkakati wa Mwokozi kwa ajili ya kila mtenda
kazi kutumika.
Mbadala Wa Shetani
Sasa, tazama mbadala alioleta Shetani. Ukweli ni kwamba
Agizo Kuu lilifanya kazi. Yaani, lilifanya kazi mpaka Shetani akaona
vibaya. Lilifanya kazi vizuri sana kiasi kwamba ilimchukua miaka
200 kuondokana na kipigo alichopata na kupanga upya majeshi yake.
Hatimaye, akapambana na Agizo Kuu kwa mpango mbadala wake.
Si vigumu kuona kwamba Agizo Kuu la kwanza limevurugwa kiasi.
Limerekebishwa, na kwa karne nyingi sana, makanisa mengi
yameangukia katika mpango wa Shetani. Pigo kubwa sana la Shetani
dhidi ya Agizo Kuu lilielekezwa kwenye ile hoja ya kwanza, ya
kutumika kila mtenda kazi.
Mapema kabisa katika historia ya Kanisa, Shetani alianzisha
mgawanyo katika Kanisa. Likawa na sehemu mbili, naye akakazia
kupita kiasi zile tofauti. Walio wengi aliwaita “walei – wasiokuwa
wachungaji” na wale wachache akawaita “wachungaji – watumishi”. 44
Na hoja yake kubwa ilikuwa kwamba walei hawana uwezo na
hawana vipawa, na kwamba hawahusiki katika kazi halisi ya kanisa
hata hivyo. Shetani basi akasimamia ujenzi wa tabaka ya watu wa
dini walio wataalamu. Hawa wataalamu walitakiwa (1) kupigana vita
zote za kiroho, na (2) kufanya kazi zote za kiroho. Vipi shughuli ya
“walei”? Kumtegemeza na kumsaidia huyo mtaalamu kiongozi na
kulipia mpango wake kufanyika (ambapo katika Agano Jipya, watu
ndiyo mpango mkuu).
Basi, “ngazi ya kiroho” ikatengenezwa Kanisani. Juu kabisa
ya ngazi alikuwepo “mishenari”, halafu anayefuata ni mchungaji,
halafu watendaji wengine wataalamu wa kidini, na mwisho wa ngazi,
mshirika wa kawaida. Kuna mtu amesema kwamba kizazi chetu ni
“kizazi cha mtazamaji”. Mpira wa miguu una wachezaji 22 kwa mara
moja, lakini unaweza kuwa na watazamaji mamilioni wakati huo
huo! Michezo mingine ina wachezaji 18. Mpira wa vikapu una
wachezaji kumi, ngumi wachezaji ni wawili, na kuna michezo
mingine katika Olimpiki yenye mchezaji mmoja tu. Lakini michezo
hiyo yote ina mashabiki mamilioni. Mchekeshaji mmoja aitwaye
Fred Allen alisema hivi: “Kama jamii itaendelea kama ilivyo, baada
ya muda tutakuwa na dunia iliyojaa watu wenye macho makubwa
kama sahani za vikombe vya chai, na akili zenye ukubwa wa harage”
(kwa kuwa wakati wote watu wanakodoa macho, na kutumia muda
mwingi katika ushabiki)!
45
Matatizo Kanisani Ya Watu Kutokuwa Na Kazi, Na Kazi Kidogo
Kanisa limetengeneza matatizo mawili ya “kutokuwa na
ajira” na hayo yanaungana mkono mara zote, na kufanya mambo
kuwa mabaya zaidi. Kuna tatizo la kutokuwa na kazi kwa washirika
katika kusanyiko la mahali. Kwa kuwa mshirika wa kawaida katika
kanisa la kawaida hatimizi kazi yake aliyopangiwa na Mungu,
“mshahara” wake unapunguzwa na kuwa posho tu kwa ajili ya
kuishi. Wajibu wake hautimizwi, thawabu yake inapotea, dunia
inabakia gizani, na Shetani anatosheka vizuri sana.
Halafu kuna tatizo linalokaribiana na lile, ambalo ni mtumishi
kutofanya kazi ipasavyo. Mchungaji wa kawaida katika kanisa la siku
hizi ana kazi nyingi, lakini hafanyi kazi ipasavyo! Wakati Henry M.
Stanley aliporudi kutoka Afrika kwenye kumtafuta David
Livingstone, mwanahabari mmoja alimwuliza swali hivi: “Ni kitu
gani kilichokusumbua zaidi wakati ukiwa Afrika? Ni wale simba, au
ni nyoka?” Stanley akajibu hivi, “Wala! Walionisumbua zaidi ni
mbu!” Wachungaji wetu hawapati kuona simba na chui kwa sababu
daima wako kwenye mapambano na mbu. Wakati vita kuu za
atomiki zinapiganwa katika ulimwengu wa roho, wao wanajitahidi
kupambana na kukabiliana na mashambulizi ya mbegu ndogo ndogo
tu! Ongezeko la vitu vingi vidogo vidogo – vishughuli vingi vya
kidini ambavyo vinachokesha, pamoja na picha bandia ya huduma ya
mchungaji ambazo zimechorwa njiani mwake vinamfanya mchungaji
ashindwe kutekeleza kazi pekee ambayo Mungu amempa.46
Hivi karibuni nilipata taarifa kutoka Ofisi Kuu ya Jimbo
kwamba wachungaji 300 wa Kibaptisti wanaondolewa makanisani
kila mwezi. Sina uhakika na idadi hiyo, lakini najua kwamba tatizo
hilo ni kubwa sana. Pia nilisikia taarifa miaka kadhaa iliyopita
kwamba wachungaji zaidi ya elfu moja wa Kibaptisti wanaachana na
madhabahu zao. Sina uwezo wa kuthibitisha idadi hiyo, lakini najua
kwamba tatizo hilo ni kubwa sana pia. Pengine sababu kubwa ya
huko kutatizika kwa uongozi unaoitwa ni kwamba kiongozi huyo
hatosheki kwa “ajira ndogo” inayomkabili – hana kazi za kumtosha
kuridhika!
Ukristo Tazamaji Katika Kanisa
Tumetengeneza Ukristo tazamaji katika kanisa, ambao katika
huo, wachache ndiyo wasemaji, na wengi ni wasikilizaji. Kanisa
limejaa “umoja wa mashabiki” – mashabiki wa imani. Hebu fikiri
kuhusu duka la kuuza vitu jumla, ambalo lina meneja mauzo ambaye
kazi yake ni kuuza hivyo vitu na kufundisha kuhusu sifa ya vitu
hivyo na mbinu za uuzaji. Tuseme pia kwamba duka hilo lina kundi
kubwa tu la “wauzaji” ambao kazi yao kubwa ni kuwatafuta
wasikilizaji na kuwatia moyo kusikiliza tu mafundisho ya meneja
mauzo. Kingekuwa kituko cha namna gani hicho? Je, duka hilo
lingedumu kwa muda gani? Ndugu James S. Stewart wa Edinburgh,
Uskochi, alisema hivi: “Tatizo hasa la Ukristo si wasemao hakuna
Mungu wala wenye mashaka, bali ni Mkristo asiyeshuhudia, asiyezaa 47
matunda, anayejaribu kuingiza roho yake mbinguni kwa njia ya
magendo, yeye mwenyewe.” Huo ndiyo mkakati wa Shetani, na zaidi
ya hayo, ametumia sana neno “ninyi” mpaka imefikia kwamba hata
hao “watumishi” si wote wanaoshuhudia!
Hebu tazama jamii ya Kikristo. Kanisa liko upande gani –
upande wa Mkakati wa Mwokozi, au upande wa Mbadala wa
Shetani? Nadhani jibu liko wazi kabisa, na linasikitisha. Ni lazima
tutazame upya Amri yetu ya Kusonga Mbele!
2. KUINGIA SHAMBANI
Hoja ya pili katika muhtasari wetu kuhusu Agizo Kuu ni
kuingia shambani kote. Neno “enendeni” ni neno tendaji, lenye
nguvu – neno linalo-onyesha kwenda au kutembea.
Mkakati Wa Mwokozi
Mkakati wa Mwokozi ni dhahiri. Katika Mathayo 13:38,
alisema hivi: “Shamba ni dunia”. Hili si shamba kwa ajili ya kanisa,
bali ni shamba kwa ajili ya kanisa lako la mahali! Yesu Kristo
anakutazamia uhusike na dunia nzima! Mifano ambayo Yesu
anatumia kusema kuhusu Wakristo na Injili imefungamanishwa
pamoja kwa kitu kimoja. Yote ina tabia ya kupenya – kuingia ndani.
Yesu alitumia mfano kama nuru, chumvi, funguo, mkate, na maji.
Nuru haina faida kama haipenyi na kufukuza giza. Chumvi haina
faida kama inabakia ndani ya chupa yake. Lazima ipenye na kuingia 48
katika mboga au viazi. Mtoto mmoja mvulana alisema hivi, “Chumvi
ndiyo huharibu viazi – ukiacha kuiweka.” Funguo hazina maana
kama haziingii katika kitasa. Mkate hauna faida ukiwa nje ya mlaji,
na maji hayatoshelezi hitaji la mtu mwenye kiu kama
yasipomwingia. Vivyo hivyo, Wakristo wanatakiwa kuingia na
kupenya duniani kila mara.
“Huwezi kumtaja Mungu bila kwenda. Hakuna uzuri bila
kwenda. Huwezi kutamka neno Injili bila kwenda, na huwezi kuitii
Injili na kuwa mtumishi mzuri wa Mungu usipokwenda – kwa
masharti Yake. Ukristo ni kitu cha kwenda kwa asili yake na
msukumo – si cha kushikilia. Kila Mkristo anapaswa kuishi kikazi
(yaani, kama Mkristo) kwenye eneo la kupenya – iwe ni katika
maabara ya kisayansi, maktaba, kiwandani, shamba la matunda, kazi
ya kugawa vitu, cheo kikubwa, kwenye ndege ya kisasa, katika
hospitali ya tabibu wa magonjwa ya akili, au katika ofisi ya
mchungaji. “Dunia” yetu ni popote tulipo, penye watu. Katika Luka
10:1-3, Biblia inatuambia, “Basi, baada ya hayo Bwana aliweka na
wengine, sabini, akawatuma wawili wawili wamtangulie kwenda kila
mji na kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe. Akawaambia,
‘Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni
Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake.
Enendeni. Angalieni, nawatuma kama wanakondoo kati ya
mbwamwitu”. Ona maeneo ambayo nimekazia kwa kutumia wino
mwepesi. Maneno hayo yamejaa! Kila Mkristo anapaswa kuwa 49
mwanzilishi, mtangulizi kwa ajili ya ujio wa Kristo “kila mahali
alipokusudia kwenda mwenyewe.” Wanakondoo kati ya mbwamwitu
watarajie kupona kwa muujiza tu!
Tena – neno “enendeni” katika Agizo Kuu SI AMRI.
Kulihesabu kwamba ni amri ni kuendeleza ile dhana ya “ngazi ya
kiroho katika Ukristo”. Lingekuwa ni amri, kila ambaye angekwenda
mbali ili kuihubiri Injili au kumshuhudia Kristo angehesabiwa kuwa
mtu maalum. Lakini, neno tendaji lina maana hii: “Mnapokuwa
mkienda”, au hata, “Kwa kuwa mnakwenda”. Yesu asingekosa akili
kiasi hicho, atuagize kufanya kitu ambacho tunafanya tayari! Je,
kanisa lako liko wapi Jumanne mchana saa tisa? Kwani liko
kanisani? Hapana, “linakwenda”. Swala hapa si kwamba mbona
kanisa haliendi duniani? Swala ni hili: Je, kanisa linatimiza kazi yake
linapoingia na kupenyeza?
Nilikuwa katika mji mkubwa mzuri sana katika nchi ya
kigeni fulani, miaka kadhaa iliyopita. Nilihubiri kwenye kanisa la
Kiingereza hapo Jumapili asubuhi. Nikawahi ili nipate nafasi ya
kuzungumza na watu walipokuwa wanafika ibadani. Mbona
nilishtushwa sana na watu wenyewe! Walikuwepo Wamarekani
wengi, na walikuwa wafanya kazi katika shirika la mafuta la
kimataifa, wenye mishahara mikubwa sana. Nilipowauliza jinsi
walivyokuwa wanafurahia kukaa huko, wote walilalamika kwamba
wanachoshwa na mambo yale yale kila siku. Wengi wao walikuwa
hapo kwa mikataba ya miaka miwili. Katika mahubiri yangu, 50
niliuliza ni kwa nini wasijifunze lugha ya pale na wawe na
vipeperushi vyenye ujumbe wa Injili katika lugha ya pale na wafanye
umisheni, uinjilisti na kuleta watu kwa Yesu wakiwa huko. Nadhani
walipuuza wazo hilo bila hata ya kulifikiria! Ni hivi: Kuna mtu
ambaye ametuuzia wazo baya kabisa lenye kupelekea usaliti mkubwa
sana wa Yesu na Agizo Lake. Wao walikuwa “wamekwenda” (tena,
kwa kulipwa na shirika la mafuta), lakini hawakutambua wajibu wao
“wakiwa katika kwenda”.
Mbadala Wa Shetani
Shetani ameingiza mbadala wa kijanja na siri sana katika akili
za Kanisa. Maneno makuu mawili katika Injili ni “njoo” na
“enenda”. Tukisha kuja kwa Kristo (Mathayo 11:28-30, kwa mfano),
tunapaswa “kwenda na kuwaeleza” watu wote yale tuliyopata katika
Kristo. Shetani ni bingwa wa kutumia watu, na kubadili maneno.
Yeye akaingiza upotofu wa polepole kanisani, kuliondoa kwenye
“nenda ukaeleze” na kulitia kwenye “njoo usikie”. Mkomunisti
mmoja alitania Kanisa kwa maneno haya, “Kauli mbiu ya Wakristo
inaonekana ni, ‘Njooni hapa mpate ujumbe wa Mungu, mwende
mbinguni. Au acheni kuja, mwende jehanamu’!” Ndugu mmoja
aitwaye Paul Little alisema hivi, “Tatizo si kwamba Injili imepoteza
nguvu yake. Tatizo ni kwamba kanisa limepoteza walengwa wake.”
Mwingine naye akasema, “Roho Mtakatifu hawezi kuwaokoa
watakatifu na viti – lakini Kanisa limejaa vyote!”51
Fikiri mfano wa kimatibabu. Tuseme kwamba Wizara ya
Afya inaogopa kwamba kutatokea mlipuko wa surua. Ingefanya nini
ili kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo? Bila shaka ingewatenga wenye
ugonjwa huo na kuwaweka karantini wote ambao wamekwisha
upata, na kwa njia hiyo ugonjwa ungezuilika. Sasa hebu fikiri –
Wizara ya Jehanamu itake kuzuia mlipuko wa Ukristo wa Agano
Jipya. Bila shaka ingefanya kila liwezekanalo kuwatenga “wabebaji”
na kwa njia hiyo kuzuia kuenea kwake. Na hicho ndicho
kinachotokea Kanisani kwa sehemu kubwa. Tunakaa ndani ya
Kanisa kwa “mkao mtakatifu”. Timu yetu haiendi uwanjani, mahali
ambapo ili kupata ushindi mchezo lazima ufanyikie. Na kuna
wanaopenda mpango huu na uzuri wake na usalama wake. Maana,
umewahi kumsikia mchezaji aliyeumizwa akiwa hajaingia uwanjani?
Kwa hiyo, tunapanga mikakati yetu, tunafanya uchambuzi kuhusu
adui yetu, tunarudiarudia mambo na hata kulaumu wachezaji
wenzetu. Tunawaza kuhusu uanachama, mipango yetu, majengo na
fedha. Kila juma tunakuwa na “gwaride” na amri yetu kuu ni “tubaki
kama tulivyo”. Nimechanganya mifano hapo, lakini nadhani ujumbe
umefika. Daima tunaongeza shughuli zetu za kidini, tunakamilisha
mipango yetu kishirika, tunapanua na kukuza taasisi zetu za kidini,
na kuimarisha taratibu zetu kiuongozi katika dini, na yote
tunayofanya katika makanisa mengi ni kudumisha kawaida na
kujistarehesha sisi wenyewe tu! Bila shaka Shetani anafurahi sana!
52
Kanisa la kawaida linafanya kazi kwa kufuata mpango mbadala wa
Shetani, badala ya kufuata mkakati wa Mwokozi.
3. KUPANUA MAONO
Sehemu ya tatu katika Agizo la Bwana wetu ni kuendelea
kupanua maono. Upana wa eneo letu la utendaji katika Agizo hili ni
“mataifa yote”.
Mkakati Wa Mwokozi
Hebu tujikumbushe tena – Yesu Kristo hafanyi mchezo nasi.
Anatutazamia kabisa “tukabiliane” na dunia nzima! Naye ametupa
Mpango ambao kwa huo tunaweza kufanikiwa! Je Mkristo – ni nia
yako kugusa mataifa yote kwa “kuwageuza watu kuwa wanafunzi”?
Hiyo kazi kuu ndiyo agizo la Bwana wetu. Kugusa dunia ndiyo
utume wetu. Lengo letu lazima liwe kujulisha na kugusa dunia nzima
mpaka mwisho wa nchi, mpaka ukamilifu wa dahari.
Hii hoja ya tatu katika Agizo inawezekana kuwa ndiyo ya
maana kuliko zote. Hapa ndipo motisha kwa ajili ya kuwafanya watu
kuwa wanafunzi inapotokea. Ningependa kutumia nafasi zaidi hapa
ili kuhakikisha kwamba sote tunatambua ukuu wa Agizo la kuigusa
dunia nzima. Dakta D. Martyn Lloyd-Jones alisema hivi katika
kitabu chake kiitwacho The Miracle of Grace, “Sitasita kusema
kwamba hatimaye, hakuna kipimo kamili cha ukiri wetu binafsi wa
imani kama hali tuliyo nayo moyoni juu ya shughuli ya umisheni ya 53
Kanisa.” Mimi niongeze maneno yangu hapa kwamba, “shughuli ya
umisheni ya Kanisa” si kutuma waamini wenye mzigo maalum
kwenda nchi za mbali tu. Huanza katika moyo wa kila aaminiye, na
hutekelezwa kwa kila aaminiye kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo
anayetambua kuhusu dunia nzima, anayelemewa na dunia nzima,
anayeona dunia nzima, na mwenye kuwajenga na kuwaongeza
wanafunzi wengine wenye kuiona dunia nzima na kuigusa dunia
nzima.
Je, maono yako binafsi ni maono “makubwa kama ya
Mungu”? Je, unakusudia kufika wapi na kugusa watu? Kipimo cha
kufanikiwa kwako kama mwanafunzi wa Kristo kunaweza
kuonekana katika jinsi unavyojibu maswali haya: Je, ushawishi ulio
nao unafika mbali kiasi gani? Je, nini ukubwa wa eneo lako la
uwezo? Isaya 54:2 inasema, “Panua mahali pa hema yako, na
wayatandaze mapazia ya maskani yako; usiwakataze. Ongeza urefu
wa kamba zako, vikaze vigingi vya hema yako.” Mstari huu unatoa
kauli mbiu kamili kabisa kwa ajili ya wote wanaofanya wengine
kuwa wanafunzi (yaani, wanafunzi wote wa kweli wa Kristo), na
hutoa mwito kwa ajili ya kukuza maono kusikokoma kwa kila
aaminiye, ili kuigusa dunia nzima.
Hapa tena naomba ukabiliane na swali hili: Je, nini ukubwa
wa eneo lako la uwezo na ushawishi? Je, unatenda kazi chini ya
maono kama kofia, ambapo maisha ya Kikristo yanaanza na kuishia
kwa ajili ya manufaa yako binafsi – ili uishi na upate kitu? Au je, 54
maono yako ni kama mwavuli, yenye nafasi kwa ajili ya watu wawili
au watatu hivi? Au je, maono yako ni kama kibanda cha simu, yenye
nafasi ya kufunika watu kati ya watu hadi wanne? Au je, ni kama
chumba, yenye kuwaingiza marafiki kadhaa? Au pengine yako kama
nyumba, yenye uwezo wa watu kama 25 hadi 50 hivi? Au ni kama
duka kubwa, yenye uwezo wa watu mia kadhaa, na hata elfu kadhaa?
Au ni kama uwanja wa michezo, yaliyo na upana wa kutosheleza
makumi elfu? Au pengine unatamani kuwa na maono kama anga,
ambayo yanaweza kuwahusisha watu wote duniani na vizazi vyote
vitakavyokuja? Kumbuka kwamba Agizo linahitaji maono
yanayolingana na Yesu, yenye ukubwa wa Mungu, nasi tunatakiwa
tuzidi kufanana na Kristo, kwa hali hiyo kuendeleza Tabia ya Mungu
Mwenyewe. Tunakuwa “washiriki wa asili Yake ya Uungu” (ktk
2Petro 1:4) tunapo-okoka, na sehemu inayobaki ya maisha yetu
inapaswa kutumika katika kushirikiana na kupanuliwa kwa Asili
Yake ndani yetu. “Yeye hana budi kuzidi, bali mimi nipungue” (ktk
Yohana 3:30). Sehemu ya huku kupanuka inamaanisha kuongezeka
katika kujitambulisha na “Kinachomsumbua” Mungu – kumjulisha
na kugusa kila mtu duniani kwa Ujumbe wa Injili Tukufu ya Kristo.
Ni dhahiri kutokana na kusoma Injili hata kwa juu juu tu
kwamba, Yesu alikuja ili kuvamia, kufahamisha na kugusa dunia
nzima. Angeweza kusema, “Mimi ni nuru ya Galilaya”, lakini
hakufanya hivyo. Alisema, “Mimi ni nuru ya dunia” (ktk Yohana
8:12). Hakusema, “Mimi ni nuru ya Wabaptisti au WaPresbiterian au 55
WaMethodisti”. Hakusema, “Mimi ni nuru ya waliolelewa vema au
waliosoma vizuri au waliolishwa vizuri”. Angeweza kusema,
“Mungu aliwapenda sana Wayahudi” lakini hakufanya hivyo.
Alisema, “Mungu aliipenda sana dunia” (ktk Yohana 3:16). Yesu
alikazia tena na tena kwamba hakuwa na mpango wa kufikia
kisehemu kidogo au watu wachache – mpango Wake ulikuwa ni
dunia nzima. Yeye ndiye nuru pekee ya kiroho kwa ajili ya kila nchi
na kwa ajili ya kila mtu aliyeko katika kila nchi duniani.
Inasemekana kwamba askari wa jeshi la Napoleon walikuwa
wanabeba ramani ya dunia katika mikoba yao, pamoja na bendera ya
Ufaransa. Walikuwa ni wafungwa, mateka, watumwa wa wazo la
kuiteka dunia kwa ajili ya Ufaransa. Enyi ndugu zangu Wakristo na
dada zangu – Bwana wetu Mwenyezi ameweka maono yanayowaka
ya dunia nzima mbele ya macho ya watu Wake na amewaomba kila
mmoja kuyaruhusu yawake mpaka yachome moyo. Na haya maono
yanapaswa kushika mawazo yetu kila wakati, mipango yetu, ndoto
zetu, shughuli zetu kwa muda wote tunaoshi. Mara maono
yatakapoanza kutushika, tutatambua kwamba Yesu aliweka mpango
kwa ajili yetu – wewe na mimi kama watu binafsi – ili kutekeleza na
kukamilisha maono yenyewe. Kufanya wanafunzi wenye maono
ndiyo hilo! Unalionaje hilo?
Hebu tafakari swali hili kwa moyo wako wote. Je, Biblia na
Ukristo vilitokea katika jimbo mojawapo kati ya majimbo hamsini ya
Marekani? Hapana. Ukristo uliingizwa Marekani. Yesu hakuzaliwa 56
nyumba ya jirani na kwetu, wala katika mtaa wetu. Biblia haikuwa
imeandikwa kwa Kiingereza au Kiswahili tangu mwanzo. Sisi
Wakristo wa Tanzania (au wa Afrika) ni matokeo ya wamishenari
Wakristo. Je, na sisi tumejitoa kufanya katika sehemu zingine za
dunia yale ambayo hawa wamishenari walitutendea sisi? Kama
ungekuwa mmojawapo wa waliopotea katika Bara la Asia, Afrika au
Marekani ya Latin, ungetamani mtu akuletee ujumbe wa Nuru na
Uzima? Hakika sisi Wakristo wenye ubinafsi na wenye kujali zaidi
taasisi na “makanisa ya kujikimu” lazima tutubu hasa na kuomba
huruma na msamaha wa Bwana wetu, kwa sababu tumejaribu
kumfanya Yeye kuwa mali yetu (kama Wayahudi walivyofanya)
badala ya kuruhusu atutawale na kutumiliki kabisa. Na toba yetu
lazima iwe ya kiwango cha ndani sana kiasi cha kufikia mahali pa
kusahihisha hii hali ya “Ukristo wa kibinadamu” (neno langu,
ambalo hata hivyo linapingana katika maana yake).
Ndugu John Oxenham katika kitabu chake kiitwacho Bees in
Amber, aliandika hivi:
Nasikia sauti dhahiri kabisa ikiita, ikiita,
Inaita wakati wa usiku, hivi:
Enyi mnaoishi katika Nuru ya Uzima,
Tuleteeni na sisi hiyo nuru!
Tumefungwa katika minyororo ya giza,
Macho yetu hayapati kuona,
Enyi ambao hamjawahi kufungwa wala kuwa vipofu,57
Tuleteeni nuru!
Haiwezekani – hamwezi kutusahau,
Sisi tulioko katika usiku wa giza kuu zaidi,
Sisi ni watu tunaozama, sisi ni watu tunaokufa,
Tuleteeni – Jamani, tuleteeni Nuru!
Sasa Mkristo, usije ukaanza kutafuta maandiko ya kunipinga
au ya kuthibitisha kwamba watu pasipo Mungu wamekufa na
hawawezi kusema hivyo! Najua hayo yote – amini hivyo! Hivyo
sivyo watu wasiomcha Mungu wanavyoishi, wanavyofikiri au
wanavyozungumza – lakini, ndivyo kila aaminiye anavyotakiwa
kufikiri! Hatuwezi kuwaeleza watu waliokufa habari za kifo, wala
hatuwezi kutazamia dalili za uhai, matendo na maneno kutoka kwao.
Wala hatupaswi kuwatazamia wao kufufuka toka kwa wafu pasipo
kuisikia sauti inayofufua wafu! Warumi 10 inaweka wazi kabisa
kwamba, hakuna tangazo kwa waliopotea pasipo waliotumwa ili
kutangaza ujumbe. Hakuna kusikia bila tangazo, hakuna imani
pasipo kusikia, na hakuna wokovu pasipo imani (ktk Warumi 10:12-
17)! Katika uhalisi, mambo yanaanzia wapi? Kwenye kutuma na
kwenye kusema! Je, kanisa lenu liko katika shughuli ya kutuma? Je,
linatumia fedha ili kutuma ili ujumbe uweze kusemwa? Uchaguzi
pekee ni kutokutii amri ya Mfalme wa Wafalme na Bwana wa
Mabwana. Je, tutajisikiaje na tutafikiri nini tutakapohudhuria mbele
ya Kiti cha Hukumu cha Kristo kama tulitumia huduma zetu
58
tukikazia wale “Nyuki Wanaoua” – majengo, bajeti, miili,
vipeperushi, majigambo, na kadhalika?
Kabla ya karne iliyopita kufika katikati, Charles Kingsley
alitembelea visiwa vya New Hebrides huko Bahari ya Pacific ya
Kusini na kushangazwa na ukatili na ulaji watu vilivyokuwepo.
Aliporudi Uingereza aliandika makala kali iliyosema kwamba
serikali ya Uingereza ingefanya huduma muhimu sana kwa binadamu
kama wangetuma merikebu ya vita ili kuwaangamiza hao “washenzi”
waishie baharini kama nzi wasumbufu, kwa kuwa hawakuwa
binadamu na hakuna kitu ambacho kingeweza kufanyika ili
kuwainua kutoka kiwango walichokuwa nacho.
Lakini, walikuwepo watu wengine ambao hawakukubaliana
kabisa na tathmini ya Kingsley. Miongoni mwao alikuwepo Mkristo
aliyempenda Mungu sana, jina lake John Paton kutoka Dumfries,
Uskochi. Paton aliamini kwamba Injili ya Yesu ni nguvu ya Mungu
iletayo wokovu (ktk Warumi 1:16), na kwamba Injili ina nguvu za
kuhuisha, kuwafufua wale waliokufa katika dhambi (ktk Waefeso
2:1). Baada ya safari ndefu, Paton alifika kisiwa cha Tana huko New
Hebrides, na akiwa hatarini daima ya kuuawa, alimhubiri Kristo kwa
hao watu. Namwalika msomaji yeyote mwenye mashaka afanye
utafiti wa matokeo yeye mwenyewe. Paton alipokufa, wenyeji wa
kule walitengeneza kumbukumbu juu ya kaburi yake, iliyokuwa
imeandikwa hivi: “Alipokuja, hapakuwa na nuru. Alipokufa,
hapakuwa na giza”. Wapendwa – leo hii tunaweza kupenyeza kwa 59
urahisi katika dunia nzima, kwa gharama ndogo kabisa na matatizo
madogo tu ya usafiri. “Tumeketi” juu ya rasilmali kubwa sana
ambazo zingeweza kutumika kwa ajili ya kuwainjilisha na
kuwafanya wengi sana kuwa wanafunzi hapa duniani. Maelfu ya
Wakristo, makanisa, na watu waliopotea wangekaribisha na kuitikia
upendo wetu katika nchi za karibu na mbali, nasi mara nyingi
tunaketi tu katika hali ya kujidanganya katika makanisa yaliyokufa
na yanayokufa mahali tulipo. “Mahali ambapo hakuna maono, watu
huangamia.”
Siku ile ile Bandari ya Pearl Harbor iliposhambuliwa na
madege ya kivita ya Japani, mishenari aliyerudi kutoka Mashariki ya
Mbali alikutana na rafiki yake ambaye alikuwa hamwungi mkono
katika anachofanya, naye akimtazama kwa jicho la kejeli na
kuzungumza kwa sauti ya dharau alisema, “Ehe! Unasemaje kuhusu
WaJapani wako sasa?” Yule mishenari akamjibu kwa upole na
utaratibu, na kwa ujasiri kabisa, kana kwamba anamchoma upanga,
“Nashukuru. WaJapani wangu hawajambo, wametulia katika neema
ya Mungu. Kama unazungumza juu ya wale waliopiga mabomu meli
za KiMarekani, hao ni WaJapani wako – wale ambao wewe
unawajibika nao, lakini hukufanya chochote juu yao. Wao ndiyo
wenye kuleta matatizo yote hayo. Lakini WaJapani wangu
wanaendelea vizuri tu, wakidumu katika kumtumaini Bwana Yesu
Kristo”. Wapendwa – vipi kuhusu WaBrazili “wetu”, au WaZaramo,
au WaFipa, au WaDigo, n.k.? Vipi kuhusu WaRundi “wetu”, 60
WaNyarwanda “wetu”, WaKongo “wetu” na kadhalika? Ndugu
aitwaye Frank Laubach alisema hivi: “Kama Marekani wangetumia
fedha nyingi kwa ajili ya umisheni Japani kabla ya Vita Kuu ya Pili
ya Dunia kama zilizotumiwa kujenga merikebu moja ya kivita kati ya
zile zilizozamishwa hapo Pearl Harbour, pengine hiyo vita
isingetokea kabisa.” Je, wewe unajihusisha kwa namna yoyote katika
kuigusa dunia? Je, unakwenda kama aliyetumwa ili kumfanya Kristo
ajulikane? Kama hapana, ni kwa nini?
William James ambaye ni mwanasaikolojia wa Chuo Kikuu
cha Harvard Marekani, aliandika juu ya nyumba aliyoishi huko
Chocorua, jimboni New Hampshire akiwa mtoto mdogo. “Aah! Ni
nyumba ya kupendeza sana katika nyumba ulizowahi kuona. Ina
milango kumi na nne, na yote inafunguka kuelekea nje.” Ile kanuni
ya usalama inayowekwa na serikali za mitaa kuhusu majengo yetu ya
kanisa inazungumza mengi sana yenye hekima kwetu sisi. Mkristo,
kanisa, maono yanayomshika mtu, yenye kufanya kazi na milango
yote ikifunguka kuelekea nje ni kitu “cha kupendeza sana”, lakini
kwa kweli, Mkristo mwenye kutazama ndani tu, na kanisa lenye
kutazama ndani tu, inatakiwa liwe likiwa hai na ile hali yake ya
kukata tamaa, kuchanganyikiwa, kushindwa kufanikiwa, na
kushindwa kabisa!
Dunia yetu imekuwa ikipungua ukubwa kama puto ambalo
halina upepo. Ndege siku hizi zinakwenda kasi kiasi cha
kumwezesha mtu asafiri mapema asubuhi kutoka London hadi New 61
York. Sijawahi kusafiri nchi za ng’ambo bila ya kukutana na idadi
kubwa tu ya wasafiri wenye kuzunguka dunia. Sauti inayonaswa kwa
redio inasikika upande wa pili wa dunia haraka sana kuliko
inavyosikika mwisho wa chumba ambapo maneno yake yanatamkwa.
Tukio linalorekodiwa na televisheni huonekana nchi za mbali wakati
huo huo linapotokea. Tunaishi katika chumba cha mbele cha dunia.
Dunia nzima imekuwa ujirani mdogo tu. Je, tunafanya nini kuhusu
jirani zetu?
[USHUHUDA WA MWANDISHI – Natazama nyuma
kwenye kanisa langu la mwisho nililochunga kwa miaka kumi, na
kujaribu kukumbuka njia tulizotumia ili kutengeneza maono ya dunia
na mguso wa dunia kwa washirika wetu.
(1) Tulitumia mpango tuliouita “weka akiba chenji yako”.
Kila mshirika alitiwa moyo kila mwisho wa kila siku kutoa chenji
yote iliyokuwa imebaki mfukoni na kuitenga kwa ajili ya umisheni,
ila abakize noti moja (au sarafu basi) ya kila kiwango. Mwezi
Desemba, tulifanya “maandamano ya umisheni” na katika hayo
tuliweka sadaka hizo zote mbele za Bwana kwamba aziongeze kwa
ajili ya kufikia mwisho wa dunia.
(2) Tulitumia mpango tuliouita “Dola Moja Kwa Juma Kwa
Ajili Ya Umisheni”. Tulimwomba kila mshirika atoe dola moja zaidi
kwa juma kwa ajili ya umisheni wa kuifikia dunia. (Mmarekani gani
ataona amepoteza kitu?)
62
(3) Tulitumia mpango wa “Kamati Ya Umisheni Inayotenda
Kazi”. Tuliwachagua washirika wenye maono na roho ya umisheni,
na kuwaomba “waweke dunia mbele yetu” daima. Tulitenga ibada
kila baada ya miezi mitatu kwa ajili ya kukazia umisheni – na
wasemaji walikuwa wamishenari (na wake zao na watoto wao), na
kusoma barua za wamishenari, maombi maalum kwa ajili ya
wamishenari “wetu”, na kadhalika.
(4) Tulitumia mpango wa “nyumba ya umisheni”. Tulikuwa
na nyumba mbili ambazo tulizitumia kuwaweka wamishenari
waliokuwa wamerudi nyumbani kupumzika na tukawaomba
“wajaze” kanisa letu kwa habari walizo nazo na ushawishi walio
nao.
(5) Tulitumia mpango wa “kutafiti dunia yetu”. Tuliomba
taarifa za kijiografia, kisiasa, kiuchumi na kadhalika kuhusu mataifa
mengi ya dunia. Sana sana tulijitahidi kujifunza kuhusu maeneo
“yaliyoiva”, yaani, ambayo yanaitikia zaidi Injili.
Katika kufafanua, tulitumia hoja kama hii. Tuseme kwamba
una shamba la matunda. Katika eneo A, mtenda kazi angevuna ndoo
tano kwa saa. Katika eneo B, kuvuna ndoo moja kunaweza kuchukua
masaa matano. Katika eneo C, hakuna cha kuvuna kwa sababu
matunda bado mabichi. Kama una wafanya kazi thelathini leo,
ungewatuma wapi? Nadhani ningetuma ishirini na tisa kwenda eneo
A ili nisipoteze matunda pale. Halafu yule mmoja ningemtuma eneo
B akafanye kinachowezekana hao, na pia kutazama eneo C. Wajibu 63
wa huyu mmoja ungekuwa kunijulisha wakati hayo maeneo mengine
yameiva ili niweze kuwapanga upya wale watenda kazi. Yesu alijiita
“Bwana wa Mavuno” (ktk Mathayo 9:39). Je, hajasimamia vizuri
kazi Yake? Hapana kabisa, ila – kama kawaida – watenda kazi Wake
hawajamsikiliza Yeye. Je, WEWE umekuwa ukimwomba Bwana wa
mavuno kwamba “apelike watenda kazi katika mavuno Yake”?
Kumbuka hivi: “Shamba ni dunia nzima” (ktk Mathayo 13:38).
(6) Tulitumia mpango wa “tuma mishenari”. Mimi kama
mchungaji ningetoshekaje kama Mungu angekuwa hawaiti vijana
kutoka kanisani kwangu au katika eneo langu la ushawishi kwenda
kufanya umishenari katika vituo mbalimbali duniani? Hakika
ningekuwa na mashaka na huduma yangu. Hivi karibuni tulikuwa na
mgeni nyumbani kwetu ambaye amerudi kutoka Mashariki ya Mbali
(katika nchi “iliyofungwa”). Karudi nyumbani kwa muda mfupi tu ili
atafute misaada zaidi na kuongezea ujuzi wake wa kufundisha ili
aweze kuwa “mishenari wa kawaida” (ambayo ni kichekesho maana
maono ya umisheni yamemtawala kabisa!) katika hiyo nchi
anayohudumia. Kiasi cha mwaka mmoja uliopita, alihusika sana na
kumleta kijana mmoja kwa Kristo na kumfanya mwanafunzi, na
tayari, huyo kijana amekwisha leta kumi wengine kwa Kristo – katika
nchi “iliyofungwa”! Huyu “mishenari” alimaliza chuo kikuu akiwa
na shahada ya ufundi umeme, kisha akarudi chuoni tena baada ya
miaka minne jeshini ili kujifunza sayansi ya kompyuta kusudi aweze
kupata nafasi ya kufundisha katika chuo kikuu cha nchi hiyo hiyo 64
Mashariki ya Mbali. Ninapoandika maneno haya, amerudi tena
nyumbani, akiboresha taaluma yake ya kompyuta na ujuzi ili awe
mwalimu bora wa chuo kikuu. Kwa nini? Kwa sababu amepata
maono ya kufanya wanafunzi yenye kuigusa dunia. Aliniambia tena
juu ya safari yake katika mpango wa kufanya watu kuwa wanafunzi
(na jinsi anavyoshukuru) pamoja na kuambukizwa maono ya kuigusa
dunia yaliyokuwepo katika kanisa nililokuwa nalichunga.
(7) Tulitumia mpango wa “kutuma wamishenari wa muda”.
Sasa hivi dunia iko wazi kwa ajili ya upenyo wa umisheni wa muda
wa vikundi vidogo vidogo vya watu kutoka makanisa mbalimbali ya
nchi za Nje. Bado mlango wa dunia uko wazi. Mto wa kudumu wa
Wakristo wanaokua, wenye furaha, waliohamasika, wenye kugusa
dunia, unapaswa kuwa ukielekea kwenye maeneo mbalimbali hadi
miisho ya dunia. Baadhi ya “makanisa makubwa” yanapaswa kuwa
yanatuma haidhuru watu 200 hadi 500 kila mwaka kwenda kwenye
miradi ya umisheni ya kuzunguka dunia. Mimi binafsi nimehusika
katika safari kubwa zaidi mia moja za kimisheni huku nikiendelea na
ratiba yangu nzito kabisa nyumbani. Hivi karibuni, mlei mmoja
aliyekuwa anatembelea mji wetu aliniambia hivi: “Ningeogopa sana
kwenda nchi yoyote nje ya Marekani”. Kuogopa? Hilo halipaswi
kukaa katika akili ya Mkristo aina yoyote. Hebu jisomee 2Wakor.
11:23-33, uone ni hofu kiasi gani iliyotawala maisha ya Mtume
Paulo. Cha kusikitisha ni kwamba, rafiki yangu alikuwa anakiri
kushindwa kwa kanisa lake kumwingizia Agizo la Kristo.65
(8) Tulitumia mpango wa “jifunze dini za ulimwengu”. Huu
unajieleza wenyewe, na kila ilipowezekana, tulitafuta kusikia
shuhuda kutoka kwa watu waliokuwa wahusika katika dini zingine,
wakaokoka.
(9) Tulitumia mpango wa “onyesha umisheni”. Wakati Agizo
Kuu linapolipuka katika akili ya mchungaji, kwamba ni nguvu ya
Injili, hakika atawashirikisha watu wake jambo hilo katika kila
nafasi. Atajifunza mahusiano ya kila itikadi kwa mpango huu.
“atatoa damu” ya mkazo huo katika kila mahubiri na kila nafasi
anayopata ya kutangaza Injili. Atawafanya watu wake wajue
kujitolea kwa umisheni kwa waaminio wenye maono. Yeye
mwenyewe atakwenda kwenye maeneo mengi ya umisheni kiasi
anachoweza, na kuwachukua ndugu zake Wakristo wengi kiasi
anachoweza, ili waende naye. MWISHO WA USHUHUDA]
Ewe Mkristo – je, “unaota ndoto” na “kuona maono” kuhusu
kuifikia dunia? Kwa Kiyunani – “ta ethne” – makundi yote ya watu,
mataifa yote – ng’ambo ya barabara na duniani kote. Je, Mungu
amekuvamia kwa “Shambulizi la Ramani” – ili “ubebe” dunia nzima
kwa ajili Yake? Je, unafuata mkakati wa Mwokozi, au umekubaliana
na mbadala wa kijanja sana wa Shetani?
Kongamano kuhusu Kristo na kazi Yake ya ukombozi
liitwalo “Summit III” lilifanyika mjini Chicago mwezi Desemba
mwaka wa 1986. Dakta Ralph Winter, ambaye ni Mkurugenzi Mkuu
wa Kituo cha Marekani cha Umisheni Duniani, alihudhuria. 66
Mwishoni mwa kongamano, yeye alikuwa miongoni mwa watu
wawili waliotakiwa kutoa maitikio yao kuhusu kiini na mambo
yaliyosemwa. Katika itikio lake, Dakta Winter alionyesha kwamba
maelezo yote hayakuwa yamegusia kazi ya Wakristo na Kanisa ya
kumshuhudia Kristo na kazi Yake kwa dunia. Yaani, wajibu wa
waaamini kushuhudia dunia haukuwa umetajwa.
Baada ya majibu yake, mwenyekiti wa kikao ambaye naye ni
Mkristo msomi maarufu na anayejulikana sana, alimtazama Dakta
Winter kwa macho ya kejeli na kusema, “Sawa. Tulipaswa kujua
kwamba ungetaja kitu kuhusu jambo lako unalopenda sana, ukipewa
nafasi.” Swali: Je, kuigusa dunia ni jambo wanalopenda mashabiki
wachache tu wenye mzigo, au linapaswa kuwa mapigo ya moyo wa
kila – KILA – Mkristo? Hivi kweli tunaweza kukiri kwamba Yesu
Kristo ni Bwana na wakati huo huo tupuuze wajibu pekee aliotupa
sisi kama amri ya kusonga mbele? Zaidi – je, kundi lolote la
Wakristo linaweza kujadili kwa usahihi au inavyotakiwa Nafsi na
Kazi ya Kristo bila ya kutaja kuhusu mkazo Wake kwa dunia nzima?
Ni kitu kinachotupasa sisi kutafakari maswali hayo mpaka mwisho
kabisa, kwenye kupata jibu lenye kuridhisha. Ukweli ni kwamba kila
Mkristo anapaswa kuwa Mkristo wa dunia nzima. Yeye anapaswa
kuwajibika kuwa”ambukiza” wengine, kuombea wamishenari,
maeneo ya umisheni, na Wakristo wengine, anapaswa kuivamia
dunia, anapaswa kupata na kutawanya habari, na kwa njia hiyo
67
kumkaribisha Mungu aongeze maisha yake kwa ajili ya kuifikia
dunia.
Rafiki zangu, dunia inawaka moto – moto wa mabadiliko,
vurugu, hofu, mapinduzi, fujo, vita – mambo yanayofaa kabisa kwa
ajili ya Injili. “Mapinduzi kila dakika” yanatokea. “Je, si kitu kwenu,
enyi wote mnaopita tu?”
Hadithi moja maarufu sana katika kitabu cha Washington
Irving kiitwacho Sketch Book ni ya mtu aliyeitwa Rip van Winkle.
Huyu jamaa alilala usingizi wa miaka ishirini – ili aepukane na hali
yake ya kutokuwa na faida, uzembe, pamoja na mke aliyekuwa
mkorofi. Alipopata usingizi na kulala, jimbo lake la New York
lilikuwa koloni la Uingereza, lililokuwa linapigania haki na uhuru wa
watu kujitawala ili kupinga ukandamizaji. Lakini, “ukandamizaji
mkubwa” ule haukumsumbua Rip, uliokuwa unamsumbua ni ule
mdogo, wa mahali pamoja, wenye ubinafsi wa nyumbani kwake.
Lakini kwa kulala mara moja tu na kwa muda mrefu, Rip
alikombolewa kutoka ukandamizaji wote. Ee Mkristo, unasikiliza
hilo? Hadithi hii ya Rip ni mfano uliofichika. Wachungaji
wanateseka kutokana na ukandamizaji mdogo, wa mahali pamoja, na
mara nyingi huingia katika usingizi uletwao na “dawa” (hakuna
maono, hakuna nguvu, hakuna kuigusa dunia) kiasi kwamba wala
hawana habari na ukandamizaji wa duniani, ambao ni utawala wa
nguvu juu ya dunia nzima unaofanywa na Shetani (ktk 1Yohana
5:19b). Sasa, ikawaje katika hadithi? Rip akalala usingizi mzito, na 68
hakuamka mpaka baada ya miaka ishirini. Akiwa amelala, vita ya
Kimapinduzi ikapiganwa. Rip alipokwenda kulala, alikuwa
anatawaliwa na George wa Tatu wa Uingereza – mfalme.
Alipoamka, alikuwa anaishi katika jamhuri ya kidemokrasia, na
George mwingine – Jemadari George Washington – alikuwa
anajiandaa kutawala. Rip Van Winkle alifunga macho yake na kulala
wakati wa mapinduzi! Je, Mkristo, unasikia hilo? Mtu hawezi kujua
anachokosa akiwa amelala. Ndiyo maana Shetani anataka wewe
ujione mwenyewe – utazame kujisikia hatia kwako, ujali maombi
yako, kusoma Biblia kwako, imani yako tu, ushuhuda wako tu,
uaminifu wako tu, huduma yako tu, kanisa lako tu, dhambi zako tu,
hofu zako tu – Ukristo wa kibinadamu, wenye kutafuta kujikimu.
Amka ewe Mkristo, umtazame Mwokozi wako, utazame Biblia yako,
utazame dunia yako, utazame nafasi na fursa ulizo nazo kupitia
macho mapya kabisa!
Mbadala Wa Shetani
Turudi kwenye hoja yetu ya tatu kuhusu Agizo, katika
Mathayo 28:18-20. Tumekuwa tukitazama kwa upana sana mkakati
wa Mwokozi chini ya kichwa hiki: “Panua Maono Yako”. Sasa, hebu
kwa kifupi tutazame mbadala anaotoa Shetani hapa. Daima Shetani
anarudisha usikivu wetu kwenye mapambano yetu sisi, kujikimu
kwetu, taasisi ya mahali ambapo tunatumika (na mafanikio yake), na
kadhalika. Daima anatafuta kupunguza maono yetu yawe kitu cha 69
kawaida, yaendane na taasisi yetu au ubinafsi wetu, na kwa njia hiyo
wingi wa watu duniani wasipate nafasi ya kusikia hata habari za
Kristo na Injili. Yesu alitupa mpango wa kuigusa dunia nzima, lakini
tunakubali kupokea mbadala mdogo, wenye kupotosha, na usiozaa
matunda aina yoyote. Je, wewe unafuata mpango gani, mkakati wa
Mwokozi ambao kwa huo, wewe – naam, WEWE – unaweza kuifikia
na kuigusa dunia, au mbadala wa Shetani wenye kufanikisha
punguzo linalodumu la jamii ya Kikristo na kuhakikisha kwamba
mabilioni ya watu watapotea pasipo kupata habari?
4. KUWASHUHUDIA WAHUSIKA
Hoja ya nne katika Agizo Kuu ni Kuwashuhudia Wahusika.
Agizo Kuu lina maneno saba ambayo ni matendo, lakini amri pekee
ni “kuwafanya watu kuwa wanafunzi”. Katika fungu zima (Mathayo
28:16-20), neno tendaji pekee ni hilo – “kuwafanya watu kuwa
wanafunzi”. “Uinjilisti” huu ni wa aina fulani maalum – si kupata
watu “watakaokata shauri kumfuata Kristo” bali ni kupata
“wanafunzi”watakaoipindua dunia.
Mkakati Wa Mwokozi
Fikiri jambo hili kwa makini sana: Kwa kuwa ni amri ya
Yesu – Agizo Lake pekee kwa Kanisa Lake kwamba Lisonge Mbele
– bila shaka haiwezekani kuwa mwanafunzi wa kweli kama hufanyi
watu kuwa wanafunzi – kulingana na matakwa Yake na mkakati 70
Wake. Kipengele hiki cha “kufanya wanafunzi” si nyongeza kwenye
mpango wa Yesu, bali ndiyo amri yenyewe. Swala si kupata
“waongofu” bali ni kupata “wanafunzi”. Basi, mkakati wa Mwokozi
hapa si kuokoa roho za watu tu, bali ni kufanya watu kuwa
wanafunzi. Maana yake ni kwamba, kile ambacho Yesu alifanya kwa
wanafunzi Wake Mwenyewe, aliwaagiza nao wakafanye kwa
wengine. Walipaswa kutenda mkakati ule ule, nidhamu zile zile, na
taratibu zile zile kwa wengine, ambazo Yesu Mwenyewe alikuwa
amezitumia kwao. Rafiki yangu mpendwa: Hebu soma fungu hili lote
polepole, kwa makini sana, na katika hali ya maombi mara kadhaa
kabla ya kuendelea mbele. Tutalitazama neno ”mwanafunzi” kwa
upana zaidi hapo baadaye.
Mbadala Wa Shetani
Nini mpango mbadala wa Shetani kuhusu kufanya watu kuwa
wanafunzi? Sehemu moja ya mpango wake ni kuhakikisha kwamba
waliopotea wanaendelea kupotea, au, kuwazuia kuokoka. Sehemu ya
pili ni kuwazuia waaminio kuwa wanafunzi wenye maono ya dunia
yote, na wanaotaka kuigusa dunia yote. Au basi, kama waaminio
wakiwa wanafunzi, kusudi la Shetani ni kuwafanya wawe wanafunzi
wa wazo lao wanalopenda tu, au utaratibu wao wanaopenda tu –
mradi kitu chochote ili kuwazuia wasiwe wanafunzi wa kweli,
wanaofanana na Kristo, kama inavyotakiwa na Agano Jipya.
71
5. KUWAHUSISHA WALIOSHUHUDIWA
Hoja ya tano katika Agizo Kuu ni Kuwahusisha
Walioshuhudiwa. “Mkiwabatiza katika jina la Baba, na Mwana, na
Roho Mtakatifu”.
Mkakati Wa Mwokozi
Mkakati wa Mwokozi kwa ajili ya kila aaminiye ni
kujitambulisha na Yesu Kristo kwa njia yenye kudhihirisha kifo kwa
kila kitu ambacho huyo mwamini aliishi kwa ajili yake kabla ya
hapo, na ufufuo wenye kumaanisha kwamba sasa anamwishia Kristo
tu. Kwa kubatizwa, amwaminiye Kristo anakiri kufia wakati wake
uliopita – dhambi zake za zamani, ubinafsi wake wa zamani, motisha
yake ya zamani, mtindo wake wa maisha wa zamani, jinsi
alivyokuwa anafikiri zamani – wakati wake wote wa zamani, na
anakubali kwamba sasa ana lengo na kusudi moja tu la maisha –
Kusudi lenye kutawala kila kitu na kumwishia Huyo Yesu Kristo
mtukufu. Ubatizo ni kuingia katika kaburi la maji, ambayo ni picha
ya kuingia katika kifo cha Kristo, na kufufuka tena kutoka kaburini
humo, ambayo ni picha ya kushiriki pamoja na Kristo katika
kufufuka Kwake. Basi, ubatizo hudhihirisha kujiunga kikamilifu
kabisa na kuhusika kikamilifu kabisa katika uanafunzi wa Kikristo.
Ukweli kwamba unafanywa “katika jina la Baba, na Mwana, na
Roho Mtakatifu” maana yake ni kwamba mwamini huyo anaingizwa
katika kuhusika kikamilifu katika Mpango kamili na Nafsi ya 72
Mungu. Hakuna kitakachohifadhiwa katika maisha ya mtu kwa ajili
ya makusudi yake mwenyewe. Kifo kimefutilia mbali uwezekano
huo. Ufufuo umesababisha mwelekeo mwingine kabisa kwa ajili ya
maisha yake. Sasa, kila rasilmali na uwezo ulioko katika nafsi yake
iko kwa ajili ya Bwana Yesu Kristo.
Mbadala Wa Shetani
Katika hoja hii ya Agizo Kuu, nini mbadala anaotoa Shetani?
Shetani anatafuta kusukuma mawazo ya wanadamu kwenye sehemu
mbili, ambazo zote ni zaidi ya kawaida. Kwa upande mmoja,
anasema ubatizo ni zoezi la kimwili, lisilofanya chochote rohoni, na
ambalo ni taratibu tu. Basi, halina maana yoyote. Kwa hiyo – kwa
mfano – dhehebu la Quakers halibatizi kabisa watu – kwa sababu
hiyo. Kwa upande wa pili, Shetani analeta wazo kwamba ubatizo ni
muhimu sana kuliko kitu chochote, na kwamba wenye dhambi
hawawezi kuwa na uzima wa milele wasipobatizwa. Basi – kwa
mfano – madhehebu mengi tu yanafanya ubatizo kuwa ndiyo jiwe
kuu la pembeni kwa habari ya wokovu. Hapo katikati, kuna
wanaoshikilia wazo dhaifu kabisa kwamba ubatizo ni “ishara tu – ni
mfano” – kama makanisa mengi, pamoja na WaBaptisti.
Mwanamume mmoja alifika kazini siku moja akiwa
amevimba macho na uso mzima. Mwenzake wanayefanya pamoja
akamwuliza, “Vipi? Ulipatwa na nini?” Jibu likatoka, kwa sauti
ndogo sana, “Mke wangu alinipiga”. Yule mwenzake akasema, 73
“Unataka kuniambia uliruhusu mwanamke tu akutendee hayo?”
Jamaa alijibu hivi, “We! Mke wangu si ‘mwanamke tu’!” Wapendwa
– tunaposema kwamba agizo lolote la Yesu ni “mfano tu”, si
tunaunga mkono upande mbadala wa Shetani? Hakuna chochote
alichowahi kusema Yesu ambacho ni “kitu tu”! Je, umeona ukubwa
wa kuungana kwako na Yesu Kristo na kuhusika kwako na Yesu
Kristo?
6. KUWAELIMISHA NA KUWAJENGA WALIOJIUNGA
Hoja ya sita katika Agizo Kuu ni Kuwaelimisha na
Kuwajenga wote waliojiunga. “Mkiwafundisha kuyashika (kutii)
yote niliyowaagiza ninyi.” Hapa tena, neno tendaji ndiyo
linalotangulia. Linaonyesha shughuli inayoendelea, ya kudumu,
isiyokoma, isiyokatizwa.
Mkakati Wa Mwokozi
Hakuna wakati wowote katika maisha yangu kama Mkristo
ambapo siwi katika kufundisha! Iwe ni kwa mfano wa makusudi,
kwa tamko la wazi, kwa kufuata mtaala ulioandaliwa, kwa ushawishi
wa kimya, katika hali iliyopangwa au isiyopangwa, mimi ninapaswa
kuwa mwasilishaji wa Yule ambaye ni uzima wangu. Kila aaminiye
anapaswa kuwa mwalimu, awe na karama ya kufundisha au asiwe
nayo. Njia za mawasiliano zilizoko leo ni nyingi mno na zenye
kutenda kazi vizuri kabisa kiasi kwamba Mkristo hana udhuru wa 74
aina yoyote wa kutokufundisha. Kuna kanda za sauti ambazo zina
kila aina ya mada ya Kikristo unayoweza kutaka, zilizoandaliwa na
wataalamu wa mawasiliano Wakristo wanaomcha Mungu. Kuna
mikanda ya video ya hali ya juu sana na yenye mada nzuri tu. Kuna
maktaba kubwa sana za vitabu ambavyo vinaweza kupatikana kwa
kuazima au kununua. Kuna chapisho mbalimbali zenye makala
nyingi tu za mafundisho, na kadhalika. Nyumba ya kila Mkristo
inapaswa kuwa ghala na kituo cha kusambaza vitu hivyo vya
kufundishia. Kila Kanisa la Kikristo linapaswa kuwa kituo cha
kusambaza kweli ya Injili, kwa kutumia kila mbinu iwezekanayo na
kila mwanachama apatikanaye ili kupenya na kuingia katika mioyo,
nyumba, jumuiya mbalimbali na kadhalika, kwa ajili ya kufikisha
kweli kamili ya Injili. Kila Mkristo anapaswa kuwa makini kwa ajili
ya kufanya watu kuwa wanafunzi na kufundisha jinsi ya kufanya
watu kuwa wanafunzi, bila kikomo. Maono ya dunia nzima na
huduma kwa dunia nzima vinapaswa kuwa mbele za kila Mkristo na
kila kanisa. Nini lengo la yote hayo? Ili kila Mkristo na kila kanisa
kupata moyoni mwake kile kilicho moyoni mwa Mungu – kugusa
dunia nzima kwa kuwajenga na kuwasambaza Wakristo wenye
maono ya dunia nzima, na watakaoigusa dunia yote.
Mbadala Wa Shetani
Shetani ana mbadala gani kwa mpango huu? Kwanza,
anatafuta kuzuia mafundisho yenye upako ya kweli kuu za Biblia. 75
Halafu anatafuta kuwafanya Wakristo “waonja mahubiri”. Kwa hali
hiyo, hawataathirika na Ukristo wa kweli kwa sababu wamepokea
chanjo ndogo tu. Au anawafanya waaminio kuwa wachambuzi na
wachuja ukweli, wakidhani kwamba wanaweza kupambanua na
kutambua ukweli pasipo msaada wa Roho Mtakatifu. Basi,
wanajifanya wakuu juu ya kweli na juu ya mwalimu afundishaye
kweli. Neno hupokonan katika Agano Jipya, yaani “utii”, maana
yake ni “kusikia chini ya,” na picha itokanayo na neno hilo ni mtu
anayesikiliza kweli ya Mungu akiwa kwenye hali ya kudumu ya
unyenyekevu. James M. Barrie alisema hivi: “Maisha ni somo moja
refu sana, la unyenyekevu”, na ni kweli kabisa hasa katika maisha ya
Kikristo. Lakini, mkakati wa Shetani ni kufutilia mbali uwezekano
huu wa kusikiliza kweli kwa unyenyekevu, na basi kumfanya
mwamini arudie maisha yake ya kujitawala mwenyewe, kwa kujijali
mwenyewe, na kujipa umuhimu.
Mpango wa Shetani kwa ajili ya mwamini uko wazi sana kwa
Mkristo msikivu na mwenye kutambua mambo. Hebu nitumie neno
lenye kuonyesha mwisho au hatima ya mpango wa Shetani. Ni neno
“kuning’iniza mbele ya”. Shetani anafurahi sana wakati aaminiye
anapokwenda kanisani Jumapili kwa Jumapili na kuruhusu kweli
ipite mbele yake bila kuifanyia chochote. Anapofanya hivyo mara ya
kwanza, bila kupokea kwa unyenyekevu kweli hiyo iingie katika
udongo laini wa moyo mnyenyekevu, mtii na wenye kusikia,
anakuwa amepuuza kweli hiyo. Ni rahisi kuona kwamba hiyo ndiyo 76
kawaida ya mshirika wa kawaida kanisani Jumapili kwa Jumapili,
juma baada ya juma, mwezi baada ya mwezi, na mwaka baada ya
mwaka. Amekwisha amini kwamba kuhudhuria kanisani na
kusikiliza mahubiri NDIYO maisha ya Kikristo. Jambo hilo
likiendelea hadi mtu asiweze kukubaliana na ukweli wenyewe kwa
unyenyekevu, kuvunjika na utii katika kuomba, Mungu huingia
katika hali hiyo na kumgeuzia msikilizaji kibao. Anakuwa “mkaa
kitini” asiye na uhai, asiye na nguvu, asiye na maono katika kanisa la
mahali. Anaweza kuleta matatizo kwa kanisa na mchungaji wake –
au asilete – kutegemeana na kiwango cha kujisikia hatia kwake juu
ya jinsi alivyo. Ni hivi: Watu waliokuwa wanakwenda kanisani kila
wakati na kila mara “wakaushika” ukweli ndiyo waliokuwa na hatia
ya mawazo ya kurudi nyuma na hatimaye dhambi isiyosameheka. Ni
wale Waandishi na Mafarisayo, watu waliokuwa bora sana na wenye
kushika dini sana katika siku zao (ona Mathayo 12). Kwa hiyo,
Shetani anataka sisi tuwe “Wakristo wa kwenye foleni ya chakula”,
ambao daima wanatazama na kupima ukweli, wenye kuchagua na
kuchukua kulingana na kweli zetu tunazopenda, na wahubiri wetu
tunaowapenda na mahubiri yetu tunayopenda. Basi, hoja ya sita
katika Agizo Kuu inabatilishwa kwa mkakati mbadala wa Shetani.
Ewe Mkristo – uko upande gani? Je, unafuata mkakati wa
Mwokozi kwa juhudi zote za roho yako yenye unyenyekevu, au
“unakanyaga na kuchafua nyua za Mungu” kama msikilizaji wa siku
77
zote ambaye hazai matunda kwa aina yoyote katika kutimiza Agizo
Kuu?
7. TUMTARAJIE KUTENDA KAZI
Hoja ya saba katika Agizo Kuu ni Kumtarajia Yesu Kristo
Kutenda Kazi. “Tazama, Mimi niko pamoja nanyi siku zote, hata
mwisho wa dunia”. Neno “tazama” ni baada ya neno “enendeni”.
Ahadi ya uwepo maalum wa Kristo katika mstari huu ni kwa wale tu
ambao wanatoa na kumimina maisha yao katika shughuli zote
zilizotajwa, ili kutimiza Agizo Kuu. Yaani, huwezi kudai kihalali
hiyo ahadi kama hufuati huo mpango. Hatutapata nguvu ya Agano
Jipya mpaka tutakapofuata taratibu za Agano Jipya. Basi, maombi
yetu mengi kwamba tupewe Roho Mtakatifu na nguvu Zake
yanapotea tu. Ni hivi: Tunataka hizo nguvu kwa ajili ya kitu gani?
Kwa nini tunaomba tujazwe Naye? Ni ili Mungu akubaliane na
mipango yetu? Au ni ili tukuze kujulikana kwetu? Au ni ili tupate
kiasi fulani cha mafanikio katika juhudi zetu kwa ajili Yake?
Usisahau jibu la Mungu kwa maombi ya yule mhubiri maarufu:
“Mwanangu! Huhitaji nguvu Zangu kwa mipango midogo kama
yako.”
Mkakati Wa Mwokozi
Nini mkakati wa Mwokozi? Kuhusika Yeye Mwenyewe
Binafsi katika kila juhudi za kila mtu mwenye kufanya watu kuwa 78
wanafunzi, na kumpaka maishani mwake na katika shughuli zake
kwa nguvu kuu za Roho Mtakatifu. Yesu alisema, “Na tazama, Mimi
Mwenyewe (neno hilo ni la mkazo sana) niko pamoja nanyi siku
zote, mpaka mwisho wa wakati.” Kila Mkristo ni mwakilishi
asiyefaa, asiyeweza, asiyetosheleza, asiye na nguvu wa Yesu Kristo,
kama hii ahadi haitimii. (Hiyo si ahadi tu, ni kitu halisi – ni ukweli).
Lakini kila mtu anayeanza katika kila eneo la utendaji anajua jinsi
ambavyo inatia moyo na kumwezesha sana wakati anapokuwepo
yule mtaalamu pamoja naye. Je, Yesu alimaanisha nini aliposema,
“Mimi Mwenyewe niko pamoja nanyi”? Alimaanisha kwamba
Uwepo halisi wa Yesu uko pamoja na yule mwenye kufanya
wengine kuwa wanafunzi. Roho Mtakatifu anaeleweka vizuri zaidi
kuwa ni “Nafsi nyingine” ya Yesu. Alimaanisha kwamba Uwepo wa
Yesu wa kudumu, unaokaa utakuwa pamoja na yule mwenye
kufanya watu kuwa wanafunzi. Hakuna wakati, hakuna hali, hakuna
mazingira ambapo mwenye kufanya wanafunzi ataishi katika
kutimiza Agizo la Kristo ambapo hatakuwa na Uwepo wa Mwana wa
Mungu Mfufuka, Mwenye Nguvu. Siku haitafika ambapo Bwana
Yesu hatakuwepo kwa nguvu nyingi sana katika maisha ya mtakatifu
Wake anayefanya watu kuwa wanafunzi. Alimaanisha kwamba
mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi anao Uwepo tendaji wa
Yesu pamoja naye wakati wote. Yesu hayuko nasi kama mwenzi
mkimya au asiyejulikana au asiyefanya chochote. Mstari wa mwisho
wa Injili ya Marko unasema kwamba “walikwenda na kuhubiri kila 79
mahali, Bwana akitenda kazi pamoja nao, na kulithibitisha Neno kwa
ishara” (ktk Marko 16:20, TLR). “Ishara” zinaweza kuwa za aina
mbalimbali na za hapa na pale, lakini Uwepo wa Yesu unadumu
wakati wote!
John Wesley White alisema hivi: “Ukijawa ‘enendeni
takatifu’, umejazwa na ‘Roho Mtakatifu’.” Mara nyingi watu
hutumia ahadi hii nje ya mantiki yake. Wakiwa katika mambo
magumu, wanautumia mstari huu kusema kwamba Bwana yuko
pamoja nao daima. Lakini, mstari huu si dawa kwa ajili ya nyakati
ngumu. Kuna mistari mingi sana katika Maandiko, ya kutumiwa kwa
kusudi hilo – si huu – isipokuwa kama wakati mgumu unatokana na
kutimiza Agizo Kuu. Huu mstari ni kwa ajili mwenye kufanya
wanafunzi. Yaani – kama utatamani mahali pa kumpata Yesu leo,
lazima utafute mahali ambapo wanafunzi wanazaliwa. Yeye hupita
kando ya makanisa mengi tu ambayo yanahubiri mahubiri (hata
mahubiri mazuri sana), mahali ambapo watu wanaomba (tena
maombi ya dhati kabisa), na mahali ambapo makundi yanakusanyika
(na yanaweza hata kuwa makundi makubwa sana) na kwenda Zake
kuthibitisha na kuweka upako juu ya mtu yeyote anayefanya
wanafunzi kulingana na utaratibu Wake wa Agano Jipya.
Je, ungependa kujua Yesu atahudhuria ibada wapi Jumapili
ijayo? Mtafute katika kanisa ambapo wanaandaliwa watu wenye
maono ya dunia, wenye kuigusa dunia ambao nao watazalisha
wengine wa aina hiyo. Kumbuka: Si “Wakristo wazuri” tu, kwa 80
sababu huo ni Ukristo wa kibinadamu. Yesu hahudhurii na kutia
mafuta makanisa mengi na maisha ya waamini wengi kwa sababu
moyoni mwao hawana kile kilichoko moyoni mwa Mungu,
“kuwafanya watu wote kuwa wanafunzi katika mataifa yote”. Kwa
upande mwingine, wakati Mungu anapoliona kanisa lenye kufanya
watu kuwa wanafunzi (kuwajenga wanafunzi kwa kufuata utaratibu
Wake na kwa kumtegemea Yeye Mwenyewe kikamilifu kabisa
katika shughuli hii), anajihusisha kikamilifu kabisa hapo. Anaingia
ndani, kulia, juu, chini na kwa kila njia anasisimka na kufurahia sana
jambo hilo – na anajiunga na kanisa hilo mara moja. Naye atakutana
na watu wa kanisani humo muda wote anaoweza kuwa hapo na
kufurahia.
Hatuhitaji uthibitisho mkubwa zaidi wa ukuu wa Agizo
kuliko kuona maneno ambayo Yesu alitanguliza na kufuatisha.
“Mimi nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” Halafu,
“Tazama, Mimi Mwenyewe niko pamoja nanyi siku zote, mpaka
ukamilifu wa dahari.” “Siku zote” – za hatari au usalama, siku za
kushindwa au za ushindi, za uhuru au kuzuiwa, za amani au za vita,
za kupanda au za kuvuna, za kujifunza au za utendaji. Hakuna siku
hata moja ambapo kweli hii haitatimia.
Wakati Fretyof Nansen, mgunduzi maarufu wa Norway
aliposafiri mwaka wa 1896 kwenda kutoboa theluji iliyoko kaskazini
mwa dunia ili kujifunza na kutafiti mwendo wa theluji hiyo, kila mtu
alijua ameingia kwenye shughuli ngumu na hatari. Alichukua idadi 81
kubwa tu ya njiwa wenye uwezo wa kusafiri kurudi alikotoka, na
kupeleka habari. Alipofika kila kituo kikubwa cha safari hiyo hatari,
alimwachilia njiwa mmoja akiwa na ujumbe mguuni. Kitabu cha Bibi
Nansen cha kumbukumbu nyumbani kilikuwa na maneno haya:
“Nilifurahi sana kila mara nilipomwona njiwa mmojawapo akiwa
ametua dirishani kwangu. Nilipomwona huyo ndege, nilijua kwamba
mume wangu yu hai na ananikumbuka.” Miaka elfu mbili na zaidi
iliyopita, Bwana Yesu Kristo aliyetukuzwa alimwachilia Njiwa wa
Mbinguni – Roho Mtakatifu – nafsi yake Nyingine – kuja duniani
Siku ile ya Pentekoste – kuachilia kwa Nguvu kamili ya Mungu kwa
ajili ya utimizwaji wa Mpango wa Mungu. Tunapomtii na kuona
utendaji wa Roho Wake mwenye nguvu, tunajua Yu hai na ni mzima,
na anatukumbuka, na yuko pamoja nasi akitenda kazi. Ni shauku
Yake na raha Yake kutenda hivyo wakati wote. Huo ndiyo mkakati
Wake.
Mbadala Wa Shetani
Nini mbadala wa kijanja wa Shetani hapa? Yeye hujaribu
kutupotosha ili tujenge taasisi na mambo mengine ambayo si ya
maana sana, na kwa njia hiyo kuondoa utendaji wa Roho Mtakatifu
pamoja nasi. Au, anajaribu kutushawishi kwamba tuko peke yetu
kabisa, wala hakuna anayesikia tunapoomba. Anajaribu kutufanya
tusiojua habari za Roho Mtakatifu, au kutomjali Yeye, na uwepo
82
wake na nguvu Zake, au kujishughulisha kutafuta ujuzi mbadala,
wenye kuwa na msingi wake juu yetu wenyewe.
Mpendwa Mkristo – unaangukia upande gani katika hili?
Agizo Kuu, au Kuacha Kukuu?
Tumelitazama Agizo ambalo linaamua wajibu au majukumu
yetu. Kumbuka, ndiyo amri ya kusonga mbele pekee aliyowahi kutoa
Bwana Yesu kwa Kanisa Lake. Lakini, Shetani siku zote anajaribu
kuupinga huo Mpango wa Mungu kwa kuhakikisha mpango wake
unatenda kazi. Popote ambapo Kanisa LINAPOTOSHWA na kuingia
katika ujenzi wa taasisi, au katika kujihifadhi, au katika kufanya
“Wakristo wazuri” tu, mkono wa Shetani ni wazi hapo. Kwa hali
hiyo, Agizo Kuu limekuwa “Kuacha Kukuu”. Jamani – wakati
haujafika turudishe Agizo Kuu mahali pake?
Nilifundisha somo hili kuhusu Agizo Kuu miaka kadhaa
iliyopita, katika darasa la wenye ndoa vijana. Mwishoni mwa somo,
mama mmoja kijana mwenye ndoa aliomba sala hii ambayo niliitoa
kwenye kanda baadaye.
Baba! Ninashukuru kwamba kuna mtu – mwanadamu –
mbinguni kwa ajili yetu wakati huu. Na kama YUPO na BADO ni
mwanadamu kweli, basi bila shaka anazo hisia za kibinadamu.
Anaweza kufurahia, kushukuru, kuumia na kuteseka. BILA SHAKA
MOYO WAKE UNASIKITIKA anapotafuta kuendeleza kazi Yake
hapa duniani, lakini anaona mwili Wake wa hapa duniani ukifuata
83
mkakati ambao ni KINYUME KABISA kwa kila hali, na ule mkakati
aliowapa wanafunzi Wake.
Je, ni Agizo Kuu au ni Kuacha Kukuu? Wakati haujafika
turudishe Agizo Kuu katika nafasi yake?
84
Sura Ya 3Wazo Lenye Kuamua Njia Tutakayotumia
“Mkawafanye watu kuwa wanafunzi ….” Mathayo 28:19
Kama kweli tunataka kuwa watii kabisa kwa Yesu Kristo na
kwa Agizo Lake Kuu, ni lazima tujilazamishe kuwa sahihi kabisa
katika kuelewa Agizo hilo. Hatuwezi kujiruhusu starehe ya ujinga au
kutokujua ipasavyo. Tunaishi kwa “kila neno litokalo kinywani mwa
Mungu” na hakuna mahali popote ambapo neno hilo linatufunga
kama kwa habari ya Agizo Kuu. Kwa kuwa amri pekee katika Agizo
hilo ni “kuwafanya watu kuwa wanafunzi”, maswali kadhaa muhimu
sana yanapaswa kuulizwa. La kwanza ni hili: Mwanafunzi ni mtu wa
namna gani? La pili ni, Nini maana ya kuwafanya watu kuwa
wanafunzi? Na la tatu ni hili: Tunafanyaje hilo? Siwezi kufikiri
maswali mengine ambayo ni muhimu kwa ajili ya kanisa la leo.
Vinginevyo, tunaendelea kufuata kwa ujinga kabisa “mbadala wa
Shetani” badala ya kutii mkakati wa Mwokozi.
Tumeona jinsi ambavyo maono ni muhimu kwa ajili ya
utendaji wa kiroho, na tumetazama kwa makini sana Agizo Kuu,
ambalo ndilo lenye kutupa sisi wajibu wetu. Sasa, tutachunguza
dhana au wazo lenye kuamua mbinu au njia tutakayotumia. Dhana ni
hiyo ya kufanya watu kuwa wanafunzi. Ili tuelewe dhana hiyo
kikamilifu kabisa, tunahitaji kuchunguza maneno yenye kuhusiana
85
nayo. Baadhi yake yanapatikana na yanatumika katika Biblia, na
baadhi yake yanatokana na maneno yanayotumika katika Biblia na
jinsi yanavyotumiwa.
KUFANYA WANAFUNZI
Dhana inayoamua njia yetu ni uanafunzi. Yesu aliamuru hivi:
“Wafanyeni watu kuwa wanafunzi.” Maneno kadhaa inabidi
tuyatazame vizuri sana.
MWANAFUNZI
Neno moja muhimu ni “mwanafunzi”. “Wanafunzi ni watu
wanaompendeza Bwana na watu watakaoifikia dunia. Basi,
kitambulisho dhahiri cha mwanafunzi ni muhimu. Kuelewa
mwanafunzi ni nini na mwanafunzi anafanya nini ndiyo mambo
makuu muhimu kwa ajili ya kanisa. Cha kushangaza katika kanisa ni
kwamba, tunalitumia neno ‘mwanafunzi’ ovyo ovyo tu kwa uhuru,
na mara nyingi pasipo kulifafanua. Hali hiyo ni sawa na kiwanda cha
viatu kujaribu kutengeneza kitu bila vipimo au kufuata masharti.
Kitakachotokea mwisho huko ni cha ajabu sana.” (Maneno ya Bill
Hull katika kitabu kiitwacho The Disciple Making Pastor, uk. Wa
54).
Neno hili “mwanafunzi” kwa bahati mbaya sana
limepunguzwa nguvu yake katika kanisa la kisasa. Inasemekana ni
“mwongofu” hadi kuwa “aaminiye mwenye kukiri”. Kwa kawaida, 86
“kufanya watu kuwa wanafunzi” hufafanuliwa kuwa ni “kuleta watu
kwa Kristo”. Kuleta watu kwa Kristo ni sehemu muhimu, sehemu ya
kwanza, sehemu ya lazima katika kufanya watu kuwa wanafunzi,
lakini ni mwanzo tu. Kama utaratibu mzima utakomea kwenye kuleta
watu kwa Kristo tu, mwenye dhambi mhusika “hajaletwa” kabisa.
Katika Agano Jipya, neno lenyewe linatumiwa katika njia
kadhaa za jumla, halafu kwa maana inayozidi kulengwa. Kwanza,
linatumiwa kusema kuhusu msikilizaji wa kawaida tu. Wale wote
waliofika kumsikiliza Yesu mwanzoni mwa huduma Yake wanaitwa
“wanafunzi”. Halafu, linatumiwa kumwelezea msikilizaji aliyesadiki
– mtu ambaye anakubali kwamba kile anachosikiliza ni kweli,
ingawa anaweza asibadilishe maisha yake au mtindo wake wa kuishi
kwa sehemu kubwa. Soma Yohana sura ya 6 kwa makini sana,
ukitazama hasa mstari wa 63 hadi 66. Wale wasikilizaji wa kawaida
na ambao walikuwa wamesadiki, walipokuwa bado hawajawa
wafuasi halisi, walimwacha Yesu, “wasifuatane naye tena”. Ni hivi
wapendwa: Kanisa leo limejaa watu ambao wanatosheleza maelezo
hayo. Hawa ndiyo sehemu kubwa ya “waketi vitini” wanaojaza
makanisa yetu Jumapili baada ya Jumapili, lakini ambao hawana
nguvu na Mungu katika kubadilisha dunia, kwa sababu wao
wenyewe hawajabadilishwa kwa undani na kwa ukweli.
Matumizi ya tatu ya neno “mwanafunzi” katika Agano Jipya
yanaeleza mtu anayejifunza maisha yake yote, aliyejitolea, na
anayefuata. Haya matumizi ya mwisho ndiyo anayokusudia Yesu 87
katika Agizo Kuu, na ndiyo amri yetu ya kusonga mbele. Tunapaswa
kwenda kila mahali na “kuwafanya watu kuwa wanaojitolea,
wanaojifunza maisha yao yote, na wafuasi wa Yesu Kristo.” Hii
ndiyo maana iliyo katika neno “mwanafunzi”. Mwanafunzi ni
anayeshikamana (sawa na gundi, kwa mwingine) au ni mwenye
kujifunza kwa Yesu Kristo. Pima kila neno vizuri kabisa. Tumia
muda kutafiti maneno hayo. Mwanafunzi ni mtu aliye katika
mafunzo. Au, ni kiongozi aliye mafunzoni.
Tertuliano, mmoja kati ya viongozi wa kanisa la kwanza,
aliwaita Wakristo “wanafunzi katika shule ya Mungu”. Mwanafunzi
kwanza huzaliwa, kisha hutengenezwa. Anazaliwa kwa Roho wa
Mungu akiwa na vifaa vyote vinavyohitajika ndani yake. Lakini,
lazima ajengwe, afunzwe, afundishwe na kuelekezwa ajitolee kwa
Yesu Kristo.
Waldron Scott, mtu maarufu katika kufanya wanafunzi,
aliandika hivi: “Shughuli ile ya kutengeneza hali mpya za moyo,
kupata utaalamu mpya, kuanzisha mahusiano mapya, kugundua,
kuthubutu, kutafuta, kurekebisha, kufanya upya – yaani, kujifunza –
hufanya maisha kuwa kitu cha kusisimua kama Yesu alivyoahidi.
Kama hujifunzi, ni kwamba huishi. Ni rahisi tu kiasi hicho.”
Lakini, pamoja na maneno mazuri kiasi hicho kutoka kwa
mtu wa hali ya juu hivyo, bado tunapaswa kuwa makini sana. Kuna
kitu kinachotakiwa kuongezwa katika maneno ya Ndugu Scott, hivi:
Mkazo wa huko kujifunza na kuishi unapaswa kuwa Yesu Kristo, na 88
matokeo yanapaswa kuwa kufanana na Yesu Kristo kihalisi kabisa.
Mwanafunzi wa Agano Jipya amevaliwa kabisa na Yesu Kristo na
mawazo yake yote ni kwa Yesu Kristo kiasi kwamba hali yake hiyo
inameza kila jambo lingine dogo linalowezekana. Basi, naye anazidi
kuwa kama Kristo zaidi na zaidi kihalisi kabisa – anayefundisha
daima, anayehudumu daima, anayejenga maisha ya watu daima,
anayerekebisha daima kila inapotakiwa, na anayekwenda duniani
kote daima!
Basi, kuwa kama Kristo kihalisi si ile hali ya kuwa na tabia
ya upole, ya uoga, ya kutokutaka kufanya kitu ambayo tumeiruhusu
kuwepo katika kanisa la siku hizi – bila ya kufikiri. Dada Eugenia
Price alikaribia kweli muhimu sana aliposema, “Dhambi kuu zaidi ya
kanisa la leo ni kumfuga Yesu Kristo.” Sam Shoemaker, aliyesifiwa
na Billy Graham kwamba, “Alikuwa mtu wa maana kwa kanisa
kama taasisi duniani kote kuliko yeyote mwingine wa kizazi chake”
aliwahi kuandika hivi: “Si kazi kubwa ya kanisa kufanya kazi nyingi,
kuwa na orodha ndefu ya washirika, au kuchangisha fedha nyingi.
Kazi kubwa ya kanisa ni kuwatengeneza watu wenye tabia kama
Yesu Kristo – na huo si mtindo wa maisha dhaifu, wala si jinsi watu
wasivyotenda. Hawa watu watakaofanana na Kristo hawawezi
kuchongwa kutokana na makundi makubwa ya watu wa kawaida tu.
Inabidi watengenezwe mmoja mmoja.”
Hebu fananisha makanisa yetu ya siku hizi na mikakati yake,
ambayo utaratibu wake ni sawa sawa na kulipua bonge la majabali na 89
kutazamia kupata sanamu kadhaa zilizochongwa na kusadifiwa
vizuri. Shoemaker aliendelea kusema hivi: “Makanisa yetu
yanapaswa kupunguzwa mpaka yawe mashirika madogo yenye
uwezo wa kutoa nafasi kwa wachungaji na walei kujifunza utaalamu
mkuu wa kiroho wa kuwaleta wengine kwa Yesu na kuwafundisha.
Inaonekana kuwa ujuzi wa dunia nzima kwamba, mtu asipoweka
kazi hii kuwa ya kwanza katika maisha yake, itafukuzwa maishani
mwake kabisa mwisho wa siku. Akili zetu, hisia zetu, masaa ya siku
zetu – vyote hivyo vinapaswa kujawa na kundi maalum la watu
wakati wote – watu ambao tunatafuta kuwavuta, watu tunaotaka
kuwafundisha wachukue wajibu, watu ambao sisi wenyewe
tunawahitaji kwa ajili ya kushirikiana kiroho, na kupata msaada.”
Mtindo huo wa maisha ndiyo Yesu aliofuata, na unatakiwa kuigwa
na sisi mpaka tuujue kabisa.
Knofel Staton aliandika vizuri kabisa, kama ifuatavyo: “Nani
aliye mwanafunzi wa Yesu, na tunafanyaje ili mtu awe mwanafunzi
wa Yesu? Bila ya kuwa na picha dhahiri ya malengo yetu, tutapoteza
wakati tu mahali pamoja, na kutumia muda wetu na nguvu zetu, na
bado hatutakuwa na wanafunzi.” Neno “mwanafunzi” linatumika
mara 270 katika Injili na Kitabu cha Matendo ya Mitume. Halafu,
neno hilo halitokei tena katika vitabu 22 vilivyosalia vya Agano
Jipya. Kulikoni? Mbona neno hilo litoweke? Roho Mtakatifu
anasema nini hapa? Katika Luka 6:40, Yesu alisema hivi: “Utaratibu
ukikamilika, mwanafunzi atakuwa kama mwalimu wake”. Kwa hiyo, 90
tutazamie maneno mengine kujitokeza yenye kuonyesha hali ya
kuendelea. Na kweli – Neno “Mkristo” linaanza kutumika. Neno
“mtakatifu” – mtu ambaye ametengwa kimaalum kwa ajili ya
kutawaliwa na Kristo – linaanza kutokea. Neno “aaminiye” – mtu
ambaye ni mwamini wa kudumu na mwenye kuendelea kumwamini
Yesu Kristo, kumshika Yeye na kufuata makusudi Yake katika
maisha yake ya kila siku binafsi – linatumika mara nyingi na mara
kwa mara.
MWENYE KUFANYA WATU KUWA WANAFUNZI
Neno kuu la pili ni neno “afanyaye wanafunzi”. Huyu ni mtu
“anayewafanya watu kuwa wanafunzi”. Huyu ni mwanafunzi
anayekomaa, maana mtu hawezi kuwa mwanafunzi wa Yesu huku
anapuuzia amri pekee ya kusonga mbele ambayo Yesu aliitoa kwa
kanisa Lake. Yaani, ni kitu kisichowezekana kuwa mwanafunzi
pasipo kuwa mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi. Afanyaye watu
kuwa wanafunzi ni mwanafunzi mwenza, anayewatafuta na
kuwaongoza wengine, huku wakijifunza pamoja.
KUFANYA MWANAFUNZI
Neno la tatu muhimu ni “kufanya mwanafunzi”. Amri ya
Yesu kwamba “mfanye watu kuwa wanafunzi” imejaa vitu vingi
sana, kutokana na mfano wa Yesu Mwenyewe, na mafundisho Yake.
Hii ni harakati ya kuwajenga watu wawe wanafunzi. Christopher 91
Adsit katika kitabu chake kiitwacho Kufanya Wanafunzi Kibinafsi
anafafanua jambo hilo kuwa ni “kutafuta kutimiza amri ya Agizo
Kuu kwa kufanya juhudi za makusudi kuwasaidia watu waelekee
kwenye ukomavu kiroho – kwa kutumia nguvu na maongozi ya Roho
Mtakatifu, kutumia rasilmali za kanisa la mahali, na kutumia
kikamilifu karama, vipawa na ujuzi ambao umepatikana kwa miaka
na miaka.”
Kitendo cha kufanya mtu kuwa mwanafunzi hufanywa na
mwingine, si na kitu fulani. Hufanywa na watu, si mipango.
Hufanikishwa na watu binafsi, sio taasisi. Kimsingi, kufanya mtu
kuwa mwanafunzi ni tendo la Mkristo mmoja akimgawia au
kumwingizia mtu mwingine maisha yake yote, kwa njia ya mfano,
uongozi na mahusiano. Ni uhamishaji maisha siku zote.
Kuna tofauti kubwa sana kati ya kuwasafisha wenye dhambi
na kuwafanya watakatifu kuwa wanafunzi. Kazi nyingi za kanisa –
kazi ya kichungaji, kuabudu, juhudi za kuelimishana, juhudi za
kuhamasishana na kadhalika – husababisha kusafisha wenye dhambi
kwa kiasi kidogo sana, na wala hakuna kiasi kikubwa cha kuwafanya
watakatifu kuwa wanafunzi. Unataka uthibitisho wa hilo? Rahisi
kabisa. Wakristo wengi katika makanisa mengi hawana “uzito
kiroho” wa ziada kwa ajili ya Kristo kuliko ule waliokuwa nao kabla
ya kuokoka!
Kusafisha wenye dhambi humfanya mwenye dhambi aokoke,
halafu humwingiza katika kisanduku cha kiroho cha akiba, na 92
anapotokea humo anatokeza kama mwanadamu mwungwana,
aliyefugwa na kufundishwa vizuri. Kinyume chake, kuwafanya
watakatifu kuwa wanafunzi ni tendo la ujenzi mzuri wa mtu
aliyeokoka ili aweze kubadilisha dunia kwa njia kubwa sana, kwa
kuendeleza utaratibu huo huo.
Tofauti itaonekana katika mfano huu, ambao unalinganisha
kuhubiri na kufanya watu kuwa wanafunzi. Hebu tuseme kwamba
una mtu amesimama nyuma ya mstari fulani akiwa ameshikilia ndoo
ya maji. Mbele ya mstari huo, kiasi cha mita 10, kuna chupa ishirini
ndogo za maziwa. Kuhubiri ni sawa na kutupa maji kutoka kwenye
ile ndoo nyuma ya mstari, kwa matazamio kwamba kiasi fulani cha
maji kitaingia katika zile chupa. Lakini, mafanikio ya tendo hilo
yanatabirika sana: si maji mengi yatakayoingai katika zile chupa. Na
hata kama yataingia, yatafyonzwa upesi na jua kama hayatatumiwa
kwa faida. Lakini, tendo la kufanya mtu kuwa mwanafunzi ni sawa
na kwenda na ile ndoo yenye maji mpaka kwenye kila chupa na
kumimina maji ndani ya chupa mpaka ijae. Ni dhahiri kwamba
mafanikio makubwa yako hapo.
Au, kuhubiri ni kama kuchukua kifuniko cha chupa ya dawa
na kusimama dirishani katika gorofa ya tatu, na kuimimina huko
chini kwa matazamio kwamba itamwingia mtu jichoni. Lakini,
kufanya watu kuwa wanafunzi ni tendo la kumkaribia mtu na
kumtilia dawa moja kwa moja jichoni, mkiwa ana kwa ana.
93
Pasipo kuwa na kiwango maalum cha kufanya watu kuwa
wanafunzi, tutagawa kweli kwa ujumla na kwa wingi na kuwahesabu
watu – ingawa tunaweza kuwa tunazaa watu wachache sana wenye
maana. Kufanya watu kuwa wanafunzi kwa mtindo ambao Yesu
aliutumia kutarekebisha tatizo hilo. Wakati wanafunzi walipomsikia
Yesu akisema kwamba wanapaswa “kuwafanya watu kuwa
wanafunzi”, walitakiwa kuelewa kwamba walitakiwa kuwafanya
wengine kuwa kama Yesu alivyowafanya wao. Kufanya watu kuwa
wanafunzi ni pamoja na kufuata utaratibu mzima wa kufanya watu
kuwa wanafunzi – tangu kuongoka mpaka kufikia mtu afanyaye
wengine kuwa wanafunzi, aliyefundishwa. Hicho ndicho kiini cha
yale ambayo Kristo anatazamia kwa Kanisa Lake.
NIDHAMU
Neno muhimu la mwisho hapa ni “nidhamu”. Nidhamu ni
maeneo katika maisha yenye kudhihirisha gharama ya uanafunzi.
Hudson Taylor, mwanzilishi wa China Inland Mission na mmoja kati
ya wamishenari maarufu sana wenye maono makubwa, aliandika
hivi: “Mtu anaweza kuwa amewekwa wakfu, amejitoa na
anamaanisha, lakini hatakuwa na thamani kubwa kama hana
nidhamu.”
Je, wajibu alitooa Kristo ni wa dhati kiasi gani? Je, kanisa
limeshindwa kiasi gani kutii amri moja tu ya Agizo hilo? Je, kuna
94
ushahidi wowote halisi kuhusu kushindwa huko? Ninaamini kwamba
kuna ushahidi tele na wa kudumu kabisa.
[USHUHUDA WA MWANDISHI – Nilikuwa katika kikao
zamani na Mkristo mzee mwenye mvi, ambaye amekwenda
Mbinguni kupumzika zamani. Yeye na mimi tukawa peke yetu
ofisini mwake kwa muda, na hapo akaniuliza “ninafanya nini siku
hizi” katika kanisa nililokuwa nachunga. Nikamwambia, “Ninafanya
kila ninachojua ili kuwageuza washirika wa kanisa kuwa wanafunzi
wenye maono ya dunia ambao nao wanazalisha wanafunzi wengine
wenye maono ya dunia pia.” Kwa huzuni sana akanijibu, “Ndugu
Hodges, sikuwa na mafanikio yoyote katika kuzalisha
watakaozalisha wengine katika kanisa lolote nililochunga.”
Nikauliza, “Basi, ulifanya nini?” Alijibu kwa masikitiko sana,
“Niliendelea na kujitahidi kufanya kazi yote mimi mwenyewe.”
Alijihukumu mwenyewe, na ilikuwa kitu cha kusikitisha sana!
Nilikuwa nimeketi katika mgahawa mmoja nikiwa na
wachungaji watatu tukisubiri tuletewe chakula. Tukawa
tunazungumza (kwa maelekezo yangu nadhani) kuhusu kufanya watu
kuwa wanafunzi. Mchungaji mmoja mzuri tu katika kundi letu akatoa
tathmini ya ukweli kuhusu historia yake ya utumishi (na alikuwa
mchungaji mzuri tu na maarufu sana, mwenye kuamini Injili).
Alisema hivi: “Herb, ninatazama katika makanisa yangu mawili
niliyochunga kwa muda mrefu, na ninaona watu wawili tu katika kila
kanisa wanaoweza kustahili kuwa aina ya watu wale unaowataja”. 95
Hakuwa anazungumza kwa kulaumu au kwa hasira, bali kwa
uchungu na huzuni tu. Inasikitisha sana, lakini ndiyo kawaida!
Tukijitahidi sana, tumekuwa tukizalisha “Wakristo wazuri” ambao
mara nyingi maana yake ni watu wenye kujitazama sana ndani,
badala ya wanafunzi na wenye kufanya wengine kuwa wanafunzi
wanaogusa dunia na kuzalisha wengine. MWISHO WA
USHUHUDA]
Lengo dhahiri la Yesu lilikuwa kuzaa “wanafunzi” ambao
wangekuwa “wafanya wanafunzi”, wanaojihusisha katika kazi ya
“kuwafanya wengine kuwa wanafunzi” katika maisha yao yote na
kutekeleza zile “nidhamu” ambazo ni muhimu kwa ajili ya kutimiza
kusudi hilo.
KUFANYA WANAFUNZI KUNAKOSABABISHA HUDUMA
YA MAONGEZEKO
Halafu, Agano Jipya linaongeza jambo lingine muhimu kwa
jukumu letu. Tunatakiwa kuhusika katika kufanya uanafunzi wenye
kuzalisha huduma ya maongezeko. Ni dhahiri kwamba ilikuwa nia ya
Kristo kwamba kila mwanafunzi ahusike katika huduma ya
maongezeko. Nini maana ya maongezeko? Ni wakati wanaofanya
watu kuwa wanafunzi wanapoanza kuzaa wanafunzi wengine
wanaofanya watu kuwa wanafunzi wenye maono, na wenye kugusa
dunia. Ni hivi: Mpango wa Mungu ni kuifikia dunia kwa mtindo ule
ule uliotumika kuijaza – kwa kuongezeka. Katika Mwanzo 9:1 96
Mungu alisema, “Zaeni mkaongezeke, na kuijaza dunia”. Kuna mtu
aliyesema kwamba hiyo ndiyo amri ya kwanza iliyowahi kutolewa
kwa mwanadamu, na ndiyo pekee aliyoitii. Agizo la Yesu la
kiinjilisti ni sawa na lile la Mungu la kimwili.
Kwa nini watu wanashindwa kuongezeka kimwili?
1. Wengine hawaingii katika ndoa, au, hakuna muungano kati
ya wanaume na wanawake. Basi, maongozeko hayawezi kutokea.
2. Wengine wana maradhi au matatizo katika sehemu
muhimu za mwili, zinazohusiana na uzazi.
3. Wengine hawaongezeki kwa sababu hawajakomaa. Sidhani
kama kuna anayefahamu wazazi wenye umri wa miaka mitatu!
Viungo vya uzazi vipo, lakini havijakomaa kiasi cha kutosha
kuruhusu maongezeko – au kuzaliana. Watoto hawazai.
Mapungufu hayo hayo yanahusika kwa ajili ya kushindwa
kuongezeka kiroho. Mahali ambapo hakuna muungano kati ya
Mkristo na Yesu Kristo kwa hali inayodumu na kuendelea,
hapawezekani kuwepo na maongozeko yoyote kiroho – labda kidogo
sana. Kuwepo kwa dhambi katika maisha ya mwamini pia kutazuia
mkakati na mpango wa maongezeko. Pamoja na hayo, kupoa kwa
Mkristo katika utoto wa kiroho kutazuia kuongezeka. Paulo alisema,
“Niliwaandikia kama watoto katika Kristo”, na Wakristo watoto
huko Korinto walikosa nafasi ya viwango vya kugusa dunia kwa
maongezeko kiroho.
97
Maongezeko kiroho ni maono yaliyopangwa na Mungu kwa
ajili ya kuifikia dunia yetu ya wakati huu na vizazi vyote vijavyo kwa
wale tunaowaleta kwa Yesu na kuwafundisha wakati huu. Mkakati
wa huduma ya Yesu ulikuwa wazi: Aliwatazama makundi ya watu
kupitia mtu mmoja, halafu akamjenga huyo mtu afikie makundi ya
watu. Yeye alimhudumia kila mtu aliyekuwa mbele Yake – lakini
aliwaita kwa ajili ya Ufalme Wake tu. Sisi tumepotosha kabisa
viwango hivyo katika kujenga taasisi badala ya kuwajenga watu.
Yesu alipenda kila mtu binafsi – hakika – lakini siku zote alitazama
mbele kuliko wanafunzi Wake na kuwaona watu ambao
wangewafikia na kuwafundisha (ona ktk Yohana 17:20).
Katika Matendo 2:41, 47 na 5:14, neno “akaliongeza”
linafafanua mkakati wa Mungu kihesabu, tangu mwanzoni mwa
historia ya kanisa. Lakini katika Matendo 6:1, tunasoma kwamba
“idadi ya wanafunzi ikaongezeka sana, hata kundi kubwa la
makuhani likajiunga na imani.” Halafu tunapofikia Matendo 9:31
tunasoma kwamba, “makanisa yakaongezeka sana.” Bila shaka,
kanisa halikurudi tena kwenye majumlisho madogo madogo
isipokuwa lilipotoka kwenda mstari wa mbele na kuanza tena, na
hata huko lilirudi haraka sana kwenye kuongezeka.
Watu tunaolingana umri tunapokutana na mwanafunzi
mwenzetu wa chuo kikuu au chuo cha Biblia ambaye hatujaonana
tangu shuleni, maswali muhimu huulizwa. “Vipi, umeoa/umeolewa?”
98
“Je, mna watoto?” “Wangapi?” “Mna wajukuu?” Na kama wahusika
ni wazee kiasi, wanaulizwa, “Je, mna vitukuu?”
Tutakaposimama mbele ya Kiti cha Hukumu cha Kristo,
pengine tutasikia maswali kama hayo hayo. “Je, una watoto? (Na
kama huna, kwa nini?)” “Watoto ni wangapi?” Halafu kipimo halisi
cha ushiriki wetu katika mpango wa Yesu unaanza. “Je, una wajukuu
– watu ambao wamekuwa Wakristo kwa sababu ya jinsi
ulivyowajenga watoto wako mwenyewe wa kiroho?” “Na je, una
vitukuu wa kiroho?” Haitaridhisha kujua kwamba tuliwahudumia
watu wengi sana, na wachache tu ndiyo wakawa wazalishaji.
Itatosheleza tu ikiwa tutakuwa tumetoa maisha yetu tukitafuta
kuwafanya wanafunzi wetu kuwa kama Yesu alivyowafanya wa
Kwake.
Ili tuwe na uhakika kwamba tunaona vizuri kiwango halisi na
kuelewa udhati wa kushindwa kufuata kiwango hicho, hebu
tumalizie sura hii kwa namna nzito – naam, hata ya kinyume kabisa.
Kitabu kiitwacho The Bridge Over River Kwai kinasimulia
habari ya kanali Mwingereza aliyetekwa na WaJapani wakati wa
Vita Kuu ya Pili ya Dunia. Katika kambi ya wafungwa wa kivita
iliyokuwa katikati ya msitu mkubwa huko Burma, mamia ya
wafungwa wasio na matumaini walikaa tu wakisubiri kifo. Huyo
afisa Mwingereza akapata wazo la ubunifu ili kuinua hamasa na
kuwapa waliotekwa sababu ya kuishi. Hapo karibu na kambi, adui
walikuwa wanajenga daraja la treni. Wafungwa wakasema wao 99
ndiyo watakaojenga. Watafanya kazi kwa ubora na kuonyesha
WaJapani kitu ambacho kingefanywa na mafundi wa Kiingereza!
Akijitolea na askari wake kuifanya ile kazi, yule kiongozi wa
Kiingereza aliona mabadiliko katika motisha. Lengo la kujenga
daraja hilo likawa kitu kinachomsukuma, tena kizuri. Hatimaye,
daraja likakamilika na treni ya kwanza ya KiJapani iliyokuwa
imebeba vitu ikawa inavuka. Kanali huyo aliyejivunia kazi yake
aliona makomandoo wa Majeshi ya Muungano wakiwa chini ya lile
daraja, wakijiandaa kulibomoa. Kwa sababu ya jinsi alivyokuwa
amehusika kibinafsi, alipiga kelele ya kumtaarifu yule mkuu wa
Kijapani, halafu akakimbia kama mwenda wazimu kuelekea mtoni,
ili kujaribu kuwazuia wale waliotaka kulilipua daraja.
Bila shaka mfano uko wazi kabisa hapo, sivyo? Makanisa
mengi hukaa katika hali ya kukaribia kifo. Basi, viongozi wao
wanazaa mpango mmoja baada ya mwingine, ratiba baada ya ratiba,
ili kuboresha motisha na kuwapa washirika kitu cha kuwahamasisha.
Yaani, wanaingia katika mikakati ya kujikimu na kujihami, ambayo
ndiyo kawaida kabisa katika ujenzi wa taasisi. Kama hadithi
ilivyokuwa, adui anao mpango wake, na anafurahi sana kutuingiza
sisi katika “kuutimiza”. Mara nyingi tunaupokea mpango wake na
kuufanyia kazi kwa bidii kabisa. Lengo la “kujenga daraja” linakuwa
kitu kinachotusukuma kweli kweli. Mtu yeyote akisema kwamba huo
ni mpango mbadala wa Shetani, na kwamba si mkakati wa Mwokozi,
tunamgeukia kana kwamba ni adui yetu. Tumeshikwa sana na 100
mipango hii ya kujenga taasisi mpaka tumesahau kwamba kuna vita
kubwa zaidi kuliko ujenzi wa daraja. Kama watoto wadogo
wanaocheza michezo ya kujifanya, tunaendelea kuishi tu bila ya
kutambua kwamba tunakosa agizo halisi la Yesu.
[USHUHUDA WA MWANDISHI – Mwanzoni mwa mwaka
wa 1991 nilikaa juma zima katika kanisa moja huko Texas,
nikihubiri mikutano ya jioni kuhusu mada ambazo zinaunga mkono
mkakati huu wa kufanya watu kuwa wanafunzi, na kufundisha
kwenye ibada za mchana taratibu au hatua zenyewe. Mchungaji wa
kanisa hili alitokana na huduma ya kanisa ambalo niliwahi
kulichunga. Jioni ya mwisho, wanandoa vijana wakanijia muda
mfupi kabla ya ibada kuanza, na tulipokuwa tunazungumza, yule
mke akanipa barua iliyokunjwa. Sehemu ya barua hiyo ilisema hivi:
“Sijui kama unafahamu au vipi, lakini, mimi ni mmoja katika
wajukuu zako kiroho. Mchungaji wetu amekuwa akitufanya
wanafunzi mimi na mume wangu kwa karibu miaka minne.” Halafu
kukawa na sehemu ya maelezo binafsi, na sehemu nyingine ambapo
alifanya kama muhtasari au marudio wa mahubiri ya kila jioni kwa
juma hilo. Ndipo akaandika tena, hivi:
Asante sana kwa muda wa ziada ambao umeutumia
kutufundisha juu ya uanafunzi. Japo mimi niko kama yule ndugu
aliyekiri kwa machoni katika ibada ya mchana kwamba amekuwa
Mkristo kwa muda mrefu, lakini hakuwahi kumfanya mtu yeyote
kuwa mwanafunzi. Nimewashuhudia watu kadhaa baada ya kujifunza 101
na kuwa na mchungaji wetu, lakini kwa sasa nina shauku ya
kumpokea mwanafunzi wangu wa kwanza maishani mwangu. Juma
hili limekuwa muda wa kubadilika katika maisha yangu, nami
ninafurahia jinsi ambavyo wewe umemruhusu Mungu akutumie
kunihudumia na kunihimiza na kunihamasisha. Ninapanga – na Yesu
akifanya kazi kupitia kwangu, nikufanye uwe babu-babu wa kiroho.
Asante sana kwa kuja kwako! Ni mimi dada yako na mjukuu katika
Kristo, (sahihi). MWISHO WA USHUHUDA]
Mambo halisi katika Agano Jipya yaliyotajwa katika hii barua
yanaonyesha amri ya kusonga mbele ambayo Yesu aliitoa kwa
kanisa lake. Ongezea maeneo ya kuzaa kiroho, maono ya dunia, na
taratibu halisi za kuwafanya watu kuwa wanafunzi, nawe unakuwa
umepiga hatua kubwa sana kuhusu kutimiza Agizo Lake.
Katika gazeti la chuo cha Biblia cha Kibaptisti toleo la mwezi
Mei 1983, kulikuwa na kisa cha kusikitisha sana. Majina ya
wahusika yamehifadhiwa, japo katika gazeti lenyewe yalitajwa.
“Wakati wamishenari ….. walipoandika kitabu juu ya kufukuzwa
kwao nchi ya Ethiopia, walilazimishwa kujiuliza ni kitu gani
walichoacha nyuma. Jibu likawashtua kabisa. Walitambua kwamba
walichofanya ni kumwaga mbegu tu – hawakuzipanda. Cha kushtua
zaidi kikawa utambuzi wao kwamba Wakristo kila mahali walikuwa
wanafanya makosa yale yale: wanabatiza makundi makubwa ya
watu, lakini hawafanyi watu kuwa wanafunzi. Mishenari mmoja
akasema katika ibada ya wanafunzi, ‘Hatukufanya yeyote kuwa 102
mwanafunzi. Tumeona watu wanaokiri imani tu. Na tunao hao katika
viti vya kanisa kila mahali Marekani, na duniani kote. Ni rahisi sana
kubatiza watu. Ni vigumu zaidi kufanya watu kuwa wanafunzi. Mimi
naona kanisa na Mungu wana mipango miwili tofauti ya utendaji.
Kanisa lina wasemaji na wasikilizaji, na wote hao hakuna anayetenda
kile Yesu alichowaitia Wakristo kuwa. Tunahitaji kuingia katika
mpango wa Mungu.”
Pengine maelezo haya yanajumlisha tatizo kana kwamba
Wakristo wote wanastahili kulaumiwa, pamoja na kurahisisha
ufumbuzi wa tatizo lenyewe. Hata kitabu hiki kina hatia katika eneo
hilo. Lakini, kinashughulikia kushindwa kwa muhimu sana katika
kanisa kwa ujumla, na kinatukumbusha juu ya mkakati mmoja tu
ambao Yesu alitoa.
Ukitaka kuanza kufanya kilicho sawa, huwi umechelewa –
yaani yale ambayo tumeagizwa kufanya. Mtu yeyote anaweza
“kurudi mwanzo kabisa” na kuanza ule utaratibu wa kuongeza.
Lakini, wengi wetu tungehitaji kujitoa wenyewe mara moja ili
kuingia katika shughuli ya kujifunza maisha na huduma ya Yesu,
tukiuliza hivi: “Alifanyaje na watu Wake?” na pia kujifunza mbinu
za kufanya wanafunzi na kuwaongeza, kama zitolewavyo katika
vitabu vingi maarufu.
Naona jeshi linalozidi kuongezeka la waongezaji wenye
maono ya dunia nzima na mguso wa dunia nzima ambao historia yao
yote ni kujitoa kwao kutimiza Agizo la Yesu la “kuwafanya watu 103
kuwa wanafunzi.” Mungu awapate na kuwatuma wanajeshi hao
mbele ya macho yetu
104
Sura Ya 4Ufunguo Ulioko Mlangoni Mwa Historia Ya Kanisa
“Kitabu kile cha kwanza nalikiandika, Theofilo, katika habari ya mambo yote aliyoanza Yesu kufanya na kufundisha, hata siku ile alipochukuliwa juu, alipokuwa amekwisha kuwaagiza kwa Roho Mtakatifu wale mitume aliowachagua; wale aliowadhihirishia nafsi yake, kwa dalili nyingi, baada ya kuteswa kwake, ya kwamba yu hai, akiwatokea muda wa siku arobaini, na kuyanena mambo yaliyouhusu ufalme wa Mungu. Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ‘Ile ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache.” Matendo 1:1-5
Tutaanza somo hili “mlango wa mbele” wa “Matendo ya
Mitume”. Historia ya Ukristo imekuwa na mjadala si mdogo kuhusu
jina la kitabu hiki katika Biblia. Bila shaka unajua kwamba majina ya
vitabu vya Agano Jipya hayajavuviwa. Yaliongezwa miaka mingi
sana baada ya kukamilika kwa Agano Jipya. Kuna wanaoamini
kwamba kinapaswa kuitwa “Matendo ya Baadhi ya Mitume,” kwa 105
sababu ni huduma za Petro, Yakobo, Yohana na Paulo tu ndiyo
zinazotajwa. Wengine wanadhani kinafaa kiitwe “Matendo Ya Roho
Mtakatifu” ili kukazia Mtendaji Mkuu na kuwaficha wale watendaji
wadogo. Lakini, kila mmoja anabakiza neno “Matendo” katika jina la
kitabu. Ona kwamba si nia, wala mipango, wala matumaini, wala
matakwa, wala mafunzo, wala tafakari, wala mahubiri ya Mitume. Ni
matendo ya mitume. Kama mitume wangekwamia kwenye hayo
tuliyotaja hapo kabla, hata kama ni moja tu, kitabu hicho
kisingeandikwa. Basi, ni maombi yangu kwa ajili yetu kwamba,
tunapofungua mlango wa mbele wa kitabu chenyewe, “tukamatwe
katika Matendo yenyewe”!
Tutaanzia kwenye mtazamo mpana wa mstari wa kwanza
kabisa wa kitabu. “Kitabu kile cha kwanza nalikiandika, Theofilo,
katika habari ya mambo yote aliyoanza Yesu kufanya na
kufundisha.” Hebu niingize muhtasari wa mstari huu. Kwanza, kuna
kitabu kingine kinachotajwa hapa (“kitabu kile cha kwanza”). Halafu,
kuna mwanafunzi binafsi anayetambulishwa hapa (“Theofilo”) .
Mwisho, kuna tamko la wazi kuhusu kusudi la kuandikwa kwa kitabu
kile cha kwanza, na vivyo hivyo, tamko la kusudi kwa ajili ya
kuandika kitabu hiki cha sasa.
KITABU CHA KWANZA KINACHOTAJWA
Hebu tufikiri kuhusu kitabu kile kingine kinachotajwa hapa.
Hicho “kitabu kile cha kwanza” ni kipi? Tafsiri za Lugha Rahisi 106
zinakiita “maelezo ya kwanza niliyoandaa”. Hicho kitabu cha
kwanza ni Injili kama ilivyoandikwa na Luka. Injili ya Luka ni
mojawapo katika Injili nne katika Agano Jipya. Inazo sura 24 katika
Biblia yako, na imejengwa kwenye kweli kama kumi hivi za
kihistoria kuhusu Bwana Yesu Kristo. Hizo kweli ni kama ifuatavyo:
Kuzaliwa Kwake na Bikira; Maisha Yake Yasiyo na Dhambi;
Kubatizwa Kwake; Kujaribiwa Kwake; Kubadilika Sura Kwake;
Mapambano Yake Katika Bustani ya Getsemane; Kusulubiwa na
Kufa Kwake; Kuzikwa Kwake; Kufufuka Kwake; na Kupaa Kwake.
Ili ufahamu jinsi hayo ni ya ajabu, ona cha kwanza kabisa
katika hizo kweli za kihistoria juu ya Yesu – kuzaliwa Kwake na
bikira. Kumbuka kwamba Luka alikuwa tabibu – daktari. Si rahisi
kwa madaktari kuamini uzazi wa bikira, lakini maelezo yenye
kutosheleza kabisa kuhusu kuzaliwa kwa Yesu na bikira katika
Biblia nzima yametolewa na Dakta Luka. Anatuambia mwenyewe
katika sura ya kwanza ya Injili yake kwamba alikuwa amefanya
utafiti wa habari za kihistoria kuhusu Yesu kwa ukamilifu kabisa, na
kwamba aliandika alichoandika kwa msingi wa aliyopata kwenye
utafiti. Hivyo basi, tunapata ushahidi mkubwa mwingine kuhusu
ukweli na uhakika wa habari za Yesu Kristo.
107
LUKA ALIKUWA NANI, NA ALIINGIAJE KWENYE
HABARI HII?
Hivi, Luka ni nani? Na alipataje kuingia katika hadithi ya
Injili? Yeye alikuwa mtu wa Mataifa – yaani, asiyekuwa Myahudi –
na jina lake linaonyesha hilo. Alikuwa tabibu aliyeitwa “Luka, tabibu
mpendwa” katika Wakolosai 4:14. Wakati mwingine tunawaza
kwamba kila mtu katika dunia ya siku zile alikuwa mshamba, mtu
asiyekuwa na elimu, na asiyejua mengi kama tunavyojua sisi leo.
Sivyo kabisa. Luka amekosolewa mara kwa mara kuhusu kuwa
mwanahistoria na kuhusu kuwa tabibu, lakini yeye na vitabu
alivyoandika vimevunjilia mbali nyundo nyingi sana, yaani,
wakosoaji wake. Ukweli ni kwamba, katika kila hoja ya ukosoaji
inayotolea, maandishi ya Luka yamesimama vizuri na kushinda
barabara, kihistoria na hata kitabibu.
Vitabu chungu nzima vimeandikwa kuhusu Luka, kama
mwanahistoria na kama tabibu. Kwa mfano: Dakta Hobart
alichapisha kitabu kikubwa tu kinachoitwa The Medical Language
of Luke, kinachokubaliana na ubora na usahihi wa lugha ya
kitaalamu ya kitabibu katika vitabu vyake vyote viwili. Kama ilivyo
kawaida, wakati wanasayansi wanapofanya utafiti kwa kuzingatia
ukweli, hatimaye wanaifikia Biblia!
Lakini – huyo tabibu alihusikaje na uandishi wa Injili na
matetezi ya Maandiko mpaka kufikia kuandika vitabu viwili
ambavyo vinapatikana katika Agano Jipya letu? Hebu tuunganishe 108
historia, ufunuo na uwezo wetu wa kufikiri kwa kifupi. Paulo na Sila
walifika katika eneo la Galatia wakati wa safari yake ya pili ya
kitume (ktk Matendo 16:6). Walipokuwa huko, inaonekana Paulo
alipata ugonjwa mbaya sana wa macho (au, ugonjwa aliokuwa nao
hapo nyuma ulilipuka mpaka kufikia hali ya hatari). Alipowaandikia
Wagalatia baadaye, alisema hivi: “Oneni jinsi nilivyowaandikia
barua kubwa, kwa mkono wangu mwenyewe” (ktk Wagalatia 6:11,
TLR). Tafsiri za Lugha Rahisi zinaeleza kwa njia nyingine. Moja
inasema, “Oneni jinsi ninavyoandika herufi kubwa”. Nyingine
inasema, “Mnaona hizo herufi kubwa?” Nyingine inasema,
“Nimeandika kwa herufi kubwa kwa ajili yenu.” Kwa hiyo,
unamwona Paulo akihangaika kuandika kwenye karatasi lake,
akitengeneza ‘maherufi’ makubwa kwa sababu haoni vizuri kiasi cha
kuandika kawaida.
Katika Wagalatia 4:13-15, Paulo aliwaambia hivi, “Mnajua
jinsi ambavyo kwa udhaifu wa mwili wangu niliihubiri Injili kwenu
mara ya kwanza. Na jaribu langu lililokuwa mwilini mwangu
hamkulipuuza wala kulikataa; bali mlinipokea kama malaika wa
Mungu – naam, hata kama Kristo Yesu … Kwa sababu
ninawashuhudia kwamba, kama ingewezekana, mlikuwa tayari
kung’oa macho yenu, ili mnipe mimi.” Ona kwamba Mungu
hakumponya Paulo tatizo hili zito sana. Yeye alikuwa na kitu bora
zaidi na kikubwa zaidi kuliko kumponya Mtume Wake! Alikuwa
109
anajipanga kumwita (kwa njia ya ugonjwa wa Paulo) mmoja kati ya
wasemaji Wake wakuu!
Paulo na timu yake wakasonga mbele kutoka Kusini
Mashariki hadi Kaskazini Magharibi katika “ukanda” wa Asia Ndogo
mpaka wakafika Troa, mji wa pwani uliokuwa upande wa kaskazini
wa Bahari ya Uyunani. Yawezekana alishindwa kulala usingizi
vizuri, maana hapo ndipo “Paulo akapata maono usiku. Mbele yake
alisimama mtu kutoka Makedonia, akamsihi akisema, ‘Njoo
Makedonia, ukatusaidie’.” Hapo ndipo uinjilishaji wa Ulaya Kusini
ulipoanza.
Wakati Paulo anasubiri huko Troa, alijua alihitaji kumwona
tabibu. Kuna wasomi wa Biblia wanaoamini kwamba Paulo na Luka
walikuwa wamefahamiana kabla, kwa sababu chuo maarufu cha
utabibu siku hizo kilikuwa mjini alikozaliwa Paulo. Wengine
wanapendekeza kwamba pengine Paulo aliulizia tabibu mzuri yuko
wapi, na akaelekezwa kwa Luka (ambaye kwa kweli alikuwa tabibu
mzuri sana – bingwa). Vyovyote ilivyotokea, ninaamini Paulo
alimwona Luka ili apate matibabu ya tatizo lake.
Akiwa huko, Paulo (kama kawaida) alimshirikisha huyu
tabibu Mmataifa mwenye ujuzi na akili nzuri sana habari za Kristo
na Injili Yake, na “Mungu akawasha taa” ndani ya roho yake. Dakta
Luka akaokoka na kuwa Mkristo. Aliaminishwa kuhusu dhambi zake
na kuamua kumfuata Mwokozi. Mara ile ile Paulo alianza kumfanya
mwanafunzi, lakini muda ulikuwa mfupi sana.110
Paulo na Sila walikuwa “chini ya amri”. Walikuwa kwenye
utume, na ratiba yao ilikuwa inapangwa na Roho Mtakatifu. Paulo
akamwambia Luka kwa upole, “Ndugu, lazima tuondoke sasa.”
Pengine Luka alijibu hivi: “Mwondoke? Mwende? Jamani, si ndiyo
mmefika tu? Tena, umeniongoza kwenye jambo kuu kuliko yote
niliyowahi kuyafahamu na kuyajua, ambalo ni uzima wa milele
katika Yesu Kristo. Ndiyo unasema lazima mwondoke sasa? Hiyo
haiwezekani!”
Lakini Paulo alipokaza juu ya jambo hilo, Luka alifikiri hali
yenyewe kidogo halafu akasema, “Je Paulo, unaonaje ukipata msafiri
mwingine katika timu yenu ya utume?” Bila shaka ari ya Paulo
iliongezeka, lakini pengine alimjibu hivi: “Kuna uwezekano mzuri
tu! Ila, itakuwaje kuhusu kazi yako ya utabibu?” Luka alijibu kwa
utulivu kabisa, “Aa! Mbona hiyo si kikwazo? Kazi yangu imekaa
vizuri. Itakuwa rahisi kuuza.” Ndipo Paulo akatambua kwamba Luka
alikuwa amemaanisha kabisa. Pengine aliuliza hivi: “Yaani
unamaanisha kwamba uko tayari kuuza kazi yako na kufuatana nasi
katika safari hii, sehemu iliyiosalia? Nashindwa kuamini.” Labda
Luka naye akajibu, “Lakini Paulo, unahitaji kuwa na tabibu wa
kudumu sasa hivi, nami ninakuhitaji kwa kadiri unavyonihitaji na
mimi. Naam – naona nitafanya hivyo!”
Je, unadhani natunga mawazo hayo? Hapana. Mpaka mstari
wa 10 wa Matendo 16, maelezo ya mwanahistoria huyo (yaani, ya
Luka) yanatumia neno “Wao” anapoandika kuhusu hiyo timu ya 111
kitume. Lakini unapofika Matendo 16:10 (anapozungumzia mambo
ya Troa ktk mstari wa 8), maelezo yanasema, “Mara tukakusudia
kwenda Makedonia” na ndiyo mwanzo wa sehemu za “tuka” katika
Matendo. Luka, mwandishi wa kitabu cha Matendo, alijiunga na timu
ya Paulo huko Troa!
TAFAKARI
Hebu tukatishe hadithi yetu na kuona kweli nzuri sana
zinazofaa kutafakari. Ni hivi: Tendo la kufanya watu kuwa
wanafunzi halielekei upande mmoja tu. Wakati Paulo anamfanya
Tito kuwa mwanafunzi, Tito naye anamfariji Paulo (ktk 2Wakor. 7:5,
6). Wakati Paulo anampa kijana Timoteo hekima yake ya muda
mrefu, Timotheo kijana anamhamasisha mzee Paulo. Wakati Paulo
anamfanya Dakta Luka kuwa mwanafunzi katika maisha ya Kristo,
Dakta Luka anampa mwanatheolojia Paulo ujuzi na utaalamu wake
wa kitabibu.
Je, umewahi kujiuliza mahali Paulo kama mwanadamu
alikopata mfano wake wa Kanisa kuwa ndiyo “Mwili wa Kristo”
halisi? Kibinadamu, hilo hata halifai kuwa swali. Bila shaka Luka –
kikawaida kabisa – angezungumza kuhusu utendaji kazi wa
kushangaza sana wa mwili wa mwanadamu. Pengine angefafanua hii
mashine ambayo ni mwili wa mwanadamu wakati akimtibu maradhi
yake Paulo – kama ambavyo angefanya nyakati zingine pia.
112
Labda siku moja alisema hivi: “Hivi Paulo, una akili kiasi
gani katika mwili wako, baada ya kichwa? Una hekima kiasi gani
katika mwili wako chini ya kichwa chako? Pengine Paulo angesema,
“Kweli sijawahi kufikiri sana juu yake, lakini bila shaka jibu sahihi
ni kwamba, ‘sina’.” Na Luka angejibu, “uko sawa kabisa. Lakini
basi, viungo vilivyoko chini ya kichwa chako vinajuaje kitu cha
kufanya kama havina hekima au akili ndani yake? Jibu ni muujiza
mwingine wa mwilini.”
Akaanza kumpa somo. “Ni kwamba una mfumo wa mishipa
ya fahamu katika mwili wako, yenye kuunganisha viungo vya mwili
na akili. Mishipa itokayo kwenye akili au ubongo hadi mwilini
hupitisha amri zitokazo kwenye akili hadi kwenye viungo vya mwili,
na kama viungo vyote viko katika hali nzuri kiafya, vinatii mara
moja na kutuma ujumbe wa kukubali kurudi kwenye akili, unaosema,
‘Sawa. Kazi unayotaka tutaitenda.’ Unaona huu mkono wangu wa
kuume ulionyooshwa? Kiganja kiko juu na vidole vimetawanyika.
Na mkono utabaki hivyo hivyo mpaka niuachie ufanye kitu kingine.
Kwa nini? Kwa sababu, muunganiko kati ya akili na kiungo uko
timamu – afya ni nzuri na unafanya kazi.”
Muda wote huo wakati Luka anazungumza, Roho Mtakatifu
anafanya kazi kwa nguvu sana katika akili ya Paulo. Ghafula
anasema hivi: “Hivyo ndivyo Kanisa linavyofanya kazi pia. Sawa na
jinsi ambavyo mwili wako ni chombo kwa ajili ya kujieleza, kanisa
nalo ni Mwili wa Kristo, na chombo kwa ajili ya Yeye kujieleza.” 113
Na Roho Mtakatifu anaendelea kufafanua fundisho kuhusu kanisa
kama mwili wa Kristo kwa Paulo mwanatheolojia, akipitia kwa
Luka, mishenari tabibu wa kwanza!
Muda mrefu baadaye, huyu tabibu Mmataifa – Luka –
aliyefanywa mwanafunzi kibinafsi na kwa upana sana na Paulo,
mtume mkuu wa Kikristo, alikuja kuandika vitabu viwili vya ajabu
sana ambavyo vinapatikana leo katika Agano letu Jipya. Iitokeaje
kuwa hivyo? Na inadhihirisha nini kwetu kuhusu wajibu wa kufanya
watu kuwa wanafunzi utolewao na Agizo Kuu?
Jiandae basi kupokea kweli hii kuu, ifuatayo: Ingawa Luka
aliandika vitabu viwili tu kati ya vile ishirini na saba katika Agano
Jipya, hivyo vitabu viwili ni kama moja ya nne (au robo) ya maelezo
yote ya Agano Jipya. Viliandikwa kwa ajili ya nini? Je, Dakta Luka
alikuwa na wazo lolote kwamba hivyo vitabu viwili vingekuja
kupatikana katika Biblia? Au katika Agano Jipya? Hakika hapana,
kwa sababu yeye hata hakujua kwamba “Agano Jipya” lingekuja
kuchapishwa. Basi, kwa nini aliandika hivyo vitabu viwili vya ajabu
na kushangaza sana?
114
MWANAFUNZI BINAFSI ANATAMBULISHWA
ROBO YA AGANO JIPYA ILIANDIKWA KWA MTU
MMOJA!
Pili, hebu tufikiri sasa juu ya mwanafunzi binafsi ambaye
aliandikia vitabu hivi viwili. Jina lake ni Theofilo. Linatushangaza
sana. Kwa kweli, majina yanatushangaza.
Familia moja ilipata mtoto. Baada ya kutafuta jina kwa miezi
kadhaa na kuchagua jina lenye kuvutia, walimpa jina la ajabu –
“Theofilo” – baada ya kuzaliwa kwake. Rafiki yao mmoja akauliza,
“Kwa nini? Mbona baada ya kuchagua jina zuri tu mlifikia uamuzi
wa kumwita ‘Theofilo’?” Yule baba akajibu, “Tulimwita Theofilo
kwa sababu ni mtoto mwenye sura mbaya tuliyepata kumwona!”
Jina la huyu Theofilo ni muungano wa maneno mawili katika
lugha ya Kiyunani. Sehemu ya kwanza – “Theos” – maana yake
“Mungu”. Sehemu ya mwisho – “philo” – maana yake “upendo”.
Kwa hiyo, jina lake linaweza kumaanisha “mwenye kumpenda
Mungu” au “anayependwa na Mungu”. Kwa sababu ya hiyo maana,
watafsiri wengine wa Maandiko wamesema kwamba labda si jina la
mtu mmoja binafsi, bali kundi la watu. Lakini si hivyo. Mpokea
kitabu anaelezwa vizuri sana na Luka kwamba ni mtu binafsi, katika
sura ya kwanza ya Injili ya Luka.
115
Kumbuka kwamba Injili kama ilvyoandikwa na Luka, na
Kitabu cha Matendo mwandishi wake ni mmoja, mpokeaji ni mmoja,
na vyote vina mada moja kimsingi.
Sasa, kweli kuu ya pili ni hii: Robo moja ya Agano Jipya
iliandikwa kwa mtu mmoja tu! Hapo ndipo kwenye utaalamu wa
Injili ya Kristo, tena kwa herufi kubwa kabisa! Injili ya Kristo
hukuza thamani, kusudi, maana, faida, na wajibu wa kila mtu binafsi.
Ukitaka kuona tumepotoka kiasi gani kwenye wazo na msukumo wa
Injili ya Biblia, jiulize mwenyewe swali hili: Je, umewahi kusikia juu
ya mtu yeyote hivi karibuni aliyeandika kitabu cha aina yoyote ile na
kukituma kwa mtu mmoja ili amlete huyo kwa Kristo?
Siku moja yenye jua kali ambayo haina mawingu, chukua
kioo cha kukuza maandishi na lundo la magazeti, uende nje ukafanye
jaribio. Kunja-kunja kurasa kadhaa za magazeti. Halafu, shikilia
kioo kile cha kukuza herufi juu ya hizo kurasa. Ingawa unakuza
nguvu za mionzi ya jua kupitia hicho kioo, huwezi kuanzisha moto –
ikiwa utasogeza kioo mara kwa mara. Lakini, ukikishikilia hicho kioo
kwa utulivu na kulenga sehemu moja tu na kutoa nafasi kwa hicho
kioo kukuza mionzi ile kwenye kitu kimoja, utapata nguvu za jua na
kuanzisha moto. Na moto siku zote huenea kwenye kitu chochote
kinachoungua! Katika hadithi yetu, Yesu ndiye jua, Luka ndicho kioo
cha kukuza herufi, na Theofilo ndiye sehemu iliyolengwa. Na moto
unawaka, tena, bado unaenea!
116
KWA NINI LUKA ALIANDIKA HIVYO VITABU VIWILI
KWA MTU MMOJA?
Turudie swali letu la awali: Kwa nini Luka aliandika hivyo
vitabu viwili kwa mtu mmoja huyu? Je, tuna jinsi ya kufahamu hilo?
Ndiyo!
Nini hali ya Theofilo wakati Luka alipomwandikia Injili
yake? Bila shaka alikuwa amepotea, mwenye dhambi ambaye
hajaokoka. Luka anamwita “mtukufu Theofilo” (ktk Luka 1:3).
Hivyo ndivyo mtu mkuu wa Kiyunani alivyokuwa anaitwa, kwa
hiyo, huyu Theofilo alikuwa mtu mkuu wa Kiyunani, mwenye cheo
na wadhifa mkuu. Hakuna Mkristo yeyote ambaye ameitwa hivyo
katika Agano Jipya, kwa hiyo, bila shaka mtu huyu alikuwa
amepotea dhambini. Pengine alikuwa amesikia Injili kiasi fulani (ktk
Luka 1:4), lakini hakuwahi kusadiki. Kumbuka kwamba “Wayunani
hutafuta hekima” (ktk 1Wakor. 1:22), na si wepesi kukubali wazo
lionekanalo haliwezekani kwa jinsi ya kibinadamu, kama Injili
(unapoisikia mara ya kwanza). Kwa hiyo, Theofilo alishtuka na
kuhofu ukweli wakati alipoambiwa. Lakini Luka naye alikuwa mtu
wa Mataifa (yaani, asiyekuwa Myahudi), na pia alikuwa na matatizo
ya kiakili kwa habari ya Injili. Lakini, Luka akawa ameshawishika
kabisa kuhusu uhakika na ukweli wa Yesu Kristo na Injili Yake, basi,
akajitolea kuandika maelezo fasaha yenye utaratibu mzuri kuhusu
kweli za Yesu na Injili kwa Theofilo, mtu huyo ambaye hakuwa
amekubali ukweli.117
Basi, nini kusudi la Luka kuandika? Kumleta huyu mtu
mmoja kwa Kristo, apate kumwamini! Utafiti wa muda mrefu, kazi
ngumu na uandishi wote huo – kwa sababu ya mtu mmoja tu – ili
awe na “uhakika wa mambo hayo, ambayo alikuwa amefundishwa”.
Je, Injili ya Luka ilifanikiwa katika hilo? Ndiyo! Tunajuaje? Kwa
sababu katika mstari wa kwanza wa kitabu cha pili, Luka anaondoa
lile jina la cheo chake na kumwita “Theofilo” tu. Basi, hii kazi
kubwa ya uinjilisti ilifanikiwa kwa njia ya ajabu sana. Tabibu mmoja
Myunani, mtaalamu bingwa, alifanya utafiti kuhusu Injili kwa
ukamilifu kabisa na akamwandikia mkuu wa Kiyunani ili
kumshawishi juu ya Yesu na kumfikisha kwa Kristo na wokovu
wake. Na, ilitokea.
Basi, kwa nini Luka aliandika hii barua ya pili – Kitabu cha
Matendo (sura zingine 28 katika Agano Jipya lako)?: Kama huyo
mtu alifanikiwa kumwamini Kristo kutokana na barua ya kwanza,
kwa nini itakiwe ya pili? Ndugu zangu: Jibu la swali hili
linadhihirisha kushindwa vibaya sana kwa kanisa la siku za leo.
Kusudi la Kristo linakuwa ndiyo limeanza tu wakati mtu anapo-
okolewa! Nia ya Kristo ni kumhusisha kila mmoja katika wafuasi
Wake – waaminio wote waliozaliwa mara ya pili – katika shughuli
ya kuwafanya watu kuwa wanafunzi, wenye maono ya dunia, na
wenye kuigusa dunia yote. Mpango Wake ni kwamba kila mwamini
awe mzalishaji wa wazalishaji huku akidumisha mtazamo wake wa
kutaka kufikia “mwisho wa nchi”. Nia Yake ni kwamba tufuate 118
mpango au mfano Wake – kuwaona watu makundi kwa njia ya mtu
mmoja, na kumjenga huyo mtu mmoja ili kuwagusa makundi. Basi,
Kitabu cha Matendo kiliandikwa na Dakta Luka ili kumtambulisha
Theofilo – katika dhana na mwenendo – aingie katika mkakati wa
kuifikia dunia wa Yesu Kristo.
Je, iliwezekana? Je, Theofilo alifanyika mwanafunzi mfanya
wanafunzi, mzalishaji wa wazalishaji? Kweli hatujui, na ni vizuri
zaidi kwa sababu, maana yake ni kwamba kila aaminiye anapaswa
kupewa nafasi zote kwa kuhusishwa kibinafsi, kuwezeshwa kibinafsi,
na kutumwa au kupelekwa kibinafsi - awe anazalisha au hazalishi.
Tunao ushahidi kiasi fulani kwamba Theofilo alishikwa na amri ya
kuwafanya watu kuwa wanafunzi maana, si tunasoma Kitabu cha
Matendo leo? Kwa hiyo, Luka aliandika kitabu kingine cha pili,
kirefu tu (sura 28 katika Biblia yako) ili kumwingizia mtu mmoja
wazo na kuteka moyo wake na kumkaribisha ashiriki katika kazi kuu
kuliko zote duniani.
Kama Roho Mtakatifu wa Mungu anaonyesha huku kuhusika
kwa hali ya juu sana katika maisha ya watu binafsi wa Agano Jipya,
wewe na mimi je, hatupaswi kuwa na kiasi kidogo cha watu binafsi
ambacho tutakuwa tunamimina na kuweka maisha yetu na maono
yetu kwao? Je, mimi sipaswi kuishi na ufahamu wenye kuwaka moto
kuhusu Agizo Kuu, na kutafuta kila njia ya kuufafanua na
kuushirikisha na makundi ya “watu waaminifu, ambao wanaweza
kuwafundisha wengine pia” (ktk 2Timotheo 2:2)?119
USHUHUDA BINAFSI (wa mwandishi)
Hebu niingize ushuhuda wangu binafsi hapa. Nikiwa na
maono ambayo yamekuwa yakipanuka mara kwa mara kwa zaidi ya
robo karne, nimetumia muda mwingi sana na watu binafsi wengi
sana, na makundi madogo madogo mengi sana, na makundi mengi
sana ya wachungaji na wamishenari, na makusanyiko ya makanisa,
nikitafuta kuingiza haya ninayosema. Nimeona mafanikio makubwa
sana kiasi kwamba watu ambao nimefanikiwa kuwashawishi
wametapakaa katika sehemu mbalimbali kwa sasa katika dunia –
wakiwaleta watu kwa Yesu na kufundisha wanafunzi. Vile vile
nimeona kushindwa sana (na hata mwenyewe nimeshindwa kwa njia
ambazo hakika zilimhuzunisha Roho Mtakatifu). Ninaweza kujaza
kurasa nyingi sana kwa maelezo yenye kuthibitishwa kirahisi kuhusu
wanafunzi ambao wamekwenda ili kuzalisha aina hii ya wanafunzi
katika maeneo yao ya huduma. Wengi wao ni wachungaji (nami
nimepata fursa kubwa sana ya kuwafundisha na kuwatia moyo
wachungaji wengi zaidi na kuwatia moyo wale ambao wako katika
huduma tayari), baadhi yao ni wamishenari katika nchi za nje nyingi
tu, na wengine wengi ni “walei” wenye maono hai ya kufanya
wanafunzi mahali ambapo wanakaa, wanafanya kazi na kuabudu.
Ninamshukuru Mungu kwa ajili ya fursa hii ya kipekee, nami
nimejizatiti zaidi leo kuliko wakati mwingine wowote kuhusika na
“kuwafanya watu kuwa wanafunzi”.120
TAMKO LA WAZI LA KUSUDI LA KUANDIKA VITABU
VYAKE
YOTE AMBAYO YESU ALIANZA KUFANYA NA
KUFUNDISHA
Sasa tunatazama sehemu ya mwisho ya muhtasari wetu wa
Matendo 1:1 – tamko la wazi la kusudi la kuandika kitabu cha
kwanza, yaani Injili ya Luka. Luka anasema kitabu hicho kinahusu
“mambo yote ambayo Yesu alianza kufanya na kufundisha”. Ona
maneno tendaji matatu: “alianza” “kufanya” na “kufundisha”.
Maneno mawili hayo yanatupa mtazamo wa jumla wa huduma nzima
ya Yesu. Yesu ndiye mtu pekee katika historia ambaye amefanya
mlingano kati ya shauku ya KiMungu ya kufanya na kufundisha.
Katika kila huduma nyingine, iwe ya kanisa au ya Mkristo binafsi,
kumekuwepo na kutokulingana kwa maeneo hayo mawili.
Hebu fikiri kuhusu makanisa unayofahamu wewe. Mengine
yamezidisha sana eneo la kufanya. Kanuni yao ya utendaji ni kama
inawaambia hivi, “Okoka, halafu shughulika”. Wamekazia zaidi
shughuli lakini hawana mkazo kwenye mafunzo. Wako mbele
kwenye utendaji lakini wako nyuma sana kwenye kanuni na
mafunzo. Mtu mmoja alinieleza kichekesho kuhusu kanisa lake
mwenyewe kwa kusema hivi: “Ndugu, utagundua kwamba kanisa
letu lina upana wa maili 5, na kina cha robo inchi tu”. Alimaanisha
kwamba shughuli ya kukimbizana kwao inaongeza idadi ya watu 121
daima katika kanisa, lakini kwamba kina chake kiroho hakilingani na
kukua kwake kiidadi.
Kwa upande mwingine, yapo makanisa ambayo yamekazia
kupita kiasi jambo la kufundisha. Daima wanalishwa Neno la Mungu
lakini hakuna mlingano unaofaa katika shughuli tendaji za huduma.
Washirika wa makanisa hayo wanaingia kwenye “kuwa na ugumu
wa moyo” ambayo ni aina fulani ya kuridhika na kujisikia
kunakoweza kupelekea majigambo na hatimaye hali ya kujihesabia
haki. Makanisa hayo yanakua kiasi cha kuridhisha, lakini Agizo Kuu
si ajenda muhimu ndani yao. Watabishana kuhusu maana ya kidole
cha tatu cha mguu wa kushoto kwenye sanamu ya Danieli, lakini
hawatajali hata kidogo mabilioni ya watu ambao bado hawajafikiwa
na Injili katika dunia yetu.
Yesu alikuwa na mlingano kamili kati ya kutenda na
kufundisha katika huduma Yake, na kila mmoja wetu anatakiwa
kutafuta hali hiyo kwa njia ya maombi katika maisha yetu na
makanisa tunayohudhuria na tunayofanya huduma.
Tunafikia kwenye neno “kubwa” tendaji katika Matendo 1:1.
Hilo ni neno “aliyoanza”. Injili ya Luka ilikuwa inahusiana na
mambo “yote ambayo Yesu alianza kufanya na kufundisha”. Hayo
matukio ya kihistoria katika maisha ya Yesu yanayotajwa mapema ni
mwanzo tu! Kama ni hivyo, yaani, kama “kitabu kile cha kwanza”
kilihusiana na mambo ambayo Yesu “alianza kufanya na
kufundisha,” basi kitabu hiki cha sasa, yaani Kitabu cha Matendo ya 122
Mitume, kitakuwa kuhusu mambo yote ambayo Yesu anaendelea
kufanya na kufundisha. Lakini hapa tunapata tatizo mara moja.
Katikati ya sura ya kwanza ya Kitabu cha Matendo, huyo “mtendaji
na mwalimu” – yaani Yesu, anatoweka! Sasa, aliendeleaje kufanya
na kufundisha katika sura ishirini na saba na nusu zaidi kama
ameondoka machoni pao?
YESU ANAFANYA NINI WAKATI HUU?
Hebu tupanue hilo swali, hivi: Yesu anafanya nini kwa wakati
huu wa sasa? Anaendelea kufanya na kufundisha kwa kiwango cha
nia na kusudi Lake katika dunia yetu siku hizi, kama alivyofanya tu
wakati akiwa hapa siku za mwili Wake. Lakini, sasa anafanya vipi na
huku haonekani? Anafanya kwa njia ile ile aliyofuata wakati akiwa
hapa katika mwili Wake wa kibinadamu. Je, mbinu hiyo ilikuwa ipi?
Tunaiita “kufanyika mwili” ambayo maana yake ni kwamba “Neno
(logos, ‘wazo la Mungu’) alifanyika mwili, akakaa katikati yetu”.
Kwa hiyo, Mungu alishuka mpaka kiwango chetu kama binadamu
katika Nafsi ya Mwana Wake mpendwa, Yesu, na akaishi, akatenda
na kufundisha miongoni mwa watu. Je, siku hizi anatumia mtindo
gani? Huo huo kama wakati ule, ila, kuna marekebisho kidogo, kama
ifuatavyo:
1. Anakaa katika miili ya waaminio wote waliozaliwa mara
ya pili, kwa kusudi la kuendeleza utendaji Wake na kufundisha
Kwake kupitia kwao;123
2. Tofauti na Yesu ni kwamba, kila mmoja wao (yaani sisi) ni
mwenye dhambi;
3. Kuna tofauti katika sifa kwa maana ya kwamba hakuna
yeyote kati yetu ambaye ni Yesu. Yeye ni Mwana wa Mungu wa
kipekee, mmoja tu.
Kwa marekebisho hayo kidogo, kila aaminiye anatakiwa
kuwa nyongeza ya Yesu Kristo kufanyika mwili! Mara tu mwenye
dhambi anapookolewa, Yesu Kristo huingia ndani kabisa ya maisha
ya mtu huyo kwa Uwepo na nguvu za Roho Mtakatifu. Roho
Mtakatifu ameelezwa kama “Nafsi Nyingine Ya Yesu” na anaweza
kueleweka kwa urahisi tu kwamba ni Yesu pasipo mwili”. Basi, kila
aaminiye ni kasha lililo hai la Uwepo Binafsi wa Mwana wa Mungu,
na kusudi la msingi kwa ajili ya hilo ni ili huyo aaminiye awe
mwendelezo wa kudumu wa utendaji na mafundisho ya Yesu.
JE, YESU ALITUMIA WATU AINA GANI?
Hii inasabisha swali lingine, tena la muhimu sana. Je, Yesu
alitumia watu wa aina gani katika Kitabu cha Matendo, ili
kuendeleza utendaji na mafundisho Yake baada ya kupaa Kwake?
Cha kufurahisha ni kwamba, katika ile mistari ya kwanza ya Kitabu
cha Matendo tunapata jibu kamili la swali hilo. Mistari hiyo inatupa
picha nzuri tu ya wafuasi wa kwanza wa Kristo. Hebu tuchore picha
zao.
124
1. WATU WA KAWAIDA
Cha kwanza ni kwamba, walikuwa watu wa kawaida.
Tunahitaji kukumbuka tu yote tuyajuayo juu yao kutoka katika Injili
kuona ukweli huo. Walikuwa ni mchanganyiko kutoka katika jamii,
watu wa kawaida kabisa. Wote isipokuwa mtu mmoja walitoka
Galilaya, na huyo mmoja alikuwa “yai bovu” – Yuda Iskariote.
Galilaya lilikuwa jimbo dogo lililodharauliwa sana katika Dola ya
Kirumi, na watu kumi na moja wa kwanza kabisa waliomfuata Yesu
walitoka huko. Walikuwa kundi la watu ambao “si chochote wala
lolote”, lakini akawatengeneza mpaka wakawa mashujaa Wake. Hili
linapaswa kumfanya kila mmoja wetu ajisikie vizuri sana kwa
sababu Yesu Kristo hahitaji kitu chochote kwetu kwa ajili ya
kufanikisha kusudi Lake kupitia kwetu isipokuwa kujitoa kwetu –
sisi ambao ni udongo wa kawaida tu.
2. WATU WALIOCHAGULIWA
Kinachofuata ni kwamba, walikuwa watu waliochaguliwaa.
Tazama mstari wa 2 wa Matendo sura ya kwanza. Watu Wake wa
kwanza wanaitwa “Mitume aliokuwa amewachagua”. Walichaguliwa
kwa ajili gani? Neno “mitume” linatupa kuona mambo makubwa
sana. Neno “mtume” linamaanisha “mtu aliyetumwa”. Aliwachagua
ili awatume popote alipotaka waende ili waweze kuwa, waseme na
kufanya chochote alichokitaka! Na hii ndiyo sababu alikuchagua
wewe na mimi! Ona lile neno “aliowachagua” mwishoni mwa mstari 125
wa pili. Kila neno tendaji la Kiyunani hutumika katika sauti tatu:
sauti ya kutenda, kutofanya chochote, na sauti ya katikati. Katika
sauti tendaji, mhusika hutenda, kama vile “Ninakimbia,”
“ninasimama,” “unatembea”, “unazungumza”. Katika kila tukio,
mada hutenda. Kutofanya chochote maana yake ni kwamba mhusika
hutendewa. Kwa mfano, “Nilikanyagwa!” Sauti ya katikati
huunganisha zile zingine mbili kiasi kwamba mhusika hutenda,
lakini kwa njia ambayo matokeo ya tendo humrudia yeye.
Sasa hili neno tendaji “waliochaguliwa” ni la sauti ya katikati
na hutupa kweli moja ya muhimu na ya kushangaza sana. Maana
yake ni kwamba, wakati Mungu alipokuchagua wewe, alikuchagua,
si kwa sababu ya wewe kufaidika – yaani upate afya, mali na furaha,
bali alikuchagua kwa ajili Yake Mwenyewe! Wewe ni Mkristo kwa
ajili ya Kristo! Uko hai kwa ajili Yake! Basi, wewe si Mkristo ili
mahitaji yako yatoshelezwe, au ili ujitosheleze mwenyewe na
kujiridhisha, bali ili utumiwe na kutumwa na Yesu Kristo kama
mwendelezaji wa utendaji Wake na kufundisha Kwake.
Nilipokuwa mvulana mdogo, baba yangu alinifundisha
kupenda mchezo wa kandanda. Kujua kwangu mchezo huo kulitoka
kwa baba, na ushindani wangu katika mchezo huo ulitoka kwa mama
yangu. Watoto wa pale mtaani walikuwa wanacheza kandanda mara
nyingi siku za Jumamosi katika sehemu iliyokuwa wazi kando ya
nyumba yetu. Nakumbuka jinsi nilivyokuwa nawakasirikia wakuu wa
timu kwa sababu, juma baada ya juma sikuwa nachaguliwa kuingia 126
kwenye timu, na kwa sababu hiyo, sikupata kucheza. Lakini pia
nakumbuka siku ya kwanza nilipochaguliwa kucheza. Hawakuwepo
wachezaji wa kutosha, ndipo mimi nikachaguliwa! Sikuhitaji muda
mrefu kutambua kwamba yule kiongozi wa timu hakunichagua kwa
sababu alinipenda. Yeye alinichagua kwa sababu alifikiri
kunichagua kungemsaidia ashinde mchezo.
Sijui kama mfano huo unaeleweka. Yesu Kristo ananipenda,
na hakuna ninachoweza kufanya kitakachomfanya aache kunipenda!
Hanipendi kwa kuwa ninapendeka, au ni mzuri, au nina upendo.
Ananipenda kwa sababu Yeye ni upendo – basi! Lakini,
hakunichagua kwa sababu alinipenda tu, pamoja na kwamba upendo
Wake ni mkubwa kama ulivyo. Alinichagua (pia) kwa sababu
alijisikia kwamba kunichagua mimi kungesaidia upande Wake
kushinda mchezo! Sasa je, kushiriki kwangu katika utume Wake wa
dunia nzima kunaweza kumfanya aone kwamba uchaguzi Wake
“ulistahili”? Au je, mimi “nimetulia huko Sayuni” tu, bila ya kufanya
chochote kuhusu kusudi la Kristo la dunia nzima?
Kila Mkristo asomaye maneno haya anapaswa atulie hapa na
kujiambia hivi: “Nimechaguliwa na Mfalme wa Wafalme wote!
Nimechaguliwa na Bwana wa utukufu! Je, ninatimiza kusudi Lake la
kunichagua?”
127
3. WATU WALIOSADIKI
Halafu, walikuwa watu waliosadiki. Tunasoma hivi katika
Matendo 1:3, “Yesu Mwenyewe alijidhihirisha kwao akiwa hai
baada ya kufa Kwake kwa uthibitisho mwingi sana (yaani, ushahidi
usioweza kupingwa), akionekana nao kwa muda wa siku arobaini.”
Ndiyo maana baadaye, mmoja wao alikuja kuandika hivi,
“Tumeliona Neno la Uzima sisi wenyewe, kwa macho yetu” (ktk
1Yohana 1:1, TLR).
Vile vile kuna kipengele kingine cha haya maneno machache
tu kutoka Matendo 1:3 ambacho kinahitaji kutazamwa kwa makini.
Kinatokana na neno la Kiyunani “dia” ambalo maana yake “kati ya”.
Yesu “alionekana nao kati ya siku arobaini”. Hee! Mbona ni neno la
ajabu hilo! Nini maana yake? Maana yake ni kwamba kuonekana
Kwake na wanafunzi hakukuwa moja kwa moja katika siku zote
arobaini. Alionekana na kutoweka kama alivyopenda Mwenyewe
kwa hizo siku arobaini. Alitokea akaonekana, halafu akatoweka
asionekane, kama alivyopenda mwenyewe katika kipindi hicho cha
siku arobaini.
Hebu tuseme kwamba mimi na rafiki yangu tuko katika
mazungumzo mazito. Katika hali hiyo tunatazama vizuri. Lakini
ghafula, mwili mwingine unatokea katikati yetu! Wee! Kitu cha aina
hiyo kinashtua sana! Ndiyo maana ilikuwa kawaida kwa Yesu
kuanza mawasiliano Yake kwa maneno haya, “Msiogope” au “amani
iwe kwenu”. Sasa, mimi na rafiki yangu tunasahau kabisa 128
mazungumzo yetu na kushikwa kabisa na huyu mtu “aliyeingilia
kati”. Na hebu tuseme kwamba, tukiwa tumemkazia macho kiasi
hicho, mara tena anatoweka! Hayo ndiyo yaliyotokea mara kwa mara
katika kipindi cha siku zile arobaini baada ya kufufuka Kwake. Yesu
alitokeza na kutoweka tena na tena katika kipindi hicho.
Kitu cha ajabu hicho! Kwa nini alifanya hivyo? Alikuwa
anataka wanafunzi Wake wajue bila ya mashaka wala maswali
kwamba, awe anaonekana au haonekani, alikuwa pamoja nao wakati
wote! Na ni kweli hata siku hizi. Yesu Kristo yupo sana katika Nafsi
ya Roho Mtakatifu, kiasi kwamba anaweza kutokea katika umbo la
mwili – akitaka kufanya hivyo. Lakini kusudi Lake alilotamka ni
kwamba kila aaminiye ampe Yeye “mwili” kwa kuutoa mwili wake
kuwa “hekalu”, kuwa “Patakatifu pa Patakatifu”, kuwa mahali teule
kwa ajili ya Yesu kujionyesha Mwenyewe.
Unaonaje? Si ungesadiki kabisa kama ungemwona Yesu
kama wao walivyomwona? Kuwa mwangalifu sana hapo. Yesu
Mwenyewe alionyesha kwamba, kwa sababu ya Uwepo wa Roho
Mtakatifu, sisi ndiyo wenye faida, wala si wale waaminio wa kwanza
(ktk Yohana 16:7).
Swali: Wewe unasadiki kiasi gani kuhusu uhalisi wa Yesu?
Kuhusu uhalali wa madai Yake? Kuhusu ukweli wa nafsi Yake?
Kuhusu uwezo alio nao na mamlaka Yake? Kuhusu kusudi Lake la
utume duniani kote? Hakuna kazi kubwa ya Mungu iliyowahi
129
kufanyika kupitia watu wasiosadiki. Mungu na afungue macho yetu
kwa upya na kwa ukamilifu kuhusu Nafsi na kusudi la Yesu.
4. WATU WALIOPEWA AMRI
Kisha, walikuwa watu walioamrishwa. Matendo 1:2 inasema
kwamba, “Yesu kwa njia ya Roho Mtakatifu aliwapa amri”. Mstari
wa 4 unaongezea yafuatayo: “Baada ya kukutanika nao, Yesu
aliwaamuru kwamba wasiondoke Yerusalemu, bali waingojee ahadi
ya Baba, ambayo, kama alivyowaambia, ‘Mmeisikia kutoka
kwangu’.” Hiyo “ahadi ya Baba” ni Siku ya Pentekoste, siku ambapo
nguvu za ukombozi kamili za Roho Mtakatifu zilitolewa, siku
ambayo ingefuata muda si mrefu baada ya hapo.
Je, unaweza kufikiri kidogo mawazo ya mtu kama Simoni
Petro, mtu asiyetulia, asiye na subira kwa wakati huyo? Pengine
alisema hivi: “Yesu! Mbona huamui unachotaka? Umetumia miaka
mitatu kutuandaa twende, na sasa unatuambia tungoje!” Lakini,
hakuna hoja kama hiyo iliyotolewa. Kufikia wakati huu, Mitume
walikuwa wamekwisha jifunza kwamba Yesu si wa kubishana Naye.
Maana, Yeye ambaye ni Bwana Mkuu wa ulimwengu wote, yuko
sahihi wakati wote! Kanisa la leo lipate hekima kama hiyo!
Linatakiwa kutumia muda wake mwingi katika kuomba na
kuchunguza Biblia ili lisadiki kwamba linatenda kulingana na Akili
ya Kristo, halafu litumie muda wake mwingi kumtii Yeye!
130
Waarabu wa kale walikuwa wanazalisha aina maalum sana
ya farasi, na wakati mwingine walikuwa wanaitwa “farasi wa
KiArabu”. Hapo kwanza walikuwa wanazalishwa kwa ajili ya
kupandwa na wafalme tu. Sasa – kama sehemu ya mafunzo yao,
mfundishaji alikuwa anabeba firimbi na kamba ya ngozi kwenye
shingo yake. Kwa muda wa miezi mingi sana, farasi alikuwa
anafundishwa kuacha kufanya kila kitu akisikia firimbi ya mwalimu.
Alitakiwa kumwelekea yeye. Ilikuwa lazima kutii kikamilifu. Kukataa
kidogo tu kulihesabiwa ni kutokutii kabisa. Ndipo kwa muda wa siku
tano farasi angenyimwa chakula, na kwa siku tatu angenyimwa maji
ya kunywa. Katika kipindi hicho cha kumalizia mafunzo, alikuwa
anafungiwa katika zizi.
Siku ya mwisho, vyombo vyenye chakula na maji viliwekwa
mahali panapoonekana, kiasi cha mita kama hamsini hivi kutoka
zizini. Farasi angejitahidi kukifikia chakula na maji, kwa sababu ya
kuwa na njaa. Halafu ghafula, mlango wa zizi ungefunguliwa, na
yule farasi aliyeshangaa angeanza kuelekea kwenye vyombo vyenye
chakula na maji. Lakini akiwa anakaribia kufika, mwalimu
aliyesimama pembeni angepuliza filimbi! Farasi yule
angechanganyikiwa. Ilibidi afanye uchaguzi kwa haraka. Wa aina
gani? Je, aende kwenye vyakula na maji, au amfuate mwalimu?
Kama farasi angeendelea kwenda kwenye vyombo na kutosheleza
njaa yake na kiu yake, na kwa kufanya hivyo awe amekataa kumtii
mwalimu, basi angeanza upya mafunzo, au angetolewa katika 131
utaratibu huo wa mafunzo. Kama farasi huyo angechagua kinyume
cha hisia na kujisikia kwake na kumtii mwalimu na kufuata utaratibu
wa mafunzo kwa kumwendea mwalimu kwanza, basi aliruhusiwa
kwenda kunywa maji na kula chakula kilichokuwepo.
Wapendwa: Kila siku sisi tunakabiliwa na uchaguzi kama
huo. Tutachagua nini – vyombo vya chakula, yaani kujitosheleza, au
amri za Mwalimu. Hao walikuwa watu walioamrishwa, na Yesu
anatazamia na sisi tufanye hivyo hivyo kama wao.
5. WATU WALIOTAWALIWA
Hatimaye, walikuwa watu waliotawaliwa. Katika mstari wa
4, Yesu alisema nao kuhusu “ahadi ya Baba” iliyokuwa inahusu ujio
wa Roho Mtakatifu kwa ajili ya kuliwezesha Kanisa Lake Siku ile ya
Pentekoste.
Katika mstari wa 5 alisema hivi, “Mtabatizwa katika Roho
Mtakatifu siku si nyingi zijazo”. Tulisema Roho Mtakatifu ni kama
“Yesu asiye na mwili”. Basi, atafanya mambo yale yale, atafuata
makusudi yale yale na kujenga watu aina ile ile ambayo Yesu
alijenga, alipokuwa hapa katika mwili. Kama Yesu alitoa watu wasio
na mwelekeo na wasiosikia la mtu, basi na Roho Mtakatifu atatoa
watu aina hiyo hiyo. Lakini, Yesu hakutoa watu wa namna hiyo.
Alitoa watu waliokuwa wameandaliwa vizuri kitaaluma, wenye
ujuzi, na wenye kuhusika. Walikuwa watu ambao wangeweza
kumwakilisha Yeye katika hali yoyote. Walikuwa watu 132
walioshughulikia mambo yote kuhusu Neno la Mungu na kulifanyia
kazi vizuri kabisa katika kila hali.
Na sasa, tangu Siku ya Pentekoste, Roho Mtakatifu ni “Rafiki
Anayekaa Nasi” aliyeko kila wakati na aliye tayari kutawala na
kututia nguvu kwa ajili ya Utume wa Bwana wetu. Je, umejazwa na
huyo Roho Mtakatifu aliye mkuu na mpole? Je, unatawaliwa na
Yeye kwa ndani ili aweze kuamua tabia yako, mwenendo wako, na
ratiba utakayofuata maishani – au unayofuata maishani?
133
Sura Ya 5Vinavyotakiwa Ili Kufanya Wanafunzi
Au
Dawa Ya Daktari Kutibu Tatizo La Kuacha Agizo Kuu
“Kwa kuwa watu wengi wametia mikono kutunga kwa taratibu habari za mambo yale yaliyotimizwa katikati yetu, kama walivyotuhadithia wale waliokuwa mashahidi wenye kuyaona, na watumishi wa lile Neno tokea mwanzo, nimeona vema mimi nami, kwa kuwa nimejitafutia usahihi wa mambo hayo yote tangu mwanzo, kukuandikia kwa taratibu, Theofilo mtukufu, upate kujua hakika ya mambo yale uliyofundishwa.”
Luka 1:1-4
“Maana (kama inavyojulikana vizuri tu) wengi wamechukua jukumu la kupanga kwa utaratibu na kuandika maelezo (kamili) ya matendo yaliyothibitika na kutimizwa kwetu na katikati yetu, kama tulivyosimuliwa moja kwa moja na wale ambao tangu kuanza (rasmi kwa huduma ya Yesu) walikuwa mashahidi waliojionea kwa macho yao wenyewe na wahudumu wa lile Neno (yaani, fundisho kuhusu kupatikana kwa wokovu katika ufalme wa Mungu kwa
134
njia ya Kristo) . Nilipoona kwamba ni vizuri na kitu cha kutamanika kwangu pia (nimekusudia), na baada ya kufanya uchunguzi kwa bidii na kufuatilia mambo yote kwa ukaribu na kwa usahihi, kuanzia mwanzo kabisa, yale mambo makubwa hadi madogo kabisa, kukuandikia maelezo yenye kufuata utaratibu mzuri, Ewe Theofilo mheshimiwa, (kusudi langu ni) ili upate kujua kweli kamili, na kuelewa kwa uhakika na kwa usalama dhidi ya makosa maelezo (au historia) na itikadi za imani ile ambayo ulijulishwa, na ambayo ulifundishwa kwa kuelezwa tu.”
Tafsiri Ya Biblia Fafanuzi
“Kwa kuwa waandishi wengi wamechukua jukumu la kuandika masimulizi kuhusu kweli ambazo zilithibitishwa miongoni mwetu, kama ambavyo mashahidi walioona mambo hayo ambao walikuja kuwa wahudumu wa ujumbe huo walivyotuambia, mimi nami, Ee mheshimiwa Theofilo, kwa kuwa nimechunguza yote kwa makini sana tangu mwanzo, nimejisikia niyaandike kwa mfululizo mzuri kwa ajili
135
yako, ili uweze kujua vizuri uhakika wa mambo hayo uliyofundishwa.”
Tafsiri ya Biblia ya Williams
“Mwandishi, kwa Theofilo:- Waandishi wengi wamejitahidi kuandika maelezo ya matukio yaliyotokea miongoni mwetu, wakifuata mapokeo tuliyopewa na wale walioyaona kwa macho yao wenyewe na watumishi wa Injili. Basi na mimi kwa zamu yangu, Ee Mheshimiwa, kama mtu aliyepitia kwa makini sana mambo hayo yote, nimeamua kuandika simulizi lenye umoja kwa ajili yako, illi nikupe maarifa hakika kuhusu mambo ambayo umeambiwa.”
Tafsiri Ya Biblia Mpya Ya Kiingereza
Katika Zaburi 119:18 kuna sala hii: “Fungua macho yangu
Ee Bwana, nipate kuona mambo ya ajabu yaliyo katika sheria Yako”.
Hebu nikushauri wewe pia uombe sala hii daima unaposoma na
kujifunza sura hii. Halafu, tunasoma hivi katika Zaburi 119:130,
“Neno Lako linapoingia, linaleta mwanga; linatoa ufahamu kwa
asiyekuwa na ufahamu.” Na iwe hivyo tunapojifunza kwa pamoja.
Basi tuanze mafunzo yetu kwa kutazama kwa makini sana
mtiririko ulioko kwenye mchoro huu:
136
NENO MWILI NENO MWILI NENO (weka
jina lako hapa) NENO MWILI.
Mtiririko huu unawakilisha jinsi ambavyo Injili huenea
miongoni mwa watu katika historia ya Ukristo (ktk Warumi 10:14).
Unaanzia kwa “Neno” – “Logos” – kufanyika mwili na kukaa
katikati ya wanadamu (ktk Yohana 1:14). Baada ya hapo, kila kuenea
(au kusonga mbele) ni mtindo ule ule ambao umerekebishwa kidogo,
yaani, Neno kufanyika mwili. Katika muda muafaka, kwa muujiza
wa neema ya Mungu na uwezo Wake, wokovu Wake “ulifanyika
mwili” ndani yako. Hapo, jina lako likaingia katika mtiririko kama
ilivyoonyeshwa hapo juu – na mwelekeo wako wa maisha pamoja na
kazi vikabadilika milele. Sasa, swali muhimu sana: Kwa kuwa jina
lako limeingizwa katika mtiririko huo, je, mtiririko utaendelea
kupitia kwako? Au kiunganisho hicho kitakatikia kwako
utakapokufa? Je, mtiririko unaweza kuwa kama ifuatavyo? MWILI
NENO MWILI …? Je, mtiririko uliokusudiwa kuendelea
utakomea kwako?
Hebu kabiliana na hilo swali kwa mara nyingine tena: Je,
mtirtiriko utaendelea katika historia kutokana na nafasi au sehemu
yako uliyofanya wakati ukiwa hai? Ili mtiririko uendelee na wewe,
kuna kazi ambayo lazima ujifunze, nayo imekwisha fafanuliwa na
kupangwa kwa ajili yako vizuri sana katika Neno la Mungu. Kama
utakachofanya ni kumleta mtu kwa Kristo tu, kiunganisho kinaweza
kukatikia kwa huyo mtu utakayemleta kwa Kristo. Kama utamleta 137
mtu kwa Kristo na kumfundisha pasipo kufahamu kikamilifu na
kutekeleza kile “kiwango” (cha kufanya wanafunzi wenye maono ya
dunia, mguso wa dunia, na wenye kujiongeza), huenda huo mtiririko
ukakatikia kwa huyo utakayemleta kwa Kristo na kumfundisha.
Ukweli ni kwamba, utamfanya kuwa “Mkristo bora” tu. Ni pale
unapomleta mtu kwa Kristo na kumfundisha kulingana na kiwango
kilichofunuliwa katika Biblia ndipo Mungu atakapohakikisha
kwamba mtiririko ule hautakatika, na wewe mwenyewe utahakiksha
kuendelea kwake kwa kuweka msingi kwa ajili ya vizazi vingi vya
baadaye.
Injili ya Luka, iliyoandikwa na mtu pekee ambaye hakuwa
Myahudi, ni kitabu kikubwa sana chenye kujaa shughuli ya kufanya
wanafunzi watakaofikia dunia nzima. Kufanya wanafunzi wenye
maono na watakaofikia dunia nzima ndicho kiwango cha kuendelea
mbele kwa Injili katika Agano Jipya. Kumbuka kwamba Luka
hakuwa mtume, hakuwa mhubiri, hakuwa mwinjilisti, wala hakuwa
hata shemasi. Luka alikuwa mtu wa Mataifa – asiyekuwa Myahudi.
Alikuwa mwanasayansi, tabibu na mwanahistoria asiyekuwa
mtaalamu ambaye aliwezeshwa na Roho Mtakatifu kuandika kitu
ambacho hakina makosa. Luka alifanya aliyofanya kwa sababu ya
kupenda shughuli hiyo. Dakta Luka ni mfano mkuu wa milele wa
kile kiwango cha NENO KUWA MWILI KUWA NENO katika
Agano Jipya. Mistari minne ya kwanza katika Injili kulingana na
Luka inafanyika utangulizi wa kitabu hicho, na ni kama iliandikwa 138
baada ya kitabu chote kukamilika (kutokana na jinsi maneno
yalivyopangwa). Katika hiyo mistari, tunaona mfano mmoja mkuu
sana wa kufanya mwanafunzi upatikanao katika Biblia.
Katika utangulizi wake wa ajabu sana, Dakta Luka
anaonyesha tabia nne muhimu sana za mtu anayefanya wengine
kuwa wanafunzi, aliye na maono ya dunia na mwenye lengo la
kugusa dunia na kujiongeza. Mwanafunzi yeyote anayetaka kujua
uhalisi wa ukubwa wa maono ya Mungu yeye mwenyewe na kwa
ajili ya kizazi chake na vizazi vifuatavyo, lazima aingize tabia hizo
na kuzifanya zake katika maisha yake, na ni lazima naye azijenge na
kuzitia ndani ya kila mwanafunzi ambaye Mungu atampa.
Dakta Luka alikubali wajibu binafsi kwa ajili ya kumjenga
Theofilo. Aliingia katika utafiti mzito kwa niaba ya Theofilo.
Aliandaa vitendea kazi thabiti kwa ajili ya kumwezesha Theofilo, na
alifanya kila kilichowezekana kibinadamu kuzalisha kwa mpango wa
kudumu wanafunzi wengine wenye maono ya dunia, wenye mguso
wa dunia na wenye kujiongeza, kwa njia ya Theofilo. Soma sentensi
ya mwisho kwa makini sana, ukifikiri vizuri kabisa – “Yatafakari
ninayosema, na Bwana akupe ufahamu katika mambo yote” (ktk
2Timotheo 2:7).
WAJIBU BINAFSI
139
Kama wewe unataka kufuata kiwango cha Agano Jipya,
lazima ukubali kuwajibika kibinafsi kwa ajili ya kuwajenga watu
kuwa wanafunzi kulingana na Agano Jipya.
Luka alianza kwa kukubali juhudi nzuri za wengine, katika
kutayarisha maelezo kuhusu maisha na huduma ya Yesu. Ingawa
wengine walikuwa wamefanya kazi kubwa na ngumu ili kuandika
masimulizi kuhusu Yesu, Luka alisema, “Niliona ni vizuri hata mimi
pia …” Roho Mtakatifu alikuwa anafanya kazi kwa njia ya Luka ili
atende zaidi ya jinsi Luka alivyoweza kufikiri. Luka aliona mtu
mmoja tu – Theofilo. Mungu aliona vizazi vingi sana – mpaka na
sisi! Luka aliandika kitabu kimoja kwa mtu mmoja. Mungu aliandaa
Injili ya ajabu sana kwa ajili ya vizazi vyote vya wakati ujao! Sisi
tunawea kuona mwanafunzi mmoja tu, lakini Mungu anaona
makundi ya watu ambao watafikiwa na kuguswa na huyo
mwanafunzi mmoja.
Historia ya Kanisa la Kikristo inathibitisha kwamba hii dhana
ya KiMungu ni rahisi sana kiasi cha akili za kibinadamu kushindwa
kuiona. Usipofanya watu kuwa wanafunzi, ni kwamba hukubaliani na
kiwango cha Yesu, na unaacha kutii amri ya Yesu. Usipowajenga
wanafunzi wako kufikia kiwango cha kuwa na maono ya dunia
nzima, kuweza kuigusa dunia nzima, na kukamilisha utaratibu wa
kufanya wanafunzi wanaoweza kujiongeza wenyewe, hujakubaliana
wala kulingana na kiwango cha Yesu – pasipo kujali mengine yote
yanayoendelea katika maisha yako! Injili yenyewe imejengwa 140
kwenye kukubaliana na Mungu (ktk Warumi 10:9; Mathayo 10:32,
mahali ambapo “kukiri” maana yake kukubaliana na) kuhusu sisi
kutolingana na kiwango Chake. Basi, tunaletwa na Roho Mtakatifu
kwenye kukubaliana na Mungu kuhusu jinsi anavyomwona Mwana
Wake, Yesu Kristo. Maisha yetu yote baada ya hapo yanapaswa
kuwa ni makubaliano na Mungu na mapenzi Yake. Tunapotazama
amri Yake na kiwango Chake, tunaona kwamba haitoshi kwa
Mkristo binafsi kuanza tu kuwahudumia watu, kuwa mtu mzuri kwa
watu, kutafuta kukutana na mahitaji ya watu, au kuwa mhudhuriaji
mzuri tu na mwaminifu kanisani. Lazima tuamue kati ya sisi
wenyewe (“kujikana wenyewe,” ktk Mathayo 16:24) na kukubaliana
na Mungu. Na kwa kuwa tunaambiwa kulitimiza Agizo la Yesu
“tukiwa tunakwenda”, hatupaswi kupiga hatua hata moja bila ya
kutekeleza Agizo Lake na Mbinu Zake pia.
Fikiri maneno ya Bwana wetu katika Yohana 15:16, “Ninyi
(mkazo mkubwa kabisa) hamkunichagua Mimi, bali Mimi (mkazo
mkubwa) ndiye niliyewachagua ninyi na kuwaweka, ili ninyi (mkazo
mkubwa) mwende na kuzaa matunda (tendo linaloendelea, mkazo
mkuu) na kwamba matunda yenu yapate kudumu (kitu
kinachoendelea wakati huo huo), ili chochote mtakachomwomba
Baba kwa jina Langu, aweze kuwapa.” Je, nini kazi ya matunda? Mti
unaozaa matunda hauli matunda yake wenyewe; ni kwa ajili ya
mwingine. Sehemu moja ya tunda ni ili kuliwa, lakini sehemu
nyingine ya tunda ni ili kuzaliana. Mbegu katika tunda huendeleza 141
utaratibu wa kuzalisha chakula na kupatikana kwa matunda mengine.
Je, katika embe kuna mbegu ngapi? Moja tu! Lakini, kuna maembe
mangapi katika hiyo mbegu moja? Mungu tu ndiye ajuaye!
Umeingizwa katika Ufalme wa Mungu ili uwajibike kibinafsi
kwa ajili ya mtu anayekuja. Lakini, hakuna kitakachotokea tu! Leo
utakutana na watu wengi wasiohesabika katika makundi ya maishani,
ambao wanaweza kupatikana kwa ajili ya shughuli ya kufanya watu
kuwa wanafunzi (wakiingizwa kazini vizuri, na wakipata habari
sawasawa, na kufundishwa sawasawa) – na pengine hutamjali hata
mmoja wao. Bila ya “kuona na kusikia” kwa mtazamo wa Mungu
hutaweza kutimiza wajibu wako binafsi kwa ajili ya mtu anayefuata.
Naomba nikukumbushe kwamba, lile swali “Kwani mimi ni
mlinzi wa ndugu yangu?” lilitolewa kwa Mungu kutoka moyoni mwa
muuaji wa kwanza duniani, aliyekuwa anajitetea na mwenye kujaa
chuki moyoni! Nisipojiunga na Yesu katika kuwajibika kibinafsi kwa
ajili ya kumjenga mtu anayefuata ili afikie dunia nzima, mimi
ninajiunga na mawazo ya muuaji. Jibu la Mungu kwa swali la Kaini
likawa, “Ndiyo. Wewe ni mlinzi wa ndugu yako. Tena – muhimu
zaidi – wewe ni ndugu ya ndugu yako!” Sasa, unafanya nini kuhusu
Habili wako? Hebu useme pamoja na Luka kwamba, “Niliona ni
vizuri na mimi pia. Ninachukua wajibu binafsi kwa ajili ya mtu
ambaye Mungu kanipa.”
UTAFITI MZITO142
Kama unataka kufuata kiwango cha Agano Jipya, lazima
uingie katika utafiti mzito wa Neno kwa ajili ya mwanafunzi wako.
Yesu alisema hivi: “Ninajitakasa mwenyewe kwa ajili yao”, na
maisha yako lazima yalingane na Yake. Haitoshi tu kujifunza Biblia.
Kuna watu kila mahali ambao wamo katika kujifunza Biblia ambao
hawatawahi kumjenga mtu mmoja anayefanya watu kuwa wanafunzi
ambaye anajiongeza, atakayeigusa dunia. Kwa nini? Sababu ni rahisi
tu: mtazamo wa mwalimu wa Biblia na hata wa mwanafunzi
anayejifunza Biblia hiyo hawana maono kwa ajili ya kuigusa dunia.
Wale wanaohusika katika kujifunza Biblia hawaioni kama njia kwa
ajili ya kuifidia dunia, wala hawatengenezi mtaala kutokana na
kujifunza Biblia kwao ili kuwajenga watu watakaoigusa dunia kwa
makusudi. Badala yake, wanajifunza Biblia ili “kujua zaidi” na kuwa
“Wakristo bora zaidi”. Mpaka inafikia mahali pa kutiliwa mashaka
ikiwa kweli hayo ni makusudi mazuri na yanayofaa kwa ajili ya
Mkristo. Yanaonekana kama ni malengo ya “kuufanya Ukristo
kununulika kwa mteja”. Kibaya zaidi ni kwamba, hilo huzalisha
kuingia kubaya kwa Injili, badala ya upandaji utakaozaa, wenye
kusababisha mavuno makubwa sana ya kiroho hadi miisho ya dunia,
mpaka wakati wa mwisho kabisa. Mtu yeyote anaweza kujisomea
Biblia kwa faida yake mwenyewe. Lakini, uwezo wa kuigusa dunia
unatokana na maisha ya wale ambao kwa makusudi kabisa wanaingia
katika utafiti wa dhati kabisa kwa ajili ya kusudi la kumjua na
143
kumfuata Kristo kweli kweli na kumfanya Yeye ajulikane kwa
wengine.
Tazama Luka 1:3 na utazame lile neno “kuchunguza”. Hili
neno lina uzito sawa na “kutumia kwa uhalali” katika 2Timotheo
2:15, na ndiyo neno “kujulikana kabisa” katika 2Timotheo 3:10,
ambapo Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Wewe umeyajua vizuri
mafundisho yangu, jinsi ninavyoishi, makusudi yangu, imani yangu,
uvumilivu wangu, upendo wangu na subira yangu …” Neno la
Kiyunani litumikalo katika Luka 1:3 na 2Timotheo 3:10 ni
parakolutheo, ambalo maana yake ni “kutembea na mtu mguu kwa
mguu, kufuata kwa karibu, kusikiliza kwa makini sana.” Katika
lugha ya mfano, neno parakolutheo linamaanisha kufuata kwa karibu
njia ya kifikra iliyowekwa wazi na mtu ambaye ameipitia sana,
akichunguza kila kitu na kutokuacha kugeuza jiwe lolote. Hebu
msomaji na atafakari kwa kirefu sana juu ya hiyo sentensi ya
mwisho. Na kwa mara nyingine tena, “Fikiri hayo ninayosema, na
Bwana akupe kuelewa mambo yote” (ktk 2Timotheo 2:7). Hii njia ya
kifikra katika mstari huu ni yale matukio halisi yenye kumhusu Yesu
Kristo tangu milele hadi milele. Wakati Yesu alipotoka mbinguni na
kuingia katika wakati, alianzisha njia mpya katika ardhi ngumu
yenye vingi, ya kihistoria. Kila Mkristo anapaswa kuifuata njia hiyo
kifikra na kiroho, akichunguza kila jambo ili aweze kuzalisha hayo
mambo katika maisha yake mwenyewe na kujenga kutokana na hayo
144
somo na mtaala kwa ajili ya wanafunzi wake mwenyewe. Hii itahitaji
utafiti mzito.
Neno parakolutheo lina maana nyingine. Linamaanisha
“kufuatilia”. Wazo hapo ni kama vile mtoto mdogo anavyofuatisha
mchoro kwenye karatasi. Anachofanya ni kuweka karatasi nyepesi
juu ya kile anachotaka kukichora, na kwa utaratibu na uangalifu sana
anafatisha kila mstari, kila kitu kinacho-onekana. Matokeo yake ni
nakala halisi kabisa ya kile kilichokuwa kinaigizwa. Basi, Luka
anajitokeza ili kufuatisha tabia na kuzalisha moyo na shauku ya Yesu
wa Nazareti. Wakati Luka alipoondoa chombo alichotumia kuandikia
Injili ya Luka kwenye ukurasa wake wa mwisho, uzuri wa Yesu, na
ubinadamu Wake na huruma Yake kwa ajili ya wanadamu
vilidhihirishwa kwa hali ya juu sana. Kazi ya Luka iliyokamilika
haifanani na yoyote nyingine ya mwandishi wa Injili. Roho
Mtakatifu ndiye aliyeongoza kalamu ya Luka kufuatisha mfano wa
Mungu ulioko katika ubinadamu wa Yesu. Sisi nasi tunapaswa
kufuata mwongozo wa Luka katika kufuatisha tabia ya Yesu, njia
aliyofuata, na mtaala alioutumia katika kuwagusa watu – na
tunapaswa kwenda na kufanya vivyo hivyo!
Mapema kidogo tulitaja 2Timotheo 2:15. Neno la Kiyunani
linalotumiwa hapo na kutafsiriwa “kutumia kwa usahihi” linahusiana
na neno letu parakolutheo. Ni neno orthotomeo. Hebu lifikiri kidogo.
Neno lenyewe ni maneno mawili – orthos lenye kumaanisha “sawa,
sahihi,” na temno lenye kumaanisha “kukata, kugawa, kutumia kwa 145
utaalamu”. Hakika, Luka alikuwa tabibu mwenye ujuzi na utaalamu
sana, ambaye alifahamu maana ya kuwa makini na kujali vitu
muhimu kutokana na kazi na taaluma yake. Luka alielewa kwamba
kama ishara moja au dalili moja ingeshindikana kuonekana,
mgonjwa wake angekufa. Alikuwa mtumiaji mwenye kuwajibika wa
ujuzi na habari na matumizi ya taaluma katika maswala ya uzima na
kifo. Naye alijua kwamba mada yake aliyokuwa anaishughulikia
wakati huo ilikuwa swala la uzima au kifo – kwenda mbinguni au
kwenda jehanamu!
Utafiti bora zaidi kihistoria unaonyesha kwamba Luka
alikuwa amefundishwa sayansi na kuelimishwa katika matibabu
katika kile chuo cha uganga kilichokuwa Tarso. Kuna wasomi
wengine wamefikia mpaka hatua ya kupendekeza kwamba Paulo,
Luka na Theofilo walikuwa wanafunzi pamoja katika chuo kikuu cha
Tarso. Basi, alikuwa amepata mafunzo bora zaidi kwa habari ya
utabibu yaliyokuwa yanapatikana wakati ule. Vyovyote vile,
yawezekana kwamba Luka, mwanafunzi bora sana wa utabibu,
alimfahamu Sauli, aliyekuwa mwandishi na mwanatheolojia stadi,
kabla ya kukutana katika Kitabu cha Matendo (ktk Matendo 16).
Inaonekana kwamba Paulo, kwa sababu ya tatizo kubwa la kiafya (na
kitabu cha Wagalatia kinaonyesha lilikuwa tatizo kubwa sana la
macho) alikwenda kutafuta msaada wa Dakta Luka. Inawezekana pia
kwamba Paulo (pengine katika kuhudumiwa) alimshirikisha Dakta
Luka Injili na habari za Kristo. Wakati Luka alipokuwa anamtibu 146
Paulo macho ili kurekebisha tatizo lake, Mungu Roho Mtakatifu
alipenya katika giza la upofu kiroho wa Luka na kuleta “nuru tukufu
ya Injili ya Kristo, aliye mfano wa Mungu” (ktk 2Wakor. 4:4).
“Mungu” huyo huyo, “aliyeamuru nuru ing’ae gizani”, aliangaza
katika moyo wa huyo daktari, “ili kutoa nuru ya maarifa ya utukufu
wa Mungu katika uso wa Yesu Kristo” (ktk 2Wakor. 4:6)! Baadaye
kidogo, wakati Paulo alipotamka nia yake ya kuondoka Troa akiwa
na timu yake ya utume kwenda eneo lingine walilopangiwa, Luka
akaomba kuambatana naye. Pengine Paulo alisema hivi: “Lakini
Daktari, mbona una hospitali yako hapa? Huwezi kuiacha tu!” Na
pengine Dakta Luka akajibu hivi: “Hapana, ila, ni nzuri, na ninaweza
kumwachia mtu mwingine kwa urahisi tu.” Basi Luka akaiuza
hospitali yake pengine, na kujiunga na mtume Paulo katika safari
zake za kitume zilizokuwa zimesalia!
Luka ndiye mwandishi pekee wa Injili aliyekuwa amesomea
sayansi ya udaktari. Sasa, anaingiza mafunzo yake yote na utaalamu
katika kukusanya kweli za habari ya Kristo kutoka kwa wale
waliokuwa mashahidi, waliojionea mambo ya Yesu. Katika kusafiri
kwake na Paulo, na bila shaka katika safari zake binafsi, alikutana na
hao watu waliojionea mambo hayo katika Asia Ndogo, katika
sehemu mbalimbali za Palestina, na hasa huko Yerusalemu. Kidogo
kidogo, madaftari ya Luka yakaanza kujaa kutokana na mahojiano
binafsi mengi aliyokuwa amefanya. Hii ni kawaida kabisa, kwamba:
alama moja ya mtu anayefanya wanafunzi wenye maono ni daftari 147
linaloendelea kujaa! Daftari la Luka liliendelea kujaa maneno
aliyosema Yesu na mambo aliyofanya. Kila alipokutana na mtu
yeyote ambaye alikaa na Yesu kwa muda fulani, au aliyekutana na
Yesu au aliyeona miujiza ya Yesu, angeuliza maswali muhimu ya
kutafiti: “Je, wewe ulimjua Yesu kibinafsi?” “Alikuwa anafanya nini
wakati ulipomwona?” “Je, Yesu alisema nini?” “Niambie kila kitu
unachojua kuhusu Yeye.” Baadhi ya watu aliowahoji kwa karibu
sana ni Petro, Yakobo, Yohana na wengine katika wale Mitume wa
kwanza. Bila shaka alizungumza na Yohana Marko kwa ukaribu
sana, ambaye naye alikuwa anamalizia Injili yake wakati huo (yaani,
Injili ya Marko). Kuna ushahidi mzito kabisa kwamba Luka alifanya
mazungumzo ya hali ya juu sana na Mariamu, mama yake Yesu.
Daktari aliandika maelezo mapana sana kuhusu kuzaliwa kwa Kristo
na bikira kuliko mwandishi yeyote mwingine wa Biblia, na
madaktari si wepesi kuamini sana kwamba bikira huzaa! Kuna
mwandishi mmoja anayeitwa William Hobart aliyeandika kitabu
kikubwa tu kuhusu lugha ya kitabibu ya Dakta Luka, na ndani yake
anaonyesha zaidi ya maneno mia nne maalum kabisa ya kitabibu
ambayo Luka aliyatumia alipoandika Injili yake na Kitabu cha
Matendo. Ni kwamba Daktari huyu aliamini kabisa kuhusu kuzaliwa
kwa Kristo na bikira kutokana na ushahidi wenye nguvu na usioweza
kupingika. Aliweza kuona na kupata habari kamili kuhusu kuzaliwa
kwa Yesu kupitia mahojiano ya moja kwa moja na Mariamu
mwenyewe. 148
Sasa – kwa utaalamu wa hali ya juu sana kisayansi, tabibu
huyo maarufu na mwenye utaalamu aliandika simulizi lenye
mpangilio mzuri sana kuhusu maisha ya Bwana Yesu. Anatoa taarifa
yenye upana na maelezo mazuri kuhusu kuzaliwa Kwake, maisha
Yake na mafundisho, kifo Chake, kufufuka Kwake, baadhi ya
matukio katika zile siku arobaini baada ya kufufuka Kwake, na
kupaa Kwake. Ni wazi kwamba Luka alifanya juhudi kubwa sana
kutafiti kuhusu Nafsi, mafundisho, matendo na mafanikio ya Yesu.
Katika Luka 1:3, neno “kamili” linatokana na neno la Kiyunani
akribos, ambalo maana yake ni “kwa bidii, kwa makini, au kwa
uangalifu sana.” Luka alimtafiti Yesu kuanzia juu (akron – kiwango
cha juu kabisa) hadi chini (abussas – chini kabisa, shimoni). Luka
anasema, “Ee Theofilo, sikuacha kujitahidi katika kumtafiti Yesu
tangu maelezo ya hali ya juu zaidi hadi kweli za ndani kabisa.” Luka
alikuwa na uhakika kwamba amefanya juhudi zake zote kutafiti kila
kitu kuhusu maisha ya Yesu – tokea juu hadi chini.
Zile Injili nne za Agano Jipya hazikuandikwa katika utupu
usio na uchafu wowote, bali katika purukushani za kawaida za
maisha. Ingawa kila Injili imevuviwa na Roho Mtakatifu, inazo
alama pekee na vidokezo vya mwandishi wake. Yohana inasikika
kama Yohana, Marko kama Marko, Mathayo kama Mathayo –
ingawa kila mmoja anaandika kitabu ambacho ni kamilifu, na hata
ingawa kila kitabu ni juu ya Mhusika kamili. Katika Luka 1:1,
Daktari alisema kwamba maelezo yake yana mambo kuhusu Yesu 149
ambayo yalitimizwa na kukamilishwa mbele ya watu wa wale
aliokuwa amewahoji. Yohana ambaye ni mwandishi mwingine wa
Injili alisema katika barua yake ya kwanza kwa watu wote kwamba
hao mashahidi walikuwa wamemwona, kumsikia na kumgusa Yesu.
Hivyo, walitoa ushahidi wa mambo waliyoona, waliyosikia na
waliyogusa wenyewe. Neno “shahidi aliyeona” kwa Kiyunani,
litumikalo katika Luka 1:1 ni autoptes, ambalo ni maneno mawili
yenye maana ya “kujionea mwenyewe”. Maelezo ambayo Luka
alisikia toka kwa hao watu waliojionea kwa macho yao wenyewe
mambo hayo yalikuwa na nguvu sana kumshawishi yeye mpaka
akawa na uhakika kwamba yangeshawishi, kusadikisha na
kumtosheleza yeyote ambaye angeyatafiti mwenyewe kwa ukamilifu
zaidi. Katika Kitabu cha Matendo, anayaita “vithibitisho vingi
visivyotiliwa mashaka” au
”ushahidi usiopingika” (ktk Matendo 1:3). Anaandika Injili yake ili
kutoa huo ushahidi wenye nguvu sana utokanao na maelezo hayo.
Tena, Luka anatuambia kwamba alitafuta habari na ushahidi
toka kwa wale watumishi wa mwanzo kabisa wa Kristo, wengi
ambao walikuwa wametoa maisha yao au wangekuja kuyatoa
baadaye, kutia muhuri ushuhuda wao kuhusu Yesu kwa damu zao
wenyewe. Neno “watumishi” linalotumika katika Luka 1:2 kwa
Kiyunani ni huperetes, ambalo maana yake ni “mpiga makasia wa
chini”. Neno hili lilitumika kusema kuhusu mtumwa aliyefanya kazi
150
katika merikebu, aliyekuwa anaketi mahali pa chini kabisa kwa ajili
ya kumfikisha mtu mwingine mahali alipotaka kwenda.
Mtumwa wa kwenye merikebu alipelekwa mpaka pande za
chini za merikebu hiyo na kufungwa mnyororo hapo, kwa ajili ya
kufanya kitu kimoja tu. Kazi yake pekee ilikuwa ni kumtazama yule
akida mpiga ngoma na kuvuta makasia kwa kushirikiana na wale
watumwa wengine kwa amri ya akida. Hawa “watumishi” walikuwa
wamesadiki kabisa kuhusu enzi na Nafsi ya Yesu Kristo kiasi cha
kuwa watumwa wapiga makasia kwenye ile “merikebu njema ya
Neema,” wakiishi kwa ajili ya kumtazama na kumtii Nahodha wao,
Bwana Yesu Kristo. Kusudi lao pekee lilikuwa kumfikisha mwingine
mahali alipotaka kwenda. Luka anaonyesha kwa nguvu sana kazi
hiyo yao na mtindo wao wa maisha wakati alipotafiti habari za Yesu
na kuandika hiki kitabu cha ajabu na kushangaza sana kwa ajili ya
kumfikisha mtu mmoja – Theofilo – hadi mwisho mzuri katika
maisha haya, na mwisho mzuri katika maisha yajayo. Injili ya Luka
na Kitabu cha Matendo vimejaa mfano wa mtu anayefanya watu
kuwa wanafunzi – mtu mwingine, mtu mwingine, mtu mwingine ….
Kila Mkristo anapaswa kujiona kama mtumwa aliyefungiwa katika
merikebu, anayefanya kila linalowezekana kuijua hii Injili, kufuata
maagizo yake, kutengeneza mtaala, na kujenga wanafunzi, vyote
hivyo kwa ajili ya kumfikisha mtu mwingine mahali anapotaka
kwenda – mwisho mzuri.
151
VITENDEA KAZI THABITI, VINAVYOFAA
Ukitaka kufuata kiwango cha Agano Jipya, lazima uandae
vitendea kazi thabiti, vinavyofaa, kwa ajili ya kuwajenga wanafunzi
wengine. Luka aliahidi kumpa Theofilo maelezo yaliyoandikwa ya
Injili ya Yesu Kristo ambayo ni makamilifu, yenye kufuata utaratibu.
Hapa katika mstari wa kwanza Luka anatumia neno la kijeshi,
anatassomai, ambalo maana yake ni kupanga askari, au vitu, au
kweli fulani, katika utaratibu na mpango wake. Luka alitafuta
kupanga kweli kuhusu Yesu katika mpango mzuri unaofaa kama
jeshi la askari lililoandaliwa na kupangwa kwa ajili ya kuiteka dunia
nzima. Luka akamkumbusha Theofilo kwamba alikuwa ametafiti
habari za Yesu kutoka juu hadi chini na kuweka mambo aliyogundua
katika “mtiririko” au “mpangilio mzuri”. Hakuna mwanafunzi
mwenye kufikiri vizuri anayeweza kuepukana na kusudi dhahiri la
Luka la kuweka mpango mzuri katika mtaala kwa ajili ya kufanikisha
kikamilifu malengo yake katika maisha ya mtu mwingine.
Luka – kama Paulo, aliyemfanya yeye kuwa mwanafunzi –
alianza mkakati wa kuwajenga watu ambao wangeweza kutumia kwa
usahihi Maandiko (ktk 2Timotheo 2:15). Paulo alimwambia
Timotheo katika 2Timotheo 3:10 kwamba, “umeijua kabisa itikadi
yangu.” Paulo alikuwa amepanga vizuri sana kweli kuu za Injili kwa
ajili ya Timotheo, ili aweze kuzishika vizuri na kusimikwa kwa
uthabiti ndani yake, na kuzieleza kwa usahihi na ufasaha kwa mtu
mwingine. Luka alifanywa mwanafunzi na Paulo, na sasa anatoa 152
mfano mkamilifu mzuri kabisa wa sheria ya Yesu aliyesema hivi:
“Utaratibu ukikamilika, mwanafunzi atakuwa kama mwalimu wake”
(ktk Luka 6:40). Vile vile, Luka anatuonyesha katika mistari hii
mfano mkamilifu wa mwanafunzi anayetayarisha mtaala kwa ajili ya
kufanya wanafunzi wengine. Yeye “aliandaa maelezo sahihi” na
“kwa utaratibu” kuhusu kweli za Yesu kwa ajili ya kufundisha,
kuingiza kazini, kujenga na kumtuma mtu mmoja ili afikie dunia.
Mwalimu maarufu aitwaye F.F. Bruce anasema kwamba “maneno
hayo yanaonyesha mfuatano wa maelezo katika utaratibu, kimada au
kufuata matukio, badala ya maelezo tu yasiyo na mpangilio.” Kabla
ya barua hii, Luka (au pengine Mkristo mwingine) alikuwa
“amemfundisha” (Luka 1:4) Theofilo kwa ushuhuda wa maneno tu
kuhusu Yesu. Neno katecheo ni neno la Kiyunani ambalo maana
yake ni kufundisha kwa utaratibu na mpangilio, hasa kwa maswali,
majibu, maelezo na marekebisho. Luka anaonyesha umuhimu
mkubwa sana kwa ajili ya kueleza Injili kwa maneno kwa mpangilio
ili kumleta mwanafunzi kwa Kristo, na umuhimu wa kuwa na mtaala
ulioandikwa kwa mpangilio kwa ajili ya kumjenga mwanafunzi huyo
katika imani na maisha ya Kikristo na huduma.
Luka alifanya hayo yote ili Theofilo afikie kwenye ufahamu
kamili wa Yesu Kristo, na kusababisha uhakika usiotikisika juu
Yake. Alfred Plummer alifafanua neno “kwa uhakika” katika mstari
wa nne hivi: “Theofilo atajua kwamba Injili ina msingi usiovunjwa
wa kihistoria.” Sisi nasi tunapaswa kuanza kuandaa mtaala na 153
kutayarisha jedwali la vielelezo (hebu tazama mifano (au hekaya)
itolewayo na Yesu ambayo Luka ameiandika katika Injili yake),
kutumia kila kitu kinachofaa KiMaandiko tunachoweza kupata ili
kuwajenga wanafunzi wetu juu ya msingi usiotikisika wa Injili
tukufu ya Bwana wetu Yesu Kristo.
Kuna Wakristo wengi wazuri, wenye nia njema tu, na wenye
kujua mengi sana ambao hawatalenga kumjenga mwanafunzi mmoja
mwenye maono ya dunia, mwenye kuigusa dunia, na mwenye
kujiongeza. Kwa nini? Kwa sababu, hawatajali sana juu ya jukumu
lao la kujenga (au basi kupata) mtaala unaofaa, wenye utaratibu
mzuri kwa kusudi la kufikisha mtu mwingine kwenye hatima yake ya
mwisho. Ili hata mtu wa kawaida asije kukwepa kweli hiyo, F.F.
Bruce anatukumbusha kwamba Luka alikuwa “mtu wa kawaida tu,
asiyekuwa Myahudi na asiyekuwa mhubiri”. Luka alikuwa tabibu
maarufu na mzuri sana, mwenye ratiba iliyombana sana! Lakini
alipata wakati (yaani, alitengeneza wakati) ili “kuandika kwa
utaratibu” maelezo “yenye mpangilio” kuhusu maisha ya Bwana
wetu, huduma Yake, mafundisho Yake, mambo aliyofanikisha, na
kazi Yake – kwa ajili ya mtu mmoja tu.
MPANGO WA KUDUMU WA KUZALISHA
Kama unataka kufuata kiwango cha Agano Jipya, lazima
ufanye kila liwezekanalo kibinadamu kuwa na mpango wa kudumu
wa kuzalisha wanafunzi. Kila mtu anayefanya wengine kuwa 154
wanafunzi, mwenye maono, lazima afanye kila linalowezekana
kibinadamu, kwa kumtegemea Mungu kabisa, kufanikisha na
kuendeleza uzalishwaji wa wanafunzi. Hawa wanafunzi lazima
waone dhahiri kwamba dunia nzima ni eneo lao la kazi, na lazima
waishi kwa makusudi kabisa ili kuigusa dunia hiyo. Mwanafunzi
yeyote mwenye maono anajua kwamba hawezi kumfanya mtu
mwingine yeyote aone kiwango au afuate lengo pasipo uwezo wa
Mungu wa kimuujiza, lakini pia anajua kwamba kama yeye
mwenyewe hatakimbia hadi kiwango cha nuru yake na uwezo wake
katika kufukuzia kiwango hicho, Mungu hatamfanya mtu mwingine
yeyote akimbie pamoja naye. Kanuni ya Agustino bado ni halisi:
“Pasipo Mungu, sisi hatuwezi; pasipo sisi, Mungu hatafanya”.
Luka ametupa mfano usioweza kusahaulika wa mtu
anayefanya wengine kuwa wanafunzi, mwenye moyo na bidii.
Alielewa kikamilifu kabisa umuhimu wa kile alichokuwa anafanya.
Luka alifanya uchunguzi kwa bidii kabisa kuhusu maisha ya Yesu wa
Nazareti, akatafuta kwa makusudi kuwa sahihi katika maelezo yake,
na alijua umuhimu wa mpangilio au utaratibu. Luka alijitia katika
kazi hiyo kwa bidii, akakusanya kweli zote zilizokuwa zinaweza
kupatikana (zilizoandikwa na za mdomo), kisha akaandika kitabu
hiki kwa mtu mmoja aliyepotea – Theofilo.
Theofilo alifanya nini na kitabu hicho? Alisadiki kabisa
kuhusu ukweli wake mpaka akakipokea, akamwamini Yule
aliyetajwa humo pamoja na ujumbe wake, na akatafuta kukihifadhi 155
na kukifikisha kwa wengine. Japo kitabu hiki kiliandikiwa mtu
mmoja tu, wewe unayo nakala yake! Ni mfano ulioje huo wa
kiwango cha Yesu cha kufanya mtu kuwa mwanafunzi ili kuigusa
dunia nzima – kiwango ambacho anamwamuru kila mmoja katika
wafuasi Wake kukifuata. Amri Yake hiyo inaitwa “Agizo Kuu”.
Luka alimleta Theofilo kwa Yesu Kristo kwa kumwandikia
kile tunachoita sasa “Injili Kama Ilivyoandikwa Na Luka”. Wakati
Theofilo alipomwitikia Kristo kwa imani binafsi, Luka akaanza mara
ile ile kumfanya Theofilo kuwa mwanafunzi kwa kuandika kitabu
kingine chenye sura ishirini na nane, tunachokiita Kitabu cha
Matendo, ili kumtambulisha Theofilo kwenye wajibu na mtindo wa
Yesu wa kuigusa dunia. Ni mfano wa kushangaza vipi na wa ajabu
sana wa kile kiwango cha Mungu cha Neno kuwa mwili! Kumbuka
kwamba kiwango hiki kilitendwa na mtu wa kawaida tu aliyekuwa
tabibu ili kujikimu kimaisha, lakini ambaye kazi yake kubwa ilikuwa
ni “kuwafanya watu kuwa wanafunzi”.
[USHUHUDA WA MWANDISHI – Mchungaji mmoja rafiki
yangu aitwaye Jim Davidson alinishirikisha mfano huu, ambao nami
nakushirikisha wewe kikamilifu kabisa.
Babu yetu mzaa babu aliyeitwa Isaac Kilgore alijiunga na
jeshi la Majimbo ya Kusini ya Marekani mwaka wa 1862 akiwa na
umri wa miaka kumi na nane. Vita yake ya kwanza kubwa ilikuwa
mahali palipoitwa Shiloh. Ili upate picha ya ukali wa hiyo vita ni
kwamba, baadaye, wakati wowote askari aliposimulia jinsi vita 156
ilivyokuwa mbaya, alikuwa anasema hivi: ‘Yaani! Niliogopa kuliko
nilivyo-ogopa kule Shiloh.’
Mzee Izaki aliendelea, akapigana huko Chickamauga,
Chattanooga, Mlima wa Kennesaw, Atlanta, Franklin na Nashville –
kwa uchache. Zote zilikuwa vita kali. Na kwa muda, yeye alikuwa
mbeba bendera wa kikosi, na kwa maana hiyo alikuwa rahisi kabisa
kupigwa risasi, lakini alipona hata hilo. Watu zaidi ya laki sita na
ishirini elfu walikufa katika vita hizo zote. Hebu fikiri jinsi hilo
lilivyoathiri idadi ya watu leo.
Baada ya Mzee Izaki kutoka jeshini mwisho wa vita,
alitembea kwa miguu kutoka jimbo la Carolina Kaskazini hadi eneo
la Walker huko Alabama. Akaoa mara mbili na kujipatia watoto
kumi na saba. Hebu fikiri jinsi hilo lilivyoathiri idadi ya watu leo!
Na kwa kuwa hakufa vitani, alipata wazao na kuongeza vizazi.
Mmoja wao ni mimi, nami nina watoto wawili, ambao bila shaka nao
watapata watoto. Lakini je, ingekuwaje kama Mzee Izaki angekufa
vitani?
Siri ya hayo yote ni hii: Kama utapata mafunzo sahihi kama
anavyopaswa askari, na kama hutakufa vitani – na tuko vitani –
utazaa wakati wote, kizazi baada ya kizazi kwa ajili ya Yesu Kristo.
Lakini, lazima ufikiri na hili pia: Utazaa vizazi hivyo kwa ajili ya
Yesu Kristo ikiwa tu utakubali kuifia nafsi yako. Yesu alisema hivi:
‘Mbegu ya ngano isipoanguka ardhini na kufa, inabakia peke yake.
157
Lakini ikifa, inazaa mbegu nyingi sana na kunakuwa na mavuno
mengi sana’.” MWISHO]
Je, utakubali kuwajibika kibinafsi kwa hilo na kuingia katika
utafiti mzito ili kulifanikisha? Utakubali kukuza na kutumia rasilmali
thabiti na za uhakika kwa ajili ya kuwajenga wanafunzi wa Agano
Jipya, na kujitoa mwenyewe kwa Mungu kuhakikisha kwamba kuna
uzalishaji wa kudumu katika vizazi vijavyo? Mungu anakusubiri, na
dunia ya wanadamu pia!
158
Sura Ya 6Mpango Wa Mungu Wa Kuongeza
“Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”
Matendo 1:1-5
Kuanza kwa safari ya kiroho uliosababishwa na Siku ya
Pentekoste kukawa kumekamilika. Kanisa la kwanza lilikuwa
lisukumwe na nguvu na uwezo wa jambo hilo hadi miisho ya dunia
ya wakati ule. Petro alikuwa amemalizia mahubiri yake, akieleza
Injili ya Kufa na Kufufuka kwa Yesu na kuja kwa Roho Mtakatifu,
halafu katika mstari wa 41 wa Matendo sura ya 2 tunasoma hivi:
“Ndipo wao waliolipokea neno lake kwa furaha wakabatizwa, na
siku hiyo hiyo wakaongezeka kwao kama watu elfu tatu.” Du!
Nyongeza kubwa sana! Hakuna mchungaji yeyote duniani ambaye
asingefurahishwa na kuokoka kwa watu elfu tatu kwa siku moja
baada ya kuhubiri Injili. Jali sana neno “wakaongezeka” maana
linatumika tena katika mstari wa 47 wa sura hiyo hiyo. Pitia kwa
haraka mstari wa 42 hadi 47a, halafu sikiliza sentensi hii: “Na Bwana
akaliongeza kanisa kila siku, kwa watu waliokuwa wanaokolewa”.
Umeona tena neno “kuongezeka” hapo?
159
Sasa hebu tuone Matendo 5:14. Kisa cha kusikitisha sana cha
dhambi na hukumu ya akina Anania na Safira kimemalizika
kusimuliwa. Mstari wa 13 unasema, “Na katika waliosalia hakuna
mtu aliyethubutu kujiunga nao, ila watu waliwatukuza na kuwapa
heshima kubwa.” Ungejisikiaje kuwa mshirika wa kanisa lenye
nguvu sana kiroho kiasi kwamba watu wanaogopa kujiunga nalo?
Lakini tena katika mstari wa 14 tunasoma hivi: “Na waamini
wakazidi kuongezeka zaidi kwa Bwana, makundi ya wanaume na
wanawake.” Ile “mashine ya kuzidisha” imeharibika! Hawawezi tena
kuwahesabu kwa sababu wengi sana wanaongezwa kwa Bwana.
Sasa ona badiliko muhimu. Katika sura ya sita, mkakati wa
Mungu kihesabu kwa ajili ya kukua kwa kanisa la kwanza bila shaka
unaongezeka kwa kasi kubwa. Katika mstari wa kwanza tunasoma
hivi: “Na katika siku zile, idadi ya wanafunzi ilipozidi kuongezeka,
kulitokea manung’uniko ya Wayunani kinyume cha Waebrania, kwa
sababu wajane wao walikuwa wanapuuzwa katika huduma ya kila
siku. Unaona utaratibu huo? “Kuongezeka,” “kuhudumiwa,” na
hatimaye “kunung’unika”. Washirika wanapoongezeka kanisani,
huduma za ziada lazima zifuate, ili kuwahudumia na kuwapa
shughuli ya kufanya, na baada ya hapo – hakika kabisa kama nuru
inavyofuata giza, manung’uniko yatafuatana na maongezeko. Ni kitu
halisi kabisa kwamba watu zaidi siku zote maana yake ni matatizo
zaidi. Kwani, si hata wewe ni tatizo kwa namna moja au nyingine?
160
Angalia asili ya tatizo lenyewe. “Ushemasi” wa kila siku
(maana hasa ya neno ‘huduma’) ulikuwepo ili kugawa chakula, vitu
na fedha kwa idadi kubwa ya Wakristo wapya waliojikuta katika
matatizo ya ghafula kiuchumi na kijamii kutokana na wao
kumwamini Kristo. “Wayahudi wa Kiyunani” walikuwa Wayahudi
waliozungumza Kiyunani, waliokuwa wamezaliwa nje ya Uyahudi
na waliokuwa wamerudi nyumbani karibuni tu kwa ajili ya sikukuu
ya Pasaka na Pentekoste. “Wayahudi wa Kiebrania” walikuwa ni
wazaliwa wa nyumbani, waliosema Kiaramu, lugha ya Wayahudi
waliokaa Palestina. Wale wa Kiyunani walikuwa ndiyo wachache, na
wale Waebrania walikuwa ndiyo wengi.
Basi, manung’uniko yalitoka kwa wale waliokuwa wachache
(kihalali kabisa) kama hoja kuhusu wajane wao kupuuzwa katika
ugawaji wa kila siku wa vitu. “Walio wengi walikuwa wanawajali
watu wao kiasi cha kuwapuuza na kuwanyanyasa walio wachache”.
Ili kushughulikia tatizo, Mitume waliwachagua watu saba, na wote
walikuwa na majina ya Kiyunani. Hiyo ni busara, sivyo? Kutatua
tatizo na kumaliza malalamiko, watu kutoka miongoni mwa
walalamikaji walichaguliwa kusimamia ugawaji wa vitu. Tatizo
likawa limetatuliwa, “na Neno la Mungu likazidi kuenea, na idadi ya
wanafunzi IKAONGEZEKA sana Yerusalemu, na idadi kubwa ya
makuhani wakaitii imani” (Matendo 6:7). Maongezeko yalikuwa
makubwa kiasi cha kuwepo na wingi waliotoka katika ukuhani wa
Wayahudi kuingia katika jamii ya wanaomwamini Yesu huko 161
Yerusalemu. Ona kwamba kuanza sasa, kuongezeka ndicho kiwango
cha kawaida kwa ajili ya kukua kwa kanisa la kwanza.
Katika sura ya 9, kasi inaendelea. Sura ya tisa ni masimulizi
ya kuokoka kwa Mkristo mkuu kuliko wote – Sauli wa Tarso. Baada
ya vurugu zilizotokana na kuokoka kwake na mahubiri yake ya
kwanza kumalizika, tunasoma hivi katika mstari wa 31: “Ndipo
makanisa yakapumzika katika Uyahudi yote na Galilaya na Samaria,
tena, yakajengwa. Na, yakitembea katika kumcha Mungu na katika
faraja ya Roho Mtakatifu, yalizidi kuongezeka sana.” Kwa kuwa
sentensi yenyewe imekaa ilivyokaa, inaweza isiwe rahisi kuona
kiwango cha kuzidishwa hapa. Sasa makanisa yanaongezeka! Swali:
Je, Ukristo wa namna hiyo ulipotelea wapi? Hawakuwa na mashirika
ya kimishenari, wala kamati za kuanzisha makanisa na watenda kazi
wa kamati hizo. Hawakuwa na wamishenari wa ndani na nje ya nchi
waliokuwa rasmi, lakini makanisa yalizidi kuongezeka. Tunauliza
tena: Ukristo wa aina hiyo ulipotelea wapi?
Jibu linaweza kuonekana kwa urahisi kabisa ukifanikiwa
kuhudhuria makongamano au mikutano yoyote ya wachungaji.
Wahubiri wanaoanza kukutanika, wanauliza maswali kadhaa ya
kawaida kabisa. “Vipi, Jumapili yako ilikuwa nzuri?” Jibu: “Naam –
ilikuwa nzuri kabisa.” Swali linalofuata ni lipi? “Umekuwa na watu
wangapi walio-ongezeka?” Wapendwa: Hatuwezi kuwagusa wakazi
wa dunia hii wanaozidi kuongezeka kwa sisi kuongeza makanisa
yetu, hata kama maongezeko yetu yatakuwa makubwa kiasi gani. 162
Kasi ya kuzidishwa haiwezi kufikiwa na maongezeko kamwe! Kuna
mtu mahali katudanganya kuhusu kitu cha muhimu sana. Mungu
ametuita kuongezeka!
Hatupaswi kupuuza thamani na umuhimu wa watu kuokoka
(au, kuongezwa) katika jamii ya Wakristo, lakini, inabidi
tujilazimishe kukabiliana na kosa kubwa sana katika taratibu zetu za
utendaji kazi kama huko kuongezeka hakutakuwa mwanzo wa kuzidi
kwa jamii ya Wakristo duniani kwa ujumla.
Amri pekee ya kusonga mbele iliyowahi kutolewa na Yesu
kwa kanisa Lake inaitwa Agizo Kuu. Kuna maneno tendaji saba
katika Agizo hilo, lakini moja tu ndiyo amri. Kuna neno moja tu zito,
lenye nguvu, ambalo ni amri moja, katika Agizo Kuu! Neno tendaji
hilo linatafsiriwa “kufundisha” ingawa hapo tena ni dhahiri kwamba
kuna jambo tunalofichwa hapa. Kwa sababu, maana ya neno hilo ni
zaidi ya kufundisha tu! Maana ya neno tendaji hilo ni “kufanya
wanafunzi”. Tunahitaji kuacha kuuliza, “Umepata maamuzi mangapi
katika ibada yako?” na kuanza kuuliza hivi: “Je, unajenga wanafunzi
wangapi?”
Kanisa la kwanza lilijizidisha kwa kutumia mfumo na
utaratibu uliokuwa umeonyeshwa vizuri na kwa ukamilifu kabisa
katika huduma ya miaka mitatu ya Yesu Kristo na wale mitume
Wake kumi na mbili. Yeye ndiye wa kwanza kufanya watu kuwa
wanafunzi, na utaratibu aliofuata lazima uchunguzwe, tujifunze,
tuufahamu na kuuiga kama tunataka kuzalisha wazalishaji kama 163
Yeye alivyofanya. Mimi binafsi siamini kwamba mtu anaweza kuwa
mwanafunzi bila ya kuwa mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi pia.
Kutii kwetu UBwana wa Yesu Kristo unahusisha kuweka kipau
mbele kwenye kutimizwa kwa Agizo Lake Kuu. Ninaamini kufanya
watu kuwa wanafunzi ni kitu kilichomo ndani ya mkataba wetu wa
kuwa mwanafunzi. Kama mtu ni mwanafunzi kulingana na Agano
Jipya, basi atakuwa mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi pia.
PICHA YA MWANAFUNZI ANAYEJIZIDISHA
Sasa fungua Timotheo wa Pili sura ya 2. Katika sura hiyo,
tunapata picha saba nzuri sana za mwanafunzi, na maelezo yanayofaa
sana ya mpango wa Mungu wa maongezeko. Kwaanza, tuangalie
picha za mwanafunzi. Kila moja katika zile saba inatoa sehemu
ndogo ya picha ya mwanafunzi wa Agano Jipya.
NI “MWANA”
Kwanza kabisa, mwanafunzi wa Agano Jipya ni “mwana”
(ktk mstari wa kwanza). Yeye ni mwana wa Mungu kwa kuzaliwa
kutoka juu, lakini hapa ni mtoto wa kiroho wa aaminiye
atakayemleta kwa Kristo. Paulo alimwita Timotheo “mwanangu”
kwa sababu alimwongoza kumjua Kristo. Katika safari zake, Paulo
alifika kwenye mji ambako Timotheo alikuwa anaishi, katika safari
zake za kitume. Akakuta familia yenye wanafunzi wawili maarufu
164
sana wa Agano la Kale, bibi mmoja aliyeitwa Lois, na mama mmoja
aliyeitwa Eunike (ktk 2Tim. 1:5).
Eunike alikuwa na mtoto mchanganyiko aliyeitwa Timotheo.
Baba yake alikuwa Myunani. Alipogundua jinsi kijana huyo
alivyokuwa amefundishwa Biblia vizuri, alimwongoza kwa Kristo
kwa urahisi sana. Alipoanza kumfanya kuwa mwanafunzi, akaona
uwezo mkubwa sana wa kiroho ndani ya yule kijana, ambao ulikuwa
wa kipekee sana. Paulo alipoondoka kuendelea na safari yake ya
kitume, alimtia moyo kijana huyo kukua katika mwendo wake na
Kristo. Paulo aliahidi kumwombea kila siku, na pia aliahidi kwamba
angerudi ikiwezekana.
Baadaye sana, katika safari nyingine ya kitume, Paulo alirudi
mjini kwa Timotheo. Alipomfuatilia yule kijana, ndoto zake kuu
zikawa zimetimizwa. Kijana alikuwa amekua kiroho kuliko Paulo
alivyokuwa ametazamia. Alipokaribia kuondoka, Paulo alisema,
“Sasa Timotheo, unaonaje? Ungependa kusafiri na mimi?” Pengine
Timotheo akatekewa. “Mimi? Nisafiri na wewe?” Paulo akamjibu,
“Ndiyo.” Timotheo akauliza, “Huko safarini tutafanya nini?”
Pengine Paulo alimjibu hivi, “Wewe nitazame mimi, niombee, halafu
tutazungumza usiku.” Unapokuwa Mkristo mwenye maono, huko ni
kumfanya mtu kuwa mwanafunzi!
Je, mwana au mtoto mzuri anafanyaje? Anajifunza kutoka
kwa mzazi wake, anampenda mzazi wake, anamtii mzazi wake, na
165
kuongeza au kukuza tabia za familia. Ndivyo na mtoto wa kiroho
anavyofanya.
NI “ASKARI”
Pili – mwanafunzi wa Agano Jipya ni “askari”. “Hakuna
apigaye vita ajitiaye katika shughuli za dunia, ili ampendeze yeye
aliyemwandika awe askari.” Je, askari mzuri hufanya nini?
Anaachana na mipango yake yote na makusudi yake yote, ili
kutimiza jukumu alilopangiwa. Anaingia katika mafunzo kwa bidii
na udhati mkubwa sana. Anatetea maslahi ya nchi yake. Anapigana
inapokuwa lazima. Kwa kifupi ni kwamba, yuko tayari kwa ajili ya
mapambano na kujitoa, ambavyo ni vitu muhimu kama atafanikisha
jukumu lake.
Ee Jemadari mpendwa, ulijeruhiwa vitani.
Mimi nisishangae kama nitaumizwa kidogo.
Badala yake, Ee Bwana, hebu swali langu kuu liwe
Je, nitapata kujeruhiwa vitani pamoja Nawe?
NI “ASHINDANAYE” (Mwanariadha)
Tatu – mwanafunzi wa Agano Jipya anafananishwa na
“mwanariadha” ashindanaye. Mstari wa 5 unasema hivi: “Hata mtu
akishindana katika machezo, hapewi taji, asiposhindana kwa halali.”
Imekisiwa kwamba katika Agano Jipya, mashindano ya mbio
yametajwa zaidi ya mara hamsini. Je, mwanariadha mzuri anafanya 166
nini? Anajitia kabisa katika mchezo wake, anafanya mazoezi
magumu na kwa mpangilio, anapata ujuzi unaotakiwa, anajitahidi
kuwa na nidhamu kiakili pamoja na kimwili, na anafanya juhudi ili
ashinde. Mwanafunzi Mkristo hatafanya pungufu ya hapo katika
kumfuata Kristo.
NI “MKULIMA”
Nne ni kwamba, mwanafunzi wa Agano Jipya anafananishwa
na “mkulima” (ktk mstari wa 6). Je, mkulima mzuri hufanya nini?
Anafanya kazi kwa bidii. Anatifua udongo, anapanda mbegu,
analima, na anavuna mavuno aliyolima. Pia anatenga mbegu kwa
ajili ya kupanda baadaye, kuvuna, na kuongeza mazao yake.
Shughuli hizo zote zina mifano inayofanana na iliyo wazi kabisa
katika zoezi la kiroho la kuwa mwanafunzi na kuwafanya wengine
kuwa wanafunzi.
NI “MTENDA KAZI”
Kitu cha tano ni kwamba, mwanafunzi wa Agano Jipya ni
“mtenda kazi” (ktk mstari wa 15), tena, mtenda kazi bingwa. Yeye
anapaswa kuwa “mtenda kazi asiyekuwa na sababu ya kutahayari,
akilitumia kwa uhalali neno la kweli”. Ili kufanya hayo, lazima
“kujifunza ili kujionyesha kuwa amekubaliwa na Mungu”. Kama
wanafunzi Wakristo, sisi tupo ili tufanye kazi kwa bidii, sio
kuzembea.167
NI “CHOMBO”
Cha sita ni kwamba mwanafunzi wa Agano Jipya ni
“chombo” (ktk mstari wa 20 na 21). Je, chombo ni nini? Chombo ni
kitu chenye nafasi, iliyokusudiwa kujaa kitu au mtu. Sisi kama
Wakristo, tumekusudiwa kumjaa na kufikisha uzima wa Kristo
Mwenyewe kwa watu. Je, chombo kizuri hufanya nini? Kinaketi
kabatini kwa mwenyewe, kikiwa kitupu na chenye kupatikana, na
kumsubiri mhusika akijaze, akipenda. Mwanafunzi Mkristo hawi
katika hali ya kujiuliza ikiwa Bwana wake anataka kumjaza au vipi.
Waefeso 5:18 inamwagiza “kujazwa na Roho”. Chombo
kikishajazwa, kinamsubiria mwenyewe akimimine. Yaani, kinasubiri
tu akitumie kama vyombo vinavyotumika. Ndivyo tunavyopaswa
kuwa na sisi kama wanafunzi wa Kikristo.
NI “MTUMISHI”
Mwisho, mwanafunzi wa Agano Jipya ni “mtumishi” au
mtumwa wa upendo. Mtumwa hana mapenzi yake mwenyewe, hana
ratiba yake mwenyewe, hana haki zake, na hana mali yake. Yeye ni
mali ya bwana wake. Lakini, hana kupungukiwa katika rasilmali.
Hazina yote ya bwana wake inatosheleza kazi yoyote ile anayoweza
kupewa na bwana wake. Ndivyo ilivyo pia kwa mwanafunzi Mkristo.
168
UTARATIBU WA KUZIDISHA WANAFUNZI
Sasa, baada ya kuona picha ya mwanafunzi kama itolewavyo
katika 2Timotheo 2, hebu sasa tutazame utaratibu wa kuwazidisha
wanafunzi. Mimi nimeuita “mpango wa Mungu wa kujiongeza.” Huo
unapatikana katika mstari wa 2, pale ambapo Paulo alimwambia hivi
Timotheo: “Na mambo yale uliyoyasikia kwangu [mimi] mbele ya
mashahidi wengi, [wewe] wakabidhi watu waaminifu, watakaoweza
[nao] kuwafundisha na wengine pia.” Hapo tunaona vizazi vinne vya
wanafunzi katika mstari huu mmoja: “Mimi … wewe … watu
waaminifu … wengine pia”. Kama inavyooneshwa kwenye mchoro
huu.
Watu Waaminifu Wengine
Paulo Timotheo Watu Waaminifu Wengine
Watu Waaminifu Wengine
Bila shaka unapata picha kwamba mpango huo ni sawa na kitu
kinachozidi kupanuka, sehemu ndogo ikiwa pale ambapo Paulo na
Timotheo wamesimama. Kila kitu kinaanza na “mimi” na “wewe”,
Paulo na Timotheo, na hiyo hali ya muungano inaonyesha vitu viwili
muhimu sana kuhusu kuwafanya watu kuwa wanafunzi.
(1) Umuhimu wa mtu mmoja, na
(2) Umuhimu wa mahusiano mazuri.
169
Ondoa yeyote kati ya hao watu wawili – Paulo au Timotheo –
na utaratibu wote unaporomoka tangu mwanzo. Hakuna kuongezeka
kunakoweza kutokea pasipo mshikamanishaji hapo mwanzo, na
wengine wa kuunganisha nguvu naye.
Paulo na Timotheo lazima wawe watu ambao ni wa sifa au
hali aina fulani na wenye msimamo kama wanafunzi, ikiwa
kuongezeka kutafanyika. Halafu, lazima wawe na mahusiano kwa
jinsi ambayo ni ya wazi, yenye kuaminika na ya kipekee. Loo!
Kanisa linahitaji kutafiti na kufanyia kazi theolojia ya mahusiano
kwa hali ya juu sana! Hiyo ni dunia nyingine nzima ambayo
haiguswi hata kidogo na kanisa kwa jumla. Kama Paulo na Timotheo
hawakuwa na mahusiano yaliyojengwa kwenye kuaminiana na
kupatikana, mnyororo ungekatikia pale mwanzoni kabisa. Lakini
kwa neema ya Mungu na kwa faida yetu sisi na vizazi vyote vya
baadaye, Paulo alikuwa balozi mzuri sana, wa kuvutia, mwenye
uwezo mkubwa wa kutenda kazi kwa ajili ya Kristo. Na Timotheo
naye alikuwa mwanafunzi mwaminifu, anayepatikana na mwenye
kufundishika kwa urahisi.
UTARATIBU HUO UNAMFIKIAJE MWANAFUNZI?
Swali: Je, Paulo “alimfikishiaje” Timotheo? Utaratibu huo
ulimfikiaje Timotheo? Yeye aliwezaje kupata hali ya Paulo mpaka
naye akaweza kuiendeleza? Paulo alisema hivi: “Mambo yale
ambayo wewe umeyasikia kwangu …” Je, ni swala la kusikia tu? Je, 170
mtaala ni dhana za kielimu tu, au mawazo ya kifilosofia tu, ambayo
yanawea kufundishwa darasani kutoka kizazi hadi kingine? Hapana
kamwe! Sasa basi, neno “kusikia” lina maana gani katika Agano
Jipya? Mbona kusikia kunasimamishwa ili kuonyesha kuingizwa
kwa mambo ya kiroho badala ya kuona, au kunusa au kuonja au
kugusa? Ni kweli kwamba kuna mifano kiroho inayolingana na hizo
hisia za kimwili. Basi, mbona kusikia kunatengwa na kukaziwa
zaidi? Je, yaweza kuwa ni kwa sababu kusikia ndiyo hisia ambayo
kwa hiyo utambuzi halisi huenda moja kwa moja hadi ndani ya mtu?
Katika upokeaji wa hisia zingine zote, lazima kuwe na tafsiri. Picha
zinazoonekana na macho lazima zitafsiriwe ili kueleweka kama
mawazo na dhana, ndipo zifike ndani ya mtu. Ni kweli hata kuhusu
vitu tunavyogusa, kunusa au kuonja. Lakini katika kusikia,
mawasiliano ya moja kwa moja yanafanyika. Basi, “imani huja kwa
kusikia, na kinachosikilizwa ni Neno (rhema, ujumbe muhimu,
uliosemwa kwa upendo) la Mungu.”
JE, MPANGO WA KUSIKIA UNAHUSISHA NINI?
Katika mpango wa kufanya watu kuwa wanafunzi, huko
“kusikia” kunahusisha kitu gani? Katika 2Timotheo 3 kuna mistari
miwili inayoweza kutudokeza kidogo maana yake (ms. 10 na 11).
Paulo aliandika hivi: “Wewe umejua kabisa (Paulo aliishi maisha ya
wazi kabisa mbele ya Timotheo – uwazi … kufikisha ujumbe …
mabadiliko, ndiyo utaratibu) mafundisho yangu, maisha yangu 171
(mtindo), kusudi langu, imani yangu (au, uaminifu katika utendaji),
uvumilivu wangu (uwezo wa kuteseka kwa muda mrefu), upendo
wangu, subira na mateso yangu (kumbe Paulo hakumficha Timotheo
ukali wa dhiki yote aliyopata).”
Hayo ni matokeo ya kawaida kabisa ya kanuni ile inayoitwa
“pamoja naye, pamoja nami”. Yesu aliwaweka kumi na mbili ili
wawe pamoja naye” (ktk Marko 3:14). Kuwa mwanafunzi na
kufanya wengine kuwa wanafunzi ni mtindo wa maisha ambao
hunaswa zaidi ya kufunzwa. Hebu fikiri – kuna mtu anayeweza
kusafiri safari ndefu na Paulo bila ya kubadilishwa na safari hiyo?
BAADA YA MWANAFUNZI KUWEZESHWA, ANAFANYA
NINI?
Sasa basi, baada ya Timotheo “kuwezeshwa” au
“kukamilishwa” au “kufundishwa ipasavyo”, anafanya nini?
“Mambo yale uliyoyasikia kutoka kwangu mbele ya mashahidi
wengi, wewe nawe uyakabidhi hayo kwa watu waaminifu”.
Maneno mawili hapo ni muhimu sana katika kufafanua nafasi
na kazi ya Timotheo. Yeye anapaswa kukabidhi (ile imani yote,
mtindo wa maisha na kujitolea) kwa watu “waaminifu”. Hapa tuwe
makini sana. Hili ni mojawapo kati ya mambo ya hali ya juu sana
kuhusu akili ya Kikristo. Kitu hiki kinapofanya kazi sawasawa, siku
zote wanapatikana viongozi wa kizazi cha pili na cha tatu. Hii ndiyo
sababu ni muhimu sana sana kwamba mwenye kufanya watu kuwa 172
wanafunzi atafute tu kuingiza utaratibu huo katika watu waaminifu.
Kama wanafunzi wake watakuwa si waaminifu, mpango mzima
unaishia kwao, na vizazi vyote vya baadaye vinaweza kuachwa
pasipo uongozi wa kiroho wenye ujuzi.
Neno lingine linalopaswa kutazamwa vizuri tu ni lile neno
kuu katika mstari. Ni neno “wakabidhi”. Hapa tena, lazima tuwe
makini sana kuelewa vizuri maana yake. Ni neno la kibenki. Maana
yake halisi ni “kuweka fedha”. Unapokwenda benki kuweka fedha
katika akaunti ya kuweka fedha, unatazamia kupata faida fulani.
Ndivyo ilivyo unapofanya mtu kuwa mwanafunzi. Huwi
unayemsafisha mwenye dhambi tu ili awe safi. Unafanya uwekezaji
wa wingi na wa hali ya juu ambao utazaa faida isiyo na mwisho hadi
umilele wote!
JE, NI UWEKEZAJI AU NI MATUMIZI?
Basi, hebu niulize swali zito: Je, maisha yako ya sasa hivi ni
matumizi zaidi au ni uwekezaji? Je, unayatumia au unayawekeza?
Fikiri kwa umakini kidogo hapa. Kama unayatumia, basi matumizi
hayo ni mwisho. Hakuna faida kutokana na tendo hilo. Na ukweli
lazima usemwe. “Shughuli nyingi za Kikristo” tunazojihusisha nazo
– iwe ni kuhudhuria kanisani, kusoma Biblia, maombi, n.k. – ni
matumizi kuliko kuwa uwekezaji. Ni shughuli za “kujihami” tu
ambazo hutufanya sisi kuwa “Wakristo wazuri” badala ya kuwa
173
uwekezaji ambao utaigusa dunia hadi miisho ya nchi mpaka mwisho
wa wakati. Hivyo, shughuli hizo zinasaliti Agizo la Yesu Kristo.
Timotheo alitakiwa achukue akiba yote ya maisha ya Kristo
ambayo ilitoka kwa Paulo ikamfikia yeye, naye “aiweke” katika
maisha ya watu waaminifu, na utaratibu huo haujafanikiwa mpaka
nao waweze “kuwafundisha wengine pia.” Basi, utaratibu huo
unatakiwa kuzidi kuongezeka mpaka uwe kitu kikubwa chenye
kuhusika na eneo pana zaidi na zaidi na kuwahusisha watu zaidi na
zaidi.
MIFANO YA KUONYESHA UMUHIMU NA UWEZEKANO
WA MAONGEZEKO
Hebu tutumie mifano michache ya kawaida tu ili kuonyesha
umuhimu na uwezo wa kuongezeka.
MWINJILISTI
Hebu tudhanie kwamba yupo mwinjilisti ambaye angeweza
(na kweli wapo) kuleta watu elfu moja kila siku kwa Kristo. Kama
idadi ya watu duniani sasa hivi “ingegandishwa” hapo ilipo –
asiwepo mtu yeyote kuzaliwa na mtu yeyote kufa mpaka kila mtu
afikiwe na kumfuata Kristo, muda ambao ungehitajika kufikia idadi
ya sasa ya watu duniani ni zaidi ya miaka elfu kumi na tano! Na hapa
tukumbuke kwamba, hao watakuwa wameokoka tu, si kwamba ni
wanafunzi wa Yesu.174
KILA SIKU IWE YA PENTEKOSTE
Au, tuseme kwamba kila siku ingekuwa Siku ya Pentekoste,
wakiokoka watu elfu tatu kila siku. Ingechukua miaka kama elfu tano
hivi kuwaleta watu wote walioko duniani sasa hivi kwa Kristo! Na,
zingatia kwamba idadi ya watu haijanganda! Inaongezeka kwa kasi
kubwa sana. Basi, mambo yanakatisha tamaa, sivyo?
Hii ndiyo sababu lazima tufanyie kazi kanuni ile ya Biblia ya
kujizidisha. Sasa, mfano ufuatao ni wa kihesabu, wa kinadharia, na ni
kitu kisichokuwepo, lakini utatusaidia kuona uwezekano wa
kujizidisha kiroho. Tuseme kwamba mwanafunzi mmoja anayefanya
wengine kuwa wanafunzi ameguswa kabisa na kuingiziwa uwezo wa
kuwa mwalimu wa kufundisha wengine kuwa wanafunzi, naye
amtafute mwanafunzi mmoja ili amfundishe kwa mwaka mmoja kwa
njia ya kumwezesha na yeye kuwa na mwanafunzi na kumfundisha
kwa mwaka unaofuata, na hayo yaendelee hivyo hivyo bila
kubadilisha chochote katika utendaji na maongezeko, mpango huu
ungempita yule mwinjilisti “anayeokoa watu elfu moja kwa siku”
baada ya miaka 23, na (ni hoja tu) watu wote duniani wangefanywa
kuwa wanafunzi katika muda wa miaka 35. Ona tofauti kati ya
“waongofu” wa mwinjilisti na “wanafunzi” wa yule mzalishaji
mwenye maono.
Onyo: Mifano kama hii isitumike kupambanisha shughuli za
wainjilisti na wavuna roho dhidi ya wanaofanya watu kuwa 175
wanafunzi. Hizo ni nafasi zinazotegemeana, ambazo kila moja ni ya
muhimu. Kwa kweli ni vizuri hata nafasi hizo zote mbili
ziunganishwe katika kila mwamini anayekomaa na kuukulia wokovu.
Kwa nini kufanya watu kuwa wanafunzi kunaendelea kwa
kusuasua sana? Ukweli ni huu: Mungu amekosa watu wanaofaa na
wenye sifa za kuwa waanzilishi wa shughuli hiyo. Yaani, hakuna
wazalisha wanafunzi wa kutosha kuanzisha mpango huo duniani
kote. Lakini, hilo lisituvunje moyo. Tukiwa na maono na
mawasiliano, jambo hilo linaweza kurekebishwa haraka sana kuliko
tunavyofikiri. Tena kumbuka, mambo yanaanzia kwa Paulo kwenda
kwa Timotheo, ambaye ndiye anayefuata. Na mpango au utaratibu
mzima unategemeana na ubora, kujitolea, maono na utendaji wa hao
watu wawili wa kwanza. Kwa sababu, kikawaida, wao ndiyo mifano
inayoonekana pale mwanzoni kabisa na wenzao, pamoja na kwamba
hilo ni jambo la kutisha.
Umuhimu wa maongezeko ya kila siku ni mkubwa sana kwa
ajili ya kuhitimisha mpango mzima. Hakuna mtu anayetakiwa
kushindwa. Mkristo mmoja akishindwa kufanikisha sehemu yake ya
kuongezeka, anapunguza uwezo wa kutimiza Agizo Kuu katika
kipindi cha uhai wake kwa nusu nzima. Lakini, kama Mkristo mmoja
tu akifanikiwa (na kujizidisha), anaongeza mara mbili uwezo huo
katika kipindi cha uhai wake.
176
MAONO YA KUIGUSA DUNIA NZIMA KWA KUFANYA
WATU KUWA WANAFUNZI
Ewe Mkristo, unayo maono ya kuigusa dunia nzima kwa
kufanya watu kuwa wanafunzi? Je, unawekeza vizuri kabisa ule
mtindo wa maisha ya Yesu, maono ya Yesu, na kujitolea kwa Yesu
katika maisha ya watu binafsi ili nao wawe na maono hayo hayo na
kujitolea, na kuweza kuwapa wengine? Kuna mtu ambaye amesema
hivi, kwa busara kabisa: Ili uweze kugawa maono kwa wengine,
lazima wewe mwenyewe:
Uyaone waziwazi,
Uyaseme kwa ubunifu,
Uyaonyeshe kila wakati,
Uwashirikishe watu wengine kwa bidii, na
Uyalinde kwa uangalifu sana.
177
Sura Ya 7Hekima Ya Mkakati Wa Yesu
Tunaianza sura hii kwa kutazama andiko linaloonekana si
kitu kabisa. Ukweli ni kwamba, unaweza kusoma barua ya Paulo ya
Kwanza kwa Wathesalonike mara mia bila hata ya kujali mstari huu.
Lakini – na hii ni kawaida katika Maandiko – mara nyingi Mungu
huficha hekima ya Mbinguni katika maandiko yasiyokuwa wazi
sana, na huu ni mfano mmoja. Katika mstari huu kumefichwa
utukufu wote na hekima ya Ukristo. Mstari wenyewe ni 1Wathes.
3:8, unaosema hivi: “Kwa kuwa sasa twaishi, ikiwa ninyi
mnasimama imara katika Bwana”.
Kumbuka kwamba Agano Jipya liliandikwa kwa lugha ya
Kiyunani, na uzuri mmoja wa lugha ya Kiyunani ni kwamba
mpangilio wa maneno katika sentensi hudhihirisha kama hayo
maneno yana uzito, na kama ndivyo, uzito huo ni mdogo (mfano:
Roho Mtakatifu anapandisha sauti Yake) au ni mkubwa (mfano:
Roho Mtakatifu anapiga kelele). Sasa – katika 1Wathes. 3:8, maneno
yamepangwa kwa njia kwamba neno moja limebeba mkazo, na ni
mkazo mkubwa. Mara nyingi nimewauliza watu kukisia ni neno gani
lililokaziwa, na wameshindwa. Ni hivi: Hatuwezi kwa akili zetu
kama binadamu kukisia na tukapata usahihi kuhusu Mungu. Hata
kama tutabahatisha jibu sahihi, jibu letu bado ni kosa kwa sababu
178
tulikisia. Hii ndiyo sababu imetupasa kujifunza Biblia, “tukilitumia
kwa uhalali Neno la Kweli” (ktk 2Timotheo 2:15).
Neno moja ambalo limekaziwa (tena kwa mkazo mkubwa
kabisa) ni neno “ninyi”. Hebu soma mstari wote kwa sauti, ukipaza
sauti unapotamka neno “ninyi”. Je, sasa unaweza kuelewa maana
yake? Je, sasa unaona hekima na akili ya Ukristo? Je, sasa unaona
wazi kwa nini neno “ninyi” liwe ndiyo neno kuu? Hebu tuchunguze
kwa upana zaidi mpaka tupate mahali panapofaa kushika na
kufahamu.
Kuna namna mbili za maisha ambazo wanadamu wanaweza
kuzifuata. Watu wengi hawatambui injili, lakini njia moja ni mtindo
wa maisha wa Shetani, na njia nyingine ni mtindo wa maisha wa
Mwokozi. Njia moja ndiyo mtindo wa maisha wa kawaida wa
mwenye dhambi (na yawezekana kuwa ndiyo njia pekee ya maisha
ambayo mtu aliyepotea anaweza kuishi), na ile nyingine ni mtindo
wa maisha wa kawaida kabisa wa mtakatifu mtendaji. Nayatumia
maneno haya kwa makini na uangalifu sana, kwa sababu mtu yeyote
aliyeokoka anaweza wakati wowote kurejelea mtindo wa maisha wa
Shetani.
Ngoja nichore mchoro utakaotuwezesha kuona vizuri mitindo
hii ya kinyume ya maisha.
179
Nauita mtindo huu wa maisha wa “kutoka nje kuingia ndani”.
Haya ndiyo maisha yasiyoepukika, ya lazima ambayo ni kawaida
kwa kila mtu ambaye hajawahi kuzaliwa na Mungu. Anaishi kama
sponji – siku zote ananyonya au kufyonza vitu kutoka katika
mazingira yake kwa ajili ya faida yake binafsi. Huo ndiyo mtindo wa
maisha wa Shetani. Hilo ndilo lililomfanya Shetani kuwa Shetani,
kule kusema, “Nita”. Alirudia hilo tena na tena, akihamisha imani
yake kutoka kwa Mungu mpaka kuwa kwake mwenyewe. Hiyo
ndiyo tafsiri ifaayo ya dhambi – “Ubinafsi”. Dhambi ni “mkunjo
binafsi” wa maisha unaomfanya kila mwanadamu kugeuzia kila kitu
ndani yake mwenyewe. Dhambi ni jitihada za mwanadamu kutafuta
maana na utoshelevu katika maisha kwa ajili yake binafsi na ndani
yake mwenyewe – pasipo Mungu.
Sasa, ni lazima tukiri – japo inasikitisha – kwamba, mtu
aliyezaliwa mara ya pili anaweza pia kurejea mpaka kwenye mtindo
huo wa maisha. Kwa kuwa alichukua “mwili” na kuingia nao katika
maisha yake mapya ndani ya Kristo, wakati wowote anaweza 180
kujiamini mwenyewe na kutafuta kujinufaisha badala ya kumwamini
Kristo na kuishi kwa ajili ya utukufu wa Mungu. Wakati Mkristo
anapoishi kwa ubinafsi, anatumbukia katika mojawapo ya makundi
mawili. Anaingia katika kundi la kuishi “kwa ubinafsi” au katika
maisha ya “kujiponya”. Kila kitu anachofanya kinamtia katika hali
ngumu ya kuishi kwa ajili ya faida yake binafsi au kwa ajili ya
kujiponya. Hata kama atasoma Biblia, aombe na kujaribu
kumtumikia Mungu, atafanya hivyo kwa sababu fulani ya kibinafsi
tu. Biblia inasema, hiyo ni hali “ya kimwili”.
Mtindo mwingine wa maisha unaweza kuonekana kwenye
mchoro huu. Upande wa kushoto unamwakilisha Yesu na upande wa
kulia ni mwamini aliyezaliwa mara ya pili.
Mtu aliyezaliwa mara ya pili anakuwa na mwenzi – Yesu
Kristo. Huyu anakuwa amehamishia matumaini yake kutoka kwenye
ubinafsi na juhudi binafsi, na kuyaweka kwa Kristo. Kumekuwepo
na hali ya kuunganika na kuwasiliana kati yake na Kristo. Maisha ya
Kristo yameingia ndani yake, na “kiini cha msimamo” ndani yake 181
kimehama kutoka kwake hadi kwa Kristo. Hii inaitwa “wokovu,
kuongoka, kuzaliwa tena, kuzaliwa mara ya pili” kwa lugha ya Biblia
na imani. Maneno hayo yote yanaonyesha muujiza kabisa wa Mungu
ambao unamtikisa mwenye dhambi kutoka katika kiini chake cha utu
na kumwondolea ubinafsi, na kumtia Bwana Yesu Kristo mtukufu
katikati kabisa ya maisha yake badala ya yule nafsi aliyeingiliwa na
Shetani, mwenye ubinafsi. Nasema tena, huu ni muujiza kamili wa
Mungu! Watu ambao hawajaokoka siku zote hawataelewa vizuri
kuzaliwa mara ya pili ni kitu gani. Wao wanafikiri ni mwanzo mpya
tu au kuupuuza kwamba ni ushika dini wa kupindukia. Swali la
kipuuzi: Je, mtu ambaye hajazaliwa, anaweza kweli kuelewa maisha
ya mwanadamu?
Mchoro wa pili unaonesha picha ya mtindo wa maisha
tunaweza kuuita “kutoka ndani kwenda nje” ambao ni mtindo wa
maisha wa Mungu Mwenyewe. Yesu “alijitoa mwenyewe kwa ajili
yetu” na hapo akatuonyesha jinsi Mungu anavyofanya kazi
kikawaida kabisa. Na Mkristo mtendaji huishi katika mahusiano ya
imani na Yesu Kristo, siku zote akipokea uwezo ule wa kushangaza
sana wa maisha ya kweli kabisa ya imani ya kweli. Hayo yote hupitia
kwake na kumtosheleza yeye, na kutoka na kumwendea mwingine
pia.
Sasa, hebu tusome tena ule mstari wetu. “Kwa kuwa sasa
twaishi, ikiwa NINYI mnasimama imara katika Bwana.” Wakristo
wengine hawaelewi vizuri mstari huu, kwa hiyo wanafikiri hivi: 182
“Ninaishi kama ninaomba vya kutosha.” Kama Mkristo, “ninaishi
kama ninasoma Biblia kiasi cha kutosha.” Au “ninaishi ikiwa
nimejitoa kabisa.” Au, “ninaishi kama mimi ni mwaminifu kabisa.”
Au, “ninaishi kama ni mwema kiasi cha kutosha.” Au “ninaishi kama
nimehamasika kabisa”. Au, “ninaishi kama ni mtendaji mwaminifu”.
Lakini, hayo maneno yote mazuri sana yana ule uwezo uliofichika
wa kugeuza maisha ya mtu huyo kurudi kwake na ndani yake tena.
Huu ndiyo ule mkunjo uliofichika sana wa ubinafsi utokanao na
mwili, na huwadanganya watu wengi sana waliokwisha okoka.
Yesu alisema hivi: “Yeye atakaye kuyaokoa maisha yake
mwenyewe (yaani, maisha ya kujitakia faida, kujijali, kujihami)
atayapoteza, lakini yeye atakayetoa maisha yake kwa ajili Yangu na
Injili, atayaokoa.” Basi kumbe, maisha yanayosimuliwa huko nyuma
ni maisha ya hasara, lakini yale maisha ya kujisahau mwenyewe,
kujitoa mwenyewe, kutojijali mwenyewe katika maelezo ya pili
ndiyo maisha yaliyo-okoka.
Sasa hebu tubadilishe michoro kidogo. Kama ilivyo kwa watu
binafsi, ni kweli pia kwa makanisa. Hata makanisa pia yanaweza
183
kujielekea yenyewe, yakaishi kibinafsi au kichoyo kwa ajili ya faida
yao wenyewe au usalama wao pamoja na kwamba yanakuwa katika
kutafuta watu, ila, ni kwa faida yao wenyewe ya ndani!), badala ya
kukuza na kumaliza kabisa njia zao za kujisaidia kufikia kiwango
kwamba wanasukuma na daima kupima rasilmali za miujiza ya
Mungu.
Mtindo wa maisha ya Kikristo ni kuishi kwa mahusiano, bila
ubinafsi, kwa kujisahau wenyewe, kuwafikiria wengine kiasi kwamba
Mkristo mmoja anaishi kweli ikiwa mwanafunzi wake anasimama
imara katika Bwana. Paulo alisema, “Mimi ninaishi ikiwa ninyi
mnasimama imara katika Bwana.” Basi, Mkristo anaishi katika, kwa
njia ya, kwa ajili ya, na kupitia wanafunzi wake!
Huo si ndiyo mtindo wa Yesu kabisa, na jinsi ya kuifikia
dunia? Yeye alijijenga Mwenyewe katika watu kumi na mbili kiasi
kwamba, baada ya kipindi cha mafunzo cha miaka mitatu, alisema,
“Kwaherini! Sasa maisha Yangu yako katika uangalizi wenu. Mimi
ninaishi kama mtasimama imara!” Wapendwa wangu, hiyo ndiyo
hali nzima ya kufanya watu kuwa wanafunzi.
Inasemekana kwamba “Mazoezi Humfanya Mtu
Kukamilika”. Hii kanuni imesemwa kana kwamba ni kitu
kisichobadilika, kisichoonekana, na kisichopingwa. Lakini mimi
naomba niulize swali lenye maana. Tuseme kwamba kiwango
kinachofanyiwa mazoezi si kikamilifu. Yawezekana kweli mazoezi
yote duniani yatakayofanyika yakibadili hicho kuwa “kikamilifu”? 184
Bila shaka hapana! Ni hivi: Mazoezi hufanya kitu kikae daima;
haimaanishi kwamba kinafanya kila kitu kuwa kamilifu. Hebu
tufafanue na kutoa maana. Bila shaka inawezekana kwamba kanisa la
Yesu Kristo limetenda kwa kufuata kanuni za kawaida na mapokeo
kiasi kwamba “kujizoeza” kwake kwote kunazidi kulikita katika
kiwango kisichokuwa kamilifu.
Kama dhana ya mafunzo haya ni sahihi, kwamba Agizo Kuu
linawakilisha “Amri ya Kusonga Mbele” ya pekee iliyotolewa na
Yesu Kristo kwa Kanisa Lake, na kama jinsi ya kuelewa Agizo hilo
Kuu kulikotajwa katika mafunzo haya ni sahihi, basi mkakati wa
kawaida kabisa wa kanisa la kawaida una makosa. Je, kujenga taasisi
badala ya kujenga watu kumechukua nafasi kubwa katika kanisa la
leo? Kumbuka kwamba maana ya “kufanya watu kuwa wanafunzi”
inatokana na njia na agizo la Yesu. Kazi Kuu anayotoa inatajwa
vizuri sana katika amri moja iliyoko katika Agizo Kuu: “Wafanyeni
watu kuwa wanafunzi.” Na njia Yake inaonyeshwa katika mkakati
Wake wa kuwashirikisha watu binafsi katika kikundi kidogo – watu
kumi na mbili.
Hebu tuulize tena swali hili. Je, Ukristo unaowakilishwa sasa
na kanisa lako ungeweza kusababisha Kitabu cha Matendo ya
Mitume? Hili swali linatia aibu, kwa hiyo halina jibu la haraka. Au
tuseme kwa njia nyingine. Je, Ukristo wa Kitabu cha Matendo ya
Mitume ungevumilia hali iliyoko duniani kwa sasa – hali kwamba
karibu nusu ya binadamu wote wanaokaa duniani bado hawajasikia 185
Injili (miaka elfu mbili na zaidi baada ya Kristo!) na kwamba 4/5 ya
binadamu wote wamesikia Injili kijuu-juu tu? Je, Ukristo wa Kitabu
cha Matendo ya Mitume ungevumilia hali iliyoko kanisani katika
kila nchi iliyofikiwa duniani, inayosimuliwa katika kitabu cha
Patrick Johnstone kiitwacho Operation World hivi: “Nchi hii
inahitaji sana viongozi walioelimika?” Jibu linalotia aibu la maswali
hayo yote ni “Hapana!” ya sauti kubwa sana. Sasa basi, hii mikakati
na njia za sasa vitarekebisha huku kushindwa? Mpaka kitabu hiki
kinapoandikwa, haijafanikiwa. Sawa. Si basi tuziache, na kwa ujasiri
mkubwa tupitie tena ule mkakati wa kwanza wa Yesu, na tuone ni
tofauti zipi zimetuondoa kwenye huo mkakati Wake?
Kuna maneno ya kawaida kabisa yanayotumiwa kanisani,
ambayo tumeyadhania tu. Maneno hayo ni “kama Kristo”. Nadhani
Wakristo karibu wote wangekiri kwamba lengo la maisha ya Kikristo
ni kumfanya mwamini binafsi kuwa kama Kristo. Ukweli ni
kwamba, hilo ndilo lengo la Mungu ambalo limetamkwa wazi wazi
kwa ajili ya kila mtoto Wake. Katika Warumi 8:29 tunaona kwamba
hilo limekuwa lengo na kusudi la Mungu siku zote kwamba
“tufananishwe na mfano wa Mwana Wake,” au, kutufanya kama
Kristo. Lakini tena, tumepungukiwa sana na kiwango cha Biblia
katika kufafanua maana yake. Sisi tunafafanua tu na kutoa maelezo
kwamba linahusiana na “tunda la Roho” katika Wagalatia 5:22, 23.
Lakini, nani anaweza kupingana na maelezo hayo? Kama mtu akizaa
tunda la Roho, tabia yake ya ndani ni kama ile ya Kristo bila shaka. 186
Lakini, hebu tufuate mfano wa matunda. Je, tunda lina jinsi ya ndani
tu, au pia lina umbo la nje? Tutumie mfano huu. Mnunuzi wa
matunda anapokwenda kutafuta malimau, anatafuta “hali ya
ulimau”? Hapana. Yeye anatafuta tunda dogo la mviringo, lenye
rangi ya manjano na ganda gumu kidogo. Yaani, limau lina umbo
lake halisi la nje, lenye kueleweka, ambalo ni tofauti na umbo la
boga, embe au ndizi. Pendekezo langu ni kwamba, tunda la Roho ni
mwanzo mzuri katika jitihada za kuwafafanua Wakristo. Je, kuwa
kama Kristo kuna umbo la nje pamoja na jinsi ya ndani?
Ngoja niliseme vizuri kwa sentensi moja tu: hutaweza
kufanya kitu chochote kitakachozidi lengo lako la kuwa kama Kristo
kuliko kuwafundisha makundi ya watu kuishi katika umoja na Yesu
Kristo kwa ndani, na kujiongeza, kujizidisha, na kuifikia dunia nzima
kwa nje. Maneno muhimu kimkakati ni “kufundisha,” (kwa kutumia
mkakati na mtaala uliotolewa na Yesu), “makundi” (kwa kufuata
ukubwa wa kikundi uliotolewa na Yesu), “muungano au umoja”
(kwa njia hiyo, kufanya maisha ya Kristo, huduma na motisha kuwa
vyetu), “kujiongeza na kujizidisha” (ambalo ni jukumu la kila mtoto
wa Mungu) na “kuifikia dunia nzima” (ambayo ni kama lengo la kila
saa kwa ajili ya kila mtoto wa Mungu). Na hayo yote yataamua
mikakati tutakayotumia kufanikisha hilo lengo.
Katika muda mtakatifu sana kihistoria unaotajwa na Yohana
19:30, Yesu alisema neno moja ambalo pengine ndiyo la maana
kuliko yote yaliyowahi kusemwa. Neno lenyewe ni tetelestai, 187
“imekwisha” au “ni tayari”. Kazi iliyokuwa imekwisha na
kukamilika wakati huo ni kazi ya ukombozi, neno moja
linalojumlisha kila kitu ambacho Mungu amekifanya ili kuwaokoa
wenye dhambi kabisa.
Yesu analitumia tena neno hilo katika Yohana 17:4.
“Nimekutukuza hapa duniani, nimemaliza kazi uliyonipa kuifanya.”
Je, Yesu alikuwa amemaliza kazi gani hapa? Wasomi wengi
wanasema kwamba tamko hilo pia linahusiana na kazi ya ukombozi
ambayo Yesu aliikamilisha pale msalabani, lakini sidhani. Yesu
anatumia neno la wakati uliopita, na msalaba ulikuwa bado mbele
Yake! Hapa hakuwa anasema kuhusu kazi ya ukombozi, bali kazi ya
uzalishaji. Hapa, utaratibu Wake wote wa mafunzo kwa ajili ya watu
Wake ulikuwa umekamilika. Kumbe Yesu alikuja duniani kufanya
na kukamilisha kazi mbili muhimu sana: Ukombozi na uzalishaji.
Bila kazi ya ukombozi iliyokamilishwa na Kristo kufa msalabani,
kusingekuwa na kitu chochote cha kuzalishwa, lakini tena, bila kazi
ya kuzalishwa kupitia kuongezeka kwa Wakristo, kazi ya ukombozi
ingejulikana kidogo tu, au kwa sehemu tu, au kwa hali ya chini sana
(ambayo ndiyo hali ya dunia ya leo, na hata ya kanisa la leo).
Hapa tena, swali muhimu. Nini maana ya “kuzalisha” kwa
maana ya Agano Jipya? Ni watu wangapi wanaotazamiwa kuzalisha,
na wanatazamiwa kuzalisha kiasi gani? Je, uzalishaji huo ni kufyatua
tu (kiwango cha kuvuna roho, au kuwaleta wenye dhambi kwa
Kristo) au ni kitu kinachotakiwa kusababisha maongezeko? Kama ni 188
maongezeko, yawe ya ukubwa gani? Na je, malengo halali katika hili
yafikiwe vipi? Hapa tena, mbinu na njia ya Yesu viwe mwongozo
wetu.
Hebu tuchukue mfano mmoja ili tuuchunguze kwa haraka. Je,
Yesu alifuata mfano gani katika kuzalisha? Je, alizalishaje watu
watakaowazidisha wengine? Je, aliwezaje kusababisha mtazamo na
nia katika watu kumi na mbili uliopelekea dunia nzima kuguswa
mpaka sehemu za mwisho kabisa za dunia ya wakati Wake katika
kipindi cha miaka sitini tu baada ya kifo Chake? Soma tena sentensi
hii ya mwisho na uiruhusu kweli yake iingie katika akili zako.
Ruhusu swali lake lisisimue moyo wako? Ilikuwaje? Yeye aliwezaje?
Aliwezaje kusababisha mtazamo na nia? Tena, katika watu kumi na
mbili!!?? Ambavyo vilipelekea dunia nzima kufikiwa? Mpaka
miisho ya dunia iliyojulikana siku zile? Katika kipindi cha miaka
sitini tu baada ya kifo Chake? Yeye hakuwa na televisheni,
uchangishaji wa fedha, simu, njia zozote za mawasiliano ya kisasa.
Yeye alitumia mbinu ya mtu kumwambia mtu! Vipi? Ilikuwaje?
Ilitokeaje? Hakuna chochote katika mpango Wake kilichotegemea
watu wengi. Hakuna chochote katika mpango Wake kilichotegemea
mahubiri (japo aliwasiliana na watu wengi kutoa huduma,
kufundisha, na kuibua wanafunzi wa baadaye). Hakuna chochote
katika mpango Wake kilichokuwa taasisi (na hapa tunachosema ni
ukweli tu, si kwamba tunafanya tathmimi ya taasisi). Hakuna
189
chochote katika mpango Wake kilichojengwa kwenye kwenda
kanisani (japo Mwenyewe alihudhuria kanisa kwa uaminifu).
Sasa basi MKAKATI WAKE ULIKUWA NINI? ALITUMIA
MBINU GANI? ALITUMIA NJIA GANI?
Pengine tutapata dokezo kwa kutazama orodha za wale watu
aliowaita “mitume” kama zinavyoonekana katika Biblia. Hebu
tuseme kwanza kabisa kwamba Yeye aliwafundisha ili awatume
mbali Naye, si ili aongeze makundi ya watu mahali alipokuwepo.
Huu mkakati haufanani kabisa na kanisa la leo hata kidogo tu,
ambalo lina tabia ya kutathmini kufanikiwa kwake (na mafanikio ya
viongozi wake) kwa kawaida kupitia kipimo. Orodha zile nne za
Mitume zinapatikana katika Mathayo 10, Marko 3, Luka 6 na
Matendo 1. Hizo orodha peke yake zinapaswa kusababisha mafunzo
mengi sana. Kuna masomo yasiyoelezeka na ya milele kutokana na
kujifunza hizo orodha tena na tena. Tuzitazame hapa.
Mathayo Marko Luka Matendo
Simoni (aitwaye Petro) Simoni (aitwaye Petro) Simoni (aitwaye Petro) Petro
Andrea Yakobo wa Zebedayo Andrea Yohana
Yakobo wa Zebedayo Yohana Yakobo Yakobo
Yohana Andrea Yohana Andrea
Filipo Filipo Filipo Filipo
190
Batolomayo Batolomayo Batolomayo
Tomaso
Tomaso Matayo Matayo
Batolomayo
Matayo Tomaso Tomaso
Matayo
Yakobo wa Alfayo Yakobo wa Alfayo Yakobo wa Alfayo Yakobo
wa Alfayo
Tadayo Tadayo Simoni Mzelote Simoni
Mzelote
Simoni Mzelote Simoni Mzelote Yuda wa Yakobo Yuda wa
Yakobo
Yuda Iskariote Yuda Iskariote Yuda Iskariote
Ona yaliyo dhahiri hapa. Jina lile lile linatokea mwanzo
kwenye kila orodha. Labda tuseme hivi, ni mtu yule yule, ingawa jina
halifanani kila mahali. Kwanza, “Simoni Petro” halafu “Petro”.
Turekebishe kidogo tena. Ni mtu yule yule – lakini ni dhahiri pia
kwamba si mtu yule yule! Safari ya kuhama toka kwa “Simoni”
mwenye kutawala, hadi kufikia kwa “Petro” mwenye kutawala ni
somo kubwa sana kuhusu mkakati, mbinu, njia na utaratibu wa Yesu
191
katika kuwajenga wanafunzi. Je, hilo tu si ndiyo amri pekee iliyoko
katika Agizo Kuu Lake alilotupa sisi (yaani, kuwajenga wanafunzi)?
Kama ndivyo, basi tunatakiwa kufuata kwa makini sana na kwa kiasi
tunachoweza mkakati, mbinu, njia na utaratibu wa Yesu (la sivyo,
tutazamie matokeo tofauti – ambayo kwa bahati mbaya, ndivyo
imekuwa katika kanisa la siku hizi). Ni mafunzo yenye maana sana
kufuatilia tu ule utartatibu wa mafunzo ambao Yesu aliupitia kwa
ajili ya Simoni Petro peke yake. Kama mafungu yale yenye kueleza
jinsi Yesu na Petro walivyokutana, walivyozungumza na
walivyofundishana, na kama yatakuwa ndiyo kiwango kwa ajili ya
kujenga wanafunzi katika kanisa la siku hizi, basi ni rahisi kabisa
kuona kwa nini tunateseka na hali ya kutokuwa na matokeo yafaayo
(yaani, kuwa na Wakristo ambao hawajajengwa na kuwa na dunia
ambayo kwa sehemu kubwa haijafikiwa). Ingewezekana kila Mkristo
ajifunze somo hili ingekuwa vizuri sana. Kutazama utaratibu ambao
kwa huo Yesu alimaliza “Simoni” (jina lake kabla hajaokoka, lenye
kuonyesha hali yake ya kimwili) na kumwibua “Petro” (jina lake
linalotumiwa kikawaida katika Kitabu cha Matendo) ni kitu
kinachofungua macho ya mtu yeyote anayetamani kujua njia ya Yesu
katika kuwajenga wanafunzi.
Unapotazama mstari wa pili kwenye ile orodha, utaona
kwamba majina hayafanani. Ndivyo ilivyo kwa mstari wa tatu na wa
nne. Lakini –– katika mstari wa tano jina ni lile lile. Hii ni muhimu
ili kuelewa mkakati wa mafunzo aliotumia Yesu. Mstari wa sita 192
hauna jina moja, wala wa saba, wala wa nane. Lakini –tena – katika
mstari wa tisa jina ni lile lile moja. Mstari wa kumi una majina
tofauti, na wa kumi na moja, na wa kumi na mbili (kama utajaza
nafasi iliyoachwa wazi na kifo cha Yuda Iskariote kwa kuandika jina
la mtu aliyechaguliwa kumrithi, yaani Matiya).
Pengine mpaka hapo tumeanza kuona njia ya msingi kabisa
iliyotumiwa na Yesu katika kujenga wanafunzi wenye maono ya
dunia nzima, wenye uwezo wa kuigusa dunia nzima, na wenye
kuzalisha wanaojiongeza kama wao wenyewe. Tunajua bila shaka
yoyote kwamba mkakati wa Yesu ulikuwa umejengwa kwenye kundi
dogo la watu kumi na mbili. Pia tunajua kwamba Yesu aliweka
“mayai” Yake yote katika hicho “kikapu” Chake kidogo sana.
Mpango Wake wote kwa ajili ya kuigusa na kuifikia dunia ulikuwa
umewekwa katika mikono (na uzalishaji) ya watu kumi na mbili!
Tena, orodha ya Mitume inaonyesha pia njia Yake katika kuwajenga
watu hao. Bila shaka Yeye (na ni dhahiri ukitazama tu) aliwagawa
watu Wake hao kumi na mbili katika makundi matatu yenye
kulingana, yenye watu wanne kila moja, na kuweka kiongozi kwa
ajili ya kila kundi. Tuna ushahidi gani kuhusu hili? Mbona ni
mkubwa tu ushahidi huo? Haiwezi kuwa ni bahati au bahati mbaya.
Watu wote katika kundi la kwanza (na hao tu) ndiyo walikuwa
wafuasi wa Yohana Mbatizaji waliokuja kumfuata Yesu kwa sababu
ya kutiwa moyo na kiongozi wao. Hao watu wote katika kundi la
kwanza ni watu wenye uwezo na machachari, kama Simoni Petro, 193
kiongozi wao. Yakobo na Yohana waliitwa “Wana wa Ngurumo” na
Yesu Mwenyewe! Kitabia walikuwa kama ngurumo inayotaka
kuanza kazi. Andrea bila shaka ndiye mwenye uwezo mkubwa
kuliko tunavyofikiri kwa kawaida. Yeye ndiye alikuwa mishenari wa
kwanza kufanya kazi nyumbani (ktk Yohana 1:40-42), mtenda kazi
kwa ajili ya vijana na kwa ajili ya jamii (ktk Yohana 6:8, 9), na ndiye
alikuwa mishenari wa kwanza kufanya kazi nje ya nyumbani (ktk
Yohana 12:20-22). Haiwezekani kwamba mtu mpole aliyezubaa
angeweza kufanikisha mambo yote hayo ambayo yanatajwa katika
maandiko hayo! Basi, hawa walikuwa watu wenye uwezo katika
utendaji.
Kundi la pili linaongozwa na Mtume Filipo, ambaye katika
Injili anaonekana kuwa mtu mfikiriaji, au mwanafalsafa. Na kila mtu
katika kundi lake alikuwa hivyo hivyo – Tomaso “mwenye mashaka”
na Lawi Matayo, aliyeandika Injili yenye mafundisho ya hali ya juu
sana ya Yesu. Ona kwamba Yesu hakumweka mwanafalsafa kuwa
kiongozi mkuu katika kundi Lake maana asingefanikisha chochote!
Kwa kawaida, watu aina hiyo ni wenye mashaka sana, wenye
maswali mengi, watafiti wakuu, wapinzani wakuu, wepesi kuzembea
na ni wachangiaji wakubwa kuhusu utume wa Kikristo. Lakini,
hawawezi kuwa viongozi wa kundi. Lakini, tusipuuze umuhimu na
ulazima wa watu hawa tunapotafakari hoja hii. Ni kwamba tunaona
tena jambo lingine kubwa na la maana sana katika mkakati wa Yesu.
194
Sasa – kaa tayari. Kundi la tatu lilikuwa na wanamapinduzi
wa kisiasa tu! Kiongozi wao – Yakobo mwana wa Alfayo – pengine
ndiye alikuwa mpole kuliko wote katika kundi hilo! Pengine jina la
pili la Yuda, “Iskariote” laweza kutokana na kisu kidogo kilichokuwa
kinabebwa na baadhi ya wanamapinduzi waliokuwa wamejizatiti
kukitumia kumwua afisa yeyote wa Kirumi ambaye wangefanikiwa
kumpata katika kundi la watu (au popote pale ikiwezekana). Hili ni
jambo la ajabu. Kuna ushahidi mkubwa tu kwamba Yakobo na
Matayo (ambao wote wanaitwa “mwana wa Alfayo”) walikuwa
ndugu. Je, hili linakusisimua kiasi? Mbona mmoja (Matayo) akawa
msaliti kwa kuunga mkono Rumi, akitoa maisha yake kulipisha kodi
toka kwa Wayahudi kwa ajili ya serikali ya Kirumi, ambayo
waliichukia? Mbona yule mwingine (Yakobo) akawa mzalendo
hodari wa Kiyahudi? Je, kuna aliyeitikia maoni ya mwenzake ya
kupita kiasi? Je, uzalendo wa Yakobo ulimfanya Matayo aisogelee
Rumi? Au je, usaliti wa Matayo ulimfanya Yakobo kuingia katika
matendo ya kisiasa na kimapinduzi? Au? Hoja yoyote tutakayotoa
inadhoofishwa na ukimya wa Maandiko, lakini swali hilo linaibua
maswali na fikira sana. Yule anayeitwa “Mzelote” anatambulishwa
kwa jina lake na chama cha siasa kilichokuwa cha kizalendo sana,
chenye uasi na ukatili sana kilichoitwa hivyo hivyo. Je, ulijua
kwamba kama Simoni Mzetole angekutana na Matayo mtoza ushuru
katika hali “ya kawaida” tu, angemwua upesi sana? Ndiyo maana
nasema, Muujiza Mkuu wa Yesu haukuwa kuwalisha watu wenye 195
njaa kwa kuongeza chakula, au kuwaponya wagonjwa, au hata
kufufua wafu. Kwangu mimi, Muujiza Wake Mkuu ulikuwa ni
kujenga – kwa kutumia vifaa “visivyowezekana” – kundi la Watu
Kumi na Mbili ambao wangetikisa dunia kwa Uzalishaji wa Kiroho
hadi miisho ya dunia ya siku zile! Na, kama kanisa lisingebadilisha
mkakati wa Yesu (wa kujenga watu) na kuweka kitu mbadala
kinachowafaa wao, ambacho hakika kinatokana na chanzo kingine
(kujenga taasisi zenye kujijali kwa ndani), mawimbi hayo
yaliyoanzishwa na wanafunzi yangekuwa yanaitikisa dunia mpaka
miisho yake hadi leo, na kuendelea kufanya hivyo bila kuzuiwa wala
kupungua hadi mwisho wa dahari.
Charlie Chaplin – mchekeshaji maarufu sana duniani –
alipokuwa hai, yalifanyika mashindano ya “Wanaofanana na Charlie
Chaplina” huko nchi ya Monaco. Bwana Chaplin alisafiri mpaka
huko, akaingia kwenye shindano hilo pasipo kujulikana, na akawa
mshindi wa tatu! Kweli najiuliza Yesu wa kweli angeshika nafasi
gani katika kanisa la siku hizi kama yangefanyika mashindano ya
“Wanaofanana na Kristo”???
Usielewe hii sura vibaya. Hakuna amri ya wazi
inayotulazimisha sisi kufuata mpango wa vikundi huo. Lakini, busara
ya kawaida tu ingeshauri kwamba, “kama Kristo” maana yake “kama
Kristo”. Hilo linaonekana jepesi kabisa, lakini ukweli wake
umeshindwa kupatikana katika kanisa. Ukubwa wa kundi la Yesu
unaonekana kuwa wa busara sana, pamoja na migawanyo yake, 196
maana inatoa nafasi ya uwajibikaji, mgawanyo wa kazi, ushirika na
kadhalika. Lakini hakika, makundi hayo hayakuwa yamefungwa na
yasiyoweza kubadilika. Matokeo yanathibitisha kwamba Yesu
alikuwa Bingwa wa jinsi vikundi vinavyofanya kazi na kushirikiana.
Mbona sisi tusiwe na hekima ya kufanya hivyo? Je, kweli sisi tuna
hekima tusipofanya hivyo?
Narudia tena: wewe … na wewe … na wewe … hamtafanya
kitu kama Kristo katika maisha yenu yote kitakachozidi
kuwafundisha watu binafsi kwa kufuata mkakati wa Yesu (yaani,
“kuwafanya watu kuwa wanafunzi”) ili kuifikia na kuigusa dunia
nzima.
Je, wakati haujafika wa sisi kukagua shughuli zetu zote ili
kuhakikisha kwamba tunatimiza lile Agizo la Yesu kikamilifu, kwa
uzito na kwa mtiririko wa utaratibu unaofaa?
197
Sura Ya 8
Jinsi Kiwango Hiki Kifanyavyo Kazi Kanisani
“Lakini kila mmoja wetu alipewa neema kwa kadiri ya kipimo cha kipawa chake Kristo. Hivyo husema, ‘Alipopaa juu aliteka mateka, akawapa wanadamu vipawa.’ Basi neno hilo ‘Alipaa’, maana yake nini kama siyo kusema kwamba yeye naye alishuka mpaka pande zilizo chini za nchi? Naye aliyeshuka ndiye yeye aliyepaa juu sana kupita mbingu zote, ili avijaze vitu vyote. Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo; ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu.”
Waefeso 4:7-14198
Je, Ukristo ambao sasa unawakilishwa kanisani kwenu
ungesababisha Kitabu cha Matendo ya Mitume? Hili swali ni kali na
lenye uzito. Kuwa wazi ni kutoa jibu moja tu: Hapana! Basi, nini
tofauti kati ya Ukristo uliosababisha Kitabu cha Matendo ya Mitume,
na huu mbovu wa ajabu kabisa unaopatikana na kuonekana karibu
katika kila kanisa?
Katika kanisa la kwanza, walifuata mfano wa Yesu katika
kuwajenga watu muhimu, lakini siku hizi sisi tunahesabu watu katika
makundi. Tuna kawaida ya kupima mafanikio kwa kutazama ukubwa
na wingi wa watu. Tena, mfano tunaofuata sisi sana sana ni wa
kusafisha wenye dhambi ili waishi maisha safi. Wao walifuata mfano
wa kuwafanya watakatifu kuwa wanafunzi kwa ajili ya kuifikia na
kuigusa dunia, ingawa pamoja na hayo, maisha masafi
hayakupungua. Tunachofanya sisi ni kama kuwaweka walio-okoka
katika sanduku la kuwahifadhi liitwalo “usalama wa milele” badala
ya kila mwamini kuwekeza maisha yake yote katika watu wengine
waliokolewa ili kutengeneza wazalishaji wenye maono ya dunia
nzima, wenye kuigusa dunia nzima na kuifikia, ambao nao
watawazaa wengine wenye maono ya dunia nzima, wenye kuigusa
dunia nzima na kuifikia, ambao nao watawazaa wengine …..
Sasa – tofauti kati ya Ukristo wa mwaka wa 4BK na Ukristo
wa mwaka wa 2008BK? Je, Yesu amebadilika? Hapana.
Tunamwabudu na kumtumikia Yesu yule yule waliyemjua wao. Je, 199
Roho Mtakatifu ni mwingine? Hapana. Roho Mtakatifu
tunayehusiana siku za leo ni yule yule “aliyekuja” kikamilifu kabisa
katika uwezo wa ukombozi Siku ile ya Pentekoste. Je, Biblia ni
tofauti? Hapa, uwe makini kidogo, kwa sababu jibu sahihi ni
“ndiyo”. Wao hawakuwa na Biblia kamili. Walikuwa ndiyo
wanamalizia kuandika Biblia kupitia shughuli zilizoandikwa katika
Kitabu cha Matendo. Kwa hiyo, kama kuna faida ya kuwa na Biblia
kamili iko kwetu, si kwao. Je, kulikuwa na tofauti katika teknolojia au
mafanikio kwa habari ya usafiri? Aah! Swali gani tena hilo? Sisi tuko
vizuri katika kila hali – wao hawakuwa vizuri katika kila hali. Mungu
alikuwa ameandaa amani ya dunia nzima kupitia nguvu za kijeshi za
Kirumi na akatayarisha mtandao wa barabara zilizofika kila mahali
ambao ulijengwa na Warumi, lakini hayo yalikuwa machache sana
ukilinganisha na manufaa ya leo tuliyo nayo sisi. Wao hawakuwa na
simu, barua pepe, vipindi vya televisheni ili kuchangisha fedha – wao
walikuwa na “mwambie mtu”. Hawakuwa na vyombo lakini
walikuwa na KWELI MUHIMU! Lakini, na sisi pia tunazo! Sasa,
kilichowawezesha wao kuigusa dunia nzima iliyojulikana wakati ule
katika kipindi kifupi sana, wakati leo hii kiasi cha mbili kwa tano cha
binadamu wote hakijasikia kabisa Injili, na kiasi kingine cha mbili
kwa tano cha dunia nzima kimepata Injili kwa hali ya chini sana, ni
nini? Halafu, idadi ya moja kwa tano iliyobakia ina uwezo mkubwa
sana katika kila hali kuliko waliokuwa nao Kanisa la kwanza. Lakini,
kwa faida gani? Je, tofauti kati yetu na wao ni ya kujitolea? Kuna 200
ambao watatoa hoja ndefu na kwa sauti kubwa kabisa kwamba hiyo
ndiyo tofauti, lakini, si hiyo tu. Katika kanisa la kwanza, watu
waliokuwa wamejitoa si wengi kuliko Mkristo wa kawaida wa siku
hizi ambaye anahudhuria ibada kwa uaminifu mara tatu kwa juma
pamoja na siku maalum – lakini bado hana ushawishi wa aina yoyote
juu ya watu kama bilioni 2 nukta tatu ambao hawajasikia habari za
Kristo siku hizi. Ukristo wa Kitabu cha Matendo usingeweza
kuvumilia takwimu za jinsi hii, lakini kanisa la leo lina uwezo wa
kuendelea katika shughuli zake zote za kawaida bila hata ya kujali
hali ya kushindwa kwake iliyo kuu.
Sasa – nini tofauti basi kati ya Ukristo wa Iskanda, Rufo,
Trofena na Andoniko wa karne ya kwanza, na ule wa Jo, Suzie,
Samweli na Edwadi wa karne yetu? Mimi nasema hivi: Tofauti ni ya
mkakati peke yake. Wenzetu walitenda kazi kwa kufuata mkakati
tofauti na ule tunaotumia sisi!
Angalia mfano huu, ambao ni picha ya desturi ya taasisi ya
makanisa ya leo. Fikiri kuhusu basi lenye kusafiri kwenda mahali,
ambalo linabeba watu njiani. Kanisa ndiyo mfano wa hilo basi.
Mchungaji ni kama dereva wa hilo basi. Dereva (yaani mchungaji)
anawakaribisha abiria wapande kwenye basi (na yawezekana
wakakaribishwa na abiria wenzao pia). Wanaketi na husimama ili
kushughulikia maswala muhimu tu. Dereva (yaani mchungaji) anatoa
maelezo kuhusu vivutio vinavyoonekana njiani wakati akiwaendesha
abiria wasiofanya chochote, wenye kutazama (na pengine waliolala 201
usingizi) kuelekea mahali walipokubaliana kwenda. Abiria wa
kawaida anavumilia hiyo safari, lakini kamwe hatafuti abiria
mwingine, na mara nyingi hashuhudii kuhusu jinsi anavyofurahia
basi lile, na kampuni ya hilo basi, na njia linakopitia, wala safari
linalofanya. Yaani kwa kifupi ni kwamba, mafanikio ya safari
yenyewe yako katika uwezo na ubora wa hilo basi, na utendaji wa
dereva wake. Hii ni tofauti kubwa sana sana na ule Ukristo wa
Bwana Yesu pamoja na wanafunzi wa kwanza. Ukristo wa Kitabu
cha Matendo ulikuwa ni kitu cha watu (ktk Matendo 1:8; 8:1 na 4);
haukuwa kitu cha mhubiri au kitu cha taasisi fulani.
Eneo la dunia liitwalo North Pole lina kiwango kikubwa sana
cha barafu. Wanasayansi wanatuambia kwamba barafu hiyo ikitokea
kuyeyuka basi sehemu kubwa ya dunia itajaa maji. Wakristo wengine
wanaweza kuitwa “mali ya Mungu iliyoganda”. Kama hao wote
watayeyuka mbele za Mungu na kupata joto la kutambua maono
Yake, makusudi Yake, malengo Yake, na mkakati Wake, “dunia yote
ingejaa maarifa ya Bwana, kama maji yajazavyo bahari.”
Mfano wa Mungu aliotoa ili Kanisa Lake liufuate unaelezwa
kwa uwazi kabisa katika Waefeso 4:7-14. Mada ya jumla ya fungu
hili ni karama za kiroho, lakini karama zinazotajwa hapa si zile za
aina mbalimbali ambazo kwa kawaida hutajwa katika Agano Jipya.
Orodha ya karama katika Warumi 12, 1Wakorinto 12 na 14 na 1Petro
4 ziko tofauti. Hizo ni matoleo kutoka mbinguni zinazowekwa katika
waamini na Roho Mtakatifu. Karama hizi tunazotaja hapa sasa ni 202
viongozi wenye vipawa ambao Roho Mtakatifu huwatoa kwa Kanisa
Lake kwa ajili ya makusudi maalum ya jumla katika kanisa, na kwa
ajili ya kufanikisha au kutimiza malengo maalum.
Hebu nitoe muhtasari utakaotuwezesha kuona kwa ujumla
fungu zima (yaani, Waefeso 4:7-14). Fungu hili linatuonyesha mtoaji
wa hizo karama, karama zenyewe (yaani, watu waliopewa vipawa),
na malengo ya karama hizo kutolewa.
MTOAJI KARAMA
I. Mtoaji Anatajwa – mstari 8-10
Kweli kuu tatu zinatolewa kuhusu Yesu:
A. Alishuka, ms. 9, 10.
B. Alipaa, ms. 8, 9, 10.
C. Yuko juu ya vyote, ms. 10b.
II. Karama Zenyewe (Watu) Zinaonyeshwa – mstari 11
Viongozi wenye vipawa wanne (au watano) wanatajwa:
A. “Mitume”
B. “Manabii”
C. “Wainjilisti”
D. “Wachungaji waalimu”
III. Malengo Ya Kutolewa Karama Yanatajwa – mstari 12, 13
A. Ili kupata viungo kwa ajili ya Mwili, ms. 12b.
B. Ili kuwezesha viungo katika Mwili, ms. 12a.
C. Ili kutumia viungo kupitia Mwili na zaidi, ms. 12-16.203
Katika kile kipengele cha “Mtoaji Karama” ambacho ni mojawapo
ya maandiko maarufu sana yenye kufafanua fundisho la Nafsi ya
Kristo katika Agano Jipya, ona sheria moja inayojitokeza. Ingawa
njia ya Shetani kwenda chini ni kupanda, njia ya Mungu kwenda juu
ni kushuka. “Yeye ajiinuaye mwenyewe (kama Shetani) atashushwa,
lakini yeye ajinyenyekezaye mwenyewe (kama Yesu) atainuliwa
(kama Yesu).”
Hii orodha ya watu waliopewa vipawa (ktk mstari wa 11)
inaweza kusababisha mafundisho na mawazo yasiyo na kikomo.
Kwa mfano: Swali kuhusu zile karama mbili za kwanza ni hili: Je,
zipo katika kanisa la siku hizi? “Mtume” kama nafasi rasmi iliweza
kuwepo katika kanisa la kwanza tu kwa sababu sifa zake maalum
zilizotakiwa (yaani, kumwona Yesu na kuwa pamoja Naye)
hazipatikani kwa mwingine yeyote baada ya karne ya kwanza. Nafasi
ya “nabii” inaonekana kuwa ya Agano la Kale tu. Pia, Waefeso 2:20
inasema kuhusu mitume na manabii kuwa “msingi” wa kanisa. Siku
hizi, jengo hilo limekwisha panda sana! Kweli msingi ni wa muhimu,
lakini, ukiwa katika nafasi yake tu, si katika kuta.
Ila, kufikiri hivyo sana kusikokuwa na faida kunaweza
kutufanya tukose hoja kuu. Kuna kanuni ambayo imetajwa mara kwa
mara, kwamba, “Mfuasi ni kama kiongozi wake”. Mfuasi atakuwa
kama kiongozi wake (maneno ya Yesu Mwenyewe katika Luka
6:40). Basi, wakati Yesu alipotoa kwa Kanisa Lake viongozi wanne 204
wenye karama pekee na tofauti, bila shaka anatuambia waziwazi kile
anachokusudia Kanisa Lake liwe.
MTUME
Neno “mtume” maana yake ni “mtu anayetumwa kuondoka”.
Basi, anakusudia iwe hivyo kwa kanisa Lake lote (!!!), kwamba liwe
ushirika wenye kwenda na kutuma waendao. Watu wengi hujiepusha
na jukumu la kwenda kwa kubakia kwenye wazo la kutuma, lakini hii
haiwezi kupata kibali katika Agano Jipya. Vipi kanisa la siku hizi?
Limejaa watu wanaokuja – watu ambao Ukristo wao unaelezwa kwa
uaminifu wao katika kuja na kutumika. Neno “mtume” kama lilivyo
hutuambia ni kwa nini Yesu aliwachagua hao (ktk Waefeso 1:3;
Matendo 1:3). Lile neno “aliwachagua” linamaanisha kwamba Yesu
aliwachagua “kwa ajili Yake Mwenyewe”, wala si kwa ajili ya kukua
kwao, afya yao, mali yao, furaha yao, au hata utoshelevu wao.
Mkazo usiofaa umesababisha kuundwa “Ukristo unaofurahisha
wateja”, ambao ni kusoma vibaya Agano Jipya. Agano Jipya
linamwonyesha Mungu kuwa ndiye mteja, na sisi ndiyo
watoshelezaji wa matakwa Yake. Ndugu aitwaye Jim Elliott aliomba
kwa kumaanisha kabisa, hivi: “Ee Moto wa Mungu! Nifanye mimi
kuwa ndiyo mafuta!” Je, Yesu alituchagua sisi kwa ajili gani? Ili
twende mahali Yeye anapotaka sisi twende – “kuondoka” – siyo
“kukaa” – ili tuwe, ili tuseme, na kufanya chochote Yeye anachotaka.
Basi, lengo pekee lililo sahihi kwa ajili ya kila Mkristo lazima 205
lihusishe mkakati wa kuifikia miisho ya dunia. Tunawezaje kuona
vikomo kwenye mkakati kama huo katika Kitabu cha Matendo?
Walijaribu kuweka mipaka kwamba kiwe kitu cha mahali pamoja,
kitu chao cha ndani, lakini Mungu alituma mateso yaliyowatawanya
kama mbegu (ambalo ni neno linalotumiwa katika Matendo 8:1; 8:4
na katika 1Petro 1:1) kwenda nje na mbali mbali kabisa katika
udongo mchanganyiko wa Dola ya Kirumi. Ee Mkristo – jihadhari,
kwa sababu mateso makubwa sana ya siku zijazo yanakaribia kulijia
kanisa la siku hizi. Uislamu wenye msimamo mkali na ukorofi
umeanza kuivamia dunia, na kilichoko njiani ni kanisa maskini na
dhaifu la Yesu Kristo. Maendeleo ya kiteknolojia na makufuru ya
sayansi na ubinadamu vimezua watesaji kila mahali. Kwa hiyo, siku
za Ukristo kukaa katika ngome yake salama kwa utulivu,
zimekwisha. Utawanyiko mwingine wa Wakristo uko njiani. Na
Mungu ndiye Mpanda Mbegu! Ni hivi: Ingawa sisi ni wagumu kwa
hiari yetu kusikia kuhusu jukumu letu la kwenda, Mungu
anamaanisha kabisa kwamba twende!
NABII
Neno “nabii” maana yake “mtangazaji” (pamoja na kwamba
ni “mtabiri” wa ukweli). Nabii ni msema kweli, si msema kitu cha
kupoza moyo. Nabii alikuwa “mtangazaji” au “mshuhuda”. Basi,
Yesu alipotoa kwa Kanisa Lake manabii wenye vipawa,
anachotuonyesha ni kwamba alikusudia kanisa Lake kuwa ushirika 206
wa watu wasiokoma, walio waaminifu siku zote, walio jasiri siku
zote, wenye kuzungumza siku zote. “Waliokombolewa na Bwana na
waseme hivyo.” Hii hutimiza makusudi kadhaa ya Mungu.
Humkomaza msemaji, kwa sababu mtu yeyote atafuatilia ukiri
aliotamka, hata kama ni ukiri gani. Humtukuza Mungu, kwa sababu
anakaa ndani ya sifa na shuhuda za watu Wake. Na, hufikisha Injili
kwa kila asikiaye. Mkristo asipime joto au mapigo ya moyo ya dunia
kabla hajanena – la sivyo, hatasema kabisa! Kwanza kabisa, sisi
husema kwa Mungu, na kuhusu Mungu, na kwa ajili ya Mungu. Basi,
hatupaswi kunyamaza kimya kamwe. “Ninaamini, hivyo nimesema.”
Manabii, wahubiri, waalimu na viongozi wa kanisa lazima waseme
kwa ukamilifu, kwa uwazi na kwa ujasiri – na waamini wote vivyo
hivyo!
MWINJILISTI
Neno “mwinjilisti” maana yake ni “msema mema,” yaani,
mtu ambaye “anamsema vema” Yesu kwa watu, na watu kwa Yesu.
Injili inakiri habari mbaya sana kuhusu Shetani na mbinu zake
mbaya, mwanadamu na hali yake ya dhambi na utendaji wake,
Mungu na itikio Lake takatifu kinyume cha dhambi, na kuzimu kama
makazi ya mwisho kabisa ya mwenye dhambi anayejiona na
kujifikiria mwenyewe. Lakini cha kusikitisha ni kwamba, kanisa
limetangaza habari mbaya mara nyingi zaidi na kwa nguvu sana
kuliko ambavyo limetangaza Habari Njema. Ujumbe mkuu na wenye 207
nguvu zaidi katika Maandiko unaitwa “Injili” – euaggelion – “Habari
Njema”. Hakuna mtu aliyepokea habari njema kweli kweli mpaka
ajisikie vizuri kuhusu Mungu, kuhusu Yesu, kuhusu Roho Mtakatifu,
kuhusu yeye mwenyewe, kuhusu wokovu wake, kuhusu hali yake ya
sasa na ya baadaye, na kuhusu matokeo ya mwisho kabisa ya mambo
yote. Mungu analikusudia Kanisa Lake kuwa tukufu na lenye ushindi
katika kueleza kwake habari njema.
MCHUNGAJI MWALIMU
Halafu neno “mchungaji mwalimu” linatoa kweli ya mwisho
kuhusu kile ambacho Mungu anatazamia kwa Kanisa Lake. Neno
“mchungaji” maana yake “mtunza mifugo” na linaeleza anakusudia
watu Wake waongoze. Ili kuongoza, Mkristo lazima ajue kwa uwazi
na kwa uhakika yeye ni nani, ana nini, anakwenda wapi, jinsi ya
kufika aendako, kusudi lake leo na kila siku ni nini, na jinsi ya
kufanikisha kazi yake. Mtu yeyote anayejua mambo hayo kwa uwazi
na uhakika anaweza kumwongoza mtu mwingine. Neno “mwalimu”
linaonyesha kwamba Yesu anakusudia Kanisa Lake kuwa ushirika
wenye kueleza ukweli, kufundisha na kulisha. Na hii ndiyo kazi ya
kila aaminiye. “Kwa njia zote” (ktk 1Wakor. 9:22) – neno la papo
kwa papo, ushuhuda ulioandaliwa, mafundisho rasmi na mahubiri,
ugawaji wa maandiko, vitabu, magazeti, barua ( na Mungu yuko juu
sana kwa uandishi wa barua), kanda za sauti na video, redio na
televisheni, kuonana uso kwa uso au kwa umbali – lengo la Mkristo 208
linatakiwa kuwa ni kushawishi, kugeuza, “kuwavuta baadhi” kwa
shughuli zozote anazofanya.
Hizo ndizo karama zikionyeshwa; basi, kazi, wajibu na jinsi
ya kanisa kuwa wazi na dhahiri kabisa.
MALENGO YA KUTOA KARAMA HIZI
KUPATA VIUNGO
Tunapaswa “kuujenga” Mwili wa Kristo kwa kutumia hawa
watu wenye vipawa na wafuasi wao watakaopatikana. Hivyo,
kiwango kipya cha kupata watu lazima kitumiwe na kanisa. Masharti
yote ya kuwapata watu lazima yatumike mara moja na kanisa. Kila
kitu katika “mkataba” wa Kikristo lazima kitamkwe na kukubalika
tangu mwanzo kabisa – wakati wa kukata shauri – yaani, kujikana,
kubeba msalaba (hayo ni masharti ya “pale pale mlangoni”, si
nyongeza kwa kuwa mtu amekomaa), kuishi nje kama mtu alivyo
ndani, kujisomea Biblia kwa ajili ya kujijenga na kwa ajili ya
kutumika, kuabudu na maombi ya mapambano, na kadhalika. Na
hayo hayawezi kufanyika sehemu ya maisha kwa mafunzo ya saa
moja kwa juma, au masaa mawili, au matatu kwa juma.
Je, katika uinjilisti wetu, ni wapi penye kiwango na utendaji
kwa ajili ya kumkataa kijana tajiri yule aliyekuwa anapenda mali
yake? Kiwango hiki cha hali ya juu sana kilitumiwa na Yesu katika
kumwondoa mtafutaji muungwana, wa dhati aliyekuwa anataka 209
kujua cha kufanya (hebu jisomee Mathayo 19:16-26 kwa makini
sana). Tena ujue kwamba swali la huyu kijana – “Nifanye nini kizuri,
ili niweze kuwa na uzima wa milele?” – Yesu aliulizwa mara mbili.
Mwanasheria (“mtaalamu” wa Torati ya Musa) aliliuliza katika Luka
10:25 katika mantiki tofauti kabisa. Na hakuna wakati wowote
ambapo Yesu alitoa jibu ambalo wengi wetu tungelihesabu kuwa ni
“mpango wa wokovu unaofuata utaratibu”. Yeye aliweka “kipimo
cha katikati” pale mwanzoni kabisa – penye mlango wa kuingilia!
Ni hivi: Neno “amini” ambalo linatumika kirahisi sana na sisi
kueleza njia ya wokovu, ni muungano wa maneno mawili ambayo
maana yake ni “kwa uzima”, au “kuishi kwa”. Unavyotenda ndivyo
unavyoamini! Mengine yote ni mazungumzo tu ya kawaida kabisa,
“si lolote si chochote”, maneno mazuri tu ambayo yamejaa “kelele na
ghadhabu, yasiyo na maana yoyote ile”. Huu ni Ukristo wenye
kujadili lakini hautendi. Ni Ukristo wenye “kujitukuza” bila ya
kwenda, wenye “kufurahia” lakini usiotii, wenye kujitakasa
wenyewe kwa ajili ya usafi lakini kamwe haujimimini wala kujitoa
kwa ajili ya ushindi. Hujitokeza ili kujaza kanisa (Jumapili asubuhi)
lakini haujimwagi ili kujaza na kugusa dunia mpaka pande za
mwisho kabisa za nchi … Lazima tutaje waziwazi kama sharti la
kuingia kwamba, Kuzaliwa Upya (kitu kinachofanywa na Mungu tu)
lazima kufuatwe na Maisha Mapya) ambayo pia yanatendwa na
kuwezeshwa na Mungu pia). Basi, tunahitaji kuwapata wanachama
wapya katika kanisa la siku hizi, wanachama wenye kuelewa 210
mafunuo kamili ya Yesu. Kwa kawaida si inatakiwa mwenye kutia
sahihi karatasi yoyote asome na kuelewa mkataba mzima kabla ya
“kutia sahihi”?
KUWEZESHA VIUNGO
Halafu, kila mshirika anapaswa “kuwezeshwa” kwa ajili ya
kazi yake binafsi ya “huduma” (ktk 4:12a). Sentensi hii ina neno
moja pana sana na lenye mafafanuzi makubwa katika Agano Jipya.
Ni neno “kuwakamilisha” ila, maana kamili ya neno hilo si rahisi
kuipata. Kuna tafsiri moja ya Biblia inayosema kwamba hao watu
wenye karama au vipawa wametolewa kwa kanisa ili
“kuwawezesha” washirika. Nyingine inasema “kuwapa vitu vyote
wanavyohitaji”. Kitu kimoja ni hakika kwa tafsiri yoyote ile:
Wakristo wote – bila kukosa, bila kupendelewa, na bila kutengwa –
wanapaswa kuwezeshwa hivyo, kupewa kila wanachohitaji. Mfumo
wa taasisi yenye kutazama ndani ya kanisa la siku hizi ni kwamba,
mchungaji ndiye mchezaji pekee kwenye jukwaa, na “walei –
washirika” wanaachiwa kazi za hapa na pale kama wasaidizi wa
jukwaani, wahusika na taa na walinzi. Mfumo huu lazima
ubadilishwe mpaka ifikie mahali ambapo mchungaji atakuwa ndiye
“mwezeshaji” wa watu, na watu wawe ndiyo watumishi. Kusudi la
wazi kabisa lililotajwa hapa la kuwawezesha washirika ni ili kila
Mkristo aingie katika “kazi ya huduma”. Ni hivi: Siku ile ulipo-
okoka uliitwa kuingia katika huduma! Kanisa lingekuwa jeshi 211
kubwa, lenye ushindi sana, lenye kupenya, lenye kusonga mbele,
lenye kuimba, na lenye kelele za shangwe kama wangejua hilo! Dada
Eugenia Price alisema hivi: “Dhambi kuu kuliko zote ya kanisa la
siku hizi ni kwamba, limefanikiwa kumfuga na kumdhoofisha yule
Simba wa Yuda.” Tumezuia vitisho vyote, hatari yote na uwezekano
wa kufia Ukristo visitokee katika Ukristo. Basi, michezo au tamasha
za muziki ndiyo zenye kuweza kutoa changamoto, msisimko na hali
ya kujali kuliko kusonga mbele kwa Kanisa la Yesu Kristo.
Neno “kuwezesha” au “kukamilisha” ni neno kubwa.
Ukijifunza neno hilo katika Agano Jipya utashtuka na kushangaa.
Kwa Kiyunani, neno hilo ni “katartismon”. Kipande chake ni neno
“artis” na maana yake ni “fundi stadi”. Kumbe kazi ya kila
mchungaji mwalimu ni kumfanya kila mwamini aliye chini ya uwezo
wake kuwa fundi stadi katika kulitumia, kulielewa, kuliishia,
kutawaliwa nalo, kuhudumia, n.k. kwa kutumia Neno la Mungu. Kazi
hii ilimla Yesu sana, kama mkakati kwa ajili ya Watu Kumi na Mbili
katika mafunzo kazini ya muda wote, kwa karibu, katika kipindi cha
miaka mitatu tu. Hapo tena – nini maana ya neno “kama Kristo”?
Tukiondolea mbali Mkakati Wake, na kuondoa Agizo Lake Kuu, na
kupuuza Mfano aliotoa, kwa nini sisi tulalamike kuhusu hali ya
kanisa na ya dunia? Ni kwamba tunaishi na tulichotengeneza
wenyewe. Kumbuka kwamba Utambuzi hupelekea Taratibu, na
Taratibu kupelekea Matokeo. Kama kilichotokana na mfumo mzima
212
ni kibaya, (na hakuna awezaye kukana kwamba sivyo), basi
Utaratibu wetu lazima una makosa.
Angalia tena lile neno “kuwezesha”. Utafiti unadhihirisha
kwamba lilikuwa neno la kawaida kabisa lililotumika katika dunia ya
Kiyunani ya karne ya kwanza. Na lilikuwa na maana nyingi
mbalimbali.
(1) Kutuliza mji uliokuwa umetengana.
(2) Kutibu kiungo kilichokuwa kimeteguka.
(3) Kuendeleza viungo fulani vya mwili kwa mazoezi.
(4) Kumrejeza mtu kwenye hali yake ya kawaida.
(5) Kuwapatanisha marafiki ambao walikuwa wametengana.
(6) Kumwezesha mtu au kitu kwa ukamilifu kabisa, kwa ajili
ya kusudi fulani.
(7) Kuweka mambo kwa utaratibu, au kupanga vitu vizuri.
(8) Kuelekeza kitu kwenye mkono wa maendeleo.
Kabla ya kuachana na orodha hiyo kwa haraka, hebu tazama
kila neno na ulifafanue kulingana na maelezo ya kazi ya viongozi wa
Mwili wa Kristo. Halafu, tafsiri kila neno katika maisha na
mwenendo wa wafuasi wote, kwa sababu wanafunzi watakuwa kama
mwalimu wao (ktk Luka 6:40).
KUVITUMIA VIUNGO
Basi, zile nafasi za kawaida zilizozoeleka za “wachungaji” na
“washirika – walei” lazima zibadilishwe. “Walei” wanakuwa ndiyo 213
askari walioko mstari wa mbele (wenye silaha kamili, wenye
ufahamu kamili, na wenye utendaji kamili), na “wachungaji” na
mkutano wa kanisa lote, wapo kwa ajili ya kuwaunga mkono. Ndugu
Charles Colson alikuwa sahihi kabisa alipoandika hivi: “Kila mmoja
wetu kama waamini lazima tujione kama watumishi wa Injili. Sisi si
wahudhuriaji wa kanisa tu, walaji wa mambo ya kiroho.” Mkristo
ambaye hana huduma binafsi yenye kupelekea mguso wa dunia yote
kwa nguvu ni mfano potofu wa Mkristo. Lengo ni kumtumia Mkristo
kila wakati katika kuishi maisha ya Kikristo na kupenya na kugusa
dunia nzima kwa mkakati wa Yesu. Halafu tena, kujengwa kwa
wanafunzi wenye kujizidisha, wenye maono ya dunia na wenye
uwezo wa kuigusa dunia ndicho Kipau Mbele Kikubwa (kama katika
Agizo Kuu). Ili kanisa liweze kurekebisha mawazo potofu yake,
lazima lianze uandikishaji tofauti, liwe na uwezeshaji tofauti na
mpya, na liwe na utumaji mpya na wa tofauti. Mungu na afungue
macho ya mioyo yetu na kuijaza nuru (ktk Waefeso 1:17-19)!
Kumbe basi – kusudi la sasa katika ushirika wa waaminio ni
“kuwawezesha watakatifu”. Hii inahitaji mafunzo ya hali ya juu, ya
kikamilifu kabisa, kwa kila mwamini. Hatimaye, kusudi kuu ni
“kulijenga kanisa” – kihali, kwa kulijenga kwa ndani, na kwa idadi,
kwa kulipanua kutoka nje. Nje kwa kiasi gani? Kila kanisa lazima
lione kwamba wajibu wake ni mpaka “mwisho wa nchi”. Kwa hiyo,
lazima liongeze uwezo wake – watendaji, mapato, mipango, mikakati
na utendaji wake – hadi mwisho kabisa wa nchi. Kumbuka kwamba 214
mwangaza unaong’aa mbali zaidi hung’aa kwa nguvu zaidi
nyumbani.
MIFANO YA USHIRIKA WA WAAMINIO WA MAHALI
PAMOJA
Tumalizie mafunzo haya kwa kuonyesha michoro miwili ya
mifano ya ushirika wa waaminio walioko mahali pamoja. Mfano
mmoja ni ule wa kawaida katika makanisa yetu mengi, na ule
mwingine ndiyo ufaao, tunaosema juu yake katika maelezo yetu.
Kusanyiko/Waamini
Viongozi
Watendakazi
Mchungaji
Katika mfano wa kwanza, washirika ni watu wengi – waamini
wasiotosheka – wasikilizaji, watazamaji, waunga mkono. Wakati hali
ya kujitoa inaposhuka na kuwa nzito kidogo, yule aliyejitoa zaidi
Dunia
215
katika ushirika anafanywa kiongozi. Kadiri huko kujitoa kunavyozidi
kuwa kwa hali ya juu (sana sana katika kanisa la mahali pamoja peke
yake), wafanya kazi wa kanisani wanaanza kupatikana. Halafu, yule
aliyejitoa kuliko wengine wote kanisani ndiye anaonekana kufaa
kuwa mchungaji! Bila shaka upotofu wa huu mfano ni dhahiri. Basi,
uzito wa mwili wote na majukumu yake yote unatulia juu ya
mchungaji. Mchungaji anabeba majukumu yasiyohesabika katika
mwili au kundi hilo, na wakati mwingine ndiye anayeona au
kushughulikia majukumu ya nje ya mwili au kundi. Mipango
maalum inawashawishi wale washirika waliojitolea kabisa
kujihusisha na kazi zile “maalum” za kuleta watu kwa Yesu, kufanya
utume, huduma za kawaida katika jamii na kadhalika. Lakini mzigo
wa utendaji, mafanikio na hatimaye kuifikia dunia nzima
humwangukia mchungaji zaidi.
Matokeo ya mfano huu ni matatu:
(1) Uongozi uliovunjika moyo kabisa. Zaidi ya wachungaji
elfu moja kila mwaka wanaacha huduma. Wengine zaidi ya mia tatu
kila mwezi wanaondolewa kwa nguvu kwenye madhabahu. Je hilo
linatutia aibu? Kama hapana, linapaswa kututia aibu! Na, linaweza
kurekebishwa kabisa.
(2) Wanachama wa kanisa ambao kwa sehemu kubwa ni “wa
kimwili” (yaani, wenye ubinafsi, wanaotaka kujitosheleza wenyewe).
Katika mfano huu, washirika hawajui kazi nyingine isipokuwa
kuhudhuria kanisa, kuwa waaminifu kwa taasisi yao (au dhehebu 216
lao) na kutathmini mapato. Je, ni ajabu kwamba wanazidi kuwa
kimwili?
(3) Dunia inayobaki bila kushuhudiwa. Sehemu kubwa ya
binadamu duniani aidha hawajasikia kuhusu Jina la Yesu kabisa, au
wamesikia “kidogo” tu. Ukristo wa Kitabu cha Matendo
ulishughulika na hali iliyokuwa mbaya zaidi, wakaibadilisha kabisa
kwa muda mfupi sana. Hali iliyoko inaweza kubadilishwa vivyo hivyo
hata leo, lakini si kwa kuendeleza mfano huo mbovu.
Mfano ule wa pili ni kama kinyume kabisa cha ule wa
kwanza.
Mchungaji
Watendakazi
Viongozi
Kusanyiko/Waamini
Dunia
217
Katika huu, mchungaji ndiye mwenye kuwajibika kwanza kabisa.
Nafasi yake ni ya kuwajibika, si ya heshima! Wajibu wa nafasi kama
hiyo ni mkubwa zaidi sana kuliko heshima au sifa yoyote inayoweza
kupatikana kutokana nayo. Ukweli ni kwamba hiyo inaweza kuwa
kama sheria: nafasi yoyote katika mwili inayopelekea kuendelea
kukua kwa sifa ya kiongozi wake (kimafanikio, na kadhalika) itiliwe
mashaka kabisa katika Ukristo! Mwili hutafuta kuonekana,
kutambuliwa, kutuzwa – na hilo ni eneo moja tu la udhaifu ambalo
mwili umerithi! Mwili hauwezi kuaminiwa na aina ya pongezi na sifa
zinazotolewa kwa viongozi “maarufu” katika michezo au siasa.
Wajibu wa kwanza wa mchungaji katika mfano huu ni
kuwawezesha na kuwaambukiza watenda kazi pamoja naye maono
ya kufanya watu kuwa wanafunzi, ili kuifikia dunia nzima. Maono
haya ya kawaida na ya wote yanapaswa kuamua huduma ya kila
mtenda kazi kanisani, na kupanga malengo yake kwa ajili ya
wanafunzi ambao yeye anawajenga. Mchungaji pia anawajibika
katika kuwawezesha na kuwaambukiza viongozi maono yake, lakini
sasa ana fursa pekee. Viongozi kwa wakati huu “wanawezeshwa
mara mbili” kwa kupewa maono ya kawaida na mkakati – kutoka
kwa mchungaji moja kwa moja, na kutoka kwa watumishi wa kanisa.
Basi, mchungaji, watumishi wa kanisa na viongozi watakuwa na
umoja katika kuwawezesha watakatifu wote kwa ajili ya kazi yao ya
huduma. Wakati matarajio hayo yanapofanyiwa kazi, “mafuta ya
ziada” yataondoka, na “vijana tajiri” watahama. Lakini, macho, 218
midomo, masikio, mikono, magoti na miguu ya mwili wenyewe
vitakuwa vinaona, vinasema, vinasikia, vinatenda, vinapiga magoti
na kutembea katika muungano kamili kabisa – siku zote kuelekea nje
hadi mwisho wa dunia. Ushirika wa mahali pamoja ndiyo mahali pa
msingi pa huduma (ingawa huduma nyingi hufanyikia hapo). Ndicho
kituo chenye nguvu kwa ajili ya huduma. Watu pale wanaonyesha na
kumshirikisha Kristo popote walipo, na kwa makusudi kabisa
wanajenga mikakati kwa ajili ya wao binafsi kupenya hadi mwisho
wa nchi.
Nini matokeo wakati mfano wa pili unapokuwa halisi? Hapa
tena, matokeo ni matatu.
(1) Viongozi walio na msisimko na waliotosheka walioko
duniani.
(2) Waamini “wa kiroho” wanaozidi kuongezeka (ambao
Kristo ni wa muhimu kwao, wanamheshimu Mungu,
wamejazwa Roho na ni watakatifu wanaogusa dunia).
(3) Dunia kuzidi kushuhudiwa.
Mikakati kwa ajili ya kufanyia kazi mfano huu wa pili imo
katika Amri na Mfano wa Yesu, na Amri na Mfano wa Waefeso sura
ya 4. Lakini, lazima tuwe waangalifu sana. Mwisho wa siku,
makusudi ya Mungu yanategemea kutimizwa kwa makusudi Yake ya
sasa. Je, wewe binafsi unafundishwa kwa utendaji wa karibu kabisa
wa kazi za kuifikia dunia? Je, wewe unawajenga wengine – kwa
karibu, kwa kuwapa kazi za kuifikia dunia?219
Sura Ya 9Maneno Yake Ya Mwisho, Wosia Wake
“Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”
Waefeso 4:7-14
George Orwell, mwandishi maarufu wa kitabu kiitwacho
1984 na Animal Farm, aliwahi kuandika hivi: “Sasa tumezama
kufikia kiwango ambacho wajibu wa kwanza wa watu wenye akili
timamu ni kurudiwa kusemwa mambo ambayo ni ya kawaida.”
Katika kanisa la siku hizi, kilicho kawaida ni kitu chenye kuleta
mapinduzi na mabadiliko sana. Hakuna kitu kinachopuuzwa sana
kama lile agizo “dhahiri” au la kawaida la Yesu. Tunapotaja kitu
hicho kwa mara nyingine na kufanyia kazi, kanisa linatikiswa hadi
misingi yake.
Agizo la Yesu lilitajwa katika kila Injili nne na katika Kitabu
cha Matendo ya Mitume. Kitabu cha Matendo ya Mitume ni
maendelezo ya habari zinazosimuliwa katika Injili. Kitabu chenyewe
kimeandikwa kwa mtiririko mzuri na kinafuata utaratibu wa
kijiografia ambao unaonekana kwa urahisi sana, utaratibu
220
unaopatikana katika Matendo 1:8: “Yerusalemu … Uyahudi …
Samaria … mwisho wa nchi.” Kitabu cha Matendo kinaweza
kugawanywa katika sehemu tatu kubwa (sura ya 1 hadi 7; ya 8 hadi
12; ya 13 hadi 28), huku sehemu ya kwanza ikionyesha jinsi kanisa
la kwanza lilivyoendeleza huko Yerusalemu ile kazi ambayo Yesu
aliianzisha (ktk Matendo 1:1). Sehemu ya pili inahusiana na
maendeleo ya Injili katika Uyahudi na Samaria, na sehemu ya
mwisho inahusu kuendelezwa kwa Injili hadi “mwisho wa nchi”.
Mstari wa nane katika Matendo moja unayo maneno ya
mwisho ambayo Yesu Kristo aliyazungumza kwa wanafunzi Wake,
muda mfupi tu kabla hajapaa kwenda mbinguni. Injili ya Luka na ya
Yohana inadhihirisha kwamba mara ya kwanza Yesu alipokutana na
wanafunzi Wake baada ya kufufuka, aliwaagiza kuwa mashahidi
katika mataifa yote. Alirudia agizo hilo mara moja tena jioni hiyo
hiyo. Akalirudia tena baadaye pale mlimani Galilaya, kama
ilivyoandikwa katika Mathayo 28. Na sasa, yuko nje ya mji wa
Yerusalemu, siku arobaini baadaye, muda mfupi tu kabla ya kupaa
Kwake. Hivyo basi, agizo hilo linapaswa kuwa dhahiri kabisa kwetu
sisi. Lakini, swali moja litafunua kwamba hatujajali sana agizo hilo.
Je, unaigusa dunia nzima kwa kiasi gani katika mambo unayofanya,
unayofikiri, unayosema, au unayotayarisha? Ni hivi: Yesu alishikwa
sana na jambo la kuhusisha dunia nzima, lakini mtulivu sana kuhusu
mbinu au njia. Sisi tumefanya kinyume! Tunakwenda kongamano
221
baada ya kongamano kujifunza kuhusu mbinu, lakini tunaepuka kule
kuhusika kwenyewe, ambako ndiyo muhimu.
Amri ya Yesu ilidai matendo. Agizo Kuu halikutolewa ili
watu wajifunze tu. Ni mpango wa utendaji. Katika somo hili,
tutalitazama tena, tukitumia Matendo 1:8 kama msingi wetu. Lakini
swali kubwa ni hili: Je, utakuwa tayari kupatikana katika kila hatua
kwa ajili ya kutimizwa kwa Agizo Kuu?
MKAKATI KWA AJILI YA KUENDELEZA INJILI
Kwanza, tunaona katika tamko hili Mkakati kwa ajili ya Injili
kuendelea kuenea. Mkakati upo katika neno “shahidi”. Hili ni neno
muungano lenye mambo mengi ndani yake. Neno la asili kwa
Kiyunani ni “martutia”, ambalo bila shaka si neno kimya. Neno hilo
limezaa neno la Kiingereza “martyr” yaani, “shahidi mfia imani”.
Kumbe basi, mtindo wa maisha unaotokana na neno hili ni kuishi
maisha yenye kujihatarisha katika utendaji. Kuwa “shahidi mfia dini”
ni mradi wa kuishi au kufa.
Dada mmoja aitwaye Virginia Owens aliandika hivi: “Kuwa
Mkristo ni nafasi ya ajabu sana – si ya salama. Mtu hamfuati Kristo
akiwa anatembea katikati ya barabara iendayo kwenye kuheshimika.”
Mwanatheolojia mmoja, aliyekuwa ameanza kuelewa “nafasi ya
kupita kiasi” ya Ukristo aliandika hivi: “Hebu tukusanye Agano
Jipya zote zilizopo, tuzipeleke kwenye kiwanja mahali au juu ya
mlima, halafu, wote tukiwa tumepiga magoti, mmoja wetu aseme na 222
Mungu hivi: ‘Kichukue Kitabu hiki tena. Sisi binadamu, kama
tulivyo sasa, hatufai kushughulika na kitu kama hiki.
Kinatuhuzunisha tu.’ Wazo langu ni kwamba, sawa na wakazi wa
Gerasi, tumwombe Kristo ‘aondoke kwetu’.” Hao waandishi wawili
wameanza kuelewa dai la Yesu kwamba tuwe “mashahidi wafia
imani”.
Neno hilo “martus” linatokea zaidi ya mara 30 katika Kitabu
cha Matendo, na ni miongoni mwa maneno makuu kitabuni.
Hutujulisha kwamba tunapaswa kusahau mawazo yoyote ya mtindo
wa maisha unaotilia maanani “usalama kwanza”. Tazama mifano
ifuatayo.
Mkulima alikwenda kuwinda na mbwa wake porini, maili
nyingi mbali na nyumbani. Akagundua kwamba amesahau kopo la
kumlishia mbwa wake chakula. Aliweka bunduki yake chini na
kumwambia mbwa wake akae hapo mpaka arudi. Alipokuwa
amekwenda, moto wa pori ukatokea, na yule mbwa akafa. Baadaye,
mkulima yule aliukuta mwili wa mbwa wake – ulioungua kabisa –
kando ya bunduki yake. Kwa huzuni sana alisema, “Siku zote ilibidi
niwe mwangalifu katika ninachomwambia mbwa wangu afanye, kwa
sababu angefanya hivyo hivyo.” NDUGU WAKRISTO, Yesu Kristo
anataka na sisi tujali sana kuhusu kufanya anachosema mpaka
tusahau kuhusu moto wa porini unaowaka.
223
Profesa mmoja wa sayansi ya viumbe alitaja kanuni moja ya
sayansi siku moja darasani. Alisema hivi: “Kujihami ndiyo sheria ya
kwanza katika nguvu za asili.” Mwanafunzi mmoja Mkristo
akamwambia baada ya darasa akiwa anatabasamu, “Inashangaza
sana kuona tofauti kati ya nguvu za asili na neema. Sheria ya kwanza
ya nguvu za asili ni kujihami, lakini katika neema, sheria ya kwanza
ni kujitoa.” SAWA KABISA!
Jionee hali ya kujitoa mwenyewe ya Kalvari iliyo kiini cha
neema ya Mungu, halafu ukumbuke kwamba kanuni ya kwanza ya
uanafunzi wa Kikristo inapatikana katika maneno haya ya Yesu:
“Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike
msalaba wake, kisha aje anifuate.” Kujikana mimi mwenyewe maana
yake ni kujiambia yale maneno aliyosema Petro kwa habari ya Yesu
wakati alipomkana: “Sijawahi kumsikia kabisa mtu huyo. Simjui mtu
huyo mimi!”
Ndugu mmoja aitwaye Bruce Morgan aliandika hivi: “Tatizo
la Wakristo ni kwamba hakuna mtu anayetaka kuwaua tena.” Dada
Eugenia Price alikariri wazo hilo aliposema hivi: “Dhambi kubwa
ya kanisa ni kwamba LIMEMFUGA Yesu Kristo na kumfanya
mpole.”
224
Aina ya ushahidi ambao unatajwa katika Matendo 1:8 ni wa
asili dhahiri kabisa kiasi kwamba unatuingiza katika matatizo kila
wakati (lakini pia unaleta furaha ya daima ndani yetu, na huambatana
na miujiza ya daima pia).
Mkutano wa mamia ya viongozi wa kidini kutoka Marekani
yote ulifanyika, na ajenda kuu ilikuwa hii: “Tunawezaje kutumiwa ili
kulirejeza taifa hili kwa Mungu?” Kila mhudhuriaji alipewa nafasi
jioni moja kutoa jibu lake kwa kifupi. Kiongozi mmoja – Mmarekani
Mweusi – aliinuka na kusema hivi: “Wapendwa. Wakristo wa
Marekani hawatapata tena uwezo wa kuigusa jamii hii mpaka
wapoteze hofu yao ya kifo.” Akakaa chini. Watu wengi
waliohudhuria mkutano huo walisikika wakisema kwamba pengine
jibu bora kuliko yote katika mkutano huo lilikuwa la huyo ndugu.
Miaka mingi iliyopita, mhubiri maarufu mishenari aliyeitwa
Robert Wilder alitembelea Chuo kidogo kiitwacho Hope huko Jimbo
la Michigan ili kuhubiri katika ibada ya wanafunzi kuhusu utume wa
dunia nzima. Akaweka ramani kubwa sana ya India mbele ya kanisa,
na akaweka kimulimuli mbele ya hiyo ramani. Katika mahubiri yake
alitamka kwamba kila mara kimulimuli kilipowaka, mtu mmoja wa
India alikuwa anakufa pasipo kusikia habari za Kristo. Siku hiyo,
Kristo na maono Yake ya dunia nzima aligusa moyo wa mwanafunzi
mmoja aliyekuwa karibu kumaliza hapo chuoni aliyeitwa Samuel 225
Zwemer. Maono hayo yalipowaka moyoni mwake, alimwomba
Mungu amweke mahali pagumu kabisa duniani.
Muda si muda, alianzisha makazi katika Kisiwa cha Bahrain
huko Ghuba ya Uajemi, katikati kabisa ya jamii ya dunia ya
Kiislamu. Kisiwa hiki ni maarufu. Zwemer akaanza kuchapisha na
kugawa vipeperushi vya Injili, japo hakuwa amepata kibali cha
serikali ya Kiislamu ya mahali pale. Katika kipindi cha juma moja,
binti wawili wa Zwemer – mmoja wa miaka minne na mwingine wa
miaka saba – walikufa kwa sababu ya magonjwa na joto kali la
mahali pale. Samuel Zwemer akaomba wakuu wa Bahrain ruhusa ya
kuzika miili ya binti zake, lakini alinyimwa kibali kwa madai kwamba
walikuwa Wakristo, na miili yao ingenajisi ardhi ya pale. Zwemer
akakata rufani na akapata ruhusa – kwa sharti kwamba yeye
mwenyewe achimbe makaburi. Alifanya hivyo, na baada ya maziko,
aliweka jiwe la kumbukumbu lililosema, “Amestahili Mwanakondoo
aliyechinjwa, kupokea utajiri.” Huo ndiyo mtindo wa kishujaa wa
kutoa kila kitu hadi kufa, ambao Yesu alitaka watu waishi.
Shirika moja la zamani kidogo lililohusika na kutuma
wamishenari lilituma wamishenari sabini kwenda nchi ya Kamerun,
ambayo ni “kiungo” muhimu kati ya Afrika magharibi na Afrika
kusini na kusini kati. [Waislamu kwa sasa wanajitahidi sana kujaribu
kuipata Kamerun.] Katika hao sabini, sitini na nane walifia huko.
Wastani wa uhai wao baada ya kufika huko ilikuwa miaka miwili na 226
nusu! Inasemekana wengi wao walisafiri pamoja na majeneza yao,
wakijua kwamba uwezekano wa kurudi ulikuwa mdogo! Yesu alitaka
mtindo huo wa maisha wa kishujaa, wa kutoa kila kitu hadi kufa!
Familia moja ya kimishenari ilikwenda Uchina kuhubiri Injili
huko, chini ya “shirika la utume wa imani”. Walikwenda kama
waalimu wa shule za kawaida. Waliporudi, walirudi kama
wamishenari wa kawaida likizoni – wakiwa na boksi lenye picha na
vitu mbalimbali vya kuonyesha. Walipomaliza kuonyesha maonyesho
yao na kutoa maelezo yao, kipindi cha maswali na majibu
kikatolewa. Mshirika mmoja wa kanisa alisimama na kuuliza hivi:
“Mlipokuwa huko hamkuogopa kwamba mnaweza kufia huko?” Jibu
la baba wa familia ile ya wamishenari lilitoka, hivi: “Hapana,
maana KABLA HATUJAENDA TULIKWISHA KUFA.” Hii ndiyo
maana ya neno “martus” au “shahidi mfia imani”.
Mchungaji Charles Crowe wa KiMethodisti alikuwa
anaendesha gari lake mjini Chicago, kwenye mzunguko wa
barabara, kama alivyokuwa anafanya mara nyingi tu. Jengo la
kanisa lake lilikuwa maarufu sana hapo mjini kuwa ndiyo lenye
kilele kirefu katika makanisa yote ya Marekani Kaskazini. Juu yake
ulikuwepo msalaba mkubwa sana. Siku hii asubuhi, wakati
Mchungaji Crowe anapita mbele ya jengo hilo, aliona kundi kubwa
tu la watu wamesimama kando ya barabara mbele ya jengo, na wote 227
walikuwa wanatazama juu. Akainama kwa makini katika gari lake na
kutazama juu aone walikuwa wanatazama nini. Akaingia kwenye
eneo la kuegesha magari, akaharakisha kuweka gari lake katika
sehemu yake ya kuweka gari, kisha akaharakisha kwenda mbele ya
kanisa na kujiunga na waliokuwa wanatazama juu.
Juu ya msalaba palikuwa na mpaka rangi mwenye ndoo ya
rangi. Alikuwa amefungiwa msalabani, na kwa utaratibu alikuwa
anapaka rangi ule msalaba, akielekea chini. Msalaba wenyewe
ulikuwa unayumba kwa utaratibu kila alipopaka rangi. Watu
walikuwa wanatazama kazi yake hatari. Baada ya muda, Charles
Crowe aliondoka kwenye lile kundi la watu na akaanza kuelekea
ofisini kwake hapo kanisani. Mara Roho Mtakatifu akamwambia,
“Mwanangu! Umepita hapo mara nyingi, na hapajawahi kuwepo
mtu yeyote njiani akitazama juu kwenye ule msalaba. Nini
kilichofanya tofauti leo? Ni hiki: LEO, MSALABA ULIKUWA NA
MTU JUU YAKE! Siku zote, dunia itasimama kuona wakati mtu
mkweli atakapokuwa msalabani.”
Leo hii kanisa linaambiwa na dunia maneno yale ambayo
Tomaso alisema kuhusu Yesu katika mashaka yake na kutokujua:
“Nisipoona alama za misumari mikononi Mwake, na kutia kidole
changu katika alama hizo … sitaamini.” Wanatafuta kujitoa bila
maonyesho kwa Mkristo ambaye Kristo ndiye kiini cha maisha yake,
la sivyo, hawataamini.228
Pengine ni vizuri tutulie kidogo hapa na kujikumbusha
kuhusu mbadala pekee wa mtindo huu wa maisha ya Kikristo. Yesu
alisema hivi: “Yeyote atakayeokoa (linda, tetea, hifadhi) maisha yake
atayapoteza, na yeyote atakayepoteza maisha yake kwa ajili yangu
atayapata.” Sehemu ya kwanza inafafanua ule mtindo wa maisha
wenye kufikiri usalama kwanza, mimi ndiyo wa muhimu, nijiokoe
mwenyewe kwa gharama yoyote ile. Sehemu ya pili inafafanua ule
mtindo mwingine wa maisha – wa kuwekeza, wa kutojijali, wenye
kujali wengine, wa kuwajenga wengine, uliojawa na Kristo – ambao
ndiyo mtindo wa maisha wa Mkristo.
Wasafiri wawili walinaswa na tufani ya barafu walipokuwa
wanasafiri sehemu ya kaskazini. Walipokuwa wanakabiliana na hiyo
dhoruba, walimkuta mtu amegandia kwenye barafu, wakadhani
amekufa. Mmoja akasema, “Nina matatizo ya kutosha kujisaidia
mwenyewe. Nasonga mbele.” Yule mwingine akasema, “Siwezi
kumpita binadamu mwenzangu katika hali hii wakati bado ana pumzi
hata kidogo tu ya uhai.” Akainama na kuanza kumpa joto yule mtu
kwa kumsugua kwa bidii sana. Hatimaye yule mtu akafungua macho
yake, akarejelea uhai wake, akapata nguvu na kutembea pamoja na
yule mtu aliyemsaidia. Walipoendelea na safari, walikuta nini?
Walimkuta yule mtu aliyeamua kujishughulikia mwenyewe na
kujitafutia usalama wake akiwa amekufa kwa baridi katika barafu.
229
Yule Msamaria Mwema alihifadhi maisha yake mwenyewe
kwa juhudi zilizohitajika kumwokoa yule mtu mwingine. Msuguano
ule ulisisimua damu yake na kumfanya hai. Sheria haibadiliki wala
haishindwi: “Yeyote (Mkristo au kanisa) atakayeokoa maisha yake
atayapoteza; na yeyote atakayepoteza maisha yake kwa ajili yangu
atayapata.”
Mwandishi maarufu aitwaye C.S. Lewis alifanikiwa kunasa
uzuri na msisimko wa maisha ya Mkristo katika kitabu chake cha
“Chronicles of Narnia” kwa kumfanya mtu mmoja katika sehemu
iitwayo The Last Battle (Vita ya Mwisho) aseme hivi: “Afadhali nife
nikiwa napigania taifa la Narnia kuliko kuzeeka na kuwa mjinga
nyumbani, na pengine nishindwe kutembea mpaka nitumie kiti na
mwishowe nije kufa tu.” Rafiki zangu. Tutakufa kwa namna moja au
nyingine. Kujitoa kwa Kikristo ni kwamba, “Kristo atukuzwe katika
mwili wangu, katika uhai wangu au kwa kifo changu.”
Kwa maneno mengine, Yesu anasema hivi: “Ee mwamini!
Wewe ndiye ushahidi wangu, vitambulisho vyangu, hoja zangu,
wasifu wangu, mwenezaji wangu, matangazo yangu.” Na Msalaba
ndiyo kiini cha uwakilishi wowote wa Kristo. Mtu mmoja aitwaye
George Bernard Shaw aliuliza hivi: “Je, ni lazima Kristo asulubiwe
katika kila kizazi kwa kuwa tu dunia haina ubunifu?” Jibu kwa swali
lako, mheshimiwa, ni, “Ndiyo” nasi tunapaswa kuwa wale
230
wanakondoo wasiojijali wenyewe. “Ninyi ndiyo mashahidi wangu
wafia imani.” Huo ndiyo mkakati wa Injili kusonga mbele.
CHANZO CHA USHUHUDA WA INJILI
Pili, tunaiona asili au chanzo cha ushuhuda wa Injili. Asili
yake inaonekana katika matukio matatu ya neno “nanyi”. “[Nanyi]
Mtapokea nguvu baada ya Roho Mtakatifu kuwashukia [ninyi], nanyi
mtakuwa mashahidi wangu.” Maneno “nanyi” na “juu yenu” yako
katika wingi. Agizo limetolewa kwa Mwili wote wa Kristo na
linatimizwa na kila kiungo cha huo Mwili. Wewe Mkristo mpendwa,
unahusika kabisa – kikamilifu kabisa – katika mkakati wa Yesu.
Wewe ni asili au chanzo cha ushuhuda wa Injili.
Ona kwamba neno “nanyi” linazidi kutajwa kwa Roho
Mtakatifu mara tatu katika mstari huu. Hii si kwamba inapunguza
nafasi na jukumu Lake; bali huongeza wajibu wako. Hao “nanyi” ni
akina nani? Si malaika, si watu wasiokuwa wa kawaida, si watu
maalum. Andiko linadhihirisha “nanyi” hao katika mistari
inayofuata. Matendo 1:2 inawataja kabisa kwamba, ni wale “mitume
ambao Yesu alikuwa amewachagua”.
Ni hivi wapendwa: Mitume wote walikuwa wanaume. Hii
haipunguzi nafasi ya wanawake, inaongeza tu jukumu la wanaume.
Roho Mtakatifu bila shaka alitazamia matatizo ya historia ya Kikristo
– kwamba ingekuwa rahisi kabisa kwa wanaume kukimbia wajibu
wao na kuwaachia wanawake. Kwa hiyo , siku hizi katika makanisa 231
yetu tuna vikundi vya umisheni vya wanawake. Mungu ashukuriwe
kwa ajili ya wanawake wanaojali na wanaomcha Mungu, lakini hili
ni jukumu la wanaume kimsingi! Ni hivi: Ukifanikiwa kumpata
mwanamume, kiongozi aliyewekwa na Mungu katika idara ya msingi
katika jamii, unakuwa na nafasi bora sana ya kumpata kila mtu
mwingine katika eneo lake la utawala. Lakini ukimpata mmoja wa
watu wake kwanza (mke, watoto) unaweza kushindwa kumpata huyo
kiongozi au wengine katika eneo lake.
Zamani kidogo Ijumaa Kuu moja usiku, jengo la kanisa
liitwalo People’s Church huko mjini St. Paul jimbo la Minnesota,
Marekani, lilishika moto. Ilikuwa baada ya usiku wa manane na
idara ya zimamoto ilizuiliwa na barafu katika juhudi zake za kuuzima
moto. Walipokuja kufanikiwa, jengo likawa limeungulia chini.
Asubuhi iliyofuata, washirika wa kanisa hilo na wanamji ule
walianza kukusanyika pembeni mwa lile jengo lililokuwa bado
linafuka moshi. Jengo lenyewe lilikuwa aina fulani ya makumbusho
ya picha za kidini pamoja na jengo la kanisa, hivyo lilikuwa maarufu
sana kwa utalii.
Nyuma kabisa ya madhabahu ilikuwepo picha ya kuigiza ya
“Kristo Anayesihi” – sanamu kubwa ya marumaru iliyokuwa na
urefu wa futi nane, iliyoandaliwa na mchoraji maarufu Mdenish
aliyeitwa Thorsvalden. [ZIADA: Mishenari maarufu wa India
aitwaye Stanley Jones alikuwa anatembelea mji wa Copenhagen, 232
Denmark miaka mingi kabla. Mwongoza watalii akawa amewapeleka
kwenye Kanisa moja la Kikatoliki huko Copenhagen, mahali ambapo
sanamu ya hiyo picha tunayosema, ilikuwepo. Sanamu yenyewe
inamwonyesha Yesu akiwa amesimama, uso umetazama chini,
mikono imefunguliwa kwa dunia. Imetokana na Mathayo 11:28,
kwamba, “Njooni kwangu ninyi nyote mnaosumbuka na wenye
kulemewa na mizigo mizito, nami nitawapa pumziko.”
Sasa, walipokuwa wanaondoka hapo, yule mwongoza watalii
aliuliza, “Je, kuna yeyote aliyefanikiwa kuuona uso wa Bwana Yesu”
Jones akajibu, “Tungewezaje kuuona? Umeinamia chini.” Yule
mwongoza watalii akajibu kwa sauti ya chini ya unyenyekevu,
“Ndiyo hivyo Mzee. Ukitaka kuuona uso wa Bwana, lazima kwanza
upige magoti miguuni Pake!” MWISHO WA ZIADA]
Sasa, lile jengo la kanisa lilipoungua, ile sanamu ilianguka
na sakafu na kutumbukia shimoni katika vyumba vya chini ya ardhi.
Siku ya pili yake, masaa ya asubuhi, baadhi ya watu wa kanisa
walipata ruhusa ya kushuka na kuingia katika magofu ya kanisa ili
kuona kama kuna vitu vya thamani vilivyopona moto. Wakaikuta ile
sanamu, imepata alama za moto na majivu na moshi kidogo, lakini
haikuwa imeharibika isipokuwa kipande kikubwa kilichobomoka
kutoka sehemu ya sanamu kusimamia. Wakaiacha ipoe, halafu
mchana ule wakaibeba taratibu kutoka huko chini na kuiweka
pembeni ya barabara. Wakapanga watu sita kusimama kuilinda ili
wapitaji na watazamaji wasiiharibu, halafu wakarudi tena chini 233
kutafuta vitu vingine.Waliporudi tena baada ya muda, kundi la watu
lililokuwepo halikuwa linatazama tena lile jengo lililoharibiwa.
Badala yake, walikuwa wanatafuta nafasi katika huo mviringo, wote
wakiwa wanajaribu kuitazama hiyo sanamu maarufu.
Hebu niufanye huo mfano kuwa wa kiroho, ili kutilia mkazo
jambo moja. Ni hivi: Yesu alikuwa katika hilo kanisa kwa muda
mrefu tu, lakini alikuwa “amefungiwa minyororo madhabahuni,” na
watu wa mtaani walikuwa hawajapata kumwona. Ni wakati tu kanisa
liliposhika moto na kuungua (!) na baadhi ya watu wa kanisani (!)
kumchukua na kumweka pembeni ya barabara (!) ndipo “watu wa
nje” walipoweza kumwona kwa mara ya kwanza kabisa! Wewe,
mwamini wa Kikristo, ndiye asili au chanzo cha ushuhuda wa Injili.
MADA YA USHUHUDA WA INJILI
Halafu, mstari wetu unatuonyesha mada ya ushuhuda wa
Injili. Yesu alisema hivi, “Ninyi mtakuwa mashahidi WANGU.”
Ushahidi wetu haupaswi kuelekea kwenye kanisa, au dhehebu, au
itikadi, au fundisho, au ukiri fulani, au taratibu fulani. Unapaswa
kumwelekea Kristo. Ni fursa yetu nzuri tu kumweleza Yeye kama
alivyojieleza Mwenyewe katika Neno Lake, kwamba ni Mwokozi
mwenye Kukomboa (ktk Matendo 1:3), kwamba ni Bwana Mfufuka
(1:3 tena), na kwamba ni Mfalme Anayerudi (ktk 1:11). Mada hiyo
haina mwisho! Tena, ni kweli kuu yenye kuvuta usikivu kabisa.234
Picha kwenye ukuta wa jumba la maonyesho ya sanaa huko
Ujerumani ni mfano mzuri wa sehemu hii ya kazi yetu. Picha hiyo
inamwonyesha Martin Luther, Mjerumani maarufu aliyeleta
Matengenezo ya Kanisa, akiwa anahubiri katika mimbari ya kanisa
la Kijerumani. Mkononi mwake ameshika Biblia, na kwa mkono
mwingine amenyoosha kidole, na mdomo wake uko wazi kana
kwamba anatangaza kitu. Anaihubiri Injili. Unaweza kumwona
mhubiri na wasikilizaji wake katika picha hiyo. Lakini ukitazama
kwa makini sana, utaona kitu cha kushangaza. Hakuna msikilizaji
wake hata mmoja anayemtazama mhubiri ambaye ni Martin Luther!
Ukifuata mahali wanapotazama, unaona kitu cha kufurahisha sana.
Pembeni mwa lile jengo, kuna umbo dhahiri japo liko mbali la Yesu
Mwana wa Mungu – na kila jicho hapo linamtazama Yeye.
Wanamsikiliza Luther, lakini wanamtazama Yesu!
Hayo ndiyo matokeo tunayotaka ya kumshuhudia Kristo
kwetu. Tunamtangaza Yeye, Naye anajitambulisha mwenyewe
kupitia ushuhuda wetu. Basi, usikivu wa kila “msikilizaji” hatimaye
unamwelekea Yeye.
UPANA WA USHUHUDA WA INJILI
Mstari huo pia unadhihirisha upana wa ushuhuda wa Injili.
Ona kwa makini sana maneno yake ya kumalizia – “Nanyi mtakuwa
mashahidi Wangu katika Yerusalemu NA Uyahudi wote, NA 235
Samaria, NA mpaka sehemu za mwisho za dunia.” Sasa tuchambue
kidogo.
Watu wa karibu ni kazi yetu – “Yerusalemu”;
Watu jirani ni kazi yetu – “Uyahudi”;
Watu waliopuuzwa ni kazi yetu – “Samaria”;
(Samaria ni mfano wa watu unaowachukia kabisa, unaowabagua); na
Watu wanaofuata ni kazi yetu – “mpaka mwisho wa nchi”.
“Yerusalemu” huwakilisha hali yako ya karibu. “Uyahudi na
Samaria” huwakilisha hali yako ya jirani, na “mwisho wa nchi”
huwakilisha maeneo ya kimataifa yanayokuzunguka. “Yerusalemu”
huwakilisha ushuhuda wa mjini kwetu, “Uyahudi na Samaria”
huwakilisha ushuhuda wa nchi yetu, na “mpaka mwisho wa nchi”
huwakilisha ushuhuda wa dunia yetu.
Halafu, ona kwa makini sana kwamba si swala la “aidha au”
kuhusu watu hawa. Ni swala la “pamoja na”. Yesu Kristo
anatutazamia tuishughulikie dunia nzima – kweli kabisa, na kwa
dhati kabisa! Kwa njia gani? Kwa kujifunza na kufuata ule mkakati
wa kufanya watu kuwa wanafunzi ambao kwao tunaona makundi ya
watu kwa njia ya mtu mmoja, na kumjenga huyo mtu awaguse hao
wengi – ambao ndiyo mkakati aliotumia Yesu na wale Kumi na
Mbili aliokuwa nao.
Kitabu cha Matendo ya Mitume ni kimoja katika vitabu
vichache sana vya Biblia vyenye kujipanga vizuri. Sura ya kwanza
hadi ya saba huonyesha ushahidi wa wanafunzi wa kwanza huko 236
Yerusalemu. Sura ya nane hadi kumi na mbili katika Uyahudi na
Samaria, na halafu sura ya 13 hadi 28, “mpaka mwisho wa nchi”.
Kipimo cha kweli cha nguvu na uwezo wa Mwili wa Kristo
katika mahali pamoja ni hiki: Je, ushawishi wake unafika mbali kiasi
gani? Mungu kwa hakika kabisa analitazamia kanisa la mahali
kushugulikia dunia nzima! Maana, Yesu aliweza kufanya hivyo na
watu kumi na mbili, na alifanikiwa kabla ya kuwepo kwa siku,
televisheni, na teknolojia aina zote. Yeye alikuwa na waeleza watu
tu! Lakini, aligusa dunia nzima ya siku Zake kupitia kundi Lake hilo
dogo, la watu wa hivi hivi.
Siku hizi tunafikiri kwamba lazima tuwapate watu wa jamii
zetu nyumbani kabla ya kuanza kushughulika na wale tulioagizwa
kuwafikia duniani. Lakini, mpango huo ni kinyume. “Nuru ing’aayo
mbali zaidi inang’aa kwa nguvu sana karibu na nyumbani.” Kila
kanisa linapaswa kuwa na mpango daima jinsi linavyoweza kufikisha
Injili katika sehemu nyingi duniani kwa haraka kiasi iwezekanavyo,
na lengo lake linapaswa kuwa kuwajenga wanafunzi ambao wana
maono ya dunia, watakaoigusa dunia nzima hadi mwisho wake, hadi
ukamilifu wa dahari. Mungu alisema hivi: “Niombeni, nami nitawapa
ninyi mataifa kuwa urithi wenu, na sehemu za mbali za nchi kuwa
mali yenu” (ktk Zaburi 2:8, TLR). Sasa, kwa nini hatujapata watu wa
mataifa kuwa urithi wetu, na sehemu za mwisho za dunia kuwa mali
yetu? Sababu pekee pengine ni kwamba, hatuombi! Ni dhahiri kabisa
kwamba kanisa kwa ujumla halina kwenye moyo wake kile kilicho 237
moyoni mwa Mungu. Vipi kuhusu kanisa lenu? Kuhusu kanisa lako?
Vipi wewe mwenyewe?
Ona pia kwamba, mstari wenyewe unasema, “katika
Yerusalemu na Uyahudi yote, na Samaria, mpaka mwisho wa nchi”.
Si swala la “aidha au” bali ni “pamoja na”. Tunapaswa kuwa
tunashuhudia mahali pote hapo kwa wakati mmoja, na pote
tunapaswa kupahifadhi na kupabeba moyoni. Kivipi? Kwa kujenga
maono kwa ajili ya dunia nzima, halafu kwa kuwajenga watu wa
kutekeleza maono hayo. Upana wa eneo letu la kazi ni dunia nzima.
SIRI YA USHUHUDA WA INJILI
Hatimaye, maneno ya Yesu yanadhihirisha siri ya ushuhuda
wa Injili. Alisema, “Mtapokea nguvu, baada ya Roho Mtakatifu
kuwajilia juu yenu.” Njia nzuri ya kumfikiria Roho Mtakatifu ni
kwamba, Yeye ni Yesu pasipo mwili. Roho Mtakatifu ni mbadala wa
Kristo hapa duniani, akifanya aliyokuwa anafanya, na kuendeleza
kazi Yake.
Mvulana mmoja alimwuliza mama yake, “Mama! Mungu
analetaje mvua?” Baadaye akawa kama amekumbuka, na kujibu
swali lake mwenyewe. “Usijali, ninajua tayari. Yeye anamwambia
Roho Mtakatifu afanye hivyo. Roho Mtakatifu ndiye anayefanya kazi
yote!” Roho Mtakatifu ndiye Nafsi Mtendaji katika Uungu. Siku hizi,
Yeye ndiye hufanya kazi yote!
238
Halafu fikiria kuhusu neno “nguvu”. Neno la Kiyunani
linalotumiwa hapa ni “dunamis”, ambalo limezaa neno la Kiingereza
“dynamite” au baruti. Lakini, kiunganisho hicho kinaleta tatizo la
msingi kwetu. Kwa kawaida baruti ni kitu chenye mlipuko mkubwa.
Basi, tuna kawaida ya kutazamia nguvu za Mungu kulipuka kwa hali
ya juu sana kama kiwakilishi cha ahadi ya Yesu. Tatizo ni la aina
mbili: kwanza, hakuna hali ya kulipuka katika Injili; na pili,
Wayunani walikuwa hawana baruti. Baruti iligunduliwa na Alfred
Nobel mwaka wa 1866, ambaye ndiye mwanzilishi wa Tuzo za
Nobel. Basi, kulitafsiri neno hilo kwa msingi wa neno letu la
Kiingereza la baruti kunaweza kutupotosha kidogo, kuwafanya
Wakristo watazamie “mlipuko” badala ya kumruhusu Roho
Mtakatifu kutengeneza na kuzaa ubora na tabia ya utulivu na utendaji
iliyokuwepo katika maisha na huduma ya Yesu.
Nguvu ya Matendo 1:8 ni
Nguvu ya kubadilisha tabia,
Nguvu ya kuangaza,
Nguvu kwa ajili ya mawasiliano,
Nguvu kwa ajili ya utendaji wa dhati, endelevu.
Ni nguvu ya kushuhudia, pamoja na kuwa nguvu katika
kushuhudia. Kuna mtu anayefafanua nguvu ya tabia kuwa ni
“onyesho lenye nguvu la haiba ya mtu” na hiyo ndiyo tafsiri nzuri ya
nguvu za Mungu. Ni onyesho lenye nguvu la haiba ya Mungu – jinsi 239
Mungu alivyo. Linaweza kuwa kitu mlipuko, lakini mara nyingi
huonekana kama ushawishi ulioko ndani kabisa katika tabia ya mtu,
na kusadiki kunakomgusa yeye na wengine wanaomzunguka. Kazi
ambazo Yesu aliahidi kwamba zingefanywa na Roho Mtakatifu ---
Kusadikisha (ktk Yohana 16:7-11);
Kuangaza (ktk Yohana 16:13-16),
Mawasiliano (ktk Yohana 15:26), na
Kuifikia au kuigusa dunia (ktk Matendo 1:8)
-- zaidi sana katika eneo la ushawishi wenye nguvu kuliko
eneo la maonyesho au madhihirisho “mlipuko”.
Ona kwamba nguvu hii “inapokelewa”. “Mtapokea nguvu”.
Haipatikani kama malipo ya kazi, inapokelewa. Haifikiwi kwa juhudi
zozote, inapatikana. Haihitajiki kipawa kikubwa sana ili kupokea
chochote. Watu matajiri na maskini kabisa wanaweza kupokea kitu
chochote kitolewacho. Bila shaka mtu anakipokea tu. Mungu anataka
sana kukupa wewe nguvu ya Roho Mtakatifu – lakini kwa masharti
Yake na kwa ajili ya makusudi Yake tu. Yeye amekuagiza ujazwe na
Roho Mtakatifu, nafsi pekee ambayo ni nguvu za Mungu.
Tunasoma hivi katika 1Yohana 5:14 – “Huu ndiyo ujasiri
tulio nao katika Yeye, kwamba, tukiomba chochote kulingana na
mapenzi Yake, anatusikia.”
Kwa kuwa ametuagiza tujae Roho Mtakatifu, tuna uhakika
kwamba ni mapenzi Yake. Basi, tukae katika hali ya kutazamia
daima na kumwomba daima atujaze kwa Roho Wake, na tumpokee 240
tu katika utimilifu Wake. Ndipo kwa ujasiri kabisa tutaweza kujua
kwamba Nafsi ya Roho Mtakatifu siku zote “anasafiri nasi” popote
tuendapo, mradi tu tunaishi kutimiza Agizo Kuu la Bwana wetu.
241
Sura Ya 10Mbweha Tally Ho!
Maana Ya Jina La Kitabu
Najisikia vizuri kupata nafasi ya kujibu swali hili, kwa sababu
kazi yote ya Yesu kwetu inapatikana katika jibu nitakalotoa. Hebu
kwanza nifafanue mfano uliozaa jina la hiki kitabu.
Mbwa wanapokuwa katika kundi, wanakimbia pamoja na
kufanya moja au mengi katika haya manne yafuatayo:
1. Watalala.
2. Watajihami kwa manufaa ya usalama wao.
3. Kama hawatishiwi, watakaribisha wanachama
wapya katika kundi lao.
4. Watapigana wao kwa wao.
Lakini, kuna kitu cha kutilia maanani, nacho ni hiki: HAYO YOTE
WATAFANYA MPAKA MBWEHA APITE!
Sasa – “kanisa” ni nini? Ingawa tafsiri nitakayotoa hapa ni
dhaifu, isiyopendeza na nyepesi sana, kanisa ni Wakristo katika
vikundi, wanaokimbia pamoja. Theolojia imejaribu kueleza kanisa
kwa njia ya hali ya juu zaidi kidogo inaposema kwamba “ni
kusanyiko au ushirika wa waamini waliozaliwa mara ya pili na
242
walioitwa, walio katika Yesu Kristo, walioungana pamoja kwa ajili
ya malengo ya kiroho yanayofanana.” Tafsiri yangu mimi ni nyepesi
tu na rahisi kabisa na yenye kueleweka, lakini inaeleza hicho hicho.
Lakini, kosa kubwa la maana au tafsiri zote hizo si mfano bali ni
utendaji halisi. Makanisa mengi hayakimbii. Kweli “yanakimbizwa”
(utasikia watu wakisema, “analiendesha kanisa lake”, au, “hao ndiyo
wenye kuliendesha kanisa hili”. Au, “kanisa hili linaendeshwaje?”),
lakini hayakimbii! Yanaendeshwa kama mitambo inavyoendeshwa,
au kama biashara inavyoendeshwa, lakini yenyewe hayakimbii
kufukuzia lengo ambalo yamepewa.
Haya – turudi kwenye tafsiri yetu. Kanisa ni Wakristo katika
kikundi, wanaokimbia pamoja. Wakristo wanapokimbia pamoja
katika vikundi (na ndivyo ilivyo), watafanya moja au mengi katika
haya manne yafuatayo.
1. Watalala. Andiko linalofaa kabisa kusomewa makanisa
mengi kabisa ni hili: “Amkeni enyi mlalao, mfufuke kutoka kwa
wafu.” Miaka mingi iliyopita, mishenari aitwaye John Halsy
aliandika maneno haya, mazito kabisa:
Kama ningekuwa mwandishi mwenye kutamani kujulikana
kwa kuandika kitabu kifupi kuliko vyote, ningewaendea baadhi ya
washirika walio katika makanisa yetu maarufu ya mjini, yaliyotulia,
niwaombe kibali chao kuandika maelezo ya kile wanachomfanyia
Kristo na kufanya kwa ajili ya dunia. Historia hiyo ingekuwa fupi
kweli kweli! Pengine herufi moja au mbili tu zingetosha kueleza kila 243
kitu kinachofanywa na wengi wao kwa ajili ya Bwana aliyewanunua,
na kwa ajili ya dunia inayoangamia! Kuna andiko ambalo linaweza
kuwapa starehe sana baadhi ya watu wanaoitwa Wakristo. Ni hili –
‘Sisi tulioamini tunaingia katika pumziko.’ Lakini kumbuka kwamba
hilo ni pumziko la mtenda kazi baada ya kazi, si pumziko la mvuvi
kutokana na kazi. Ila, nina andiko lingine la kuweka pamoja na hili –
‘Ole wao waliopumzika huko Sayuni!’ Ndiyo! Ole, kwa sababu hiyo
starehe ni mwizi anayeiba hali ya kujisikia hatia, ikiwaibia waamini
na makanisa nafasi yao ya kushiriki pamoja na Kristo katika
shughuli iletayo raha kuliko zote duniani.
Ufufuo au kupaza sauti kuamsha watu si vitu vibaya katika
kufafanua hitaji la Wakristo wengi na makanisa mengi. Ninasema
hivyo kwa aibu kubwa sana, kwa sababu mimi mwenyewe binafsi
nimelala katika sauti za baragumu nyingi sana kutoka mbinguni,
zilizotolewa ili kuniita niende mstari wa mbele kwenye makabiliano
na mapambano mapya. Lakini, ukweli unabaki pale pale kwamba
makanisa mengi yenye kukiri Jina la Kristo na kusema kwamba
yamejipanga na kuungana na Ukristo ule uliosababisha Kitabu cha
Matendo ya Mitume kuandikwa, yamekufa kama makaburi. Huku
yakiwa yamelewa sana na dawa ya ubinafsi, na kuzoea sana (na
kupenda sana pia) Ukristo usiokuwa na msalaba, na yenye shauku ya
kuufanya Ukristo kupendwa sana na kuwa maarufu, wao (na sisi pia)
huonekana kama hawana mwelekeo kabisa katika kumfuata Bwana
Mkubwa (au, kama ndugu Mkristo mmoja mpendwa alivyosema, 244
“kumfukuzia Kristo hasa hasa”) au kufuata “Kusudi lile Kuu (ambalo
ni kuifikia dunia nzima) au kutekeleza ule Mpango Mkuu (yaani,
“kufanya watu kuwa wanafunzi” kwa kiwango cha Kristo na kwa
kufuata mkakati Wake). Kwa hali hiyo, wanalala tu.
[MZAHA KIDOGO – lakini wenye lengo la kufikisha
ujumbe.]
Jamaa mmoja alisema hivi, “Kama watu wote wanaolala
kanisani wangepangwa mstari – wangejisikia vizuri zaidi!”
Mwingine ametafsiri mahubiri kuwa ni “mtu mmoja
akizungumza katika usingizi wa mwingine”.
Mama mmoja alimpigia simu mchungaji wake saa tisa usiku
akasema, “Mchungaji! Nina tatizo kubwa sana. Shida yangu ni
kwamba sipati usingizi, hivyo silali kabisa. Naomba unihubirie
kidogo!” (Yaani, akisikiliza mahubiri anapata usingizi.)
Uzuri ni kwamba hivyo ni vichekesho, ingawa “wakalia vitu
kanisani” mara kwa mara hufanya hayo kuwa kweli. Ila sasa,
tunapofikiri uhalisi wa kusikitisha sana wa Wakristo kuishi maisha
yao kwa kujitakia mema na kujihudumia au kujihami, na makanisa
nayo yakielezwa kwa uwazi kabisa na kwa uhalali kabisa kuwa ni
“majitu yaliyolala” (ingawa ukweli ni kwamba si hivyo, na
inasikitisha sana kwa sababu, watu wengi hata hawajui hilo jitu
linapaswa kufanya nini au linaweza kufanya nini au lingeweza
kufanya nini kama limeamka kabisa na kwa ukamilifu. Basi,
wanaelewa kwa udogo sana jinsi ambavyo kanisa limelala kweli), 245
mbona hayo yanakuwa kama hukumu badala ya kuwa vichekesho.
Kwamba kanisa ni “jitu lililolala” ni wazo la Shetani kabisa.
Sasa, tufikie sehemu ya pili ya kanuni zile tulizotaja.
2. Watahakikisha usalama wao wenyewe. Fikiri tofauti kubwa
iliyo kati ya kujihami na kuishi tu, na huduma ya kweli. Tofauti hiyo
mara nyingi haionekani kwa sababu kwa kawaida makanisa hujitia
katika mpango ambao ni mchanganyiko wenye kupooza, ambao
unatoka katika hayo mawili. Wana “ibada” na wanatoa “nafasi za
kuhudumu” lakini je, matokeo yanakaribia utendaji na matokeo
yaonekanayo katika Kitabu cha Matendo ya Mitume? Huduma ya
kweli ina kujitolea, kujihatarisha na hali ya kutokujua kilicho mbele,
na masharti yake yanapangwa na Yeye anayesimamia shughuli
yenyewe. Wakati mtu anapoingia katika huduma ya kanisa la siku
hizi, anainuliwa kwamba ni “Mkristo wa kipekee sana,” lakini
mambo kama hayo yanaonyesha tu ujinga na kujipenda kwa
mwamini “wa kawaida”. Labda tuulize swali hapa – je, Mkristo wa
kawaida ndiye mbaya katika wazuri, au ndiye mzuri katika wabaya?
Vyovyote vile, kanisa la kawaida ni wazi kwamba liko kwenye
kujihami, likihesabu kondoo zaidi ya kuwalisha na kuwawezesha
kondoo ili watumwe kwenda kama ‘kondoo katikati ya mbwa mwitu’.
Kanisa la kawaida linajihusisha sana na majengo, bajeti, vipeperushi,
idadi ya watu na Biblia – vitu ambavyo, ingawa ni vizuri sana
vinapotumiwa sawasawa, husababisha “kifo” vinapokuwa lengo kuu. 246
Hivyo ni (au vinaweza kuwa) vitu muhimu vinavyoshikika kanisani,
lakini kuchukuliwa navyo ni hatari kwa habari ya Makusudi Halisi ya
kanisa. Kanisa linalojihami ni wazo la Shetani kabisa.
Tuangalie sehemu ya tatu.
3. Kama si tishio kwao, mbwa katika kikundi watakaribisha
wanachama wapya. Wakati mwingine, makusudi nyuma ya kutafuta
washirika wapya kanisani, kukua kwa kanisa na “mikutano ya
uinjilisti” yanahitaji kuchujwa vizuri kabisa. Makusudi ni rahisi sana
kupotoshwa na kuharibiwa kama yanakuza au kutukuza majina ya
watu na kuonyesha mafanikio ya viongozi binafsi pamoja na
mashirika au madhehebu au taasisi zinazo-ongozwa nao. Ile hali ya
kujilinda na uhasama wa baadhi ya viongozi ni dalili ya kutambua
kwao makusudi yao mchanganyiko yaliyoko nyuma ya wao
“kujenga” majengo, taasisi, taratibu, makundi ya watu na kadhalika.
Hakuna kusudi la mtu yeyote lililo safi kabisa, lakini kukua kwa
kanisa kunaweza kukuza sifa ya mtu na kuficha hali ya kujipenda na
kujisifu ya ndani, japo matangazo yatolewayo ni kwamba kuna nia
safi na shauku safi kabisa ya “kumtumikia Bwana”. Sikuzote mwili
uko karibu sana, na ni kitu hatari kilichojificha katika ngozi laini
sana ya hali ya kiroho. Hapo ninakiri udhaifu wangu pia, na kusema
ukiri wa wachungaji wengi walio wakweli na wacha Mungu ambao
nimewafahamu. Ninajua makanisa mawili madogo sana ambayo
yalijikuta katika jamii zenye kukua haraka. “Wazee” waliokuwa 247
katika makanisa hayo waliitikia kukua kwa makanisa hayo kwa njia
za ajabu sana. Kote, viongozi walimwambia mchungaji wao, “Inabidi
tuwe makini sana kuhusu hawa watu wapya wote wanaokuja maana,
ikiendelea hivi, tutapoteza utawala wa kanisa letu.” (!!!) He! Hivi
kweli, hali hiyo ya kujijali, kujifikiria na kujihami inaweza kudumu
katika kanisa “linalokua”? Je, hoja kama hizo zinaweza kutoka kwa
viongozi wa kanisa? Kila kiongozi mwenye cheo chochote kanisani
au wadhifa amewahi kukabiliana na mambo kama hayo katika
uongozi – na pengine yeye mwenyewe yuko hivyo. Hii ni namna
moja tu ya sura ambayo mwili unaweza kuvaa. Kwa kawaida, mwili
aidha unapenda utendaji au unapinga, na viongozi wa kiroho na
washirika waaminifu kanisani wanalengwa na Shetani ili
kusababisha maonyesho kama hayo, ya tabia ya mwili. Baada ya
zaidi ya miaka arobaini katika huduma, nimegundua kwamba lazima
kila mara nijitahidi kuuweka mwili “chini ya mamlaka”, na
kuuhesabu (Warumi 5:6, 11; Wagalatia 2:20).
Lakini kumbuka mahali mambo yanapobadilika katika ule
mfano wetu: MPAKA MBWEHA APITE! Mbweha akipita, na
aonekane wazi kabisa na wale mbwa, hawapati nafasi hata ya kulala.
Hawatashughulika na kujihami tena. Watawapokea wanachama
wapya katika kundi lao wanapokuja, lakini mbwa watakaokuja ni
wale walioko tayari kuingia katika mpango wa kumwinda yule
mbweha na kujiunga na wale mbwa wengine wote watakaohusika.
Ingawa mbwa wenyewe wanaweza kugongana kwa nguvu zaidi na 248
mara nyingi zaidi kuliko mwanzo, hawataona vidonda vyao na
uvimbe wao – kwa sababu wana mambo makubwa zaidi ya kufanya
kuliko kungurumiana, kubwekeana na kutaka kuumana. Mbweha
akiwa anaonekana, mbwa hao watakimbia kwa pamoja wakiwa na
maono yanayofanana na makusudi pia.
MBWEHA NI NINI?
Je, mbweha ni nini kwa Mkristo na kwa ushirika wa
waaminio? Mimi binafsi nahesabu kuwa kitu muhimu cha kufukuzia
katika maisha ya Mkristo ni Yesu Kristo. Kazi kubwa katika maisha
ya Kikristo ni “kumfuata Yesu” au “kumtafuta Yeye kwa bidii zote”.
Kwangu, hilo ndilo la mwisho kabisa. Lakini, utaratibu uliowekwa
kwa ajili ya kuwaingiza wafuasi wengine ndiye huyo mbweha
ambaye Yesu alimweka mbele ya wanafunzi Wake ajulikanaye kama
“Agizo Kuu”. Viongozi wa Kikristo wana kawaida ya kuweka
mbweha wadogo ili “watu wao” wawafukuzie – vitu kama
mahudhurio, michango kwa ajili ya bajeti, mambo ya ujenzi,
mikutano ya uamsho ya mara kwa mara, na mikazo mingine
mbalimbali. Lakini hao “mbweha wadogo” wanaweza “kuharibu
mizabibu”! Wanakuwa ndiyo kiini kikubwa na malengo makubwa,
wakielekeza usikivu wa waaminio katika shughuli na mipango
ambayo inawasaidia wao zaidi kuliko kuifikia dunia.
Wakulima kadhaa walikuwa wanapoteza muda wao wakijisifu
juu ya mbwa wao wa kuwindia. Mmoja akasema, “Nadhani mbwa 249
wangu anaweza kusikia harufu ya miaka hamsini iliyopita.”
Mwingine akasema, “Acha mchezo bwana. Hakuna mbwa
anayeweza kusikia harufu ya zamani hivyo.” Yule aliyetangulia
akasema, “Nadhani mbwa wangu anaweza.” Mwindaji wa tatu
akasema, “Ninajua jinsi ya kupata ukweli. Nakumbuka Baba yangu
akisema kwamba nilipokuwa mtoto mdogo palikuwa na mbweha
mzee aliyekuwa anapita chini ya nyumba yetu kila jioni. Ni miaka
arobaini na zaidi sasa. Si twende mpaka pale tuone kama mbwa
wako anaweza kunusa hiyo harufu?” Basi, wakampakia mbwa
kwenye gari na kwenda mpaka hiyo nyumba ya zamani.
Wakamfikisha pembeni mwa nyumba hiyo na wakamzungusha mpaka
kandoni. Mara yule mbwa akaanza kupiga kelele na kuonyesha dalili
za kunusa na kufuata – akijivuta kwa nguvu atoke kwenye kamba
iliyokuwa imemfunga. Mwenye mbwa akamwachia. Mara, mbwa yule
akakimbia mbio, akavuka uwanja uliokuwa mbele ya nyumba.
Alipokaribia kama yadi ishirini mbali na nyumba, mara aliruka juu
kama futi sita! Mtu mmoja akasema, “Huyo mbwa ana matatizo
gani?” Yule mkaazi wa pale akajibu, “Hana matatizo yoyote. Miaka
arobaini iliyopita, hapo mahali kulikuwa na uzio, na yule mbweha
alikuwa anarukia hapo!” Yule mbwa akaendelea kulia na kunusa
huku akivuka ule uwanja. Mara akakata kulia na kufuata njia kando
ya nyumba. Yule mkaazi wa zamani wa pale akasema, “Miaka
arobaini iliyopita kulikuwa na kichaka hapo na miti, na yule mbweha
alikuwa anaizunguka. Kweli, mbwa wako ananusa njia ya yule 250
mbweha wa zamani.” Mbwa akaendelea kwenda pole pole akinusa
na kulia mpaka akapotelea kabisa. Wale wawindaji walikuwa
wanamwangalia sana huyo mbwa, hawakuona akitoweka. Hatimaye
mmoja akasema, “Hebu tumfuate, tuone atatufikisha wapi.”
Wakafuata kweli, lakini pamoja na kumtafuta sana kila mahali,
hawakumpata. Baada ya kumsaka mchana kutwa, ilibidi waachilie
mbali shughuli hiyo, wakitumaini kwamba mbwa yule angerudi
mwenyewe baadaye. Lakini haikuwa hivyo. Mbwa akawa amepotea,
na hawakuweza kumpata popote. Baada ya kusubiri majuma kadhaa
na kuendelea kumtafuta hapa na pale, na kuuliza, walikata tamaa na
kuachilia mbali msako wao.
Miaka miwili baadaye, muda mrefu tu baada ya kuachilia
mbali kumtafuta mbwa na baada ya kupoteza matumaini, yule
mwenye mbwa akapigiwa simu jioni moja. Mpiga simu akasema,
“Je, hapo ni nyumbani kwa Reks, mbwa mwindaji?” Mwenyewe
akasema, “Ndiyo – alikuwa akikaa hapa, lakini amepotea kwa muda
wa miaka kama miwili hivi. Wewe nani, na kuna nini?” Akajibiwa
hivi: “Ni hivi mzee. Maelezo yangu yatakushangaza. Mimi ni meneja
wa duka kubwa sana katika mji wa New York. Nimemtambua mbwa
wako kwa jina na anwani yako uliyomwekea shingoni. Hapa dukani,
amekaa analinda vazi la ngozi ya mbweha la zamani, na
nimeshindwa kumtoa.” Mwenye mbwa akaacha kushangaa, akaifikiri
kidogo halafu akasema, “Mheshimiwa. Unaweza kumrudisha mbwa
wangu kwa gharama zangu?” Yule mwenye duka akasema, 251
“Nimefikiri hilo, na nimekwisha fanya utafiti, na gharama yake ni
kubwa sana.” Mwenye mbwa akauliza, “Hiyo ngozi yenyewe ina
thamani gani?” Mwenye duka akajibu, “Ni dola 65”. Baada ya
kufikiri kidogo, mwenye mbwa alisema hivi, “Basi mzee, naomba
unitumie hiyo ngozi, halafu uache duka lako wazi kwa dakika tano tu
kesho”.
Wapendwa – wakati umefika – kwa ajili ya Mungu na kwa
ajili ya Kristo na kwa ajili ya mabilioni ya watu waliopotea, na kwa
ajili ya ushirika wa waaminio, na kwa ajili ya kila kitu kilicho kweli
na kizuri na chema, kwetu sisi kurudi hadi “nyumbani kwetu” kiroho,
tupate tena kunusa ile harufu ya zamani (yaani, Agizo Kuu) – harufu
ambayo itakuwa na thamani na maana zaidi sana kuliko hivi vitu
vingine tunavyofukuzia – dunia na mwili – na kuanza kumfuata
Mbweha Mkuu.
Huyo Mbweha Mkuu ni nani? Ni kuifikia dunia yote. Dunia
Yote. Kuifikia dunia yote kwa ukamilifu wake wote. Ndiyo Mbweha
Mkuu wa Kristo – aliyewaagiza watu Wake wamfukuze. Kila
Mkristo anapaswa atazame kwa makini sana na kwa muda mrefu
sana huyo Mbweha Mkuu kila siku ya maisha yake. Kumtazama
huyo Mbweha kwa muda mrefu kutapelekea kuelewa mambo kadhaa
muhimu. La kwanza ni maono. Lingine ni mkakati. Lingine ni
maongezeko yaliyohamasishwa, dhana ambayo bila shaka ilikuwa
na sehemu muhimu katika kutokea kwa Kitabu cha Matendo. Na kitu
cha mwisho ni kuelewa Ufikiaji Dunia Yote kwa ukamilifu, - lengo 252
la kuifikia dunia nzima, na lengo la ufikiaji ambao utakuwa kamili –
yaani, wenye kuhusisha kila njia iliyoagizwa na kufunuliwa, ili
kukamilisha kazi yenyewe.1
1 Hakuna chochote kilichosemwa katika hii sura fupi ambacho kinapaswa kuhesabika kuwa kinyume cha kanisa kwa namna yoyote ile. Tayari kuna kulipiga kanisa kwa kila namna – mimi sitaki kuwa na hatia ya kuongeza. Ila, tahadhari hii ichukuliwe kwa uzito wake. Kanisa tukufu la Mungu – Mwili na Bibi Arusi wa Kristo, Jengo la Mungu, “nguzo na msingi wa ukweli” linahitaji kuongeza idadi ya washiriki wenye kuomba, kwenda, kutoa na kuunga mkono mkakati huo kuliko wakati mwingine wowote. Lakini, kusudi mbadala au utaratibu bandia (“mbweha wadogo”) vitaharibu utukufu wa kanisa na kuliruhusu lilaumiwe kihalali kabisa, na kukataliwa na wengi. Tunaomba Mwili wa Kristo umpe Yeye kitu tendaji kabisa kwa ajili ya kutimiza Agizo Kuu! Tunaomba Bibi Arusi wa Kristo ampende Kristo sana kiasi kwamba kule kutajwa tu kwa Agizo Kuu kusukumwe na pendo la Kristo kulitimiza! Tunaomba Jengo la Mungu liwe Hekalu la kutosha kabisa kumwonyesha Mungu wetu kwa dunia nzima!
253
KumaliziaMaisha Ya Mbwa Wa Mwituni
Wale watu ambao nimepata nafasi na fursa ya kufanya kazi
nao katika kufanya watu kuwa wanafunzi, na utaratibu wa kuifikia
dunia ni miongoni mwa Wakristo wenye motisha kubwa niliowahi
kuwafahamu. Mfano mzuri sana ni mwanafunzi kijana aitwaye Ian
Bowers. Amekuwa akisonga mbele na kuendelea katika ufahamu wa
kuwafanya watu kuwa wanafunzi na kujihusisha kwa miaka kadhaa
sasa. Wakati fulani aliwahi kutunga shairi kuhusu mfano wangu wa
“Mbweha huyo!” Nimelisoma mara kadhaa. Niliomboleza wakati
ujumbe wa shairi hilo uliponifikia na kunigusa moyoni. Kwa kibali
chake, ninamalizia kitabu changu kwa shairi hilo. Naomba na wewe
ubarikiwe kama mimi nilivyobarikiwa.
Maisha ya mbwa wa mwituni ni rahisi tu,
Ingawa si maisha ya starehe.
Hebu nitoe mtazamo mpya
Maana tunaishi maisha ya uhitaji.
Hayo mahitaji yanaonekana kututawala
Na kusimamia maisha yetu.
Lakini kila siku ninajiuliza
Ikiwa mahitaji hayo si uongo tu.
Ni hivi: Kila siku ni yetu ya kushinda
254
Hatuna ratiba yoyote ya kufuata.
Lakini, hili hitaji hutujia
Hitaji la kulala.
Katika uwanja au chini ya mti wa kivuli
Au chini ya mbingu iliyojaa nyota
Unatamani maisha ya mbwa
Unapotuona tumelala hapo chini.
Ila, usiache kuendelea na hadithi yangu sasa.
Sikiliza, na usikie vizuri sana.
Ugundue kwamba maisha ya mbwa anayelala
Ni hatua moja tu kutoka Jehanamu.
Maana nikiamshwa tu kwa dakika
Kitu fulani hujigusa ndani yangu
Nami nina njaa – njaa sana
Hitaji langu ni kula.
Mjini nitapata takataka kidogo
Msituni nitapata mnyama mdogo
Lakini nikisha tosheka
Ninarudi haraka tu kulala usingizi.
255
Na kwa hili wala sikutishwa
Nilihesabu kuwa ni hazina ya dhahabu
Wakati mbwa mvivu kuliko mimi
Alipokaribishwa kundini.
Je, bado ni maisha ya mbwa
Yanayotamaniwa na moyo wako?
Rafiki yangu, hujui hata kidogo
Maana, kuna zaidi ya hayo.
Hatimaye kisa changu kitakuwa dhahiri sana
Maana, sasa pokea mwanga
Upande mbaya wa maisha ya mbwa mwitu
Ni hitaji la kupigana.
Lakini, kupigana kwa sababu gani? Nikuulize sasa
Je, waweza kuniambia wakati
Wa kuinuka kinyume cha mbwa mwenzangu
Au pengine kumkomeshea maisha yake?
Yeye ni mbwa mwenye ngozi na mkia
Anayo meno na macho ya kuona
Lakini lazima athibitishe kwamba yeye ni bora
Au wakati mwingine ni mimi.256
Basi, unguruma na ubweke, na ung’ate
Kiburi chetu kutosheleza
Mmoja atashinda hii vita ya kijinga
Na inawezekana hata mmoja akafa.
Na vita inapokuwa imekwisha
Sikuzote ni hasara, hakuna faida
Na kile tulichothibitisha
Ni kwamba mbwa wanaweza kuwa na kiburi sana.
Sidhani kama ni sahihi kusema
Kuna hitaji la kupigana
Nadhani badala yake ni kwamba tunakosa la kufanya
Na tuko hatua moja tu kutoka kwenye kufa.
Je, unasikiliza kwa makini?
Rafiki yangu, unasikiliza kweli?
Maana hadithi yangu haijaisha.
Sasa ndiyo tu imeanza.
Kuna hitaji moja ninalokubali
Tena nasema pasipo aibu
Huyu mbwa mwitu anapenda, na hata anaishi257
Kwa ajili ya kukimbiza au kufukuza.
Lakini si kukimbiza tu, rafiki.
Ni kukimbiza ambako ni kuzuri sana
Kukimbiza kwenye kuhamasisha maisha yangu
Na kunakoshika akili yangu.
Si wale mbweha wadogo.
Hao nimewahi kuwafukuza wote.
Wao ni rahisi kuwashika na kuwamaliza
Nikawa nimechoshwa upesi nao.
Siku moja ikatokea
Kamwe sitasahau
Kulitokea harufu fulani hewani
Nikapata hamu kubwa.
Nikainua pua yangu angani
Nikasimama kwa miguu yangu
Ndipo nikawaona wale mbwa wengine
Wakiwa tayari kama mimi.
Kiongozi wetu ni Salvadori
Wa kikundi chetu cha mbwa kumi na mbili258
Ngozi yake ilikuwa manjano kabisa
Na michirizi myekundu mgongoni.
Huyu ndiye mliyekuwa mnamsubiri
Ndivyo alivyosema, huku macho Yake yaking’aa
Huyu ndiye mbweha ambaye mkimshika
Hakika itagharimu maisha yako.
Inueni pua zenu hewani
Inuseni hiyo harufu
Jifunzeni muijue vizuri,
Jifunzeni muijue vizuri.
Na wakati msipoweza kuniona
Inuieni pua zenu juu
Pateni hiyo harufu na kuifuata
Mjue kwamba nipo.
Nikahisi moyo wangu unaongeza mapigo
Shinikizo la damu likaongezeka
Kadiri hiyo harufu ilivyozidi kuwa na nguvu
Nguvu zaidi.
Halafu bila ya maonyo259
Kama radi ya umeme
Kiongozi wetu akageuka na kujitupa
Kuelekea katika giza la usiku.
Tulisimama kidogo tu
Na kutazamana machoni
Tukajua gharama itakayotukabili
Lakini hatukujua zawadi tutakayopata.
Na kama ni kumshika huyo mbweha,
Hatukupaswa kukawia zaidi.
Maana kazi ilikuwa ni kubwa sana
Harufu ilipoanza kupotea.
Lazima ibakie kwenye pua yetu
Kusudi letu lazima liwe wazi
Tutamshika huyu mbweha mwenye nguvu
Kauli mbiu yetu itakuwa HAYA TENA – MBWEHA
HUYO!!
Pua zangu zikapanuka, misuli zangu zikakaza
Nikaruka kutoka mahali pangu
Miguu yangu ya mbele ikakutana na ardhi
Na mbio zikawa zimeanza.260
Lakini rafiki yangu, usifikiri unajua
Nilichokuwa ninakimbilia
Zawadi haikupatikana katika mbweha
Ilikuwa kitu kingine zaidi.
Sikuwa naendeshwa na hitaji
La kulala au hata kula chakula
Badala yake, nilikuwa nimetawala kabisa
Kilichokuwa kinanishikilia hapo kwanza.
Je, unasikiliza kwa makini sana?
Je, rafiki yangu, unasikiliza?
Zawadi ni hii: Maisha sahihi
Niliyoishi kulingana na kusudi.
Ningepumzika nile, ningepumzika nilale
Uchovu uliniambia wakati wa kufanya hivyo
Lakini nguvu zilipokuwa zinanirudia tu
Ufukuzaji uliendelea.
Kwa habari ya kupigana, jifunze kweli hii
Hatukuwa tena na nafasi!
Tulikuwa tumepata changamoto ya maisha261
Yenye kushika akili yetu.
Maana hatukufukuzia kitu bure tu
Yaani mbweha tusiyemwona
Tulijua yeye ni mjanja
Basi, tukafukuza kwa mkakati.
Hatukuhukumu wala kutishia
Wageni waliokuja kundini
Tuliwashirikisha maono yetu kwa ujasiri
Na kuwaingiza pia katika kumtafuta.
Hii njia, hiyo zawadi kuu
Mbwa wengine hawakuiona
Na wengine waliingia katika mbio
Isingekufa na mimi.
Sasa jifunze hili somo la mbwa mzee
Jifunze vizuri, vizuri sana
Kwa kila mbwa anayekufa
Watatu zaidi wajiunge.
Kwa hiyo usifikiri unaniona sasa
Mbwa dhaifu anayekaribia kufa262
Nuru yangu itang’aa bado
Hata nitakapovuta pumzi yangu ya mwisho.
Kwa sababu nimewafundisha
mbwa wengine wa mwitu
Na nimewafundisha hilo vizuri sana
Nimewafundisha jinsi ya kuinua pua zao
Nimewafundisha jinsi ya kunusa.
Kitu kingine nilichowafundisha
Cha muhimu zaidi sana
Nimewafundisha wote mkakati nilioishi na kuufuata
“Ukimbiaji”.
Sasa mmesikia hadithi yangu.
Je, ulisikiliza kwa makini?
Je, unatamani maisha ya mbwa
Ambayo ni hatua moja tu kutoka Jehanamu?
Changamoto iko mbele yako
Je, utaongeza mfumuko?
Nenda uingie katika mbio
Kimbia na wewe, na UKIMBIE VIZURI!
- Mtunzi ni Ian Bowers263
FAHIRISI
264
Muhtasari Wa Kila Sura
Sura Ya Kwanza Maono Ni Muhimu Kiasi Gani? (Mithali
29:18)
I. Dhana Ya Kiroho
A. Umuhimu Wa Maono
B. Maana Ya Maono
II. Hali Ya Kusikitisha
A. Hakuna Maono Madhabahuni
B. Hakuna Maono Katika Viti
C. Hakuna Maono Katika Maisha Ya Kila Siku
III. Matokeo Yake Mabaya
A. Watu Huacha Kujizuia – matokeo ya kiadili ya
kutokuwepo kwa maono
B. Watu Husambaratika – matokeo ya kijamii ya
kutokuwepo kwa maono
C. Watu Huwa Tayari Kuhukumiwa – matokeo ya
kibinafsi ya kutokuwepo kwa maono
D. Watu Huangamia – matokeo ya kiroho, ya milele ya
kutokuwepo kwa maono
Sura Ya Pili Agizo Lenye Kuamua Wajibu Wetu (Mathayo
28:18-20)
I. Uhakikisho Nyuma Ya Agizo Lenyewe265
A. Mamlaka Ya KiMungu
B. Mamlaka Iliyotolewa
C. Mamlaka Stahili
D. Mamlaka Iliyofafanuliwa
II. Wajibu Katika Agizo Lenyewe
A. Amri Ya Kusonga Mbele Ya Pekee Kwa Kanisa (Kwa
Mkristo Pia)
B. Kuligawa Agizo
1. Watenda Kazi Watumiwe
2. Kuingia Shambani
3. Kupanua Maono
4. Kuwashuhudia
5. Kuwaingiza Kazini Wanaopatikana
6. Kuelimisha Na Kuwajenga Walio Kazini
7. Kumtazamia Yeye (Bwana) Kutenda Kazi
C. Je, Ni Agizo Kuu Au Ni Kupuuza Kukuu?
Sura Ya Tatu Wazo Linaloamua Njia Tutakayotumia
(Mathayo 28:19)
I. Kufanya Wanafunzi
A. Mwanafunzi
B. Mwenye Kufanya Wanafunzi
C. Tendo La Kufanya Wanafunzi
D. Nidhamu Husika266
II. Kufanya Wanafunzi Kunakosababisha Huduma Ya
Kujizidisha
Sura Ya Nne Ufunguo Ulioko Mlangoni Mwa Historia Ya
Kanisa
(Matendo 1:1-5)
I. Kitabu Cha Kwanza Kinatajwa
A. Injili Kulingana Na Luka
B. Luka Alikuwa Nani, Na Aliingiaje Katika Hadithi?
C. Kweli Za Tafakari
1. Mfano Wa Kanisa Kama “Mwili Wa Kristo”
2. Luka Aliandika Vitabu Viwili Vya Ajabu
II. Mwanafunzi Binafsi Anatajwa
A. Moja Ya Nne Ya Agano Jipya Iliandikwa Na Mtu
Mmoja!
B. Kwa Nini Luka Aliandika Vitabu Hivi Viwili Kwa
Mtu Mmoja?
C. Ushuhuda Binafsi
III. Tamko La Wazi Kuhusu Kusudi La Kuandika
A. Yote Ambayo Yesu Alianza Kufanya Na Kufundisha
B. Je, Yesu Anafanya Nini Sasa?
1. Anaendelea Kufanya na Kufundisha
2. Kila Aaminiye Ni Chombo Hai Cha
Kuhifadhi Uwepo Wake267
C. Je, Yesu Alitumia Watu Aina Gani?
1. Wa Kawaida
2. Waliochaguliwa
3. Walioamini
4. Walioamriwa
5. Waliotawaliwa
Sura Ya Tano Vinavyotakiwa Ili Kufanya Wanafunzi, au
Tiba Ya Daktari Kutibu Kuacha Kukuu
(Luka 1:1-14)
I. Wajibu Binafsi
II. Utafiti Wa Dhati
III. Vyanzo Sahihi
IV. Uzalishaji Unaodumu
Sura Ya Sita Mpango Wa Mungu Wa Kuongeza (2Tim. 2:2)
I. Picha Ya Mwanafunzi Mwenye Kuongeza Wanafunzi
A. Ni Mwana
B. Ni Askari
C. Ni Mwanariadha (mkimbiaji)
D. Ni Mkulima
E. Ni Mtenda Kazi
F. Ni Chombo
G. Ni Mtumishi268
II. Utaratibu Wa Kuongeza Wanafunzi
A. Mpango Unamfikiaje Mwanafunzi?
B. Nini Kilichomo Katika Mpango Wa Kusikia?
C. Mwanafunzi Akisha Wezeshwa, Anafanya Nini?
III. Mifano Yenye Kuonyesha Umuhimu Na Uwezo
A. Mwinjilisti
B. Siku Ya Pentekoste “Kila Siku”
C. Kuongezwa Fedha
D. Maono Ya Kuifikia Dunia Kwa Kufanya Wanafunzi
Sura Ya Saba Hekima Ya Mkakati Wa Yesu (1Wathes.
3:8)
Sura Ya Nane Jinsi Kiwango Hiki Kifanyavyo Kazi
Kanisani
(Waefeso 4:7-14)
I. Mtoa Vipawa
A. Alishuka
B. Alipaa
C. Yuko Juu Ya Vyote
II. Vipawa Vyenyewe
A. Mitume
B. Manabii
C. Wainjilisti269
D. Wachungaji Waalimu
III. Malengo Ya Kutolewa Kwa Vipawa Hivi
A. Kupata Viungo
B. Kuviwezesha Viungo
C. Kuvitumia Viungo
Sura Ya Tisa Maneno Yake Ya Mwisho, Wosia Wake
(Matendo 1:8)
I. Mkakati Kwa Ajili Ya Kuenea Kwa Injili
II. Chanzo Cha Ushuhuda Wa Injili
III. Mada Ya Ushuhuda Wa Injili
IV. Upeo Wa Ushuhuda Wa Injili
A. Hali Yako Inayokukabili
B. Mazingira Yako Hapo Ulipo
C. Eneo Lako Kimataifa
V. Siri Ya Ushuhuda Wa Injili
270
Maswali Na Mapendekezo Kwa Ajili Ya Kujifunza Hiki Kitabu
Kwa ajili ya Sura ya Kwanza, “Maono Ni Muhimu Kiasi Gani?”
1. Toa maana mbili za maono ya KiMungu.
2. Nini matokeo yanayofuata, wakati watu wa Mungu
wanapokuwa hawana maono?
Kwa ajili ya Sura ya Pili, “Agizo Lenye Kuamua Wajibu Wetu”.
1. Nini kazi saba za Agizo Kuu? Ngapi katika hizo ni amri?
2. Ni mpango gani mbadala ambao Shetani ametoa chini ya
kila kazi, katika hizo saba?
Kwa ajili ya Sura ya Tatu, “Wazo Linaloamua Njia
Tutakayotumia”.
1. Toa maelezo kuhusu kila moja katika maneno haya:
“Mwanafunzi,” “Mfanya Wanafunzi,” “kufanya
Wanafunzi,” na “Nidhamu”.
2. Nini tofauti kati ya Ukristo wa kawaida, wa kuhudhuria
kanisani, na maisha ya Kikristo yenye kuzaa huduma ya
maongezeko?
Kwa ajili ya Sura ya Nne, “Ufunguo Ulioko Mlangoni Mwa
Historia Ya Kanisa”.
1. Toa maelezo mafupi kuhusu utaratibu wa kufanya
wanafunzi wa Paulo hadi Luka hadi Theofilo.
271
2. Tuna ushahidi gani kwamba Theofilo “alishika” huo
mkakati na “kukimbia nao”?
Kwa ajili ya Sura ya Tano, “Vinavyotakiwa Ili Kufanya
Wanafunzi, au
Tiba Ya Daktari Kutibu Kuacha Kukuu”
1. Orodhesha na kueleza kwa kifupi mambo manne ambayo
Dakta Luka alifanya, na mwanafunzi Theofilo.
2. Nini umuhimu wa kila hatua katika utaratibu mzima? Je,
mfanya wanafunzi anaweza kupunguza hata moja katika
hizi na kutazamia mafanikio katika kufanya wanafunzi?
Je, ni hatua ngapi katika hizi ambazo wewe unafanyia
kazi kwa sasa kwa ajili ya kufanya mwanafunzi?
Kwa ajili ya Sura ya Sita, “Mpango Wa Mungu Wa Kuongeza”.
1. Nini picha saba za mwanafunzi katika
2Timotheo sura ya 2? Je, ndiyo
imekamilika, au ni pendekezo tu?
2. Eleza kidogo ule mkakati wa vizazi katika
2Timotheo 2:2, ukionyesha kilicho cha
lazima ili “kuhakikisha” maongezeko ya
vizazi vinne.
Kwa ajili ya Sura ya Saba, “Hekima Ya Mkakati Wa Yesu”.
1. Eleza hekima ya mkakati wa Yesu kiutaratibu,
alipowafundisha Mitume Wake kumi na mbili.
272
2. Je, unaamini maelezo ya mfumo yaliyotolewa katika hii sura
kuwa ni ya msingi, au ya bahati mbaya, au ya kubahatisha tu
katika mkakati wa Yesu?
Kwa ajili ya Sura ya Nane, “Jinsi Kiwango Hiki Kifanyavyo Kazi
Kanisani”.
1. Je, mkakati wa kufanya wanafunzi kwa vizazi ziaid ya kimoja
unaweza kufanya kazi katika kanisa la siku hizi? Kivipi?
2. Fafanua kidogo yale maelezo ya mipango miwili
yaliyotolewa katika sura hii – mfano wa kawaida na ule
utolewao na Waefeso 4:7-14.
Kwa ajili ya Sura ya Tisa, “Maneno Yake Ya Mwisho, Wosia
Wake”.
1. Ni neno gani moja katika Kitabu cha Matendo
linalodhihirisha mkakati wa Mungu kwa ajili ya kuenezwa
kwa Injili? Nini maana zake mbili? Nini uhusiano kati ya hizo
maana mbili za neno hilo?
2. Nani aliye katika “kundi la watenda kazi” wa Mungu, na
wanapaswa kufanya kazi katika maeneo gani?
3. Watenda kazi watafanikishaje kazi hiyo?
Kwa ajili ya Sura ya Kumi, “Haya Tena, Mbweha Huyo!”
1. Fafanua ule mfano wa “Mbweha”.
2. Je, mfano huo ni wa kweli kulingana na mambo uliyoona
katika kanisa la mahali?
3. “Mbweha Mkubwa” ni nini? 273